Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Inawezekana Kuamini Kuna Muumba?

Je, Inawezekana Kuamini Kuna Muumba?

Je, Inawezekana Kuamini Kuna Muumba?

“NILIPOWAZIA kwamba huenda kuna Muumba, wazo la kwamba kuna mtu aliye na nguvu za kuzuia kuteseka kwa wanadamu lakini hazitumii, lilinikasirisha sana!” Hivyo ndivyo alivyosema mtu fulani ambaye hapo awali hakuamini kwamba kuna Mungu na aliyewapoteza watu wa familia yake katika yale maangamizi makubwa yaliyotekelezwa na Wanazi. Si yeye tu aliye na hisia kama hizo.

Watu wengi wanapotendewa kikatili, inakuwa vigumu kwao kuamini kuna Mungu, au wanajifariji kwa kusema kwamba hakuna Mungu. Ni nini sababu kuu zinazowafanya watu fulani wasimwamini Mungu? Je, maisha ya wanadamu yanaweza kuwa mazuri bila kuwa na Mungu au dini, kama watu fulani wanavyosema? Je, inawezekana kwa wale wanaoamini kwamba hakuna Mungu kuamini kuna Muumba?

Dini Zimeshindwa

Kwa kushangaza, dini ndiyo sababu kuu inayowafanya watu wasiamini kwamba kuna Mungu. Mwanahistoria Alister McGrath alieleza: “Kinachowafanya watu wasiamini kuwapo kwa Mungu ni chuki ambayo watu wamekuwa nayo kwa sababu ya maisha ya anasa na ya upotovu yaliyo katika dini kubwa.” Mara nyingi dini huonekana kama kisababishi cha vita na jeuri. Michel Onfray mwanafalsafa asiyeamini kwamba kuna Mungu aliandika jinsi inavyowezekana kwa kitabu kilekile cha kidini kutokeza aina mbili za watu, mtu wa kwanza “anajitahidi sana kuwa mtakatifu,” na yule mwingine “anatenda kwa ukatili wa kinyama,” yaani, ugaidi.

Watu wengi wana uchungu wanapokumbuka mambo yaliyotukia walipokuwa katika dini. Alipokuwa jeshini, Bertil, kijana kutoka Sweden alimsikia kasisi wa jeshi akitetea jeuri kwa kutumia onyo la Yesu kwamba wale wanaochukua upanga wataangamia kwa upanga. Kasisi huyo alisababu kwamba lazima kuwepo na mtu atakayeuchukua upanga, hivyo, lazima askari-jeshi awe mtumishi wa Mungu!—Mathayo 26:52. *

Bernadette, ambaye baba yake aliuawa nchini Ufaransa wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, anakumbuka jinsi alivyokasirika kasisi aliposema hivi kwenye mazishi ya binamu yake mwenye umri wa miaka mitatu: “Mungu amemchukua mtoto huyu ili awe malaika.” Baadaye, Bernadette, alipata mtoto mlemavu na hakupata faraja yoyote kutoka kanisani.

Ciarán, ambaye alilelewa wakati wa kipindi chenye jeuri huko Ireland Kaskazini, alichukizwa sana na fundisho la moto wa mateso. Alikuwa akisema kwamba alichukizwa na Mungu yeyote ambaye alisababisha uovu na akamwambia Mungu ikiwa yupo, basi amuue. Si Ciarán tu aliyechukizwa na mafundisho hayo ya kidini yenye ukatili. Kwa kweli, huenda mafundisho ya dini yalichangia kuanzishwa kwa fundisho la mageuzi. Alister McGrath, alisema kwamba Darwin alianza kuwa na shaka kuhusu kuwapo kwa Mungu kwa sababu ya “kuchukizwa sana” na fundisho la moto wa mateso na si kwa sababu ya kuamini mageuzi. McGrath alisema pia kwamba Darwin “alihuzunishwa sana na kifo cha binti yake.”

Wengine huhusianisha dini na watu wasiotumia akili na wenye msimamo mkali. Irina, aliyekuwa amechoshwa na mahubiri yasiyo na maana na sala za kurudiwa-rudiwa anasimulia hivi: “Niliona kwamba watu wa kidini hawatumii akili.” Louis, ambaye alichukizwa sana na matendo ya kikatili yaliyochochewa na watu walioshikilia sana mambo ya kidini alikuwa na msimamo huu mkali: “Kwa miaka mingi niliona dini kuwa yenye kuchosha lakini sasa naona jinsi inavyowadhuru watu. Nilipinga vikali dini zote.”

