Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”

“Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”

“Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”

“Jitunzeni katika upendo wa Mungu, huku mkiingojea rehema ya Bwana wetu Yesu Kristo kwa kutazamia uzima wa milele.”—YUDA 21.

YEHOVA MUNGU ametuonyesha upendo wake katika njia nyingi sana. Hata hivyo, bila shaka mpango wa dhabihu ya fidia au ukombozi unathibitisha kwa njia kubwa zaidi kwamba Yehova anatupenda. Upendo wake kwa wanadamu ni mwingi sana hivi kwamba alimtuma Mwana wake mpendwa hapa duniani ili afe kwa ajili yetu. (Yoh. 3:16) Yehova alifanya hivyo kwa sababu anataka tuishi milele, na pia anataka upendo wake utunufaishe milele!

2 Hata hivyo, je, tunapaswa kufikiri kwamba Yehova atatutunza tu katika upendo wake bila kujali tunachagua kufanya nini? Hapana. Kwa kuwa katika andiko la Yuda mstari wa 21, tunasoma himizo hili: “Jitunzeni katika upendo wa Mungu, huku mkiingojea rehema ya Bwana wetu Yesu Kristo kwa kutazamia uzima wa milele.” Maneno “jitunzeni katika upendo wa Mungu” yanamaanisha kwamba tunapaswa kuchukua hatua fulani. Basi, tunahitaji kufanya nini ili tukae katika upendo wa Mungu?

Tunaweza Kufanya Nini Ili Tukae Katika Upendo wa Mungu?

3 Tunapata jibu la swali hilo katika maneno ambayo Yesu mwenyewe alisema usiku wa mwisho wa maisha yake duniani. Alisema hivi: “Mkishika amri zangu, mtakaa katika upendo wangu, kama vile mimi nilivyoshika amri za Baba na kukaa katika upendo wake.” (Yoh. 15:10) Kwa wazi, Yesu aliona kwamba ili awe na msimamo mzuri mbele za Baba yake alipaswa kushika amri za Yehova. Sasa, ikiwa Mwana mkamilifu wa Mungu alipaswa kufanya hivyo, je, sisi pia hatupaswi kufanya hivyo?

4 Njia kuu ya kuonyesha kwamba tunampenda Yehova ni kumtii. Mtume Yohana alisema hivi kuhusu jambo hilo: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” (1 Yoh. 5:3) Ukweli ni kwamba watu wengi leo hawapendi kumtii yeyote. Hata hivyo, angalia maneno haya: “Bado amri zake si mzigo mzito.” Yehova hatuombi tufanye jambo ambalo hatuwezi kufanya.

5 Kwa mfano: Je, unaweza kumuomba rafiki yako mpendwa abebe mzigo fulani ambao unajua hawezi kuuinua kwa kuwa ni mzito sana? Bila shaka huwezi! Yehova ni mwenye fadhili zaidi kuliko sisi naye anaelewa vizuri zaidi uwezo wetu. Biblia inatuhakikishia kwamba Yehova ‘anakumbuka kwamba sisi ni mavumbi.’ (Zab. 103:14) Hawezi kamwe kutuomba tufanye mambo ambayo hatuwezi. Kwa hiyo, hatuna sababu yoyote ya kuogopa kutii amri za Yehova. Badala yake, tunatambua kwamba kutii ni njia ya pekee sana ya kumwonyesha Baba yetu wa mbinguni kuwa tunampenda kikweli na tunataka kukaa katika upendo wake.

Zawadi ya Pekee Kutoka kwa Yehova

6 Katika ulimwengu huu wenye matatizo mengi, tunahitaji kufanya maamuzi mengi yanayohusu utii wetu kwa Mungu. Tunaweza kufanya nini ili tuwe na hakika kwamba maamuzi hayo yanapatana na mapenzi ya Mungu? Yehova ametupa zawadi inayoweza kutusaidia sana kuwa watiifu. Zawadi hiyo ni dhamiri. Dhamiri ni nini? Ni uwezo wa pekee unaotusaidia kujichunguza. Dhamiri ni kama hakimu aliye ndani yetu, inatuwezesha kuchunguza maamuzi tunayokabili maishani au kufikiria hatua ambazo tayari tumechukua na kuona kama ni nzuri au mbaya, zinafaa au hazifai.—Soma Waroma 2:14, 15.

