Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kodeksi ya Vatikani—Kwa Nini Ni Yenye Thamani?

Kodeksi ya Vatikani—Kwa Nini Ni Yenye Thamani?

Kodeksi ya Vatikani—Kwa Nini Ni Yenye Thamani?

VATIKANI ina vitu vingi sana vyenye thamani. Picha zake za ukutani, vinyago, na majengo yake yamesifiwa kwa umaridadi na uzuri wake. Hata hivyo, kwa mamia ya miaka watu hawakuruhusiwa kuona moja kati ya vitu vyake vyenye thamani zaidi. Kuna hati yenye thamani sana iliyohifadhiwa katika Maktaba ya Vatikani ambayo inatusaidia kuelewa vizuri zaidi sehemu za Neno la Mungu zilizoandikwa maelfu ya miaka mapema. Inaitwa Kodeksi ya Vatikani. *

Hati nyingine mbili za Biblia zinazosifiwa na wasomi ni Kodeksi ya Aleksandria na ya Sinai, ambazo zina historia yenye kusisimua ya jinsi ambavyo ziligunduliwa na kuokolewa ili zisiharibiwe. Kwa upande ule mwingine, chanzo cha Kodeksi ya Vatikani hakijulikani sana.

Hazina Iliyofichika

Kodeksi ya Vatikani ilitoka wapi? Ilirejelewa kwa mara ya kwanza katika orodha ya vitabu vilivyokuwa katika Maktaba ya Vatikani ya karne ya 15. Wasomi wamedokeza kwamba huenda iliandikiwa huko Misri, Kaisaria, au hata Roma. Hata hivyo, baada ya kuchanganua madokezo hayo mbalimbali, Profesa J. Neville Birdsall wa Chuo Kikuu cha Birmingham, Uingereza, alifikia mkataa huu: “Kwa ufupi, hatuwezi kuwa na hakika kuhusu tarehe hususa wala mahali ambapo Kodeksi ya Vatikani ilipopatikana, na pia, licha ya jitihada za wasomi, hatuna habari zozote kuhusu hati hiyo katika karne zinazotangulia karne ya kumi na tano.” Hata hivyo, Kodeksi ya Vatikani imesemwa kuwa mojawapo ya hati muhimu zaidi za Biblia. Kwa nini?

Kadiri miaka ilivyopita, wanakili waliingiza kasoro katika maandishi ya Biblia. Kwa sababu hiyo, tatizo kubwa linalowakabili watafsiri wanaotaka kutafsiri kutoka kwa hati zinazotegemeka, ni kupata hati zinazoonyesha kile kilichokuwapo katika maandishi ya awali. Hebu wazia jinsi wasomi walivyokuwa na hamu ya kuchunguza Kodeksi ya Vatikani, ambayo ilikuwa hati ya Kigiriki ya karne ya nne W.K., yaani, miaka isiyozidi 300 baada ya Biblia kukamilishwa! Kodeksi hiyo ina Maandiko yote ya Kiebrania na ya Kigiriki ya Kikristo, isipokuwa sehemu chache zilizopotea.

Kwa muda mrefu, wenye mamlaka huko Vatikani hawakutaka kuwaruhusu wasomi wa Biblia waitumie kodeksi hiyo. Msomi mwenye kuheshimika Sir Frederic Kenyon alisema hivi: “Mnamo 1843 [msomi wa Biblia Konstantin von] Tischendorf, baada ya kusubiri kwa miezi kadhaa, aliruhusiwa aichunguze kwa muda wa saa sita. . . . Mnamo 1845 msomi maarufu wa Uingereza Tregelles aliruhusiwa aichunguze lakini asinakili hata neno moja.” Tischendorf aliomba aione kodeksi hiyo tena, lakini alinyimwa ruhusa baada ya kunakili kurasa 20. Hata hivyo, kama Kenyon alivyoripoti, “baada ya kuomba tena aliruhusiwa kuichunguza kwa siku sita zaidi, hiyo ikiwa jumla ya siku kumi na nne, kwa saa tatu kila siku; na akitumia wakati huo vizuri kadiri alivyoweza, mnamo 1867 Tischendorf alifaulu kuchapisha nakala bora zaidi ya hati hiyo kuwahi kuchapishwa kufikia wakati huo.” Baadaye, Vatikani ilitokeza nakala bora zaidi ya kodeksi hiyo.

“Kuhifadhi kwa Uangalifu”

Maandishi ya Kodeksi ya Vatikani yanafunua nini? Kitabu kimoja (The Oxford Illustrated History of the Bible) kinasema kwamba maandishi hayo “yanaonyesha kuwa yalinakiliwa kwa uangalifu sana na kwa usahihi kabisa bila kukosea herufi.” Kitabu hichohicho kinaendelea kusema: “Hivyo tunaweza kusema kwamba maandishi hayo yalinakiliwa na wanakili hodari.”