Je, Ni Afadhali Kutomjua Mungu?

Basi haishangazi kwamba watu wengi wanaiona dini kuwa kizuizi cha maendeleo ya wanadamu na amani. Hata wengine wamejiuliza ikiwa wanadamu wangeweza kufanikiwa bila kumtegemea Mungu na dini. Hata hivyo, je, kukataa dini kwa ujumla kunaweza kuleta matatizo?

Voltaire ambaye alikuwa mwanafalsafa wa karne ya 18 alilalamika kuhusu matendo mabaya ya kanisa katika siku zake. Hata hivyo, aliona kwamba kuwepo kwa Mtu Mkuu Kuliko Wote kuwa ni msingi wa uwezo wetu wa kupambanua mema na mabaya. Baadaye, Friedrich Nietzsche, ambaye alikuwa mwanafalsafa Mjerumani alisema kwamba Mungu amekufa, lakini Nietzsche aliogopa kwamba hakutakuwa na viwango vya maadili na pia akaogopa madhara yanayoweza kusababishwa na kufikiri kwamba hakuna Mungu. Je, woga wake ulikuwa na msingi wowote?

Mwandishi Keith Ward alisema wanadamu walipoingia katika nyakati za kisasa, ukatili haukupungua bali “ulifikia kiwango ambacho hakikuwahi kuwaziwa kabla ya hapo.” Kuendeleza wazo la kwamba hakuna Mungu hakujawaondolea wanadamu matatizo yanayosababishwa na wanadamu wenyewe, kama vile ufisadi na kutovumiliana. Ukweli huo umewafanya watu wengi wenye akili kutia ndani wale wanaoamini kwamba hakuna Mungu, watambue umuhimu wa kuwa na imani katika Mungu.

Keith Ward anakazia umuhimu wa kuamini kwamba kuna Mungu: “Imani inasisitiza kwamba ni muhimu kuwa na viwango vya maadili, inatoa daraka la kutunza ulimwengu ambao Mungu ameumba.” Uchunguzi mwingi wa hivi karibuni unaonyesha kwamba watu wanaopendezwa na mambo ya kidini wanazidi kuwajali wengine bila ubinafsi. Kwa hiyo, kuwajali wengine huleta uradhi. Uchunguzi kama huo hukazia umuhimu wa kanuni hii ya Yesu: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.

Mfanyakazi mmoja wa huduma za jamii ambaye hapo awali hakuwa anaamini kwamba kuna Mungu, alivutiwa sana na uwezo wa Biblia wa kubadili maisha ya watu. Alisema hivi: “Baada ya kujaribu kwa miaka mingi bila mafanikio kuwasaidia watu wabadili tabia zao zilizokuwa na madhara kwao na kwa wengine, niliona jinsi inavyopendeza kuwaona watu wakibadilika na kuwa wazuri. Pia, niligundua kwamba mabadiliko hayo yalikuwa ya kudumu.”

Hata hivyo, watu fulani wanaoamini kwamba hakuna Mungu wanasema kwamba kuamini kwamba kuna Mungu kumetokeza mauaji ya halaiki na vita vingi zaidi kuliko kuwafanya watu wawe wema na wenye kuwajali wengine. Wanaweza kuelewa kwamba imani inawabadili watu fulani, lakini wao hubaki wakiwa na mashaka. Kwa nini?

Sababu Nyingine Zinazowafanya Watu Wasiwe na Imani

Watu wengi wanafundishwa kwamba mageuzi ni jambo hakika. Kwa mfano, Anila, alienda shuleni huko Albania ambako watu hawaamini kwamba kuna Mungu. “Shuleni tulifundishwa kwamba kuamini kwamba kuna Mungu ni upumbavu na ushamba,” anaeleza. “Nilijifunza mambo yenye kupendeza kuhusu mimea na vitu vingine vilivyo hai, lakini nilisema vyote vilitokea kwa mageuzi, kwa kuwa kufanya hivyo kulifanya tuonekane tunapatana na kufikiri kwa kisayansi.” Anakubali kwamba leo “uthibitisho uliotolewa ulipaswa kukubaliwa bila kupingwa.”

