Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Thamani Bora Zaidi ya Elimu ya Kimungu

Thamani Bora Zaidi ya Elimu ya Kimungu

Thamani Bora Zaidi ya Elimu ya Kimungu

“Kwa kweli naviona vitu vyote kuwa hasara kwa sababu ya thamani bora zaidi ya kumjua Kristo Yesu.”—FLP. 3:8.

1, 2. Wakristo fulani wameamua kufanya nini, na kwa nini?

ROBERT alifanya vyema shuleni tangu alipokuwa na umri mdogo. Alipokuwa na umri wa miaka minane tu, mmoja wa walimu wake alimtembelea nyumbani na kumwambia kwamba angeweza kutimiza jambo lolote lile ambalo angetaka maishani. Mwalimu huyo alimwambia Robert kwamba alitumaini siku moja atakuwa daktari. Matokeo bora aliyopata akiwa mwanafunzi wa shule ya sekondari yalimfanya astahili kujiunga na moja kati ya vyuo vikuu vilivyo bora zaidi katika nchi yao. Lakini Robert aliamua kukataa nafasi ambayo wengi waliona kuwa nafasi ya pekee sana maishani ili afuatie mradi wake wa kutumikia akiwa painia wa kawaida.

2 Kama Robert, Wakristo wengi vijana kwa wazee wanapata nafasi za kufanikiwa katika mfumo huu wa mambo. Wengine wao wanaamua kutotumia kikamili nafasi hizo, ili waweze kufuatia miradi ya kiroho. (1 Kor. 7:29-31) Ni nini kinachowachochea Wakristo kama Robert kujitoa kabisa katika kazi ya kuhubiri? Zaidi ya upendo wao kwa Yehova, ambayo ndiyo sababu kuu zaidi, wanatambua thamani bora zaidi ya elimu ya kimungu. Je, hivi karibuni umefikiria ungekuwa na maisha ya aina gani ikiwa hungekuwa na ujuzi juu ya kweli? Kutafakari kuhusu baraka fulani za pekee ambazo tunafurahia kwa sababu ya kufundishwa na Yehova kutatusaidia kuendelea kuthamini habari njema na kuwa wenye bidii katika kuwahubiria wengine habari hiyo njema.

Ni Pendeleo Kufundishwa na Mungu

3. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova yuko tayari kuwafundisha wanadamu wasio wakamilifu?

3 Kwa sababu ya wema wake, Yehova yuko tayari kuwafundisha wanadamu wasio wakamilifu. Andiko la Isaya 54:13 linasema hivi kinabii kuhusu Wakristo watiwa-mafuta: “Wana wako wote watakuwa watu waliofundishwa na Yehova, na amani ya wana wako itakuwa nyingi.” Kanuni ya maneno hayo inawahusu pia “kondoo wengine” wa Kristo. (Yoh. 10:16) Unabii fulani unaotimizwa katika siku zetu unaonyesha hilo waziwazi. Katika maono, Isaya aliona watu kutoka katika mataifa yote wakimiminika kwenye ibada ya kweli. Anasema kwamba wanaambiana hivi: “Twendeni juu kwenye mlima wa Yehova, kwenye nyumba ya Mungu wa Yakobo; naye atatufundisha njia zake, nasi tutatembea katika mapito yake.” (Isa. 2:1-3) Ni pendeleo kama nini kufundishwa na Mungu!

4. Yehova anataka wale ambao anafundisha watimize matakwa gani?

4 Tunaweza kufanya nini ili tustahili kufaidika na elimu ya kimungu? Takwa la maana zaidi ni kwamba ni lazima mtu awe mpole na tayari kufundishwa. Mtunga-zaburi Daudi aliandika hivi: “Yehova ni mwema na mnyoofu. . . . Atawafundisha wapole njia yake.” (Zab. 25:8, 9) Naye Yesu alisema hivi: “Ninakusifu hadharani wewe, Baba, Bwana wa mbingu na dunia, kwa sababu umewaficha kwa uangalifu wenye hekima na walio na akili mambo hayo, nawe umeyafunua kwa watoto.” (Luka 10:21) Je, huvutiwi na Mungu ambaye “huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa”?—1 Pet. 5:5.

5. Ni jambo gani hasa ambalo limetuwezesha kumjua Mungu?

5 Tukiwa watumishi wa Yehova, je, tunaweza kujisifu kwamba tumepata kweli kwa hekima yetu wenyewe? Hapana. Ukweli ni kwamba kwa uwezo wetu wenyewe hatungeweza kamwe kumjua Mungu. Yesu alisema hivi: “Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute.” (Yoh. 6:44) Kupitia kazi ya kuhubiri na roho takatifu, Yehova anawavuta watu walio kama kondoo, yaani, “vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote.” (Hag. 2:7) Je, hushukuru kuwa kati ya watu ambao Yehova amewavuta kwa Mwana wake?—Soma Yeremia 9:23, 24.

