Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe Mtiifu na Mwenye Ujasiri Kama Kristo Alivyokuwa

Uwe Mtiifu na Mwenye Ujasiri Kama Kristo Alivyokuwa

Uwe Mtiifu na Mwenye Ujasiri Kama Kristo Alivyokuwa

“Jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.”—YOH. 16:33.

1. Yesu alimtii Mungu kikamili jinsi gani?

YESU KRISTO alifanya sikuzote mapenzi ya Mungu. Hakuwahi kamwe kufikiria kutomtii Baba yake wa mbinguni. (Yoh. 4:34; Ebr. 7:26) Lakini hali zake duniani hazikufanya iwe rahisi kwake kuwa mtiifu. Tangu Yesu alipoanza kazi yake ya kuhubiri, maadui wake, kutia ndani Shetani mwenyewe, walijaribu kumsadikisha, kumlazimisha, au kumdanganya Yesu ili aache kuwa mwaminifu. (Mt. 4:1-11; Luka 20:20-25) Maadui hao walimfanya Yesu apatwe na maumivu makali ya kiakili, kihisia, na kimwili. Mwishowe, walifaulu kumuua kwenye mti wa mateso. (Mt. 26:37, 38; Luka 22:44; Yoh. 19:1, 17, 18) Pamoja na yote hayo, na ingawa aliteseka sana, Yesu alibaki “mtiifu mpaka kifo.”—Soma Wafilipi 2:8.

2, 3. Tunaweza kujifunza nini kutokana na utii wa Yesu hata ingawa alipata mateso?

2 Maisha ya Yesu akiwa mwanadamu duniani yalimfundisha mambo mapya kuhusu utii. (Ebr. 5:8) Huenda ikaonekana kwamba hapakuwa na jambo lingine zaidi ambalo Yesu angehitaji kujifunza kuhusu kumtumikia Yehova. Kwa kweli, alifurahia kushirikiana kwa karibu na Yehova kwa miaka mingi sana na alikuwa “stadi wa kazi” wa Mungu wakati wa uumbaji. (Met. 8:30) Hata hivyo, alipovumilia mateso kwa imani akiwa mwanadamu alithibitisha utimilifu wake kamili. Yesu, Mwana wa Mungu, alikua kiroho. Tunaweza kujifunza nini kutokana na maisha ya Yesu duniani?

3 Ingawa alikuwa mwanadamu mkamilifu, Yesu hakujaribu kubaki mtiifu kikamilifu kwa uwezo wake mwenyewe. Alisali kwa Mungu ili amsaidie kubaki mtiifu. (Soma Waebrania 5:7.) Ili tubaki watiifu, sisi pia tunahitaji kuwa wanyenyekevu na kusali kwa ukawaida ili Mungu atusaidie. Ndiyo sababu mtume Paulo aliwashauri Wakristo hivi: “Iweni na mtazamo huu wa akili ndani yenu ambao ulikuwa pia ndani ya Kristo Yesu,” ambaye “alijinyenyekeza naye akawa mtiifu mpaka kifo.” (Flp. 2:5-8) Maisha ya Yesu yalithibitisha kwamba wanadamu wanaweza kuwa watiifu hata katikati ya jamii yenye uovu. Ni kweli kwamba Yesu alikuwa mkamilifu, lakini namna gani sisi wanadamu wasio wakamilifu?

Tunaweza Kuwa Watiifu Ingawa Hatujakamilika

4. Kuumbwa tukiwa na uhuru wa kuchagua kunamaanisha nini kwetu?

4 Mungu aliwaumba Adamu na Hawa wakiwa viumbe wenye akili na wenye uhuru wa kuchagua. Tukiwa wazao wao, sisi pia tuna uhuru wa kuchagua. Hilo linamaanisha nini? Linamaanisha kwamba tunaweza kuchagua kutenda mema au mabaya. Kwa maneno mengine, Mungu ametupa uhuru wa kuchagua kumtii au kutomtii. Hivyo, tuna wajibu na tutatoa hesabu kuhusu jinsi tunavyotumia uhuru huo mwingi. Kwa kweli, maamuzi tunayofanya kuhusu maadili yanamaanisha uhai au kifo. Pia, yana uvutano juu ya watu walio na uhusiano wa karibu pamoja nasi.

