Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Mwanamume aliyeanza kuvuta bangi na tumbaku akiwa bado kijana alipata jinsi gani nguvu za kuacha zoea hilo? Ni nini kilichomwezesha mshiriki mmoja wa genge lenye jeuri kuzuia hasira yake na hivyo kushinda hisia za kuwachukia watu wa jamii nyingine? Ona yale ambayo kila mmoja wao alisema.

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU

JINA: HEINRICH MAAR

UMRI: 38

NCHI: KAZAKHSTAN

HISTORIA: ALIZOEA KUVUTA BANGI NA TUMBAKU

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa kusini mwa Kazakhstan, umbali wa kilomita 120 hivi kutoka jiji la Tashkent. Eneo hilo lilikuwa lenye ukame na lenye joto kali wakati wa kiangazi, hali ya joto ilifikia digrii 45 Selsiasi, na wakati wa baridi kali kiwango cha baridi kilishuka kufikia digrii 10 hivi chini ya sufuri, hiyo ni hali nzuri ya hewa kwa ajili ya ukuzaji wa zabibu na bangi.

Wazazi wangu walikuwa wa asili ya Ujerumani. Wote wawili walikuwa Wakristo wa dini ya kiinjilisti lakini hawakuishi kulingana na mafundisho ya dini yao. Hata hivyo, walinifundisha kusema kutoka akilini Sala ya Bwana. Nilipokuwa na umri wa miaka 14, mama yangu na dada yangu mkubwa walijifunza Biblia kwa muda fulani pamoja na Mashahidi wa Yehova. Siku moja, nilikuwa nikisikiliza wakati Mashahidi wawili waliokuwa wakijifunza Biblia pamoja na mama walipomwonyesha jina la Mungu, Yehova, katika Biblia yake ya zamani. Nilishangaa. Mama aliacha kujifunza Biblia, na mimi sikuendelea kupendezwa na mambo ya kiroho. Hata hivyo, baadaye nikiwa shuleni, mwalimu wetu alitueleza hadithi za uwongo za kila aina kuhusu dhehebu linaloitwa eti Mashahidi wa Yehova. Kwa kuwa niliwahi kuhudhuria mikutano fulani ya Mashahidi wa Yehova pamoja na dada yangu, nilimwambia mwalimu wangu kwamba mambo aliyokuwa akisema hayakuwa ya kweli.

Nilipofikia umri wa miaka 15, nilitumwa Leningrad, sasa ni St. Petersburg, Urusi, ili kujifunza kazi fulani. Niliwahubiria wale tulioishi nao mambo machache niliyojifunza kumhusu Yehova. Hata hivyo, nilianza kuvuta bangi. Nilipoenda nyumbani huko Kazakhstan, ilikuwa rahisi kwangu kununua bangi, hata ingawa ilikuwa kinyume cha sheria kufanya hivyo. Pia, nilikunywa sana pombe aina ya vodka na divai iliyotengenezwa nyumbani.

Nilimaliza masomo yangu kisha nikajiunga na jeshi la Sovieti kwa miaka miwili. Hata hivyo, bado niliendelea kukumbuka mambo fulani ambayo nilijifunza katika Biblia nilipokuwa kijana. Nafasi zilipojitokeza, nilizungumza na askari-jeshi wenzangu kumhusu Yehova na niliwatetea Mashahidi wakati watu waliposema uwongo kuwahusu.

Nilipomaliza utumishi wa jeshi, nilihamia Ujerumani. Nilipokuwa katika kambi ya wahamiaji, nilipokea kitabu kimoja cha kujifunzia Biblia kilichochapishwa na Mashahidi. Nilikisoma kwa shauku sana na nikaona kwamba mambo kilichosema yalikuwa ya kweli. Hata hivyo, nilishindwa kuacha zoea langu la kuvuta tumbaku na bangi. Baada ya muda, nilihamia karibu na jiji la Karlsruhe. Nikiwa huko nilikutana na Shahidi wa Yehova, naye akaanza kujifunza Biblia pamoja nami.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Kwa muda mrefu, niliamini kwamba Biblia ni Neno la Mungu. Na baada ya kusoma kitabu cha kujifunzia Biblia ambacho nilipewa, nilisadiki kwamba Biblia ilijibu maswali yote ya maana maishani. Hata hivyo, ilinichukua muda fulani kubadili mazoea yangu. Mwishowe, nilichochewa na shauri la Biblia kwenye 2 Wakorintho 7:1 nikaamua kujisafisha kutokana na “kila unajisi wa mwili na roho,” hilo lilimaanisha kuacha kabisa bangi na tumbaku.

Niliacha mara moja kuvuta bangi. Lakini ilinichukua miezi sita kuacha zoea la kuvuta tumbaku. Siku moja Shahidi aliyejifunza Biblia pamoja nami aliniuliza, “Una kusudi gani maishani?” Hilo lilinifanya nifikirie kwa uzito kuhusu zoea langu la kuvuta tumbaku. Nilikuwa nimejaribu mara nyingi kuacha kuvuta tumbaku. Hata hivyo, sasa niliamua kusali kabla ya kugusa sigareti badala ya kumwomba Mungu msamaha baadaye. Katika mwaka wa 1993, nilichagua siku moja ambayo ningeacha kuvuta. Kwa msaada wa Yehova, tangu wakati huo sijawahi tena kugusa sigareti.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Kwa kuwa sasa nimeacha zoea hatari na lenye kugharimu sana la kuvuta bangi na tumbaku, nina afya nzuri. Leo, nina pendeleo la kutumika nikiwa mfanyakazi wa kujitolea kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Ujerumani. Ninafurahi sana kwamba nilijifunza kutumia hekima ya Biblia katika maisha yangu! Kujua mambo ambayo Biblia inafundisha kumefanya maisha yangu yawe na kusudi kikweli.

