Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuhusu Maisha ya Familia

Kuhusu Maisha ya Familia

Tunayojifunza Kutoka kwa Yesu

Kuhusu Maisha ya Familia

Ni maoni gani kuhusu ndoa ambayo yanafanya familia ziwe na furaha?

Ndoa ni kifungo kitakatifu. Yesu alipoulizwa ikiwa mtu anaruhusiwa kumtaliki mwenzi wake wa ndoa, alisema hivi: “Je, hamkusoma kwamba yeye aliyewaumba hao kutoka mwanzo aliwafanya mwanamume na mwanamke na kusema, ‘Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’? Hivi kwamba wao si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe. . . . Mtu yeyote anayemtaliki mke wake na kumwoa mwingine, ila kwa sababu ya uasherati, anafanya uzinzi.” (Mathayo 19:4-6, 9) Wenzi wa ndoa wanapofuata shauri la Yesu na kila mmoja wao anapokuwa mwaminifu kwa mwenzake, wote katika familia wanahisi wakiwa salama na wenye furaha.

Kwa nini kumpenda Mungu kunafanya familia ziwe na furaha?

Yesu alisema: “‘Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’ Hii ndiyo amri iliyo kuu na ya kwanza.” Ni amri gani ya pili iliyo kuu? Yesu alisema hivi: “Mpende jirani yako [kutia ndani watu wanaoishi karibu zaidi nawe—familia yako] kama wewe mwenyewe.” (Mathayo 22:37-39) Kwa hiyo, siri ya kupata furaha katika familia ni kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu kwa sababu kumpenda Mungu kunatuchochea kupendana.

Waume na wake wanaweza kufurahishana jinsi gani?

Waume wanapofuata mfano wa Yesu, wanafanya wake zao wawe wenye furaha. Yesu alijidhabihu katika kumwonyesha upendo mke wake wa mfano, yaani, kutaniko. (Waefeso 5:25) Yesu alisema: “Mwana wa Mtu hakuja kutumikiwa, bali kutumikia.” (Mathayo 20:28, Biblia Habari Njema) Yesu hakuwatawala kamwe kimabavu au kwa ukali wale waliokuwa chini yake bali aliwaburudisha. (Mathayo 11:28) Kwa hiyo, waume wanapaswa kutumia mamlaka yao kwa njia ya fadhili ambayo inawafaidi wote katika familia.

Wake pia wanaweza kufaidika kutokana na mfano wa Yesu. Biblia inasema kwamba “kichwa cha Kristo ni Mungu.” Pia inasema kwamba “kichwa cha mwanamke ni mwanamume.” (1 Wakorintho 11:3) Yesu hakuona kwamba kwa kujitiisha kwa Mungu alikuwa akijishushia heshima. Alimheshimu sana Baba yake. Yesu alisema hivi: “Sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza.” (Yohana 8:29) Mke anayejitiisha chini ya ukichwa wa mume wake kwa sababu anampenda na kumheshimu Mungu anachangia sana furaha katika familia yake.

Wazazi wanaweza kujifunza nini kutokana na maoni ya Yesu kuhusu watoto?

Yesu alitumia wakati pamoja na watoto na alipendezwa kujua mawazo na hisia zao. Biblia inasema: “Yesu akawaita wale watoto, akisema: ‘Waacheni watoto wachanga waje kwangu.’” (Luka 18:15, 16) Pindi moja, watu waliwashutumu wavulana fulani ambao walisema kwa sauti kuhusu imani yao katika Yesu. Lakini Yesu aliwapongeza vijana hao, akawaambia hivi wale waliokuwa wakiwashutumu: “Je, ninyi hamkusoma hili kamwe, ‘Kutoka katika kinywa cha watoto na wanaonyonya umetoa sifa’?”—Mathayo 21:15, 16.

Watoto wanaweza kujifunza nini kutoka kwa Yesu?

Yesu aliwawekea watoto mfano mzuri kuhusu kupendezwa na mambo ya kiroho. Alipokuwa na umri wa miaka 12, alipatikana “katika hekalu, ameketi katikati ya walimu, akiwasikiliza na kuwauliza maswali.” Kulikuwa na matokeo gani? “Wote waliokuwa wakimsikiliza walikuwa wakishangazwa daima na uelewaji wake na majibu yake.” (Luka 2:42, 46, 47) Hata hivyo, ujuzi wa Yesu haukumfanya awe na kiburi. Badala yake ulimfanya awaheshimu wazazi wake. Biblia inasema hivi: “Akaendelea kujitiisha kwao.”—Luka 2:51.

Kwa habari zaidi, ona sura ya 14 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? *

[Maelezo ya chini]

^ fu. 14 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.