Nguvu Zinazoboresha Maisha ya Watu

6. Kupata “kumjua Yehova” kunaweza kuwa na matokeo gani mazuri juu ya watu?

6 Unabii wa Isaya unatumia mfano mzuri sana kuonyesha jinsi wanadamu wanavyobadili nyutu zao katika siku zetu. Watu ambao zamani walikuwa wajeuri wamekuwa wafanya-amani. (Soma Isaya 11:6-9.) Watu ambao zamani walikuwa maadui kwa sababu ya tofauti za kijamii, kitaifa, kikabila, au tofauti nyingine za kitamaduni wamejifunza kukaa pamoja kwa umoja. Kwa njia ya mfano, ‘wamefua panga zao zikawa majembe.’ (Isa. 2:4) Ni nini ambacho kimewasaidia kufanya mabadiliko hayo makubwa? Watu wamepata “kumjua Yehova” na wametumia ujuzi huo katika maisha yao. Ingawa watumishi wa Mungu si wakamilifu, wanafanyiza undugu wa kweli wa kimataifa. Kuenea kwa habari njema ulimwenguni pote na matokeo mazuri ya kazi hiyo yanathibitisha kwamba elimu ya kimungu ina thamani bora zaidi.—Mt. 11:19.

7, 8. (a) Elimu ya kimungu inawasaidia watu kupindua ‘ngome gani zenye nguvu’? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba elimu ya kimungu inamletea Yehova sifa?

7 Mtume Paulo alilinganisha kazi ya kuhubiri ya watumishi wa Mungu na vita vya kiroho. Aliandika hivi: “Silaha za vita vyetu si za kimwili, bali ni zenye nguvu kwa Mungu kwa ajili ya kupindua ngome zenye nguvu. Kwa maana sisi tunapindua mawazo na kila jambo lililo juu sana ambalo limeinuliwa kinyume cha ujuzi wa Mungu.” (2 Kor. 10:4, 5) Elimu ya kimungu inawaweka watu huru kutoka katika ‘ngome gani zenye nguvu’? Mzigo wa mafundisho ya uwongo, ushirikina, na falsafa za wanadamu, ni mifano michache tu ya ngome hizo. (Kol. 2:8) Elimu ya kimungu inawasaidia watu kushinda mazoea mabaya na kusitawisha sifa za kimungu. (1 Kor. 6:9-11) Inaboresha maisha ya familia. Na inawapa wale wasio na tumaini kusudi la kweli maishani. Hiyo ndiyo aina ya elimu ambayo inahitajiwa leo.

8 Moja ya sifa ambazo Yehova anawasaidia watu kusitawisha ni unyoofu, kama jambo lifuatalo lililoonwa linavyoonyesha. (Ebr. 13:18) Mwanamke fulani huko India alikubali kujifunza Biblia na baada ya muda akastahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa. Siku moja alipokuwa akirudi nyumbani baada ya kushiriki katika ujenzi wa Jumba la Ufalme, aliokota mkufu wa dhahabu wenye thamani ya dola 800 za Marekani karibu na kituo cha mabasi. Ingawa yeye ni maskini, aliupeleka mkufu huo kwenye kituo cha polisi ili wamtafute mwenyewe. Ofisa wa polisi aliyekuwapo hakuamini macho yake! Baadaye, ofisa mwingine alimuuliza, “Kwa nini uliamua kuleta mkufu huu?” Mwanamke huyo akaeleza hivi: “Mafundisho ya Biblia yamenibadili, sasa mimi ni mtu mnyoofu.” Polisi huyo alivutiwa akamwambia hivi mzee Mkristo aliyeenda pamoja na mwanamke huyo kwenye kituo cha polisi: “Jimbo hili lina watu zaidi ya milioni 38. Kama unaweza kuwasaidia watu kumi kuwa kama mwanamke huyu, utakuwa umetimiza jambo la maana sana.” Tunapofikiria mamilioni ya watu ambao maisha yao yameboreshwa na elimu ya kimungu, je, hatuwi na sababu nyingi sana za kumsifu Yehova?

