Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Adamu na Hawa Walikuwa Watu Halisi?

Je, Adamu na Hawa Walikuwa Watu Halisi?

Je, Adamu na Hawa Walikuwa Watu Halisi?

WATU wengi husema kwamba simulizi la Mwanzo kuhusu Adamu na Hawa ni hadithi nzuri tu. “Kwa muda mrefu sana watu katika dini kubwa zinazodai kuwa za Kikristo wameamini kwamba hadithi katika kitabu cha Mwanzo kama ile ya Adamu na Hawa si halisi,” inasema barua iliyotumwa kwa mhariri wa gazeti Time. Wasomi wengi wa Kikatoliki, Kiprotestanti, na Kiyahudi wanakubaliana na wazo hilo. Wanasema kwamba masimulizi mengi yanayotajwa katika kitabu cha Mwanzo hayapatani na historia au sayansi.

Unaonaje? Je, unaamini kwamba Adamu na Hawa ni watu halisi? Je, kuna uthibitisho wowote unaoonyesha kwamba kweli waliishi? Kwa upande mwingine, matokeo ya kusema kwamba masimulizi hayo ya Mwanzo si ya kweli ni nini?

Je, Simulizi la Mwanzo Linaweza Kuthibitishwa Kisayansi?

Kwanza, acheni tuchunguze matukio muhimu katika simulizi la uumbaji wa mwanadamu wa kwanza. Biblia inasema hivi kumhusu Adamu: “Yehova Mungu akamfanya mtu kutoka katika mavumbi ya nchi na kupuliza katika mianzi ya pua yake pumzi ya uhai, naye mtu akawa nafsi hai.” (Mwanzo 2:7) Je, maneno hayo yanaweza kuthibitishwa kisayansi?

Kitabu Nanomedicine kinasema kwamba mwili wa mwanadamu umefanyizwa kwa kemikali 41 hivi. Kemikali hizo—kaboni, chuma, oksijeni, na nyingine—zinapatikana katika “mavumbi” ya dunia. Hivyo, kama Mwanzo inavyosema, kwa kweli wanadamu wameumbwa “kutoka katika mavumbi ya nchi.”

Kemikali hizo zisizo na uhai ziliunganaje na kufanyiza mwanadamu aliye hai? Ili kuelewa ugumu wa kufanya hivyo, fikiria chombo cha NASA cha kusafiria angani, mashini tata zaidi ambayo imewahi kubuniwa. Chombo hicho kilichotengenezwa kwa ufundi wa hali ya juu kina sehemu milioni 2.5. Mainjinia walichukua miaka mingi sana kukibuni na kukiunganisha pamoja. Sasa fikiria mwili wa mwanadamu. Umefanyizwa kwa atomu octillion 7 hivi, trilioni 100, viungo vingi sana, na angalau mifumo 9 ya viungo vikubwa. * Mashini hiyo tata sana ya kibiolojia iliyoundwa kwa ustadi ilitokeaje? Je, ilijitokeza yenyewe au ilibuniwa na mbuni stadi?

Ni nini kinachomfanya mwanadamu awe hai? Chanzo cha uhai ni nini? Wanasayansi wanakubali kwamba hawajui. Kwa kweli, hata hawapatani wanapoeleza uhai ni nini. Kwa wale wanaokubali wazo la kwamba kuna Muumba, jibu ni wazi. Bila shaka, Chanzo ni Mungu. *

Vipi kuhusu ufafanuzi wa Mwanzo kwamba Hawa aliumbwa kutokana na ubavu wa Adamu? (Mwanzo 2:21-23) Kabla ya kusema kwamba simulizi hilo ni hadithi tu, fikiria mambo hakika yafuatayo: Mnamo Januari (Mwezi wa 1) 2008, wanasayansi huko California, Marekani, walitokeza kwenye maabara kiini-tete cha kwanza cha mwanadamu kutoka kwa chembe za ngozi za mtu mzima. Kwa kutumia mbinu kama hizo wanasayansi wametokeza wanyama 20 hivi. Mnyama anayejulikana zaidi, yule kondoo anayeitwa Dolly, alitokezwa mnamo 1996 kutokana na titi la kondoo aliyekomaa. *

Matokeo ya majaribio hayo hayajulikani. Lakini tunajifunza kwamba, ikiwa wanadamu wanaweza kutumia chembe kutoka katika kiumbe kimoja na kutokeza kiumbe kingine cha aina hiyohiyo, je, Muumba mweza yote hangeweza kutokeza mwanadamu kutokana na kiungo cha mwanadamu mwingine? Jambo la kupendeza ni kwamba mara kwa mara madaktari wa upasuaji hutumia ubavu ili kuunganisha tena mifupa iliyovunjika kwa sababu ubavu una uwezo wa kukua upya na kujirekebisha.