7 Dhamiri yetu inaweza kutusaidia jinsi gani? Fikiria mfano huu. Msafiri anatembea katika nyika kubwa. Hakuna njia, barabara, wala ishara yoyote. Hata hivyo, anasafiri taratibu mpaka mahali anapokusudia kufika. Anatumia nini? Anatumia dira. Dira ni kifaa chenye uso kama saa ambao unaonyesha zile pande nne za msingi na kina mshale wa sumaku unaoonyesha kwa usahihi upande wa kaskazini. Bila dira, msafiri huyo atapotea njia kabisa. Vivyo hivyo, mwanadamu asiye na dhamiri atapotea njia kila mara anapojaribu kufanya maamuzi ya maisha yanayohusu maadili na uadilifu.

8 Hata hivyo, kama dira, dhamiri pia ina mipaka. Ikiwa msafiri huyo ataweka sumaku karibu na dira anayotumia, mshale hautaonyesha upande wa kaskazini. Vivyo hivyo, tukiruhusu tamaa za moyo wetu zituongoze tunapofanya maamuzi, matokeo yatakuwa nini? Mielekeo yetu yenye ubinafsi inaweza kupotosha dhamiri yetu. Biblia inatuonya kwamba “moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” (Yer. 17:9; Met. 4:23) Kwa kuongezea, ikiwa msafiri huyo hangekuwa na ramani sahihi yenye kutegemeka, dira haingemsaidia hata kidogo. Vivyo hivyo, tusipotegemea mwongozo wa Neno la Mungu, Biblia, ulio hakika na usiobadilika, huenda dhamiri yetu haitatusaidia hata kidogo. (Zab. 119:105) Inahuzunisha kwamba watu wengi ulimwenguni wanategemea sana tamaa za moyo wao na kupuuza viwango vilivyo katika Neno la Mungu. (Soma Waefeso 4:17-19.) Ndiyo sababu watu wengi sana wanafanya mambo maovu hata ingawa wamepewa zawadi ya dhamiri.—1 Tim. 4:2.

9 Tunapaswa kuazimia kutokuwa kama watu hao! Badala yake, acheni tuendelee kuliruhusu Neno la Mungu lituelimishe na kuizoeza dhamiri yetu ili itusaidie kikweli. Tunahitaji kuisikiliza dhamiri yetu iliyozoezwa na Biblia badala ya kuruhusu mielekeo ya kichoyo ituongoze. Wakati huohuo, tunapaswa kujitahidi kuheshimu dhamiri za ndugu na dada zetu wapendwa wa kiroho. Tunajitahidi sana kuepuka kuwakwaza, huku tukikumbuka kwamba tofauti na dhamiri yetu, huenda dhamiri za ndugu zetu zikawaruhusu au kuwazuia wasifanye mambo fulani.—1 Kor. 8:12; 2 Kor. 4:2; 1 Pet. 3:16.

10 Acheni sasa tuzungumzie sehemu tatu za maisha ambazo tunaweza kuonyesha kwamba tunampenda Yehova kwa kumtii. Bila shaka, dhamiri inahusika katika kila moja ya sehemu hizo, lakini kwanza kabisa, inahitaji kuongozwa na viwango vya Biblia kuhusu mwenendo ambavyo vimeandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu. Tunaweza kumtii Yehova kwa upendo katika njia tatu zifuatazo: (1) Kuwapenda wale ambao Yehova anawapenda, (2) kuheshimu mamlaka, na (3) kujitahidi kuendelea kuwa safi machoni pa Mungu.

Wapende Wale Ambao Yehova Anawapenda

11 Kwanza, ni lazima tuwapende wale ambao Yehova anawapenda. Inapohusu marafiki, watu ni kama sifongo. Tuna mwelekeo wa kufyonza kitu chochote kilicho karibu nasi. Muumba wetu anajua vizuri sana jinsi ambavyo marafiki wanaweza kuwa hatari au wenye faida kwa wanadamu wasio wakamilifu. Kwa hiyo, anatupa shauri hili lenye hekima: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” (Met. 13:20; 1 Kor. 15:33) Hakuna yeyote kati yetu anayetaka ‘kupatwa na mabaya.’ Kila mmoja wetu anataka ‘kuwa na hekima.’ Yehova hahitaji kuongezewa hekima kwa njia yoyote ile, wala hawezi kamwe kupotoshwa na yeyote. Hata hivyo, anatuwekea mfano bora kabisa kuhusiana na kuchagua marafiki. Hebu fikiria hili—kati ya wanadamu wasio wakamilifu, Yehova anachagua marafiki wa aina gani?

