Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uzima wa Milele Duniani—Tumaini Ambalo Tumepewa na Mungu

Uzima wa Milele Duniani—Tumaini Ambalo Tumepewa na Mungu

Uzima wa Milele Duniani—Tumaini Ambalo Tumepewa na Mungu

“Uumbaji ulitiishwa chini ya ubatili . . . juu ya msingi wa tumaini.”—ROM. 8:20.

1, 2. (a) Kwa nini tumaini la uzima wa milele duniani ni la maana sana kwetu? (b) Kwa nini watu wengi wana shaka kuhusu uzima wa milele duniani?

LABDA unakumbuka shangwe ambayo ulihisi ulipojifunza kwa mara ya kwanza kwamba hivi karibuni watu hawatazeeka na kufa tena, bali wataishi milele duniani. (Yoh. 17:3; Ufu. 21:3, 4) Huenda umefurahia kuwaambia wengine kuhusu tumaini hilo linalotegemea Maandiko. Kwa kweli, tumaini la uzima wa milele ni sehemu ya maana sana ya habari njema tunayohubiri. Tumaini hilo linatusaidia kuwa na mtazamo unaofaa maishani.

2 Kwa kiwango kikubwa, dini zinazodai kuwa za Kikristo zimepuuza tumaini la kuishi milele duniani. Ingawa Biblia inafundisha kwamba nafsi inakufa, makanisa mengi yanafundisha fundisho lisilopatana na Maandiko la kwamba mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa ambayo inaendelea kuishi katika makao ya roho baada ya mtu kufa. (Eze. 18:20) Hivyo, watu wengi wana shaka kuhusu uzima wa milele duniani. Basi, tunaweza kujiuliza hivi: Je, kweli Biblia inaunga mkono tumaini hilo? Ikiwa ndivyo, Mungu aliwafunulia wanadamu tumaini hilo kwa mara ya kwanza wakati gani?

“Ulitiishwa Chini ya Ubatili . . . Juu ya Msingi wa Tumaini”

3. Tangu mwanzoni mwa historia ya wanadamu, kusudi la Mungu kwa ajili ya wanadamu lilionyeshwa wazi jinsi gani?

3 Kusudi la Yehova kwa ajili ya wanadamu lilionyeshwa wazi tangu mwanzoni mwa historia ya wanadamu. Mungu alionyesha wazi kwamba Adamu angeishi milele ikiwa angetii. (Mwa. 2:9, 17; 3:22) Bila shaka, wazao wa mapema wa Adamu walijua jinsi wanadamu walivyopoteza ukamilifu, na waliona wazi matokeo ya kutokamilika. Njia ya kuingia kwenye bustani ya Edeni ilifungwa, na watu wakaanza kuzeeka na kufa. (Mwa. 3:23, 24) Kadiri muda ulivyopita, ndivyo urefu wa maisha ya wanadamu ulivyopungua. Adamu aliishi miaka 930. Shemu aliyeokoka Gharika aliishi miaka 600 tu na mwana wake Arpakshadi aliishi miaka 438. Tera, baba ya Abrahamu, aliishi miaka 205. Abrahamu aliishi miaka 175, mwana wake Isaka aliishi miaka 180, naye Yakobo aliishi miaka 147. (Mwa. 5:5; 11:10-13, 32; 25:7; 35:28; 47:28) Inaonekana watu wengi walitambua kwamba kupungua kwa miaka ya maisha ya wanadamu kulimaanisha kuwa tumaini la uzima wa milele lilipotea! Je, walikuwa na sababu ya kutumaini kwamba uzima wa milele ungerudishwa tena?

4. Wanaume waaminifu wa zamani walikuwa na msingi gani wa kuamini kwamba Mungu angerudisha baraka ambazo Adamu alipoteza?

4 Neno la Mungu linasema: “Uumbaji [wanadamu] ulitiishwa chini ya ubatili . . . juu ya msingi wa tumaini.” (Rom. 8:20) Tumaini gani? Unabii wa kwanza kabisa wa Biblia ulizungumza kuhusu “uzao” ambao ‘ungemponda nyoka kichwa.’ (Soma Mwanzo 3:1-5, 15.) Ahadi ya Uzao huo iliwapa wanadamu waaminifu msingi wa kutumaini kwamba Mungu hangetupilia mbali kusudi lake kwa ajili ya wanadamu. Ahadi hiyo iliwapa wanaume kama vile Abeli na Noa sababu ya kuamini kwamba Mungu angerudisha baraka ambazo Adamu alipoteza. Huenda wanaume hao walitambua kwamba damu ingemwagika wakati ambapo ‘uzao huo ungetiwa jeraha kwenye kisigino.’—Mwa. 4:4; 8:20; Ebr. 11:4.

