Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Anawapenda Watu Wapole

Yehova Anawapenda Watu Wapole

Mkaribie Mungu

Yehova Anawapenda Watu Wapole

Hesabu 12:1-15

KIBURI, wivu, kujitakia makuu. Kwa kawaida watu ambao wamefanikiwa katika ulimwengu huu wanakuwa na tabia hizo. Lakini je, tabia kama hizo zinatufanya tuwe na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova Mungu? Hapana, badala yake Yehova anafurahi kuona waabudu wake wakiwa wapole. Hilo linaonekana wazi kutokana na simulizi linalopatikana katika kitabu cha Hesabu sura ya 12. Simulizi hilo linatukia katika nyika ya Sinai, baada ya Waisraeli kukombolewa kutoka Misri.

Miriamu na Haruni, dada na ndugu wakubwa wa Musa, ‘walianza kusema’ vibaya juu ya ndugu yao mdogo. (Mstari wa 1) Badala ya kuzungumza moja kwa moja na Musa, walisema vibaya juu yake, inaelekea walieneza manung’uniko yao ndani ya kambi. Kwa kuwa Miriamu ndiye anayetajwa kwanza, inaelekea ni yeye aliyeanza kunung’unika. Sababu ya kwanza ya kunung’unika ilikuwa kwamba Musa alioa mke Mkushi. Je, Miriamu alikuwa na wivu kwamba huenda mwanamke huyo ambaye si Mwisraeli angeheshimiwa zaidi kuliko yeye?

Kulikuwa na sababu nyingine za manung’uniko. Miriamu na Haruni wakawa wakisema hivi: “Je, Yehova amesema kupitia Musa tu? Je, hajasema kupitia sisi pia?” (Mstari wa 2) Je, sababu halisi ya manung’uniko ni kwamba walitamani kupata mamlaka zaidi na kutambuliwa?

Katika simulizi hilo, Musa hakujibu mwenyewe manung’uniko hayo. Kwa wazi, alivumilia kwa utulivu mambo yote mabaya yaliyosemwa juu yake. Uvumilivu wake unathibitisha maelezo ya Biblia kwamba alikuwa “mpole zaidi kuliko watu wote” duniani. * (Mstari wa 3) Musa hakuhitaji kujitetea mwenyewe. Yehova alikuwa akisikiliza, na alimtetea Musa.

Yehova aliona kwamba ni yeye waliyekuwa wakimnung’unikia. Kwa kweli, ni yeye aliyemweka rasmi Musa. Alipokuwa akiwakaripia wanung’unikaji hao, Mungu aliwakumbusha kwamba alikuwa na uhusiano wa pekee pamoja na Musa: “Mimi husema naye kinywa kwa kinywa.” Kisha, Yehova akawauliza Miriamu na Haruni hivi: “Kwa nini, basi, hamkuogopa kusema juu ya . . . Musa?” (Mstari wa 8) Waliposema vibaya juu ya Musa, kwa kweli walikuwa na hatia ya kusema vibaya juu ya Mungu. Kwa sababu ya ukosefu huo mkubwa wa heshima, wangeona hasira ya Mungu.

Miriamu, ambaye inaonekana kwamba ndiye aliyeanzisha manung’uniko, alipigwa na ukoma. Papo hapo, Haruni akamsihi Musa asali kwa ajili ya Miriamu. Hebu fikiria, Miriamu alihitaji msaada wa Musa, yule ambaye walikuwa wakisema vibaya kumhusu! Kwa upole, Musa alifanya kama alivyoombwa kufanya. Akizungumza kwa mara ya kwanza katika simulizi hili, Musa alimsihi Yehova kwa bidii kwa ajili ya dada yake. Miriamu aliponywa, lakini alivumilia aibu kwa muda wa siku saba akiwa ametengwa nje ya kambi.

Simulizi hilo linatusaidia kuelewa kwa undani sifa ambazo Yehova anathamini na tabia ambazo zinamchukiza. Ikiwa tunataka kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu, tunapaswa kujitahidi kuondoa kabisa tabia ya kiburi, wivu, na kujitakia makuu, tabia ambazo huenda tunazo. Yehova anapenda watu wapole. Anaahidi hivi: “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:11; Yakobo 4:6.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 7 Upole ni sifa yenye nguvu ambayo inamwezesha mtu kuvumilia kwa subira ukosefu wa haki bila kulipiza kisasi.