12 Yehova alimwita mzee wa ukoo Abrahamu, “rafiki yangu.” (Isa. 41:8) Mwanamume huyo aliweka mfano bora katika kuwa mwaminifu, mwadilifu, na mtiifu—mtu mwenye imani. (Yak. 2:21-23) Yehova anachagua marafiki wa aina hiyo. Leo, anafanya urafiki na watu wa aina hiyo. Ikiwa Yehova anachagua marafiki wa aina hiyo, je, si jambo la maana kwetu kuchagua marafiki kwa uangalifu, ili tutembee na watu wenye hekima na kuwa na hekima?

13 Ni nini kinachoweza kukusaidia kuchagua marafiki wanaofaa? Kujifunza mifano ya watu wanaotajwa katika Biblia kunaweza kukusaidia. Fikiria urafiki kati ya Ruthu na mama-mkwe wake Naomi, urafiki kati ya Daudi na Yonathani, au urafiki kati ya Timotheo na Paulo. (Rut. 1:16, 17; 1 Sam. 23:16-18; Flp. 2:19-22) Watu hao walidumisha urafiki wao kwa sababu moja ya maana sana: Urafiki wao ulitegemea kumpenda Yehova kikweli. Je, unaweza kupata marafiki ambao wanampenda Yehova sana kama vile unavyompenda? Uwe na hakika kwamba unaweza kupata marafiki wengi wa aina hiyo katika kutaniko la Kikristo. Marafiki wa aina hiyo hawatakuletea madhara ya kiroho. Badala yake, watakusaidia kumtii Yehova, kukua kiroho, na kupanda kwa roho. (Soma Wagalatia 6:7, 8.) Watakusaidia ukae katika upendo wa Mungu.

Heshimu Mamlaka

14 Njia ya pili ya kuonyesha kwamba tunampenda Yehova inahusiana na mamlaka. Ni lazima tuheshimu mamlaka. Kwa nini nyakati nyingine ni vigumu sana kwetu kufanya hivyo? Kwanza, wanadamu wenye mamlaka si wakamilifu. Kwa kuongezea, sisi wenyewe si wakamilifu. Tunapambana na mwelekeo wa kuasi tuliozaliwa nao.

15 Basi huenda ukajiuliza, ‘Ikiwa ni vigumu kwetu kuheshimu mamlaka, kwa nini tunahitaji kufanya hivyo?’ Jibu linahusiana hasa na suala la enzi kuu. Utamchagua nani awe mwenye enzi kuu wako, au mtawala wako? Ikiwa tunamchagua Yehova kuwa Mwenye Enzi Kuu wetu, basi tunahitaji kuheshimu mamlaka yake. Ikiwa hatufanyi hivyo, je, tunaweza kwa kweli kusema kwamba yeye ni Mtawala wetu? Zaidi ya hayo, kwa kawaida Yehova anaonyesha mamlaka yake kupitia wanadamu wasio wakamilifu ambao anawakabidhi daraka la kuwatunza watu wake. Tukiwaasi wanadamu hao, Yehova atakuwa na maoni gani kuhusu jambo hilo?—Soma 1 Wathesalonike 5:12, 13.

16 Kwa mfano, Waisraeli waliponung’unika na kumwasi Musa, Yehova aliona kwamba walikuwa wakimwasi yeye binafsi. (Hes. 14:26, 27) Mungu hajabadilika. Tukiwaasi kwa njia yoyote wale ambao amewapa mamlaka, tutakuwa tukimwasi yeye!

17 Mtume Paulo anafunua mtazamo unaofaa ambao tunapaswa kusitawisha kuelekea wale walio na madaraka katika kutaniko la Kikristo. Aliandika hivi: “Watiini wale wanaoongoza katikati yenu na mnyenyekee, kwa maana wanaendelea kuzilinda nafsi zenu kama wale watakaotoa hesabu; ili wafanye hivyo kwa shangwe na si kwa kuugua, kwa maana kufanya hivyo kungewadhuru ninyi.” (Ebr. 13:17) Ni kweli kwamba ni lazima tujitahidi kabisa kusitawisha roho hiyo ya kutii na kunyenyekea. Hata hivyo, kumbuka kwamba tunajitahidi ili tukae katika upendo wa Mungu. Je, huo si mradi unaostahili jitihada zetu zote?

