Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Kwa nini mwanamume ambaye alipenda sana michezo, kuendesha pikipiki na kutumia dawa za kulevya aliamua kuwa mhudumu wa wakati wote? Ni nini kilichomchochea mtu aliyepata riziki kwa kucheza-kamari aache zoea hilo na kufanya kazi inayoheshimika ili aitegemeze familia yake? Ni nini kilichomsukuma mwanamke fulani kijana aliyelelewa na wazazi ambao ni Mashahidi wa Yehova afikirie tena njia yake ya maisha baada ya kuacha viwango vya Biblia? Fikiria mambo ambayo watu hao wanasema.

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU

JINA: TERRENCE J. O’BRIEN

UMRI: 57

NCHI: AUSTRALIA

HISTORIA: ALITUMIA DAWA MBALIMBALI ZA KULEVYA, ALIPENDA PIKIPIKI

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilipokuwa mtoto tuliishi katika jiji lenye shughuli nyingi la Brisbane, jiji kuu la Queensland. Familia yetu ilikuwa ya Kikatoliki, lakini nilipokuwa na umri wa miaka minane, tuliacha kwenda kanisani na hatukuzungumza kamwe kuhusu dini. Nilipokuwa na umri wa miaka kumi, familia yetu ilihamia mji wa Gold Coast huko Australia. Tuliishi karibu na ufuo wa bahari, na nilitumia miaka yangu ya mapema ya ujana kucheza mchezo wa kuteleza kwenye mawimbi na kuogelea.

Hata hivyo, maisha yangu ya utotoni hayakuwa yenye furaha. Baba yangu aliiacha familia yetu nilipokuwa na umri wa miaka minane. Mama yangu aliolewa tena, na pombe na ugomvi yalikuwa mambo ya kawaida katika nyumba yetu. Usiku mmoja, baada ya wazazi wangu kugombana vikali, niliketi kwenye kitanda changu na kuapa kwamba ikiwa siku moja nitaoa, sitagombana kamwe na mke wangu. Hata ingawa tulikuwa na matatizo ya kifamilia, tulikuwa na uhusiano wa karibu katika familia yetu ambayo ilikuwa na watoto sita, mama, na baba wa kambo.

Katika miaka yangu ya mwisho-mwisho ya ujanani, vijana wenzangu waliasi mamlaka. Walitumia bangi, tumbaku, na dawa nyingine za kulevya, nao walikunywa pombe kupindukia. Niliishi maisha ya kutojali kama vijana wenzangu. Pia, nilipenda kuendesha pikipiki. Hata ingawa nilipata aksidenti chache mbaya sana, bado nilipenda pikipiki, nikaamua kuvuka nchi ya Australia kwa pikipiki yangu.

Ijapokuwa nilikuwa na uhuru mwingi, mara nyingi nilishuka moyo nilipofikiria hali ya ulimwengu na jinsi ambavyo watu wengi hawakujali matatizo ya wanadamu. Nilitamani sana kujua ukweli kumhusu Mungu, dini, na hali za ulimwengu. Lakini nilipowauliza makasisi wawili Wakatoliki maswali yangu, majibu yao yalinikatisha tamaa. Nilizungumza habari hizo pamoja na wahudumu mbalimbali Waprotestanti lakini bado nilikatishwa tamaa na majibu yao. Kisha rafiki yangu mmoja akapanga ili nikutane na Eddie, ambaye ni Shahidi wa Yehova. Nilizungumza na Eddie kwa vipindi vinne, na kila mara alitumia Biblia kujibu maswali yangu. Tangu tulipokuwa na mazungumzo ya kwanza, nilijua kwamba nilikuwa nimepata kitu cha pekee. Hata hivyo, wakati huo sikuona haja ya kubadili maisha yangu kwa njia yoyote ile.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Katika safari yangu ya kuvuka Australia, nilizungumza na Shahidi mwingine, ambaye nilikutana naye njiani. Lakini niliporudi Queensland, sikuweza kuwasiliana tena na Mashahidi kwa miezi sita.

Kisha siku moja nilipokuwa nikirudi nyumbani kutoka kazini, niliona wanaume wawili waliovalia vizuri wakiwa wamebeba mikoba wakitembea barabarani, nikakisia kwamba walikuwa Mashahidi wa Yehova. Nilienda kuzungumza nao na nikagundua kwamba ni Mashahidi wa Yehova, kisha nikawaomba wanifundishe Biblia. Na mara moja nilianza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi na hata nilihudhuria kusanyiko kubwa huko Sydney mwaka wa 1973. Hata hivyo, wakati familia yangu, hasa mama yangu, walipopata habari kuhusu nilichokuwa nikifanya, walivunjika moyo sana. Kwa sababu hiyo na kwa sababu nyingine, niliacha kushirikiana na Mashahidi. Kwa mwaka mmoja, niliendelea na mchezo mwingine niliopenda sana, mchezo wa kriketi.