Uchungu unaweza pia kuwazuia watu fulani wasiamini kwamba kuna Mungu. Mara nyingi, Mashahidi wa Yehova hukutana na mtazamo kama huo wanapoenda nyumba kwa nyumba wakiwatolea watu tumaini la Biblia. Bertil, aliyetajwa hapo awali, alitembelewa na Shahidi fulani kijana. Bertil anakumbuka akijiambia hivi: ‘Mshupavu huyu amepotea sana!’ Anasema: “Nilimkaribisha ndani na kuanza kumshambulia kwa hoja kuhusu Mungu, Biblia, na dini.”

Gus anayeishi nchini Scotland, alitatizwa na ukosefu wa haki. Mwanzoni alikuwa mbishi na alikuwa akipinga alipozungumza na Mashahidi wa Yehova. Aliuliza maswali yanayofanana na yale ya nabii Mwebrania Habakuki, aliyemwambia Mungu hivi: “Kwa nini unanionyesha jambo lenye kudhuru, nawe unaendelea kutazama taabu tupu?”—Habakuki 1:3.

Pia, wanadamu wametaabishwa kwa muda mrefu na wazo la kwamba Mungu hajali uovu uliopo. (Zaburi 73:2, 3) Simone de Beauvoir, mwandishi Mfaransa, alisema hivi wakati mmoja: “Ilikuwa rahisi kwangu kufikiri juu ya ulimwengu usio na muumba kuliko muumba anayekubali mambo yote yenye kupingana ya ulimwengu.”

Hata hivyo, kwa kuwa dini nyingi haziwezi kueleza mambo hayo yenye kupingana, je, hilo linamaanisha kwamba hakuna majibu? Gus alisema kwamba mwishowe alipata “majibu yenye kuridhisha kuhusu sababu inayomfanya Muumba mwenye nguvu zote awaache wanadamu wateseke kwa muda.” Alisema kwamba hiyo “ilikuwa hatua muhimu kwangu.” *

Huenda watu fulani wanaodai kuwa hawaamini kwamba kuna Mungu wakawa na shaka kuhusu mageuzi, wanaweza kutambua uhitaji wao wa kiroho, na huenda wakasali. Acheni tuone ni nini kilichowafanya watu walioamini kwamba hakuna Mungu na wale walioamini kwamba mambo ya Mungu hayawezi kujulikana wafikiri kwa undani kuhusu jambo hilo na mwishowe wawe na uhusiano wa karibu pamoja na Muumba wao.

Ni Nini Kilichowasaidia Wawe na Imani Katika Muumba?

Kijana aliyemtembelea Bertil alitumia mambo yanayopatana na akili kumwonyesha kwa kwamba kuna tofauti kubwa kati ya Wakristo wa kweli na dini za wale ambao ni Wakristo kwa jina tu. Bertil anaeleza ni nini kilichompendeza, zaidi ya hoja alizotoa kuthibitisha kwamba kuna Muumba: “Nilipendezwa na subira yake licha ya ubishi wangu. . . . Aliendelea kuwa mtulivu, wakati wote aliniletea vichapo, na alikuwa amejitayarisha vizuri.” *

Svetlana, aliyekuwa ameathiriwa na mageuzi na Ukomunisti, alisadiki kwamba ni viumbe wenye nguvu tu wanaoendelea kuishi. Hata hivyo, wazo hilo lenye ukatili lilimsumbua sana. Kile alichofundishwa katika chuo cha matibabu kilimfanya azidi kuchanganyikiwa: “Wakati wa somo la kwamba hakuna Mungu, tulijifunza kuwa ni viumbe wenye nguvu tu wanaoendelea kuishi. Lakini katika masomo ya kitiba tulifundishwa kwamba tunapaswa kuwasaidia walio dhaifu.” Pia alijiuliza kwa nini wanadamu, ambao inasemekana kwamba walitokana na nyani, wana matatizo ya kihisia ambayo nyani hawana. Majibu kuhusu mambo hayo yaliyomtatiza yalitoka mahali ambapo hakutarajia: “Nyanya yangu alinieleza kutoka kwenye Biblia kwamba kutokamilika kwetu ndiko kulisababisha matatizo ya kihisia.” Pia, Svetlana alifurahi kupata majibu ya Biblia ya maswali kama vile kwa nini watu wanyoofu wanateseka.