Uthibitisho Ulio Ndani ya Biblia

Watu fulani wanashangaa kujua kwamba Adamu na Hawa wanatajwa mara nyingi sana katika Biblia yote. Hilo linathibitisha jinsi gani usahihi wa simulizi la Mwanzo?

Kwa mfano, fikiria orodha ya majina ya watu wa ukoo Wayahudi inayotajwa katika kitabu cha kwanza cha Mambo ya Nyakati, sura ya 1 hadi 9, na katika Injili ya Luka, sura ya 3. Orodha hizo zina majina ya watu wa ukoo wa vizazi 48 na 75. Luka anataja nasaba ya Yesu Kristo na kitabu cha Mambo ya Nyakati kinataja nasaba ya makuhani wa taifa la Israeli. Orodha hizo zina majina ya watu wanaojulikana sana kama vile Sulemani, Daudi, Yakobo, Isaka, Abrahamu, Noa, na mwishowe Adamu. Majina hayo katika orodha hizo mbili ni ya watu halisi, na Adamu ndiye mtu wa kwanza halisi katika kila orodha.

Kwa kuongezea, Biblia inawataja tena na tena Adamu na Hawa kuwa wanadamu halisi, si majina yaliyotungwa tu katika hadithi. Ona mifano ifuatayo:

• “[Mungu] alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu.”—MATENDO 17:26.

• “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo . . . kifo kilitawala kama mfalme tangu Adamu mpaka Musa.”—WAROMA 5:12, 14.

• “Mtu wa kwanza Adamu akawa nafsi hai.”—1 WAKORINTHO 15:45.

• “Adamu aliumbwa kwanza, kisha Hawa.”—1 TIMOTHEO 2:13.

• “Enoko, wa saba kutoka kwa Adamu, alitoa unabii pia kuwahusu [waovu].”—YUDA 14.

Jambo muhimu hata zaidi ni kwamba Yesu Kristo, shahidi anayetumainika sana katika Biblia, aliwataja Adamu na Hawa kuwa watu halisi. Alipoulizwa kuhusu talaka, Yesu alijibu: “Tangu mwanzo wa kuumba ‘[Mungu] aliwafanya mwanamume na mwanamke. Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’ . . . Kwa hiyo kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Marko 10:6-9) Je, Yesu angeanzisha kanuni yenye masharti ya kisheria kwa kutumia watu wa kuwaziwa tu? La, hasha! Yesu alinukuu masimulizi ya Mwanzo kama jambo hakika.

Kikieleza kwa ufupi uthibitisho huo wa Kimaandiko, kitabu The New Bible Dictionary kinamalizia kwa kusema: “Agano Jipya linathibitisha kwamba masimulizi ya sura za kwanza za Mwanzo ni sahihi kihistoria.”

Mafundisho Yote Mashakani

Watu wengi wenye mioyo minyoofu wanaoenda kanisani wanaamini kwamba si lazima kuamini kwamba Adamu na Hawa walikuwa watu halisi ili kuwa Mkristo bora. Huenda hilo likaonekana kuwa kweli unapochunguza mambo kijuujuu tu. Lakini hebu tuchunguze mambo fulani na kuona tutafikia mkataa gani.