Hata hivyo, mwishowe nilitambua kwamba wakati pekee ambao kwa kweli nilikuwa na furaha ni wakati nilipokuwa nikijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Niliwatafuta tena nikaanza kuhudhuria mikutano. Pia, niliacha kushirikiana na marafiki wangu waliokuwa wakitumia dawa za kulevya.

Kwa kweli kile kilichonichochea kufanya mabadiliko hayo ni mambo niliyojifunza kumhusu Ayubu anayetajwa katika Biblia. Bill, Shahidi mmoja mzee kwa umri aliye thabiti lakini mwenye fadhili alikuwa akijifunza na mimi Biblia kwa ukawaida. Baada ya kujifunza simulizi la Ayubu, Bill aliniomba nitaje mtu mwingine ambaye Shetani amedai kwamba anamtumikia Mungu kwa moyo nusunusu tu. (Ayubu 2:3-5) Niliwataja watu wote walio katika Biblia ambao niliwajua, na kwa subira Bill alinijibu hivi: “Ndiyo, ndiyo, wao pia.” Kisha akaniangalia machoni na kusema, “Shetani anasema hivyo kukuhusu wewe pia!” Nilishtuka sana. Kabla ya kuanza kujifunza, nilijua kwamba mambo niliyokuwa nikijifunza yalikuwa ya kweli. Lakini sasa nilielewa kwa nini nilipaswa kutenda kupatana na mambo niliyokuwa nikijifunza. Miezi minne baadaye, nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Ninaogopa ninapofikiria jinsi ambavyo maisha yangu yangekuwa sasa ikiwa singejifunza kuishi kupatana na viwango vya Biblia. Inaelekea kwamba, ningekuwa nimekufa. Wengi kati ya marafiki wangu wa zamani walikufa kwa sababu ya kutumia dawa za kulevya au pombe. Pia, walikuwa na matatizo katika ndoa zao. Ninaona kwamba maisha yangu yangekuwa kama yao.

Sasa nimeoa, na nikiwa na mke wangu, Margaret, tunafurahia kutumika katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Australia. Hakuna mtu yeyote wa familia yetu ambaye amejiunga na mimi katika kumwabudu Yehova. Hata hivyo, kwa miaka mingi sasa, mimi na Margaret tumekuwa na pendeleo la kujifunza Biblia pamoja na watu mbalimbali na wenzi fulani wa ndoa ambao wamebadili maisha yao, kama nilivyobadili yangu. Kwa njia hiyo, tumepata marafiki wengi wazuri. Kwa kuongezea, Margaret, ambaye alilelewa na wazazi ambao ni Mashahidi, amenisaidia kutimiza nadhiri niliyoweka miaka 40 hivi iliyopita. Kwa miaka zaidi ya 25, tumefurahia maisha ya ndoa. Si kwamba sikuzote tunakubaliana katika kila jambo, lakini kufikia sasa hatujagombana. Sote wawili tunahisi kwamba Biblia imetusaidia sana katika jambo hilo.

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU

JINA: MASAHIRO OKABAYASHI

UMRI: 39

NCHI: JAPANI

HISTORIA: ALICHEZA KAMARI

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa katika mji mdogo wa Iwakura, ambao uko umbali wa nusu saa kwa gari-moshi kutoka mji wa Nagoya. Ninakumbuka kwamba mama na baba yangu walikuwa watu wenye fadhili sana. Hata hivyo, baadaye nilipata habari kwamba baba yangu alikuwa yakuza, au jambazi, ambaye kwa muda fulani aliitegemeza familia yetu ya watu watano kwa kufanya kazi ya wizi. Kila siku alilewa kupindukia, na nilipokuwa na umri wa miaka 20, alikufa kwa ugonjwa wa ini unaosababishwa na kunywa pombe kupindukia.

