Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Waandishi waliompinga Yesu walikuwa nani?

Wakati wa huduma yake, Yesu alikutana na waandishi Yerusalemu na pia katika miji midogo-midogo na vijijini. Nje ya Yerusalemu, na hata katika jamii za Wayahudi nje ya Palestina, wanaume kama hao walikuwa maofisa wadogo, wasomi wa Sheria, ambao huenda walitumikia wakiwa wanakili au waamuzi wa maeneo hayo.—Marko 2:6; 9:14; Luka 5:17-21.

Huko Yerusalemu, waandishi walishirikiana kwa ukaribu sana na serikali ya Kiyahudi. (Mathayo 16:21) Daraka lao huko, kinasema kitabu fulani (The Anchor Bible Dictionary), “inaonekana lilikuwa kushirikiana na makuhani, iwe mahakamani na pia katika kutekeleza desturi na sheria za Wayahudi, na kuendesha shughuli za kila siku katika Sanhedrini.” Wakiwa walimu mashuhuri wa Sheria, waandishi wengine walikuwa washiriki wa Sanhedrini, au mahakama kuu ya Wayahudi. Walitumika pamoja na makuhani wakuu na Mafarisayo.

Mara nyingi, waandishi walionekana kuwa wapinzani wa kidini wa Yesu. Hata hivyo, wengine wao hawakumpinga. Kwa mfano, mwandishi mmoja alimwambia Yesu hivi: “Mimi nitakufuata mahali popote unapoenda.” Yesu alimwambia mwingine hivi: “Wewe huko mbali na ufalme wa Mungu.”—Mathayo 8:19; Marko 12:28-34.

Ilimaanisha nini kumtia mtu mafuta?

Katika nyakati za Biblia huko Mashariki ya Kati, kumpaka mtu mafuta kichwani ilikuwa ishara ya kumheshimu mtu huyo au tendo la ukarimu kuelekea mgeni. Kwa ujumla, mafuta yaliyotumiwa yalikuwa ya zeituni yaliyoongezwa manukato. Pia, Waebrania walimmiminia mtu mafuta kichwani, au kumtia mafuta, alipowekwa rasmi katika cheo cha pekee cha mamlaka. Kwa mfano, Haruni alitiwa mafuta alipowekwa rasmi kutumikia akiwa kuhani mkuu. (Mambo ya Walawi 8:12) Katika kisa cha Mfalme Daudi, ‘Samweli alichukua ile pembe ya mafuta, akamtia mafuta na roho ya Yehova ikaanza kutenda kazi juu ya Daudi kuanzia siku hiyo na kuendelea.’—1 Samweli 16:13.

Katika lugha ya Kiebrania, neno linalotumiwa kuhusu kutia mafuta ni ma·shachʹ, ambalo linatokeza neno ma·shiʹach, au Masihi. Neno la Kigiriki linalofanana na hilo ni khriʹo, ambalo linatokeza neno khri·stosʹ, au Kristo. Hivyo, Haruni na Daudi wanaweza wote wawili kuitwa masihi, au watiwa-mafuta. Musa pia anaitwa kristo, au mtiwa-mafuta, katika maana ya kwamba Mungu alimweka rasmi ili atumikie akiwa mwakilishi Wake. —Waebrania 11:24-26.

Yesu wa Nazareti aliwekwa rasmi na Mungu mwenyewe kwenye cheo kikubwa cha mamlaka. Badala ya kutiwa mafuta halisi, Yesu alitiwa mafuta kwa roho takatifu ya Mungu. (Mathayo 3:16) Akiwa Mtiwa-Mafuta aliyechaguliwa na Yehova, Yesu anaitwa kwa kufaa Masihi, au Kristo.—Luka 4:18.