Leif, aliyezaliwa katika nchi za Skandinavia, aliamini sana mageuzi na aliiona Biblia kuwa kitabu cha hadithi za watoto. Hata hivyo, siku moja rafiki yake alimwuliza maswali kuhusu mambo aliyoamini: “Je, unafahamu kwamba unarudia mambo ambayo wengine wamesema bila kujua kile ambacho Biblia inasema?” Leif alieleza jinsi maneno hayo yalivyomwathiri: “Nilitambua kwamba sikuwahi kutilia shaka mageuzi, lakini nilikubali nadharia hiyo bila kuuliza maswali. . . . Ninafikiri kwamba kuwa na ujuzi kuhusu unabii mbalimbali wa Biblia na utimizo wake ni jambo moja linaloweza kumsaidia mtu asiyeamini kwamba kuna Mungu aanze kufikiri.”—Isaya 42:5, 9.

Ciarán, aliyetajwa awali, hakuona mambo wazi kwa sababu ya kujihusisha katika siasa kwa muda mrefu. Alipokuwa akifiri kuhusu uhai wazo hili lilimjia akilini: Ni Mungu tu mwenye uwezo na upendo anayeweza kutatua matatizo yaliyo duniani na kumwonyesha jinsi ya kusuluhisha hali yake yenye kuhuzunisha. ‘Ninatamani sana kumpata Mungu kama huyo,’ alijiambia hivyo kwa huzuni. Alisali hivi kwa huzuni nyingi: “Ikiwa wewe uko na unanisikiliza, nionyeshe kwamba upo, na unionyeshe jinsi ninavyoweza kujiondolea huzuni na uchungu wangu na ule unaowapata wanadamu wote.” Siku kadhaa baadaye, Shahidi wa Yehova alibisha mlango wake. Shahidi huyo alieleza kile ambacho Biblia inafundisha kuhusu ni nani anayeongoza serikali za wanadamu. (Waefeso 6:12) Maelezo hayo yalimthibitishia Ciarán mambo aliyokuwa amejionea na yakachochea udadisi wake. Baada ya kujifunza Biblia zaidi, imani yake katika Muumba mwenye upendo ilianza kuongezeka.

Uhusiano Wako na Muumba wa Wanadamu

Unafiki wa kidini, mafundisho yanayoonyesha kwamba hakuna Mungu kama vile mageuzi, na kuenea kwa uovu, kumewafanya wengi watilie shaka au hata kupinga kwamba kuna Muumba. Hata hivyo, Biblia inaweza kukupa majibu yenye kuridhisha ya maswali yako. Pia inafunua mawazo ya Mungu, “mawazo ya amani, wala si ya msiba, ili kuwapa ninyi wakati ujao na tumaini.” (Yeremia 29:11) Bernadette, ambaye alipata mtoto mlemavu na ambaye alitilia shaka kuwapo kwa Muumba, alitulizwa sana na tumaini hilo.

Maelezo ya Biblia kuhusu kwa nini Mungu ameruhusu kuteseka yamegusa akili na mioyo ya watu wengi ambao zamani waliamini kwamba hakuna Mungu. Ukitenga wakati ili kupata majibu ya Biblia kwa maswali muhimu kama hayo, wewe pia unaweza kusadikishwa kwamba kuna Mungu ambaye kwa kweli, “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.”—Matendo 17:27.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 6 Ili kujua ikiwa Wakristo wa kweli wanapaswa kujihusisha katika vita, ona makala “Je, Ukristo Unaunga Mkono Vita?” katika ukurasa wa 29-31.

^ fu. 22 Kwa habari zaidi kuhusu sababu ya Mungu kuruhusu uovu uendelee, ona ukurasa wa 106 hadi 114 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 25 Ili upate sababu zaidi zinazounga mkono uumbaji, ona Amkeni! la Septemba (Mwezi wa 9) 2006, “Je, Kuna Muumba?,” lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

Maswali Ambayo Wanamageuzi Hawajajibu

• Uhai ungetokanaje na kitu ambacho hakina uhai?—ZABURI 36:9.

• Kwa nini wanyama na mimea huzaa kulingana na aina zake tu?—MWANZO 1:11, 21, 24-28.

• Ikiwa wanadamu walitokana na nyani ambao ni wanyama wa hali ya chini, kwa nini hakuna hata sokwe-mtu mmoja ambaye yuko hai hadi leo?—ZABURI 8:5, 6.

• Ikiwa nadharia ya kwamba ni viumbe wenye nguvu tu ndio wanaoendelea kuishi, kwa nini wanadamu huwajali wengine bila ubinafsi?—WAROMA 2:14, 15.

• Je, wanadamu wana tumaini lolote la wakati ujao?—ZABURI 37:29.

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Mungu mwenye upendo angewezaje kuumba dunia ambamo watoto wanateseka?

Unafiki wa kidini umewafanya wengi wamkatae Mungu