Baba yangu alikuwa wa asili ya Korea, kwa hiyo mara nyingi familia yetu ilibaguliwa na watu katika eneo letu. Jambo hilo pamoja na matatizo mengine yalifanya maisha yangu ya ujana yawe magumu sana. Nilijiunga na shule ya sekondari lakini nilihudhuria tu mara chache, kisha nikaacha baada ya mwaka mmoja. Tayari polisi walikuwa na rekodi yangu, na pia kwa sababu nilikuwa na mzazi Mkorea ilikuwa vigumu sana kwangu kupata kazi. Mwishowe, nilipata kazi lakini niliumia magoti na hivyo singeweza kufanya kazi inayohitaji nguvu.

Nilianza kupata riziki kwa kucheza pachinko, mchezo wa kamari ambao unatumia mashine yenye mipira midogo. Wakati huo, nilikuwa nikiishi na msichana ambaye alitaka nipate kazi nzuri halafu nimuoe. Lakini nilikuwa nikipata pesa nyingi sana kwa kucheza kamari, nami sikutaka kubadili njia yangu ya maisha.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Siku moja, Shahidi wa Yehova alikuja kwenye mlango wetu na kuniachia kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? (La vie: comment est-elle apparue? Évolution ou création?) Ilikuwa mara yangu ya kwanza kabisa kufikiria swali hilo. Hata hivyo, baada ya kusoma kitabu hicho, nilikubali kujifunza mengi zaidi kuhusu Biblia. Sikuzote nilijiuliza ni nini kinachotukia mtu anapokufa. Majibu yaliyo wazi ambayo nilipata katika Biblia kuhusu habari hiyo na habari nyingine yalinifanya nihisi ni kana kwamba magamba yalianguka kutoka kwenye macho yangu.

Niliona kwamba nilihitaji kutumia mambo niliyokuwa nikijifunza katika Biblia. Kwa hiyo, nilihalalisha ndoa yangu, nikaacha kuvuta sigareti, nikanyoa nywele zangu ndefu ambazo zilikuwa zimepakwa rangi ya manjano, kisha nikaanza kuvalia vizuri. Niliacha pia kucheza kamari.

Haikuwa rahisi kufanya mabadiliko hayo yote. Kwa mfano, singeweza kuacha kuvuta sigareti kwa uwezo wangu mwenyewe. Lakini nilifaulu kuacha niliposali kwa bidii na kumtegemea Yehova Mungu. Pia, kazi ya kwanza niliyopata baada ya kuacha kamari haikunipendeza hata kidogo. Nilipata nusu tu ya pesa ambazo nilipata katika mchezo wa kamari, nayo ilikuwa kazi ngumu na yenye kuchosha. Andiko moja la Biblia ambalo lilinisaidia kuvumilia wakati huo mgumu ni Wafilipi 4:6, 7. Linasema hivi: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” Ahadi hiyo imetimia mara nyingi katika maisha yangu.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Nilipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, mke wangu hakufurahi. Lakini alipoona mabadiliko makubwa ambayo nilikuwa nikifanya katika mwenendo wangu, alijiunga nami kila mara nilipokuwa nikijifunza, akaanza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova pamoja nami. Hivi sasa sote wawili ni Mashahidi wa Yehova. Ni baraka kubwa kama nini kumtumikia Mungu tukiwa pamoja!

Kabla ya kujifunza Biblia, nilifikiri kwamba nilikuwa na furaha. Lakini sasa, ninajua maana ya furaha ya kweli. Kuishi kupatana na viwango vya Biblia si jambo rahisi, lakini nina hakika kwamba ndiyo njia bora zaidi ya maisha.

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU

JINA: ELIZABETH JANE SCHOFIELD

UMRI: 35

NCHI: UINGEREZA

HISTORIA: ALIPONDA RAHA KILA MWISHO-JUMA

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa katika mji mdogo wa Hardgate, nje tu ya jiji la Glasgow, Scotland. Nilipokuwa na umri wa miaka saba, mama yangu, ambaye sasa alikuwa Shahidi wa Yehova, alianza kunifundisha Biblia. Hata hivyo, kufikia umri wa miaka 17 nilifurahia zaidi kushirikiana na marafiki wangu wa shule na kwenda nao katika vilabu vya usiku, kusikiliza muziki wenye mdundo mzito, na kunywa pombe. Sikufikiria kamwe mambo ya kiroho. Nilipenda sana kuponda raha kila mwisho-juma. Hata hivyo, mambo yalibadilika nilipokuwa na umri wa miaka 21.

