Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ukristo Unaunga Mkono Vita?

Je, Ukristo Unaunga Mkono Vita?

Je, Ukristo Unaunga Mkono Vita?

“Ni kanuni gani ya maadili inayoonyesha kwamba vita ni dhambi? Kwa kweli, hapo kuna tashwishi.”—Oliver O’donovan, profesa wa maadili ya Kikristo

MCHORO unaoitwa Sacrifice, unaotegemea Vita vya Kwanza vya Ulimwengu uliowekwa katika Jumba la Makumbusho la Vita vya Kanada, unaonyesha askari waliouawa, waokokaji waliochoshwa na vita, na familia zao zikiwa nyumbani. Juu ya mchoro huo kuna mchoro wa Yesu Kristo akiwa kwenye msalaba. Watu fulani wameshangazwa kwamba Yesu, yule “Mkuu wa Amani,” amehusianishwa katika mchoro wa vita. (Isaya 9:6) Wengine wakiwa na shukrani kwa dhabihu ambazo mashujaa wa nchi zao walitoa, wanahisi kwamba Mungu na Mwana wake wanawatazamia Wakristo wapigane ili kulinda usalama na uhuru wa nchi yao.

Kwa karne nyingi, viongozi wa kidini wamehubiri ujumbe unaounga mkono vita. Katika mwaka wa 417 W.K., mwanatheolojia Augustine aliandika hivi: “Hupaswi kufikiri kwamba mtu anayetumika kama askari, akibeba silaha kwa ajili ya vita, hakubaliki machoni pa Mungu. . . . Wengine wanapigana na maadui wasioonekana wakisali kwa niaba yako, huku wewe uking’ang’ana kupigana na maadui wanaoonekana kwa niaba yao.” Katika karne ya 13, Thomas Aquinas alieleza kwamba “vita vinakubalika na ni vya haki maadamu vinawalinda maskini na taifa lote kutokana na hila za adui.”

Una maoni gani? Vita vinapoanzishwa kwa sababu zinazoonekana kuwa zinafaa—kulinda uhuru wa taifa au kuwakomboa wanaokandamizwa—je, Mungu anavikubali? Wakristo wanaweza kutegemea “kanuni gani ya maadili” ili kutambua maoni ya Mungu kuhusu jambo hilo?

Mfano Uliowekwa na Yesu Kristo

Je, inawezekana kupata maoni ya Mungu kuhusu jambo tata kama vile vita vinavyopiganwa siku zetu? Mtume Paulo alikubali kwamba tuna tatizo hilo, alipouliza: “‘Ni nani ameijua akili ya Yehova, ndipo amfundishe?’ Lakini sisi tunayo akili ya Kristo.” (1 Wakorintho 2:16) Ili kutusaidia, Yehova Mungu alimtuma Yesu duniani ili awe Kielelezo kwetu. Yale ambayo Yesu alisema na kutenda yalionyesha mawazo na njia ya Yehova ya kufanya mambo. Kwa hiyo, Yesu alisema nini kuhusu vita? Alikuwa na msimamo gani kuhusu vita?

Huenda ikaonekana kwamba sababu bora zaidi ya kupigana ingekuwa kulinda uhai na usalama wa Yesu Kristo. Mmoja wa mitume wake alihisi hivyo. Yesu aliposalitiwa na kukamatwa na umati uliokuwa na silaha katikati ya usiku, rafiki yake Petro ‘alinyoosha mkono wake akauchomoa upanga wake, akampiga mtumwa wa kuhani mkuu, akalikata sikio lake.’ Je, Petro alikuwa na sababu nzuri ya kutumia silaha? Yesu alimwambia Petro hivi: “Rudisha upanga wako mahali pake, kwa maana wale wote wanaouchukua upanga wataangamia kwa upanga.”—Mathayo 26:47-52.

Haishangazi kwamba Yesu alimwambia hivyo. Miaka miwili mapema, Yesu alikuwa amesema: “Ninyi mlisikia kwamba ilisemwa, ‘Mpende jirani yako na kumchukia adui yako.’ Hata hivyo, mimi ninawaambia ninyi: Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi; ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni, kwa kuwa yeye hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mathayo 5:43-45) Je, inapatana na akili kufikiri kwamba Mkristo anaweza kuwapenda adui zake na hata kusali kwa niaba yao huku akipigana nao?

Historia inafunua kwamba Wakristo walikuwa na maadui wengi. Kwa mfano, Waroma walimhukumu na kumwua Yesu Kristo. Muda mfupi baadaye, mtu yeyote aliyedai kuwa Mkristo angehukumiwa adhabu ya kifo. Yesu aliona kwamba huenda Wakristo watashawishiwa kuchukua silaha na kuasi dhidi ya ukandamizaji wa Waroma, kama Wayahudi fulani walivyokuwa wamefanya. Kwa hiyo, aliwaambia hivi wafuasi wake: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:16) Wakristo walichagua kutounga mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa. Hakuna kitu chochote ambacho kingewapa haki ya kujiunga katika jeshi, iwe ni ukosefu wa haki, uhai wao kutishwa, au nchi yao kutishwa.