5. Sisi sote tunapambana na nini, na tunaweza kufanikiwa tukifanya nini?

5 Kwa sababu ya hali ya kutokamilika ambayo tumerithi, si rahisi kwetu kutii. Si rahisi kutii sheria za Mungu sikuzote. Paulo alipambana sana ili kuwa mtiifu. Aliandika hivi: “Mimi naona ndani ya viungo vyangu sheria nyingine ikipigana na sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi iliyo ndani ya viungo vyangu.” (Rom. 7:23) Bila shaka, ni rahisi zaidi kutii ikiwa hatuhitaji kujidhabihu, kuteseka, au ikiwa hatukabili tatizo lolote. Lakini tunaitikia jinsi gani wakati tamaa yetu ya kuwa watiifu inapopingana na “tamaa ya mwili na tamaa ya macho”? Tamaa hizo zisizofaa zinasababishwa na hali yetu ya kutokamilika na pia uvutano wa “roho ya ulimwengu,” na ni zenye nguvu sana. (1 Yoh. 2:16; 1 Kor. 2:12) Ili kuzishinda, tunapaswa ‘kuutayarisha moyo wetu’ kabla hatujakabiliana na tatizo au kishawishi na kuazimia kwamba tutamtii Yehova, chini ya hali yoyote ile. (Zab. 78:8) Tuna mifano mingi katika Biblia ya wale ambao walifanikiwa kwa sababu waliutayarisha moyo wao.—Ezra 7:10; Dan. 1:8.

6, 7. Toa mfano unaoonyesha jinsi funzo la kibinafsi linavyoweza kutusaidia kufanya maamuzi yenye hekima.

6 Njia moja ya kuutayarisha moyo wetu ni kujifunza kwa bidii Maandiko na vichapo vinavyotegemea Biblia. Jiwazie ukiwa katika hali ifuatayo. Tuseme ni jioni ambayo unakuwa na funzo lako la kibinafsi. Umesali ili roho ya Yehova ikusaidie kutumia mambo unayojifunza katika Neno lake. Umepanga kutazama sinema fulani kwenye televisheni jioni inayofuata. Umewasikia watu wakiisifu sinema hiyo, hata hivyo, unajua pia kwamba ina jeuri na mambo fulani mapotovu kiadili.

7 Unatafakari shauri la Paulo kwenye Waefeso 5:3: “Uasherati na ukosefu wa usafi wa kila namna au pupa visitajwe hata kidogo katikati yenu, kama inavyowafaa watu watakatifu.” Pia, unakumbuka shauri la Paulo kwenye Wafilipi 4:8. (Soma.) Unapotafakari kuhusu shauri hilo lililoongozwa na roho ya Mungu, unajiuliza, ‘Nikiruhusu kimakusudi moyo na akili yangu ikazie vipindi kama hivyo, je, nitakuwa nikifuata mfano wa Yesu wa kumtii kabisa Mungu?’ Utafanya nini? Je, bado utatazama sinema hiyo?

8. Kwa nini tunapaswa kudumisha viwango vya juu vya maadili na vya kiroho?

8 Lingekuwa kosa kulegeza viwango vyetu vya kiroho na vya maadili, labda kwa kufikiri kwamba tuna nguvu za kutosha za kushinda uvutano wa mashirika mabaya, hata wakati ambapo huenda mashirika hayo yanahusisha burudani yenye jeuri na upotovu wa maadili. Badala yake, ni lazima tujilinde sisi wenyewe na watoto wetu kutokana na uvutano wenye kupotosha wa roho ya Shetani. Watu wanafanya kila wawezalo ili kulinda miili yao isiambukizwe na magonjwa. Ikiwa watu wanalinda sana miili yao, je, hatupaswi kuwa waangalifu hata zaidi ili kujilinda na mbinu zenye ujanja za Shetani?—Efe. 6:11.