5. Ni nini kinachoonyesha kwamba Abrahamu aliamini ufufuo?

5 Mfikirie Abrahamu. Abrahamu alipokuwa akijaribiwa, “ni kana kwamba alimtoa Isaka, . . . mwana wake mzaliwa-pekee.” (Ebr. 11:17) Kwa nini alikuwa tayari kufanya hivyo? (Soma Waebrania 11:19.) Aliamini ufufuo! Abrahamu alikuwa na msingi wa kuamini ufufuo. Yehova alikuwa amemrudishia Abrahamu uwezo wake wa kuzaa na alimwezesha yeye na mke wake, Sara, kuzaa mwana wakiwa wamezeeka. (Mwa. 18:10-14; 21:1-3; Rom. 4:19-21) Pia, Abrahamu alikuwa na neno la Yehova. Mungu alikuwa amemwambia hivi: “Ule utakaoitwa uzao wako utakuwa kupitia Isaka.” (Mwa. 21:12) Kwa hiyo, Abrahamu alikuwa na sababu nzuri za kutazamia kwamba Mungu angemfufua Isaka.

6, 7. (a) Ni agano gani ambalo Yehova alifanya na Abrahamu? (b) Ahadi ambayo Yehova alimpa Abrahamu iliwaletea wanadamu tumaini jinsi gani?

6 Kwa sababu ya imani yenye nguvu sana ya Abrahamu, Yehova alifanya agano pamoja naye kuhusu mzao au “uzao” wake. (Soma Mwanzo 22:18.) Yesu Kristo alithibitika kuwa sehemu ya msingi ya “uzao” huo. (Gal. 3:16) Yehova alikuwa amemwambia Abrahamu kwamba “uzao” wake ungeongezeka na kuwa “kama nyota za mbinguni na kama chembe za mchanga zilizo kando ya bahari”—idadi ambayo Abrahamu hakujua. (Mwa. 22:17) Hata hivyo, baadaye idadi hiyo ilifunuliwa. Yesu Kristo na wale 144,000, ambao watatawala pamoja naye katika Ufalme wake, wanafanyiza “uzao” huo. (Gal. 3:29; Ufu. 7:4; 14:1) Kupitia kwa Ufalme wa Kimasihi “mataifa yote ya dunia . . . yatajibariki.”

7 Inawezekana kwamba Abrahamu hakuelewa kikamili umuhimu wa agano ambalo Yehova alifanya pamoja naye. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba “alikuwa akingojea jiji lililo na misingi ya kweli.” (Ebr. 11:10) Jiji hilo ni Ufalme wa Mungu. Ni lazima Abrahamu awe hai tena ili apokee baraka chini ya Ufalme huo. Abrahamu ataweza kuishi milele duniani kupitia ufufuo. Na wale watakaookoka Har–Magedoni au wale watakaofufuliwa wataishi milele.—Ufu. 7:9, 14; 20:12-14.

“Roho Imeleta Mkazo Juu Yangu”

8, 9. Kwa nini kitabu cha Ayubu si simulizi tu la majaribu ya mwanamume mmoja?

8 Ayubu aliishi baada ya Yosefu, mwana wa mjukuu wa Abrahamu na kabla ya nabii Musa. Kitabu cha Biblia cha Ayubu, ambacho inaelekea kiliandikwa na Musa, kinaeleza kwa nini Yehova aliruhusu Ayubu ateseke na mafanikio aliyopata baadaye. Hata hivyo, kitabu cha Ayubu hakisimulii tu majaribu ya mwanamume mmoja; kinakazia masuala ya maana sana yanayohusu ulimwengu wote. Kitabu hicho kinatusaidia kuelewa kwa undani jinsi Yehova anavyotawala kwa uadilifu, na kinafunua kwamba utimilifu na matarajio ya kupata uzima ya watumishi wote wa Mungu duniani yanahusiana na suala lililotokezwa katika Edeni. Ingawa Ayubu hakuelewa suala hilo, hakuwaruhusu marafiki wake watatu wamfanye afikiri kwamba hakuwa mtimilifu. (Ayu. 27:5) Hilo linapaswa kuitia nguvu imani yetu na kutusaidia kutambua kwamba tunaweza kudumisha utimilifu wetu na kuunga mkono enzi kuu ya Yehova.

9 Baada ya wafariji watatu wa uwongo wa Ayubu kumaliza kuzungumza, “Elihu mwana wa Barakeli, Mbuzi, akajibu.” Ni nini kilichomchochea kuzungumza? Alisema hivi: “Nimejaa maneno. Roho imeleta mkazo juu yangu ndani ya tumbo langu.” (Ayu. 32:5, 6, 18) Ingawa mambo ambayo Elihu alisema chini ya mwongozo wa roho ya Mungu yalitimia wakati majaribu ya Ayubu yalipokoma, bado maneno yake yana maana kwa wengine pia. Yanawapa tumaini wote wanaodumisha utimilifu.