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU

JINA: TITUS SHANGADI

UMRI: 43

NCHI: NAMIBIA

HISTORIA: ALIKUWA MSHIRIKI WA GENGE LENYE JEURI

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa katika kijiji cha mashambani huko Ohangwena eneo la kaskazini mwa Namibia. Katika kijiji chetu watu walipigwa na kuuawa wakati wa vita vya miaka ya 1980. Katika kijiji chetu, kijana alionwa kuwa mwanamume ikiwa tu alikuwa mpiganaji hodari ambaye angeweza kuwapiga vijana wengine. Kwa hiyo, nilijifunza kupigana!

Nilipomaliza shule, nilienda kuishi pamoja na mjomba wangu katika mji wa pwani wa Swakopmund. Muda mfupi baada ya kufika huko, nilijiunga na genge la vijana waasi. Tulikuwa tukienda mjini katika sehemu ambazo watu weusi hawakuruhusiwa kuingia, kama vile hoteli na vilabu vya pombe, ili tu kuanzisha vita. Mara nyingi, tulipigana na walinzi wa usalama na polisi. Kila usiku nilibeba kisu kirefu au upanga wenye makali, nikiwa tayari kumshambulia yeyote ambaye angenichokoza.

Usiku mmoja tulipokuwa tukipigana na genge lingine, nilikuwa karibu kuuawa. Mshiriki fulani wa genge hilo alinifuata kutoka nyuma na alikuwa karibu kunikata kichwa wakati mshiriki wa genge letu alipompiga mpaka akazimia. Ingawa nilikuwa karibu kufa, niliendelea kuwa mjeuri sana. Nilipoanza kubishana na mtu fulani, iwe mwanamume au mwanamke, sikuzote nilikuwa wa kwanza kutupa ngumi.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Nilipokutana kwa mara ya kwanza na mwanamke mmoja ambaye ni Shahidi wa Yehova, alinisomea mistari fulani katika Zaburi ya 37 kisha akaniambia kwamba kitabu cha Biblia cha Ufunuo kina ahadi nyingine nzuri sana za wakati ujao. Lakini kwa kuwa hakuniambia mahali ambapo ningeweza kusoma kuhusu ahadi hizo, nilitafuta Biblia na kusoma kitabu chote cha Ufunuo usiku huo. Nilipenda ahadi niliyosoma kwenye Ufunuo 21:3, 4 inayosema kwamba “kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” Shahidi huyo aliporudi, nilikubali kujifunza Biblia.

Ilikuwa vigumu sana kubadili njia yangu ya kufikiri na kutenda. Lakini nilijifunza kutokana na andiko la Matendo 10:34, 35 kwamba “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” Pia, nilijitahidi sana kuishi kulingana na andiko la Waroma 12:18: “Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.”

Zaidi ya kujifunza kuzuia hasira yangu, niliacha pia zoea lenye nguvu sana la kuvuta tumbaku. Mara nyingi, nilimwomba Yehova anisaidie huku nikitokwa na machozi. Lakini ni wazi kwamba mwanzoni nilifanya mambo kwa njia isiyofaa, nilijiambia kwamba hii ndiyo mara yangu ya “mwisho” kabisa kuvuta sigareti kisha nilisali baada ya kuvuta. Shahidi aliyenifundisha Biblia alinisaidia kuona umuhimu wa kusali kabla ya kuchukua sigareti. Pia, nilihitaji kuepuka kushirikiana na watu waliokuwa wakivuta sigareti. Zaidi ya hayo, nilifuata shauri la kuzungumza na wafanyakazi wenzangu kuhusu madhara ya kuvuta sigareti. Shauri hilo lilinisaidia sana, kwa kuwa wafanyakazi wenzangu hawangeweza tena kunipa sigareti.

Mwishowe, niliacha kuvuta sigareti nikabadili kabisa mtindo wangu wa maisha. Baada ya kujifunza kwa miezi sita na kutumia kanuni za Biblia, nilitimiza matakwa, nikabatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Nilikuja kusadiki kwamba Mashahidi wa Yehova ndio wanaofuata dini ya kweli wakati nilipoona waziwazi jinsi walivyopendana, bila kujali rangi au jamii yao. Hata kabla sijabatizwa na kuwa Shahidi, mshiriki mmoja wa kutaniko ambaye ni mzungu alinialika nyumbani kwake kwa ajili ya chakula. Ilikuwa kama ndoto. Mbali na kula chakula nyumbani kwake, sikuwa nimewahi kamwe kuketi hivyo kwa amani pamoja na mzungu. Sasa nilikuwa mshiriki wa undugu wa kweli wa ulimwenguni pote.

Zamani, walinzi wa usalama na polisi walijaribu kubadili kwa nguvu njia yangu ya kufikiri na kutenda, lakini walishindwa. Ni Biblia tu ndiyo iliyokuwa na nguvu za kunisaidia kubadili utu wangu na kuwa mtu mwenye furaha.

[Blabu katika ukurasa wa 29]

“Mara nyingi, nilimwomba Yehova anisaidie huku nikitokwa na machozi”