Kwa mfano, fikiria fundisho la Biblia linaloonwa kuwa muhimu sana na watu wengi wanaoenda kanisani—fidia. Kulingana na fundisho hilo, Yesu Kristo alitoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu uwe fidia ili kuwaokoa watu kutoka kwa dhambi zao. (Mathayo 20:28; Yohana 3:16) Kama tunavyojua, fidia ni malipo yenye thamani inayolingana ili kukomboa au kununua tena kitu kilichopotezwa. Hiyo ndiyo sababu Biblia inamtaja Yesu kuwa “fidia inayolingana.” (1 Timotheo 2:6) Huenda tukauliza, inalingana na nini? Biblia inajibu: “Kama vile katika Adamu wote wanakufa, vivyo hivyo pia katika Kristo wote watafanywa kuwa hai.” (1 Wakorintho 15:22) Uhai mkamilifu ambao Yesu alidhabihu ili kuwakomboa wanadamu watiifu unalingana na uhai mkamilifu ambao Adamu alipoteza kwa sababu ya dhambi ya kwanza huko Edeni. (Waroma 5:12) Ni wazi kwamba ikiwa Adamu hangekuwa mtu halisi, dhabihu ya fidia ya Kristo ingekuwa bure kabisa.

Kukataa au kupuuza simulizi la Mwanzo kuhusu Adamu na Hawa hufanya mafundisho karibu yote ya Biblia yatiliwe shaka! * Kufanya hivyo hutokeza maswali mengi yasiyoweza kujibiwa na hufanya imani ya mtu isiwe na msingi wowote.—Waebrania 11:1.

Je, Maisha Yetu Yana Kusudi?

Mwishowe, acheni tuzungumzie swali hili la msingi: Je, kukataa simulizi la Mwanzo kunatosheleza uhitaji wa mwanadamu wa kuwa na kusudi maishani? Richard Dawkins, mtetezi maarufu wa mageuzi na imani ya kwamba hakuna Mungu, alisema kwamba katika ulimwengu “hakuna ubunifu, kusudi, uovu wala wema, hakuna chochote ila kutojali.” Huo ni mtazamo wenye kuvunja moyo kama nini na haupatani na matumaini ya wanadamu!

Tofauti kabisa na hilo, Biblia inatoa majibu yenye kuridhisha kwa maswali muhimu zaidi: Tumetoka wapi? Ni nini kusudi la uhai? Kwa nini ulimwengu umejaa uovu na kuteseka? Je, uovu utakwisha? Na maswali mengine mengi. Kwa kuongezea, imani katika fidia ya Kristo hutuwezesha tuwe na tumaini la kupata uzima wa milele katika Paradiso kama ilivyokuwa huko Edeni, ambako Mungu aliwaweka wanadamu wa kwanza, Adamu na Hawa. (Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3-5) Hilo ni taraja zuri kwelikweli! *

Ingawa huenda simulizi la Adamu na Hawa lisipatane na nadharia ya mageuzi, linapatana na sayansi. Isitoshe, simulizi hilo linapatana kabisa na sehemu nyingine za Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho yake, ambalo hueleza kwa njia yenye kuridhisha kusudi la uhai.

Kwa hiyo, mbona usiichunguze Biblia zaidi? Mashahidi wa Yehova wako tayari kukusaidia.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 7 Kulingana na mfumo wa Marekani wa kuhesabu, octillion 7 inawakilisha 7 ikifuatwa na sufuri 27, na trilioni 100 ni 100 ikifuatwa na sufuri 12.

^ fu. 8 Kwa habari zaidi, ona kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? na Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 9 Bila shaka, wanasayansi hao hawatokezi uhai. Badala yake, wanafanyiza kiumbe kutokana na chembe zilizo hai tayari.

^ fu. 25 Mafundisho hayo yanatia ndani enzi kuu ya Mungu, utimilifu wa wanadamu, mema na mabaya, uhuru wa kuchagua, hali ya wafu, ndoa, Masihi aliyeahidiwa, paradiso duniani, Ufalme wa Mungu, na mafundisho mengine mengi.

^ fu. 28 Kwa habari zaidi, ona kitabu, Biblia Inafundisha Nini Hasa? sura ya 3, “Mungu Ana Kusudi Gani kwa Dunia?,” na sura ya 5, “Fidia—Zawadi Bora Zaidi Kutoka kwa Mungu,” kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 14]

Ni wazi kwamba ikiwa Adamu hangekuwa mtu halisi, dhabihu ya fidia ya Kristo ingekuwa bure kabisa

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Kama vile tu chombo cha kusafiria angani kilivyobuniwa kwa uangalifu, ndivyo ilivyo na mwili wa mwanadamu

[Picha katika ukurasa wa 15]

Yesu alisema kwamba Adamu na Hawa walikuwa watu halisi