Endelea Kuwa Safi Machoni pa Yehova

18 Njia ya tatu ya kuonyesha kwamba tunampenda Yehova ni kujitahidi kuendelea kuwa safi machoni pake. Kwa kawaida, wazazi wanajitahidi sana kuhakikisha kwamba watoto wao wako safi. Kwa nini? Kwanza, usafi ni wa maana kwa afya na hali njema ya mtoto. Zaidi ya hayo, mtoto aliye safi anailetea sifa familia, na anaonyesha kwamba wazazi wake wanampenda na wanamtunza. Kwa sababu kama hizo, Yehova anataka tuwe safi. Anajua kwamba usafi ni wa maana kwa hali yetu njema. Pia, anajua kwamba tunapokuwa safi tunamletea sifa, akiwa Baba yetu wa mbinguni. Hilo ni jambo la maana sana, kwa sababu watu wanaweza kuvutwa kwa Mungu tunayemtumikia kwa sababu wanaona kwamba tuko tofauti na watu wengine katika ulimwengu huu uliopotoka.

19 Tunapaswa kuendelea kuwa safi katika njia gani? Kwa kweli, tunapaswa kuwa safi katika mambo yote. Katika Israeli la kale, Yehova aliwaambia watu wake waziwazi kwamba usafi wa kimwili ulikuwa wa maana sana. (Law. 15:31) Sheria ya Musa ilikuwa na maagizo kuhusu mambo kama vile kuondoa takataka, kusafisha vyombo, kunawa mikono, miguu, na kufua mavazi. (Kut. 30:17-21; Law. 11:32; Hes. 19:17-20; Kum. 23:13, 14) Waisraeli walikumbushwa kwamba Mungu wao, Yehova, ni mtakatifu, yaani, yuko “safi,” na “ametakata.” Watumishi wa Mungu aliye mtakatifu wanapaswa kuwa watakatifu pia.—Soma Mambo ya Walawi 11:44, 45.

20 Kwa hiyo, tunahitaji kuwa safi ndani na nje pia. Tunajitahidi kudumisha mawazo safi. Tunashikamana kwa uaminifu na viwango vya Yehova vya usafi wa kimaadili, hata ingawa upotovu wa kingono umeenea ulimwenguni. Jambo la maana zaidi ni kwamba tunajitahidi kabisa kudumisha ibada yetu ikiwa safi, na kuepuka uchafu wowote kutoka katika dini ya uwongo. Sikuzote tunakumbuka onyo hili lililoongozwa na roho ya Mungu kwenye Isaya 52:11: “Geukeni, geukeni, tokeni humo, msiguse kitu chochote kilicho najisi; tokeni katikati yake, jiwekeni safi.” Leo, tunaendelea kuwa safi kiroho kwa kuepuka hata kugusa kitu chochote ambacho Baba yetu wa mbinguni anakiona kuwa kichafu kiroho. Kwa mfano, ndiyo sababu tunaepuka kabisa kushiriki katika sherehe na sikukuu za dini ya uwongo ambazo zinapendwa sana ulimwenguni leo. Kwa kweli, si rahisi kuendelea kuwa safi. Lakini watu wa Yehova wanajitahidi kufanya hivyo kwa sababu hilo linawasaidia kuendelea kukaa katika upendo wa Mungu.

21 Yehova anataka tuendelee kukaa katika upendo wake milele. Lakini kila mmoja wetu anahitaji kuhakikisha kwamba anafanya yote anayoweza ili kukaa katika upendo wa Mungu. Tunaweza kufanya hivyo kwa kufuata mfano wa Yesu na kuthibitisha kwamba tunampenda Yehova kwa kutii amri Zake. Tukifanya hivyo, tutakuwa na hakika kwamba hakuna kitu chochote ‘kitakachoweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.’—Rom. 8:38, 39.

Je, Unakumbuka?

• Dhamiri yetu inaweza kutusaidia jinsi gani kukaa katika upendo wa Mungu?

