Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mashahidi wa Yehova Ni Dini ya Kiprotestanti?

Je, Mashahidi wa Yehova Ni Dini ya Kiprotestanti?

Wasomaji Wetu Wanauliza

Je, Mashahidi wa Yehova Ni Dini ya Kiprotestanti?

Mashahidi wa Yehova hawajioni kuwa dini ya Kiprotestanti. Kwa nini?

Uprotestanti ulianza karne ya 16 huko Ulaya katika jitihada za kuleta marekebisho katika Dini ya Katoliki. Neno “Mprotestanti” lilitumiwa kwanza kuwahusu wafuasi wa Martin Luther kwenye mkutano uliofanywa katika mji wa Speyer mwaka wa 1529. Tangu wakati huo, neno hilo limetumiwa kwa ujumla kuwahusu wote wanaofuata kanuni na mafundisho yaliyoanzishwa wakati wa hayo Marekebisho Makubwa ya Kidini. Hivyo, kamusi Merriam-Webster’s Collegiate Dictionary, Chapa ya 11, inafafanua neno Mprotestanti kuwa “mshiriki wa mojawapo ya dini nyingi zinazopinga mamlaka ya ulimwenguni pote ya Papa na kuunga mkono mafundisho yaliyoanzishwa wakati wa yale Marekebisho Makubwa ya Kidini, kama vile, fundisho la kwamba mtu anaweza kupata kibali cha Mungu kwa msingi wa imani peke yake, na kwamba waamini wote ni makuhani, na Biblia ndiyo chanzo pekee cha kweli iliyofunuliwa.”

Ingawa Mashahidi wa Yehova hawatambui mamlaka ya ulimwenguni pote ya papa na wanaunga mkono kwa moyo wote mamlaka ya Biblia, wanatofautiana na dini za Kiprotestanti katika njia nyingi kubwa. Kwa kweli, kitabu The Encyclopedia of Religion kinasema kwamba Mashahidi wa Yehova wako “tofauti kabisa.” Fikiria njia tatu zinazowafanya wawe tofauti.

Kwanza, ingawa dini za Kiprotestanti zinakataa mambo fulani katika ibada ya Wakatoliki, viongozi wa yale Marekebisho ya Kidini waliendelea kufuata mafundisho fulani ya Wakatoliki, kama vile Utatu, moto wa mateso, na kutokufa kwa nafsi ya wanadamu. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba mafundisho hayo yanapingana na Biblia na pia yanaeneza maoni yaliyopotoka kumhusu Mungu.—Ona ukurasa wa 4-7 wa gazeti hili.

Pili, Mashahidi wa Yehova hawaungi mkono jitihada za kupinga mafundisho ya dini, lakini wanaunga mkono jitihada za kuwafundisha watu mambo yenye faida. Wanachukua kwa uzito shauri hili la Biblia: “Mtumishi wa Bwana asigombane. Anapaswa kuwa mpole kwa watu wote, mwalimu mwema na mvumilivu, ambaye ni mpole anapowaonya wapinzani wake.” (2 Timotheo 2:24, 25, Biblia Habari Njema) Mashahidi wa Yehova wanafunua waziwazi tofauti kati ya mafundisho ya Biblia na mambo ambayo vikundi vingi vya kidini vinafundisha. Hata hivyo, kusudi lao si kurekebisha dini nyingine. Badala yake, kusudi lao ni kuwasaidia watu mmoja-mmoja walio wanyoofu wapate ujuzi sahihi kumhusu Mungu na Neno lake, Biblia. (Wakolosai 1:9, 10) Watu wenye imani tofauti wanapokataa kabisa kukubaliana nao, Mashahidi wa Yehova wanaepuka kushiriki katika ubishi usio na faida yoyote.—2 Timotheo 2:23.

Tatu, tofauti na dini za Kiprotestanti, ambazo zimegawanyika katika mamia ya vikundi vya kidini, Mashahidi wa Yehova wameendelea kuwa na undugu wenye umoja duniani pote. Inapohusu mafundisho ya Biblia, Mashahidi wa Yehova katika nchi zaidi ya 230 wanafuata shauri la mtume Paulo la ‘kusema kwa upatano.’ Hakuna migawanyiko yoyote katikati yao. Badala yake, ‘wameunganishwa kikweli katika akili ileile na katika njia ileile ya kufikiri.’ (1 Wakorintho 1:10) Mashahidi wote wanajitahidi sana kwa pamoja “kuushika umoja wa roho katika kifungo chenye kuunganisha cha amani.”—Waefeso 4:3.