Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakati Mtu Anapokuudhi

Wakati Mtu Anapokuudhi

Wakati Mtu Anapokuudhi

WATU wamesema kwamba kulipiza kisasi ni kutamu. Hiyo ni kwa sababu ni kawaida kukasirika mtu anapotuudhi au kutuumiza kwa njia fulani. Ndani yetu tuna hisia fulani inayotuonyesha ikiwa jambo ni sawa au ni kosa na hisia hiyo inadai haki itekelezwe. Lakini itatekelezwa jinsi gani?

Bila shaka mtu anaweza kutuudhi kwa njia mbalimbali, iwe ni kutupiga kofi, kutusukuma, kutudharau, kututukana, kutuvamia, kutuibia, na kadhalika. Unahisije unapoudhiwa kwa njia fulani? Leo watu wengi wanasema hivi: ‘Nitalipiza kisasi!’

Nchini Marekani wanafunzi kadhaa wa kidato cha kwanza au cha pili wamewashtaki kwa uwongo walimu waliowaadhibu ili walipize kisasi kwa sababu adhabu waliyopewa. “Matokeo ni kwamba,” anasema Brenda Mitchell, msimamizi wa Chama cha Walimu huko New Orleans, “mwalimu anaharibiwa jina lake mara tu anaposhtakiwa.” Hata baada ya mashtaka kuthibitika kuwa ya uwongo, bado madhara yanadumu.

Kazini pia kuna wafanyakazi wengi wenye hasira wanaotaka kulipiza kisasi dhidi ya waajiri wao kwa kuharibu au kufuta habari muhimu kwenye mfumo wa kompyuta wa kampuni. Wengine wanaiba siri za kampuni na kuziuza au kuwapa watu wengine. Zaidi ya kuiba faili za kompyuta, “pia wafanyakazi wengine hulipiza kisasi kwa kuiba vifaa vya kampuni,” linaripoti gazeti The New York Times. Ili kukabiliana na tisho la kulipiza kisasi, sasa kampuni nyingi huhakikisha kwamba kuna mlinzi anayeandamana na mfanyakazi aliyefutwa kazi anapofunganya virago vyake na kuondoka.

Lakini sisi hulipiza kisasi dhidi ya watu walio karibu zaidi nasi kama vile marafiki na watu wa familia. Mtu anapoumizwa na maneno na matendo yasiyo ya fadhili mara nyingi anaweza kulipiza kisasi kwa maneno au matendo. Rafiki anapozungumza nawe kwa sauti ya ukali, je, wewe humjibu kwa maneno yasiyo ya fadhili? Mtu wa familia akikuudhi kwa njia fulani, je, wewe hupanga kulipiza kisasi? Ni rahisi sana kulipiza kisasi ikiwa anayekuudhi ni mtu wa karibu.

Matokeo Mabaya ya Kulipiza Kisasi

Mara nyingi, watu wanaotaka kulipiza kisasi wanajaribu kujituliza baada ya kuumizwa hisia. Kwa mfano, Biblia inatuambia kwamba wana wa mzee wa ukoo Mwebrania Yakobo walipogundua kwamba Mkanaani anayeitwa Shekemu alikuwa amemnajisi dada yao Dina, “wakaumia hisia zao, wakakasirika sana.” (Mwanzo 34:1-7) Ili walipize kisasi kwa uovu ambao dada yao alikuwa ametendewa, wana wawili wa Yakobo walipanga njama dhidi ya Shekemu na familia yake. Wakitumia ujanja, Simeoni na Lawi waliingia kwenye jiji hilo la Wakanaani na kuwaua wanaume wote, kutia ndani Shekemu.—Mwanzo 34:13-27.