9. Ni nini kinachowawezesha watu kufanya mabadiliko makubwa katika maisha yao?

9 Nguvu za Neno la Mungu za kuwabadili watu, pamoja na msaada ambao Yehova anatoa kupitia roho yake takatifu, zinawawezesha watu kufanya mabadiliko makubwa sana katika maisha yao. (Rom. 12:2; Gal. 5:22, 23) Andiko la Wakolosai 3:10 linasema hivi: “Mjivike utu mpya, ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mpya kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba.” Ujumbe unaopatikana katika Neno la Mungu, Biblia, una nguvu za kufunua jinsi mtu alivyo kikweli kwa ndani, na unaweza kubadili njia yake ya kufikiri na hata hisia zake kuelekea mambo. (Soma Waebrania 4:12.) Mtu anapopata ujuzi sahihi kuhusu Maandiko na kuishi kupatana na viwango vya Yehova vya uadilifu, anaweza kuwa rafiki ya Mungu, na kuwa na tumaini la kuishi milele.

Kujitayarisha kwa Ajili ya Wakati Ujao

10. (a) Kwa nini Yehova peke yake ndiye anayeweza kutusaidia kujitayarisha kwa ajili ya wakati ujao? (b) Ni mabadiliko gani makubwa yatakayoikumba dunia nzima hivi karibuni?

10 Yehova peke yake ndiye anayeweza kutusaidia kujitayarisha kwa ajili ya wakati ujao kwa sababu anajua mambo yatakayotokea wakati ujao. Anajua jinsi maisha ya wanadamu yatakavyokuwa wakati ujao. (Isa. 46:9, 10) Unabii wa Biblia unafunua kwamba “siku kuu ya Yehova iko karibu.” (Sef. 1:14) Kuhusu siku hiyo, maneno ya Methali 11:4 yatathibitika kuwa ya kweli: “Vitu vyenye thamani havitakuwa na faida yoyote siku ya ghadhabu, lakini uadilifu utakomboa kutoka katika kifo.” Wakati utakapofika wa Yehova kuuhukumu ulimwengu wa Shetani, jambo la maana zaidi litakuwa msimamo wetu mbele za Mungu. Pesa hazitakuwa na thamani yoyote. Kwa kweli, andiko la Ezekieli 7:19 linasema hivi: “Katika barabara watatupa fedha yao wenyewe, na dhahabu yao wenyewe itakuwa chukizo.” Kujua jambo hilo mapema kunaweza kutusaidia kutenda kwa hekima sasa.

11. Ni katika njia gani moja elimu ya kimungu inatusaidia kujitayarisha kwa ajili ya wakati ujao?

11 Njia moja ya pekee ambayo elimu ya kimungu inatutayarisha kwa ajili ya siku ya Yehova inayokuja ni kwamba inatusaidia kutanguliza mambo ya maana zaidi maishani. Mtume Paulo alimwandikia Timotheo hivi: “Uwape maagizo wale walio matajiri katika mfumo wa mambo wa sasa wasitake makuu, na waweke tumaini lao, si katika utajiri usio hakika, bali katika Mungu.” Hata ikiwa sisi si matajiri, tunaweza kufaidika kwa kufuata shauri hilo lililoongozwa na roho ya Mungu. Kufanya hivyo kunahusisha nini? Badala ya kujitahidi sana kupata utajiri wa kimwili, tunapaswa kujitahidi ‘kufanya mema’ na ‘kuwa matajiri katika matendo mazuri.’ ‘Tunajiwekea wenyewe hazina ya msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao,’ kwa kutanguliza mambo ya kiroho katika maisha yetu. (1 Tim. 6:17-19) Maisha hayo ya kujidhabihu yanaonyesha kwamba mtu anatenda kwa hekima, kwa kuwa, kama Yesu alivyosema, “mtu atapata faida gani akiupata ulimwengu wote lakini aipoteze nafsi yake?” (Mt. 16:26, 27) Kwa kuwa siku ya Yehova inakaribia sana, kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza hivi: ‘Ninajiwekea hazina wapi? Je, ninamtumikia Mungu au Utajiri?’—Mt. 6:19, 20, 24.

12. Kwa nini hatupaswi kuvunjika moyo watu fulani wanapoidharau huduma yetu?

12 Jambo la maana zaidi kati ya “matendo mazuri” ambayo Neno la Mungu linasema Wakristo wanapaswa kufanya ni kazi inayookoa uhai ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, huenda watu fulani wakaidharau huduma yetu. (Soma 1 Wakorintho 1:18-21.) Lakini hilo halibadili thamani ya ujumbe wetu, na halipunguzi umuhimu wa kumpa kila mtu nafasi ya kuamini ujumbe huo kama bado kuna wakati. (Rom. 10:13, 14) Tunapowasaidia wengine kunufaika na elimu ya kimungu, sisi pia tunapata baraka nyingi.