9. Kwa nini tunapaswa kuazimia kila siku kumtii Yehova?

9 Karibu kila siku, kwa njia fulani tunapaswa kuamua ikiwa tutafanya mambo kulingana na njia za Yehova au hapana. Ili tuokolewe, ni lazima tumtii Mungu na kuishi kulingana na kanuni zake za uadilifu. Kwa kufuata mfano wa Kristo wa utii hata ikiwa ni “mpaka kifo,” tunaonyesha kwamba tuna imani ya kweli. Yehova atatuthawabisha ikiwa tutaendelea kuwa waaminifu. Yesu aliahidi hivi: “Yule ambaye atavumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mt. 24:13) Kwa wazi, ili kufanya hivyo tunahitaji kusitawisha ujasiri wa kweli, kama Yesu alivyofanya.—Zab. 31:24.

Yesu—Mfano Bora Zaidi wa Ujasiri

10. Ni mikazo ya aina gani ambayo huenda tukakabili, na tunapaswa kufanya nini?

10 Tukiwa tumezungukwa na mitazamo na mwenendo mpotovu wa ulimwengu huu, tunahitaji ujasiri ili kukataa kupotoshwa. Wakristo wanakabiliana na mikazo ya kiadili, kijamii, kifedha, na kidini ambayo inaweza kuwafanya waache njia za uadilifu za Yehova. Wengi wanakabili upinzani katika familia. Katika nchi fulani, vyuo vya elimu vinafundisha kwa bidii fundisho la mageuzi, na idadi ya watu wanaokubali fundisho la kwamba hakuna Mungu inazidi kuongezeka. Tunapokabili mikazo hiyo yote, hatuwezi kukaa tu bila kufanya jambo lolote. Ni lazima tuchukue hatua ili kushinda mikazo hiyo na hivyo kujilinda wenyewe. Mfano wa Yesu unatuonyesha jinsi tunavyoweza kufanikiwa.

11. Kutafakari kuhusu mfano wa Yesu kunaweza kutupa ujasiri zaidi jinsi gani?

11 Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Ulimwenguni mna dhiki, lakini jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yoh. 16:33) Hakujiacha kamwe ashindwe na uvutano wa ulimwengu. Hakuruhusu kamwe ulimwengu umzuie kutimiza kazi yake ya kuhubiri au kumfanya alegeze viwango vyake kwa ajili ya ibada ya kweli na viwango vya mwenendo unaofaa. Tunapaswa kuiga mfano wake. Katika sala, Yesu alisema hivi kuhusu wanafunzi wake: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yoh. 17:16) Kujifunza na kutafakari kuhusu mfano wa ujasiri wa Kristo kunaweza kutupa ujasiri ambao tunahitaji ili kuendelea kujitenga na ulimwengu.

Jifunze Ujasiri Kutoka kwa Yesu

12-14. Toa mifano ya jinsi Yesu alivyoonyesha ujasiri.

12 Yesu alionyesha ujasiri mkubwa wakati wote wa huduma yake. Akitumia mamlaka yake akiwa Mwana wa Mungu, bila woga ‘aliingia katika hekalu na kuwafukuza wale wote waliokuwa wakiuza na kununua katika hekalu, na kuzipindua meza za wale waliokuwa wakibadili pesa na viti vya wale waliokuwa wakiuza njiwa.’ (Mt. 21:12) Askari-jeshi walipokuja kumkamata Yesu usiku wake wa mwisho duniani, kwa ujasiri alikuja mbele ili kuwalinda wanafunzi wake, akasema: “Ikiwa ni mimi mnayetafuta, acheni hawa waende.” (Yoh. 18:8) Muda mfupi baadaye, alimwambia Petro arudishe upanga wake, na hilo lilionyesha kwamba Yesu hakuweka tumaini lake katika silaha za kidunia, bali katika Yehova.—Yoh. 18:11.