Je, damu hiyo yote iliyomwagwa ilisuluhisha tatizo hilo? Yakobo alipojua kuhusu matendo ya watoto wake, aliwakemea na kusema: “Mmefanya nitengwe kwa kunifanya kuwa kitu chenye kunuka kwa wakaaji wa nchi hii, . . . nao watakusanyika pamoja juu yangu wanishambulie, nami nitaangamizwa, mimi na nyumba yangu.” (Mwanzo 34:30) Ndiyo, badala ya kusuluhisha tatizo, matendo yao ya kulipiza kisasi yalikuwa na matokeo mabaya; sasa familia ya Yakobo ilipaswa kujihadhari isishambuliwe na majirani wenye hasira. Huenda ili kuzuia shambulizi kama hilo, Mungu alimwagiza Yakobo ahamishe familia yake kutoka eneo hilo hadi Betheli.—Mwanzo 35:1, 5.

Matukio yaliyofanyika wakati wa kunajisiwa kwa Dina yanaonyesha jambo muhimu. Mara nyingi matendo ya kulipiza kisasi yanasababisha matendo mengine ya kulipiza kisasi. Hivyo, methali hii ya Kijerumani inathibitika kuwa ya kweli: Mtu anayelipiza kisasi atalipizwa kisasi.

Kulipizana Bila Kukoma

Mtu anapata madhara kwa kukazia fikira jinsi atakavyomwadhibu mtu aliyemkosea. Kitabu Forgiveness—How to Make Peace With Your Past and Get On With Your Life kinasema: “Hasira inaweza kukuumiza. Inachukua wakati na nguvu kufikiria jinsi ulivyoumizwa wakati uliopita, kuwalaani watu waliokuumiza, na kupanga njama za kulipiza kisasi.” Kama Biblia inavyosema, “wivu hufanya mifupa iwe na ubovu.”—Methali 14:30.

Kwa kweli, mtu anawezaje kuwa na furaha akiwa amejawa na hasira nyingi na hisia zisizofaa? Mtu mmoja alisema hivi: “Ukifikiri kwamba ‘kulipiza kisasi ni kutamu,’ basi tazama nyuso za watu ambao walilipiza kisasi miaka mingi iliyopita.”

Fikiria mambo yanayotokea sehemu mbalimbali za dunia ambako kuna chuki kali za kikabila na kidini. Mara nyingi kisa kimoja cha mauaji husababisha mauaji zaidi na hilo huendeleza chuki na mauaji zaidi. Kwa mfano bomu lilipoua vijana 18 katika shambulizi la kigaidi, mwanamke mwenye huzuni nyingi alisema hivi kwa sauti, “Tunapaswa kulipiza kisasi mara elfu moja!” Kwa njia hiyo ukatili unazidi tu kuongezeka, na watu zaidi na zaidi wanahusishwa.

“Jicho kwa Jicho”

Wengine hunukuu Biblia ili kutetea mtazamo wao wa kulipiza kisasi. Wanasema, “Je, Biblia haisemi kuhusu kulipa ‘jicho kwa jicho, jino kwa jino’?” (Mambo ya Walawi 24:20) Inapotazamwa kijuujuu, sheria ya “jicho kwa jicho” inaweza kuonekana kana kwamba inapendekeza kulipiza kisasi. Hata hivyo, sheria hiyo ilitolewa ili kuwazuia watu wasilipize kisasi ovyoovyo. Kwa njia gani?

Ikiwa Mwisraeli angempiga Mwisraeli mwenzake na kumng’oa jicho, Sheria iliruhusu haki itendeke. Hata hivyo, halikuwa jukumu la mtu aliyeumizwa kumwadhibu yule aliyempiga au kumwadhibu mtu wa familia yake. Sheria ilitaka mtu yule aliyeumizwa alifikishe jambo hilo kwa wenye mamlaka, yaani, waamuzi waliowekwa, ili jambo hilo lishughulikiwe kwa njia inayofaa. Kujua kwamba mtu anayetenda uhalifu au ujeuri kwa kupenda dhidi ya mwenzake angeadhibiwa kwa njia hiyohiyo, kuliwasaidia watu wengine wasilipize kisasi. Hata hivyo, kulikuwa na mengi yanayohusika.