Wanabarikiwa kwa Sababu Wanajidhabihu

13. Mtume Paulo alidhabihu mambo gani kwa ajili ya habari njema?

13 Kabla ya kuwa Mkristo, mtume Paulo alikuwa akizoezwa ili afanikiwe katika mfumo wa mambo wa Kiyahudi. Inaelekea kwamba alipokuwa na umri wa miaka isiyozidi 13, alihamia Yerusalemu kutoka katika jiji lao la Tarso ili afundishwe na Gamalieli, mwalimu wa Sheria aliyeheshimiwa sana. (Mdo. 22:3) Baada ya muda, Paulo alianza kufanikiwa kati ya vijana wenzake, na kama angeendelea hivyo, huenda angekuwa mtu mashuhuri sana katika dini ya Kiyahudi. (Gal. 1:13, 14) Alipokubali habari njema na kuanza kazi ya kuhubiri aliacha mambo hayo yote. Je, Paulo alijuta kwa sababu ya uamuzi aliofanya? Hapana. Aliandika hivi: “Kwa kweli naviona vitu vyote kuwa hasara kwa sababu ya thamani bora zaidi ya kumjua Kristo Yesu Bwana wangu. Kwa sababu yake nimekubali hasara ya vitu vyote nami naviona kuwa takataka nyingi, ili niweze kumpata Kristo.”—Flp. 3:8.

14, 15. Ni baraka gani tunazopata tukiwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu”?

14 Kama Paulo, Wakristo leo wanajidhabihu kwa ajili ya habari njema. (Marko 10:29, 30) Je, tunakosa chochote kwa sababu ya kufanya hivyo? Robert, aliyetajwa mwanzoni, ana maoni kama ya watu wengi anaposema hivi: “Sina majuto yoyote. Huduma ya wakati wote imeniletea shangwe na uradhi, na imenipa nafasi ya ‘kuonja na kuona ya kuwa Yehova ni mwema.’ Wakati wowote nilipojidhabihu kimwili ili kufuatia miradi ya kiroho, Yehova alinipa baraka nyingi zaidi kuliko vitu nilivyodhabihu. Ni kana kwamba sikudhabihu kitu chochote. Nimenufaika sana!”—Zab. 34:8; Met. 10:22.

15 Ikiwa umekuwa ukishiriki katika kazi ya kuhubiri na kufundisha kwa muda fulani sasa, bila shaka wewe pia umepata nafasi za kuonja na kuona kwamba Yehova ni mwema. Je, kuna nyakati ambazo uliona roho yake ikikusaidia ulipokuwa ukihubiri habari njema? Je, umeona macho ya wengine yaking’aa Yehova anapofungua mioyo yao ili wasikilize ujumbe huo? (Mdo. 16:14) Je, Yehova amekusaidia kushinda vizuizi fulani, labda akifungua njia ili upanue huduma yako? Je, amekutegemeza nyakati za matatizo, na kukuwezesha kuendelea kumtumikia ulipohisi kwamba unadhoofika? (Flp. 4:13) Tunapoona Yehova akitusaidia sisi binafsi tunapotimiza huduma yetu, anakuwa halisi zaidi kwetu na tunakuwa na uhusiano wa karibu hata zaidi pamoja naye. (Isa. 41:10) Je, si ni baraka kuwa mmoja wa “wafanyakazi wenzi wa Mungu” katika kazi tukufu ya kuwapa wengine elimu ya kimungu?—1 Kor. 3:9.

16. Unahisi jinsi gani kuhusu jitihada na dhabihu unazofanya katika kazi ya kuwafundisha wengine kumhusu Yehova?

16 Watu wengi wanatumaini kutimiza jambo fulani lenye faida ya kudumu katika maisha yao. Tumeona kwamba hata mambo ya pekee sana yanayotimizwa katika ulimwengu wa leo mara nyingi yanasahauliwa haraka. Hata hivyo, kazi ambazo Yehova anatimiza katika siku zetu kuhusiana na kutakaswa kwa jina lake bila shaka zitahifadhiwa katika rekodi ya kudumu ya historia ya watu wa Mungu. Kazi hizo zitakumbukwa milele. (Met. 10:7; Ebr. 6:10) Basi, na tuthamini sana pendeleo letu la kushiriki katika kazi ya kihistoria ya kuwafundisha wengine kumhusu Yehova.

Ungesema Nini?

• Yehova anataka wale ambao anafundisha watimize matakwa gani?

• Elimu ya kimungu inaboresha maisha ya watu namna gani?

• Tunabarikiwa jinsi gani tunapowasaidia wengine kufaidika kutokana na elimu ya kimungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wale wanaofundishwa na Yehova wanakuwa undugu wa kweli wa kimataifa

[Picha katika ukurasa wa 24]

Je, si ni baraka kuwa mmoja wa “wafanyakazi wenzi wa Mungu”?