13 Yesu aliwashutumu bila woga walimu wa uwongo wa siku zake wasio na upendo na mafundisho yao ya uwongo. Yesu aliwaambia hivi: “Ole wenu ninyi, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa sababu mnawafungia watu ufalme wa mbinguni. Mmepuuza mambo mazito zaidi ya Sheria, yaani, haki na rehema na uaminifu. . . . Ninyi husafisha upande wa nje wa kikombe na wa sahani, lakini upande wa ndani vimejaa vitu vilivyoporwa na mambo yenye kupita kiasi.” (Mt. 23:13, 23, 25) Wanafunzi wa Yesu wangehitaji ujasiri kama huo kwa sababu viongozi wa kidini wa uwongo wangewatesa pia na kuwaua wengine wao.—Mt. 23:34; 24:9.

14 Yesu aliwapinga kwa ujasiri hata roho waovu. Pindi moja, alikabiliwa na mwanamume mwenye roho waovu ambaye alikuwa na nguvu nyingi sana hivi kwamba hakuna mtu aliyeweza kumfunga kwa mnyororo. Bila woga, Yesu aliwafukuza roho wengi waovu waliokuwa wakimsumbua mtu huyo. (Marko 5:1-13) Leo, Mungu hajawapa Wakristo uwezo wa kufanya miujiza kama hiyo. Hata hivyo, katika kazi yetu ya kuhubiri na kufundisha, sisi pia tunapaswa kupigana vita vya kiroho na Shetani, ambaye “amezipofusha akili za wasioamini.” (2 Kor. 4:4) Kama ilivyokuwa kuhusiana na Yesu, ‘silaha zetu si za kimwili, bali ni zenye nguvu kwa Mungu kwa ajili ya kupindua ngome zenye nguvu,’ yaani, mawazo ya uwongo ya kidini ambayo yametia mizizi ndani ya mioyo ya watu. (2 Kor. 10:4) Kwa kutumia silaha hizo za kiroho ambazo Mungu ametupatia, tunajifunza mengi kutokana na mfano wa Yesu.

15. Ujasiri wa Yesu ulitegemea nini?

15 Ujasiri wa Yesu haukutegemea ushujaa wake, bali imani. Ujasiri wetu pia unapaswa kutegemea imani. (Marko 4:40) Tunaweza kupata jinsi gani imani ya kweli? Kwa mara nyingine tena, mfano wa Yesu unaweza kutusaidia. Alionyesha kwamba aliyajua sana Maandiko na aliyategemea kabisa. Yesu hakutumia upanga halisi, bali alitumia upanga wa roho, yaani, Neno la Mungu kama silaha. Alithibitisha tena na tena mafundisho yake kwa kutumia Maandiko. Mara nyingi alitanguliza maneno yake kwa usemi huu: “Imeandikwa,” yaani, katika Neno la Mungu. *

16. Tunaweza kupata jinsi gani imani kubwa zaidi?

16 Ili kujenga imani ambayo inaweza kustahimili majaribu yasiyoepukika yanayotupata kwa sababu ya kuwa wanafunzi wa Yesu, ni lazima tusome na kujifunza Biblia kila siku na kuhudhuria mikutano ya Kikristo, kujaza katika akili zetu kweli ambazo ni msingi wa imani yetu. (Rom. 10:17) Ni lazima pia tutafakari kwa uzito kuhusu mambo tunayojifunza, na kuyaruhusu yaingie ndani ya mioyo yetu. Imani iliyo hai ndiyo tu inayoweza kutuchochea kutenda kwa ujasiri. (Yak. 2:17) Na ni lazima tusali ili tupewe roho takatifu kwa sababu imani ni sehemu ya matunda ya roho.—Gal. 5:22.