Kabla ya kutoa sheria hiyo ya kulipiza kisasi, Yehova Mungu aliliambia hivi taifa la Israeli kupitia Musa: “Usimchukie ndugu yako moyoni mwako. . . . Usilipize kisasi wala usiwe na kinyongo.” (Mambo ya Walawi 19:17, 18) Ndiyo, sheria ya “jicho kwa jicho, jino kwa jino” inapaswa kufikiriwa kwa kuzingatia Sheria yote, ambayo Yesu alisema inaweza kujumlishwa katika amri mbili tu: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote” na “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Mathayo 22:37-40) Hivyo basi Wakristo wa kweli wanapaswa kutenda jinsi gani wanapotendewa isivyo haki?

Fuatia Amani

Biblia inamtaja Yehova kuwa “Mungu wa amani” na inawahimiza waabudu wake ‘watafute amani na kuifuatilia.’ (Waebrania 13:20; 1 Petro 3:11) Lakini je, ni jambo la hekima kufuatilia amani?

Wakati wa huduma yake hapa duniani, Yesu alitemewa mate, alichapwa viboko, aliteswa na adui zake, akasalitiwa na mwandamani wake wa karibu, na hata akaachwa na wafuasi wake. (Mathayo 26:48-50; 27:27-31) Alifanya nini? “Alipokuwa akitukanwa, hakujibu kwa matukano,” akaandika mtume Petro. “Alipokuwa akiteseka, hakutoa vitisho, bali aliendelea kujiweka mkononi mwa yule ambaye anahukumu kwa uadilifu.”—1 Petro 2:23.

Petro alieleza hivi, “Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Petro 2:21) Ndiyo, Wakristo wanatiwa moyo kumwiga Yesu, kutia ndani jinsi alivyoteseka isivyo haki. Yesu mwenyewe alisema hivi katika Mahubiri ya Mlimani: “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi; ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni.”—Mathayo 5:44, 45.

Watu walio na upendo kama wa Kristo hutenda namna gani wanapotendewa makosa au kudhani kuwa wametendewa makosa? Methali 19:11 inasema hivi: “Ufahamu wa mtu hakika hupunguza hasira yake, na ni jambo lenye kupendeza anapopita kosa.” Pia, wao hutii himizo hili: “Usiache ushindwe na uovu, bali endelea kuushinda uovu kwa wema.” (Waroma 12:21) Hilo ni tofauti sana na roho ya kulipiza kisasi ambayo imeenea sana ulimwenguni leo! Upendo wa kweli wa Kikristo unaweza kutusaidia tusilipize kisasi na hivyo ‘tupite kosa’ kwa sababu upendo “hauweki hesabu ya ubaya.”—1 Wakorintho 13:5.

Je, hilo linamaanisha kwamba tukitendewa uhalifu au kutishwa kwa njia fulani tukubaliane tu na hali hiyo? La, hasha! Paulo aliposema, ‘Endeleeni kuushinda uovu kwa wema,’ hakumaanisha kwamba Mkristo anapaswa kutamani kufia imani. Badala yake tunaposhambuliwa tuna haki ya kujikinga. Ikiwa umeshambuliwa au mali yako imeharibiwa, huenda ukaamua kuwaita polisi. Ikiwa jambo hilo linahusisha mtu kazini au shuleni, kuna watu wenye mamlaka unaoweza kuwaomba msaada.—Waroma 13:3, 4.

Hata hivyo, ni vizuri kukumbuka kwamba ni vigumu sana kupata haki ya kweli katika mfumo huu. Kwa kweli, wengi wametumia muda mwingi kutafuta haki, lakini badala yake wamelemewa na uchungu na kufungia kinyongo haki hiyo ilipokosekana.

Shetani angependa sana kuwaona watu wakitengana kwa sababu ya chuki na kulipiza kisasi. (1 Yohana 3:7, 8) Ingefaa tukizingatia maneno haya ya Biblia: “Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi ghadhabu; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’” (Waroma 12:19) Kwa kuacha mambo mikononi mwa Yehova, tunajiondolea uchungu, hasira, na jeuri.—Methali 3:3-6.

[Blabu katika ukurasa wa 22]

“Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote” na “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe”

[Picha katika ukurasa wa 23]

Upendo “hauweki hesabu ya ubaya.”—1 Wakorintho 13:5