Wasomi wawili maarufu sana ambao walivutiwa na ubora wa Kodeksi ya Vatikani ni B. F. Westcott na F.J.A. Hort. Tafsiri yao ya Biblia (New Testament in the Original Greek), iliyotolewa mwaka 1881, iliyotegemea hati ya Vatikani na ya Sinai, bado ndiyo maandishi ya msingi yaliyotumiwa ili kutokeza tafsiri kadhaa za kisasa za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, kutia ndani The Emphasised Bible, ya J. B. Rotherham, na Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

Hata hivyo, wachambuzi fulani walikuwa na maoni ya kwamba Westcott na Hort hawakupaswa kuiamini Kodeksi ya Vatikani. Je, kodeksi hiyo ilipatana na maandishi ya awali kwa usahihi? Mafunjo ya Bodmer yaliyotolewa kati ya miaka ya 1956 na 1961 yaliwasisimua wasomi kwa sababu mafunjo hayo yalitia ndani sehemu za Injili ya Luka na ya Yohana zilizotokezwa mapema katika karne ya tatu W.K. Je, mafunjo hayo yangethibitisha mambo ambayo yalikuja kuonekana kwenye Kodeksi ya Vatikani?

Philip B. Payne na Paul Canart waliandika hivi katika kitabu (Novum Testamentum) fulani: “kuna mambo mengi sana yanayofanana katika maandishi ya [Kodeksi ya] Vatikani na maandishi yanayopatikana katika mafunjo ya Bodmer. Kwa sababu hiyo, inapatana na akili kukata kauli kwamba mnakili wa kwanza wa [Kodeksi ya] Vatikani aliinakili kutoka kwa hati iliyofanana sana na mafunjo ya Bodmer. Kwa hiyo, lazima mnakili huyo awe alitumia hati ya zamani sana au ile iliyonakiliwa kutoka kwa hati ya zamani sana.” Profesa Birdsall alisema hivi: “Hati hizo mbili zinafanana sana. . . . [Kodeksi hiyo] imenakiliwa kwa uangalifu sana: wanakili wake wana sifa ya kuhifadhi kwa uangalifu maandishi yaliyopokewa.”

Msaada kwa Watafsiri

Bila shaka, kwa kuwa tu hati ni ya zamani kabisa haimaanishi kwamba inapatana sana maandishi ya awali. Hata hivyo, kulinganisha Kodeksi ya Vatikani na hati nyingine kumewasaidia sana wasomi kufahamu mambo yaliyokuwapo katika maandishi ya awali. Kwa mfano, sehemu inayopatikana ya Hati ya Sinai ambayo pia ilinakiliwa katika karne ya nne W.K., haina vitabu vingi vya historia kutoka Mwanzo hadi 1 Mambo ya Nyakati. Lakini kupatikana kwa vitabu hivyo katika Kodeksi ya Vatikani kumesaidia kuthibitisha kwamba vilikuwapo katika maandishi ya Biblia.

Kulingana na kitabu kimoja (The Oxford Illustrated History of the Bible), “masimulizi yanayozungumza kuhusu Kristo na Utatu” yalitokeza ubishi mwingi kati ya wasomi. Kodeksi ya Vatikani imewasaidia jinsi gani kuelewa masimulizi hayo?

Fikiria mfano. Yesu alisema hivi katika Yohana 3:13: “Hakuna mtu ambaye amepanda kuingia mbinguni ila yule aliyeshuka kutoka mbinguni, Mwana wa binadamu.” Watafsiri fulani wameongeza maneno “ambayo [au, ambaye] iko mbinguni.” Maneno hayo ya ziada yanadokeza kwamba Yesu alikuwa mbinguni na duniani wakati uleule, wazo linalounga mkono fundisho la Utatu. Maneno hayo yaliyoongezwa yanaonekana kwenye hati chache za kati ya karne ya tano na ya kumi W.K. Hata hivyo, kwa kuwa maneno hayo hayapatikani katika hati ya mapema ya Vatikani na ya Sinai, watafsiri wengi wa kisasa wameyaondoa maneno hayo. Hilo limesaidia kuondoa utata kuhusu Kristo na hivyo kupatana na Maandiko mengine. Badala ya kuwa katika sehemu mbili wakati uleule, Yesu alikuja kutoka mbinguni na angerudi mbinguni baada ya muda mfupi, na hivyo ‘kupanda’ kwenda kwa Baba yake.—Yohana 20:17.