• Kwa nini tunapaswa kuwapenda wale ambao Yehova anawapenda?

• Kwa nini ni jambo la maana kuheshimu mamlaka?

• Kwa nini usafi ni wa maana sana kwa watu wa Mungu?

[Maswali ya Funzo]

1, 2. Yehova ametuonyesha upendo wake jinsi gani, na tunajua namna gani kwamba tunahitaji kuchukua hatua fulani ili atutunze katika upendo wake?

3. Yesu alisema kwamba alipaswa kufanya jambo gani la maana ili akae katika upendo wa Baba yake?

4, 5. (a) Ni njia gani kuu ya kuonyesha kwamba tunampenda Yehova? (b) Kwa nini hatuna sababu yoyote ya kuogopa kutii amri za Yehova?

6, 7. (a) Dhamiri ni nini? (b) Toa mfano ambao unaonyesha jinsi dhamiri inavyoweza kutusaidia kukaa katika upendo wa Mungu.

8, 9. (a) Tunahitaji kukumbuka dhamiri yetu ina mipaka gani? (b) Tunaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba dhamiri yetu inatusaidia kikweli?

10. Sasa tutazungumzia sehemu gani tatu za maisha?

11. Kwa nini tunapaswa kuwapenda wale ambao Yehova anawapenda?

12. Yehova anachagua marafiki wa aina gani?

13. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuchagua marafiki wazuri?

14. Mara nyingi ni mambo gani yanayofanya iwe vigumu kwetu kuheshimu mamlaka?

15, 16. (a) Kwa nini ni jambo la maana kwetu kuwaheshimu wale ambao Yehova amewakabidhi daraka la kuwatunza watu wake? (b) Ni somo gani la maana ambalo tunajifunza kutokana na maoni ya Yehova kuhusu uasi wa Waisraeli kumwelekea Musa?

17. Tunapaswa kujitahidi kusitawisha mtazamo gani unaofaa kuelekea wale walio na madaraka katika kutaniko?

18. Kwa nini Yehova anataka tuendelee kuwa safi?

19. Tunajua jinsi gani kwamba usafi wa kimwili ni wa maana?

20. Tunahitaji kuendelea kuwa safi katika njia gani mbalimbali?

21. Tunaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba tunakaa katika upendo wa Mungu?

[Picha/Sanduku katika ukurasa wa 20]

KITABU KINACHOWASAIDIA WATU KUWA NA MWENENDO MZURI

Wakati wa kusanyiko la wilaya la 2008/2009, kitabu chenye kurasa 224 chenye kichwa “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu” kilitolewa. Kitabu hicho kipya kimechapishwa kwa kusudi gani? Kimekusudiwa kuwasaidia Wakristo kujua na kuvipenda viwango vya Yehova, na hasa kinakazia mwenendo wa Kikristo. Kujifunza kwa uangalifu kitabu “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu” kutatia nguvu usadikisho wetu wa kwamba kuishi kupatana na viwango vya Yehova ndiyo njia bora zaidi ya maisha sasa na itaongoza kwenye uzima wa milele wakati ujao.

Zaidi ya hayo, kitabu hicho kinakusudiwa kutusaidia kuona kwamba kumtii Yehova si mzigo. Badala yake, tunapomtii Yehova tunamwonyesha jinsi tunavyompenda sana. Hivyo, kitabu hicho kitatuchochea tujiulize, ‘Kwa nini ninamtii Yehova?’

Wengine wanapofanya kosa linalohuzunisha la kuondoka katika upendo wa Yehova, kwa kawaida tatizo linahusu mwenendo wala si mafundisho. Basi ni jambo la maana kama nini kwamba tutie nguvu upendo na uthamini wetu kwa sheria na kanuni za Yehova ambazo zinatuongoza katika maisha yetu ya kila siku! Tuna hakika kwamba kitabu hicho kipya kitawasaidia kondoo wa Yehova ulimwenguni pote wasimame imara na kufanya yaliyo sawa, kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo, na zaidi ya yote kukaa katika upendo wa Mungu!—Yuda 21.

[Picha katika ukurasa wa 18]

“Mkishika amri zangu, mtakaa katika upendo wangu, kama vile mimi nilivyoshika amri za Baba na kukaa katika upendo wake”