Nilienda kuwatembelea watu fulani wa ukoo huko Ireland Kaskazini. Nilipokuwa huko, nilishuhudia Maandamano ya Orange yaliyofanywa na Waprotestanti. Nilishtuka sana nilipoona chuki kali na uadui ambao ulikuwapo wakati huo kati ya Waprotestanti na Wakatoliki. Kwa kweli, chuki hiyo ilinisaidia kufikiria maisha yangu. Nilikumbuka mambo ambayo mama yangu alinifundisha kutoka katika Biblia na nilijua kwamba Mungu hawezi kamwe kuwakubali watu wanaopuuza viwango vyake vya upendo. Kisha nikagundua kwamba nilikuwa nikitumia maisha yangu kufuatia mapendezi yangu na kupuuza njia ambayo Mungu alitaka nitumie maisha yangu. Niliamua kwamba nikirudi nyumbani huko Scotland, nitachunguza kwa makini sana mambo ambayo Biblia inafundisha.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Mara ya kwanza niliporudi kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova katika mji wetu, nilikuwa na woga na wasiwasi. Hata hivyo, kila mtu alinikaribisha. Nilipoanza kutumia mambo niliyokuwa nikijifunza kutoka katika Biblia, dada mmoja wa kutaniko mwenye fadhili alipendezwa nami kwa njia ya pekee. Alinisaidia sana kuhisi tena kwamba mimi ni sehemu ya kutaniko. Marafiki ambao nilishirikiana nao zamani waliendelea kunialika ili niende nao kwenye vilabu vya usiku, lakini niliwaambia kwamba nimeazimia kuishi kupatana na viwango vya Biblia. Mwishowe, waliacha kunitafuta.

Zamani, niliiona Biblia kuwa kitabu cha sheria tu. Sasa mtazamo wangu ulikuwa umebadilika. Nilianza kuwaona watu wanaotajwa katika Biblia kuwa watu halisi ambao walikuwa na hisia na udhaifu kama wangu. Wao pia walikuwa wamekosea katika njia mbalimbali, lakini Yehova Mungu aliwasamehe walipomwomba msamaha kikweli. Sasa nilikuwa na hakika kwamba hata ingawa nilimwacha Mungu nilipokuwa kijana, angenisamehe na kusahau makosa yangu ya zamani ikiwa ningejitahidi sana kumpendeza.

Mwenendo wa mama yangu pia ulinivutia sana. Hata ingawa nilikuwa nimemwacha Mungu, mama hakumwacha kamwe. Mfano wake katika kudumisha ushikamanifu ulinifanya nitambue kwamba kumtumikia Yehova ndiyo njia bora zaidi ya maisha. Nilipokuwa mtoto, sikufurahia kamwe kuhubiri nyumba kwa nyumba pamoja na mama yangu, na sikufikiria kamwe ninaweza kutumia saa nyingi kuwahubiria watu. Hata hivyo, sasa niliamua kuona ikiwa ahadi ya Yesu kwenye Mathayo 6:31-33 ni ya kweli. Alisema hivi: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ . . . Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote. Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.” Muda mfupi baada ya kubatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova, niliacha kazi ya wakati wote ya mshahara, nikapata kazi ya muda, kisha nikawa mhudumu wa wakati wote.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Nilipokuwa nikiponda raha kila mwisho-juma nikiwa kijana, sikuhisi kamwe nimeridhika. Maisha yangu hayakuwa na kusudi lolote. Sasa ninahisi kwamba nimeridhika kwa kuwa ninamtumikia Yehova kikamili. Maisha yangu yana kusudi na maana. Sasa nimeolewa, na mimi na mume wangu tunatembelea makutaniko ya Mashahidi wa Yehova kila juma, ili kuyatia moyo. Ninaona kazi hii kuwa pendeleo kubwa zaidi katika maisha yangu. Ninamshukuru sana Yehova kwa sababu amenipa nafasi nyingine ya kumtumikia!

[Blabu katika ukurasa wa 27]

“Tangu tulipokuwa na mazungumzo ya kwanza, nilijua kwamba nilikuwa nimepata kitu cha pekee. Hata hivyo, wakati huo sikuona haja ya kubadili maisha yangu kwa njia yoyote ile”

[Blabu katika ukurasa wa 29]

“Singeweza kuacha kuvuta sigareti kwa uwezo wangu mwenyewe. Lakini nilifaulu kuacha niliposali kwa bidii na kumtegemea Yehova Mungu”

[Blabu katika ukurasa wa 30]

“Zamani, niliiona Biblia kuwa kitabu cha sheria tu. Sasa mtazamo wangu ulikuwa umebadilika. Nilianza kuwaona watu wanaotajwa katika Biblia kuwa watu halisi ambao walikuwa na hisia na udhaifu kama wangu”