10. Ni nini kinachoonyesha kwamba nyakati nyingine Yehova alimpa mtu mmoja ujumbe ambao unawahusu wanadamu wote?

10 Nyakati nyingine, Yehova alimpa mtu mmoja ujumbe ambao unawahusu wanadamu wote. Hilo linathibitishwa na unabii wa Danieli kuhusu ndoto ya Mfalme Nebukadneza wa Babiloni iliyohusu mti mkubwa uliokatwa. (Dan. 4:10-27) Ingawa ndoto hiyo ilitimia kuhusiana na Nebukadneza, ilionyesha jambo fulani ambalo ni kubwa zaidi. Ilionyesha kwamba utawala wa Mungu juu ya dunia ambao uliwakilishwa na ufalme wa ukoo wa Mfalme Daudi ungerudishwa baada ya kipindi cha miaka 2,520, kuanzia mwaka wa 607 K.W.K. * Utawala wa Mungu juu ya dunia yetu ulianza upya wakati Yesu Kristo alipowekwa rasmi kuwa Mfalme wa kimbingu katika mwaka wa 1914. Hebu wazia jinsi utawala wa Ufalme utakavyotimiza matumaini ya wanadamu watiifu hivi karibuni!

“Mwachilie Ili Asishuke Chini Kuingia Shimoni!”

11. Maneno ya Elihu yalionyesha nini kumhusu Mungu?

11 Anapomjibu Ayubu, Elihu anasema kuhusu “mjumbe, . . . msemaji, mmoja kati ya elfu, ili kumwambia mwanadamu unyoofu wake.” Namna gani ikiwa mjumbe huyo ‘anamsihi Mungu ili amfurahie’? Elihu anasema: “Ndipo [Mungu] anapompa kibali na kusema, ‘Mwachilie ili asishuke chini kuingia shimoni! Nimepata fidia! Nyama yake na iwe laini kuliko wakati wa ujana; na arudi kwenye siku za nguvu za ujana wake.’” (Ayu. 33:23-26) Maneno hayo yalionyesha kwamba Mungu alikuwa tayari kukubali “fidia,” au “kifuniko,” kwa faida ya wanadamu wenye kutubu.—Ayu. 33:24.

12. Maneno ya Elihu yanawapa wanadamu kwa ujumla tumaini gani?

12 Huenda Elihu hakuelewa kikamili maana ya fidia au dhabihu ya ukombozi, kama vile tu manabii hawakuelewa kikamili kila jambo ambalo waliandika. (Dan. 12:8; 1 Pet. 1:10-12) Hata hivyo, maneno ya Elihu yanaonyesha tumaini la kwamba siku moja Mungu angekubali fidia na hivyo kuwaweka wanadamu huru kutokana na kifo na pia kutokana na matokeo mabaya ya kuzeeka. Maneno ya Elihu yalitoa tumaini zuri ajabu la uzima wa milele. Kitabu cha Ayubu kinaonyesha pia kwamba kutakuwa na ufufuo.—Ayu. 14:14, 15.

13. Maneno ya Elihu yanamaanisha nini kwa Wakristo?

13 Leo, maneno ya Elihu yanaendelea kuwa na maana kwa mamilioni ya Wakristo ambao wanatumaini kuokoka uharibifu wa mfumo huu wa mambo. Waliozeeka kati ya waokokaji hao watarudishiwa tena nguvu zao za ujana. (Ufu. 7:9, 10, 14-17) Tumaini la kuwaona wale watakaofufuliwa wakirudishiwa tena nguvu zao za ujana linaendelea kuwafurahisha watu waaminifu. Bila shaka, ili Wakristo watiwa-mafuta wapate uhai usioweza kufa mbinguni, na “kondoo wengine” wa Yesu wapate uzima wa milele duniani, ni lazima wawe na imani katika dhabihu ya ukombozi ya Kristo.—Yoh. 10:16; Rom. 6:23.

Kifo Kitamezwa Kutoka Duniani

14. Ni nini kinachoonyesha kwamba Waisraeli walihitaji kitu kingine zaidi ya Sheria ya Musa ili wawe na tumaini la kuishi milele?

14 Wazao wa Abrahamu walikuja kuwa taifa huru walipofanya agano pamoja na Mungu. Yehova aliwaambia hivi alipokuwa akiwapa Sheria hiyo: “Mtazishika sheria zangu na maamuzi yangu ya hukumu, ambazo ikiwa mtu atazifanya, yeye pia ataishi kwa hizo.” (Law. 18:5) Hata hivyo, kwa kuwa hawangeweza kuishi kulingana na viwango vikamilifu vya Sheria, Waisraeli walihukumiwa na Sheria na walihitaji kuwekwa huru kutokana na hukumu hiyo.—Gal. 3:13.