Pia, Kodeksi ya Vatikani inatusaidia kuelewa mistari inayohusu kusudi la Mungu kwa dunia. Fikiria mfano huu. Kulingana na tafsiri ya Biblia ya Union Version, mtume Petro alitabiri kwamba “nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea.” (2 Petro 3:10) Tafsiri nyingine zinasema hivyo, kwa kuwa zinategemea maneno ya Kodeksi ya Aleksandria ya karne ya tano na hati nyingine za baadaye. Kwa sababu hiyo, wasomaji wengi wa Biblia wenye moyo mweupe wamefikia mkataa kwamba Mungu ataiharibu dunia.

Hata hivyo, karne moja hivi kabla ya Kodeksi ya Aleksandria kunakiliwa, Kodeksi ya Vatikani (na Hati ya Sinai iliyotolewa wakati huohuo) ilikuwa imeonyesha kuwa maneno hayo ya unabii wa Petro yanapaswa kuwa “dunia na kazi zilizo ndani yayo zitagunduliwa.” Je, hilo linapatana na sehemu nyingine za Biblia? Bila shaka! Dunia halisi “haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.” (Zaburi 104:5) Basi, dunia ‘itagunduliwa’ katika maana gani? Maandiko mengine yanaonyesha kwamba neno “dunia” linaweza kutumiwa kwa njia ya mfano. “Dunia” inaweza kuzungumza lugha na kuimba nyimbo. (Mwanzo 11:1; Zaburi 96:1) Kwa hiyo, “dunia” inaweza kuwakilisha wanadamu, au jamii ya wanadamu. Je, si jambo lenye kufariji kujua kwamba Mungu hataharibu sayari yetu lakini ataufunua uovu na kuumaliza pamoja na wale wanaouendeleza?

“Litadumu Mpaka Wakati Usio na Kipimo”

Kwa kusikitisha, kwa karne nyingi ni watu wachache sana walioruhusiwa kuiona Kodeksi ya Vatikani, na mara nyingi wasomaji wa Biblia walipotoshwa kuhusu ukweli wa mistari fulani ya Biblia. Hata hivyo, tangu iliponakiliwa, Kodeksi ya Vatikani na tafsiri nyingine za Biblia za kisasa zinazotegemeka zimewasaidia watu wanaotafuta kweli wajifunze kile ambacho Biblia inafundisha hasa.

Mara nyingi, wanakili wa mapema walitia ndani maneno haya: “Mkono ulioandika [maandishi haya] unaoza kaburini, lakini kilichoandikwa kinadumu milele.” Leo tunathamini jitihada nyingi za wanakili hao wasiojulikana. Lakini sifa za kuhifadhi Biblia zinamwendea Mtungaji wake, ambaye zamani za kale alimwongoza nabii wake kuandika: “Majani mabichi yamekauka, ua limenyauka; lakini kwa habari ya neno la Mungu wetu, litadumu mpaka wakati usio na kipimo.”—Isaya 40:8.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 2 Kodeksi ya Vatikani pia inaitwa Hati Na. 1209 ya Vatikani na wasomi wengi wanaiita “B.” Kodeksi zilikuwa hati za kwanza kuunganishwa kuwa kitabu. Ona habari yenye kichwa “Kutoka Kitabu cha Kukunjwa hadi Kodeksi—Jinsi Ambavyo Biblia Ilifanywa Kuwa Kitabu,” katika toleo la Juni 1, 2007 (1/6/2007) la gazeti hili.

[Sanduku katika ukurasa wa 20]

Kutambua Tarehe ya Hati za Zamani

Ingawa wanakili fulani waliandika tarehe ambayo walimaliza kazi yao, hati nyingi za Kigiriki hazina habari hiyo hususa. Kwa sababu hiyo, wasomi hutambua jinsi gani wakati ambapo hati ya Biblia ilitokezwa? Kama tu lugha na usanii unavyotofautiana kutoka kizazi kimoja hadi kingine, ndivyo ilivyo pia na mwandiko. Kwa mfano, katika karne ya nne mbinu ya kuandika kwa kutumia herufi kubwa zilizounganishwa ndiyo iliyokuwa ikitumiwa na ikaendelea kwa mamia ya miaka. Wasomi makini wanaolinganisha hati zisizokuwa na tarehe zilizoandikwa kwa herufi zilizounganishwa pamoja na hati nyingine zilizo na tarehe wanaweza kutambua wakati ambapo hati za zamani zilitokezwa.

Bila shaka mbinu hii ina matatizo yake. Profesa Bruce Metzger wa Seminari ya Mafunzo ya Kidini ya Princeton alisema hivi: “Kwa kuwa huenda mwandiko wa mtu usibadilike maishani mwake, si jambo linalopatana na akili kukadiria tarehe inayopungua miaka 50.” Kwa kutegemea uchunguzi huo wenye uangalifu, wasomi wengi wanakubaliana kwamba Kodeksi ya Vatikani ilitokezwa katika karne ya nne W.K.