Wanaunga Mkono Ufalme wa Mungu

Wakristo wa kweli waliepuka kuuunga mkono upande wowote kama vile Yesu alivyotaka wafanye. Fikiria kilichotendeka Ikoniamu, jiji la kale huko Asia Ndogo. “Watu wa mataifa na pia Wayahudi pamoja na watawala wao walipojaribu kwa jeuri kuwatendea kwa dharau [Paulo na Barnaba] na kuwatupia mawe, wao, walipojulishwa jambo hilo, wakakimbilia majiji ya Likaonia, Listra na Derbe na nchi yenye kuzunguka; na huko wakaendelea kutangaza habari njema.” (Matendo 14:5-7) Ona kwamba walipopatwa na upinzani mkali, Wakristo hawakuchukua silaha ili kujilinda, wala hawakulipiza kisasi. Badala yake waliendelea kuhubiri “habari njema.” Walikuwa na habari gani njema za kuwaambia watu?

Wakristo walihubiri ujumbe uleule ambao Yesu alihubiri. Alisema hivi: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu.” (Luka 4:43) Yesu na wafuasi wake waliunga mkono Ufalme wa Mungu. Kristo hakutumia jeshi la taifa kutetea Ufalme huo. “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu,” akasema. “Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, watumishi wangu wangepigana ili nisitiwe mikononi mwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu hautoki katika chanzo hiki.”—Yohana 18:36.

‘Muwe na Upendo Kati Yenu Wenyewe’

Kunapokuwa na vita inajulikana kwamba waabudu wa kweli hawaungi mkono upande wowote. Yesu alisema: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Mamilioni ya watu wamefurahi kuwafahamu watu wanaoonyesha upendo kama huo, hata wanapodhihakiwa, kufungwa, au kuuawa kwa sababu wamekataa kuchukua silaha.

Huko Ulaya wakati wa utawala wa Wanazi, maofisa waliwafunga Mashahidi wa Yehova 10,000 hivi kwa sababu walikataa kuunga mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa, kutia ndani 3,000 ambao walipelekwa kwenye kambi za mateso. Wakati huohuo, zaidi ya Mashahidi 4,300 nchini Marekani walifungwa kwa kukataa kujiunga na jeshi. Hakuna Shahidi Mjerumani au Mmarekani aliyechukua silaha na kupigana na ndugu zake Wakristo au mtu yeyote. Hawangeweza kufanya hivyo na bado wadai kwamba wana upendo kati yao na kwamba wanawapenda wanadamu wenzao.

Watu wengi wanaamini kwamba vita ni muhimu ili kujilinda. Lakini fikiria jambo hili: Ingawa Wakristo wa karne ya kwanza waliteswa vikali na wakakataa kulipiza kisasi, bado waliokoka. Milki ya Roma yenye nguvu haikuweza kuwaangamiza Wakristo. Hata leo, Wakristo wa kweli wanaendelea kuongezeka na hawaungi mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa. Badala ya kulipiza kisasi, wao humtegemea Mungu awasaidie. Neno lake, Biblia, linasema hivi: “Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi ghadhabu; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’”—Waroma 12:19.

[Sanduku katika ukurasa wa 30]

VITA VILIVYOBARIKIWA NA MUNGU

Israeli la kale, taifa ambalo Mungu alichagua kwa njia ya pekee karne nyingi kabla ya Ukristo kuanzishwa, liliruhusiwa nyakati nyingine kukusanya jeshi na kupigana. Kabla ya kuingia Kanaani, nchi ambayo Mungu alikuwa amemwahidi Abrahamu, Waisraeli waliambiwa hivi: ‘Yehova Mungu wako hakika atayatia hayo mataifa saba mkononi mwako, nawe utayashinda. Unapaswa kuyaangamiza. Usifanye agano lolote pamoja nayo wala kuyaonyesha kibali chochote.’ (Kumbukumbu la Torati 7:1, 2) Hivyo, Yoshua, Jenerali Mwisraeli, aliyashinda mataifa hayo ya maadui “kama vile Yehova Mungu wa Israeli alivyokuwa ameamuru.”—Yoshua 10:40.

Je, Waisraeli walipigana vita hivyo kwa ukatili ili kunyakua ardhi ya mataifa mengine kwa pupa? Sivyo hata kidogo. Mataifa hayo yalikuwa yamejaa ibada ya sanamu, umwagaji wa damu, na matendo mengine ya ngono yaliyopotoka. Hata watoto walitolewa dhabihu kwa kutupwa motoni. (Hesabu 33:52; Yeremia 7:31) Utakatifu, haki, na upendo wa Mungu kuelekea watu wake ulimchochea kuondoa mazoea yote machafu katika nchi. Hata hivyo, Yehova alichunguza mioyo ya kila mtu, jambo ambalo hakuna kamanda wa jeshi anayeweza kufanya leo, na hivyo hakuwaua wale waliokuwa tayari kuacha njia zao mbaya na kumtumikia.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Je, Yesu aliwatazamia wafuasi wake wapigane ili kumlinda au kuwalinda Wakristo wenzao?

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kikundi cha Mashahidi wa Yehova baada ya kufunguliwa kutoka katika kambi ya mateso ya Buchenwald katika mwaka wa 1945