15. Daudi aliongozwa na roho ya Mungu kuandika kuhusu baraka gani za wakati ujao?

15 Baada ya Musa, Yehova aliwaongoza kwa roho yake waandikaji wengine wa Biblia ili waandike kuhusu tumaini la uzima wa milele. (Zab. 21:4; 37:29) Kwa mfano, mtunga-zaburi Daudi alimalizia hivi zaburi moja iliyohusu umoja wa waabudu wa kweli huko Sayuni: “Huko Yehova aliamuru baraka iwepo, naam, uzima mpaka wakati usio na kipimo.”—Zab. 133:3.

16. Kupitia Isaya, Yehova aliahidi nini kuhusu wakati ujao wa “dunia yote”?

16 Yehova alimwongoza Isaya atabiri kuhusu uzima wa milele duniani. (Soma Isaya 25:7, 8.) Kama vile “kifuniko” au blanketi inavyomfunika mtu, dhambi na kifo vimewafunika na kuwalemea kabisa wanadamu. Yehova anawahakikishia watu wake kwamba dhambi na kifo vitamezwa, au vitaondolewa “katika dunia yote.”

17. Masihi anatimiza daraka gani la kinabii ambalo linawapa watu nafasi ya kupata uzima wa milele?

17 Fikiria pia utaratibu ulioonyeshwa katika Sheria ya Musa kuhusu mbuzi wa Azazeli. Mara moja kwa mwaka, katika Siku ya Upatanisho, kuhani mkuu ‘aliweka mikono yake miwili juu ya kichwa cha mbuzi aliye hai na aliungama juu yake makosa yote ya wana wa Israeli, na aliyaweka juu ya kichwa cha yule mbuzi na mbuzi huyo alichukua juu yake mwenyewe makosa yao yote mpaka katika nchi ya jangwa.’ (Law. 16:7-10, 21, 22) Isaya alitabiri kuja kwa Masihi, ambaye angetimiza daraka kama hilo na kubeba “magonjwa,” “maumivu,” na “dhambi ya watu wengi,” na hivyo kuwapa nafasi ya kupata uzima wa milele.—Soma Isaya 53:4-6, 12.

18, 19. Ni tumaini gani linalokaziwa kwenye Isaya 26:19 na Danieli 12:13?

18 Kupitia Isaya, Yehova aliwaambia watu wake Waisraeli hivi: “Wafu wako wataishi. Maiti wangu—wataamka. Amkeni, pigeni vigelegele kwa shangwe, enyi mnaokaa mavumbini! Kwa maana umande wako ni kama umande wa miholi, na dunia itawaacha hata wale wasiojiweza katika kifo waanguke katika kuzaliwa.” (Isa. 26:19) Maandiko ya Kiebrania yanaonyesha waziwazi kwamba kuna tumaini la watu kufufuliwa na kuishi duniani. Kwa mfano, Danieli alipokuwa na umri wa karibu miaka 100, Yehova alimhakikishia hivi: “Utapumzika, lakini utasimama kwa ajili ya fungu lako mwishoni mwa zile siku.”—Dan. 12:13.

19 Kwa sababu ya tumaini la ufufuo, Martha alimwambia Yesu hivi kuhusu ndugu yake aliyekufa: “Ninajua atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.” (Yoh. 11:24) Je, mafundisho ya Yesu na maandishi ya wanafunzi wake yaliyoongozwa na roho ya Mungu yalibadili tumaini hilo? Je, bado uzima wa milele duniani ni tumaini ambalo Yehova amewaahidi wanadamu? Tutazungumzia majibu ya maswali hayo katika habari inayofuata.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 10 Ona sura ya 6 ya kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli!

Je, Unaweza Kueleza?

• Wanadamu ‘walitiishwa chini ya ubatili’ juu ya msingi wa tumaini gani?

• Ni nini kinachoonyesha kwamba Abrahamu aliamini ufufuo?

• Maneno ambayo Elihu alimwambia Ayubu yanawapa wanadamu tumaini gani?

• Maandiko ya Kiebrania yanakazia jinsi gani tumaini la ufufuo na uzima wa milele duniani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 5]

Maneno ambayo Elihu alimwambia Ayubu yanaonyesha tumaini la kwamba wanadamu watawekwa huru ili wasizeeke na kufa

[Picha katika ukurasa wa 6]

Danieli alihakikishiwa kwamba ‘angesimama kwa ajili ya fungu lake mwishoni mwa zile siku’