17, 18. Dada mmoja kijana alionyesha ujasiri shuleni jinsi gani?

17 Dada mmoja kijana anayeitwa Kitty alikabili hali inayoonyesha jinsi imani ya kweli inavyotupatia ujasiri. Tangu akiwa na umri mchanga, alijua kwamba hapaswi ‘kuionea aibu habari njema’ shuleni, na kwa kweli alitaka kutoa ushahidi mzuri kwa wanafunzi wenzake. (Rom. 1:16) Kila mwaka, aliazimia kuwahubiria wengine habari njema, lakini alisitasita kwa sababu ya kukosa ujasiri. Alipofikia umri wa utineja, alihamia shule nyingine. Alisema hivi: “Wakati huu, sitaacha tena nafasi ya kuhubiri inipite.” Kitty alisali ili apewe ujasiri na busara kama ya Kristo, na nafasi zinazofaa za kuhubiri.

18 Siku ya kwanza shuleni, wanafunzi waliombwa wajitambulishe mmoja baada ya mwingine. Wengi walitaja dini zao, na kuongeza kwamba kwa kweli hawakuishi kulingana na imani yao. Kitty alitambua kwamba hiyo ndiyo nafasi ya kuhubiri aliyoomba katika sala. Zamu yake ilipofika, alisema kwa usadikisho, “Mimi ni Shahidi wa Yehova, na ninategemea Biblia ili nipate mwongozo wa kiroho na wa maadili.” Wanafunzi fulani walikunja nyuso zao alipokuwa akizungumza. Lakini wengine walimsikiliza kwa makini na baadaye wakauliza maswali. Mwalimu hata alisema kwamba Kitty alikuwa mfano mzuri katika kutetea imani yake. Kitty anafurahi sana kwamba alijifunza kutokana na mfano wa Yesu wa ujasiri.

Onyesha Imani na Ujasiri Kama wa Kristo

19. (a) Kuwa na imani ya kweli kunahusisha nini? (b) Tunaweza kumfurahisha Yehova tukifanya nini?

19 Mitume pia walitambua kwamba matendo yao ya ujasiri yalipaswa kutegemea imani. Walimsihi Yesu hivi: “Tupe imani zaidi.” (Soma Luka 17:5, 6.) Kuwa na imani ya kweli kunahusisha mengi zaidi ya kuamini tu kwamba kuna Mungu. Imani ya kweli inatia ndani kusitawisha uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova, na kumtegemea kabisa, kuwa na uhusiano kama wa mtoto mchanga pamoja na baba yake mwenye fadhili na upendo. Akiongozwa na roho ya Mungu, Sulemani aliandika: “Mwanangu, ikiwa moyo wako umekuwa na hekima, moyo wangu utashangilia, naam, moyo wangu. Na figo zangu zitashangilia midomo yako inaposema mambo manyoofu.” (Met. 23:15, 16) Vivyo hivyo, tunapotetea kwa ujasiri kanuni za uadilifu tunamfurahisha Yehova, na kujua hivyo kunaongeza ujasiri wetu. Kwa hiyo, acheni sikuzote tuige mfano wa Yesu kwa kutetea uadilifu kwa ujasiri!

[Maelezo ya chini]

Je, Unaweza Kueleza?

• Ni nini kitakachotuwezesha kuendelea kuwa watiifu ingawa hatujakamilika?

• Imani ya kweli inategemea nini, na hilo linaweza kutusaidia jinsi gani kuwa na ujasiri?

• Tutapata faida gani tukiwa watiifu na kuonyesha ujasiri kama wa Kristo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Je, ‘unautayarisha moyo wako’ ili kushinda vishawishi?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kama Yesu, tunaweza kuonyesha ujasiri unaotegemea imani