Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Boresha Sala Zako Kupitia Funzo la Biblia

Boresha Sala Zako Kupitia Funzo la Biblia

Boresha Sala Zako Kupitia Funzo la Biblia

“Ah, tafadhali, Yehova, tega sikio lako kwa sala ya mtumishi wako.”—NEH. 1:11.

1, 2. Kwa nini tutafaidika tukichunguza sala mbalimbali zilizoandikwa katika Biblia?

SALA na funzo la Biblia ni mambo ya maana sana katika ibada ya kweli. (1 The. 5:17; 2 Tim. 3:16, 17) Bila shaka, Biblia si kitabu cha sala. Hata hivyo, ina sala nyingi, kutia ndani zile zinazopatikana katika kitabu cha Zaburi.

2 Unaposoma na kujifunza Biblia, inaelekea utapata sala zinazohusu hali unazokabili. Kwa kweli, unapotumia mawazo yaliyo katika sala zilizoandikwa katika Maandiko unaboresha sala zako. Unaweza kujifunza nini kutokana na wale ambao maombi yao ya kutaka msaada yalijibiwa na kutokana na mambo waliyotaja katika sala zao?

Tafuta na Kufuata Mwongozo wa Mungu

3, 4. Mtumishi wa Abrahamu alitumwa kufanya nini, na tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yehova alivyoongoza mambo?

3 Funzo lako la Biblia linakusaidia kuona kwamba unapaswa sikuzote kuomba mwongozo wa Mungu. Ona yale yaliyotukia wakati mzee wa ukoo Abrahamu alipomtuma mtumishi wake mwenye umri mkubwa zaidi, inaelekea Eliezeri, kwenda Mesopotamia ili kumtafutia Isaka mke anayemwogopa Mungu. Wanawake walipokuwa wakichota maji kwenye kisima fulani, mtumishi huyo alisali hivi: “Yehova . . . , litakalotokea ni kwamba mwanamke kijana ambaye nitamwambia, ‘Tafadhali, shusha mtungi wako wa maji ili ninywe,’ na ambaye kwa kweli atasema, ‘Kunywa, na pia nitanywesha ngamia zako,’ huyo ndiye utakayemchagulia mtumishi wako, Isaka; na kwa hilo unijulishe kwamba umefanya upendo mshikamanifu kwa bwana wangu.”—Mwa. 24:12-14.

4 Sala ya mtumishi wa Abrahamu ilijibiwa wakati Rebeka alipowanywesha ngamia wake. Baadaye, Rebeka alienda Kanaani pamoja na mtumishi huyo na hivyo akawa mke mpendwa wa Isaka. Bila shaka, huwezi kumtazamia Mungu akupe ishara ya pekee. Hata hivyo, atakuongoza maishani ikiwa unasali na kuazimia kuongozwa na roho yake.—Gal. 5:18.

Sala Inasaidia Kupunguza Mahangaiko

5, 6. Tunajifunza jambo gani kutokana na sala ambayo Yakobo alitoa alipokaribia kukutana na Esau?

5 Sala inaweza kupunguza mahangaiko. Huku akiogopa hatari kutoka kwa ndugu yake pacha, Esau, Yakobo alisali hivi: “Ee Yehova, . . . Mimi sistahili fadhili zote zenye upendo na uaminifu wote ambao umemwonyesha mtumishi wako . . . Nakuomba, unikomboe kutoka katika mkono wa ndugu yangu, kutoka katika mkono wa Esau, kwa sababu mimi ninaogopa kwamba huenda akaja na kunishambulia, mama pamoja na watoto. Nawe, umesema, ‘Bila shaka nitakutendea vema nami nitaufanya uzao wako uwe kama chembe za mchanga wa baharini, usioweza kuhesabika kwa sababu ya wingi wake.’”—Mwa. 32:9-12.

6 Ingawa Yakobo alichukua hatua za kujilinda, sala yake ilijibiwa wakati yeye na Esau walipopatana. (Mwa. 33:1-4) Soma sala au maombi hayo kwa makini, na utaona kwamba Yakobo hakuomba tu msaada. Alionyesha imani katika ule Uzao ulioahidiwa na alimshukuru Mungu kwa ajili ya fadhili zake zisizostahiliwa. Je, una ‘woga fulani ndani’ yako? (2 Kor. 7:5) Ikiwa ndivyo, basi huenda maombi ya Yakobo yakakukumbusha kwamba sala zinaweza kupunguza mahangaiko. Hata hivyo, sala hazipaswi tu kuwa na maombi bali pia maneno yanayoonyesha kwamba tuna imani.

Sali Ili Upewe Hekima

7. Kwa nini Musa alisali ili apewe ujuzi kuhusu njia za Yehova?

7 Tamaa ya kutaka kumpendeza Yehova inapaswa kukuchochea kusali ili upewe hekima. Musa alisali ili apewe ujuzi kuhusu njia za Mungu. Alimsihi hivi: “Angalia, wewe [Yehova] unaniambia, ‘Waongoze watu hawa [kutoka Misri]’ . . . Na sasa, tafadhali, ikiwa nimepata kibali machoni pako, nijulishe, tafadhali, njia zako, . . . ili nipate kibali machoni pako.” (Kut. 33:12, 13) Mungu alijibu sala hiyo kwa kumpa Musa ujuzi mwingi zaidi kuhusu njia Zake. Musa alihitaji ujuzi huo ili awaongoze watu wa Yehova.

8. Unaweza kufaidika jinsi gani ukitafakari juu ya andiko la 1 Wafalme 3:7-14?

8 Daudi pia alisali hivi: “Nijulishe njia zako, Ee Yehova.” (Zab. 25:4) Sulemani, mwana wa Daudi alimsihi Mungu ampe hekima aliyohitaji ili kutimiza madaraka ya kifalme katika Israeli. Sala ya Sulemani ilimpendeza Yehova, naye akampa si tu kile alichoomba, bali pia utajiri na utukufu. (Soma 1 Wafalme 3:7-14.) Ikiwa umepata mapendeleo ya utumishi ambayo yanaonekana yanakulemea, sali ili upewe hekima na uonyeshe roho ya unyenyekevu. Hivyo, Mungu atakusaidia kupata ujuzi na kuwa na hekima unayohitaji ili utimize madaraka yako kwa njia nzuri na yenye upendo.

Sali Kutoka Moyoni

9, 10. Ni jambo gani la pekee unalojifunza katika maneno ambayo Sulemani anataja kuhusu moyo katika sala yake ya kuzindua hekalu?

9 Ili sala yetu isikiwe, ni lazima itoke moyoni. Sulemani alitoa sala ya kutoka moyoni, iliyo katika 1 Wafalme sura ya 8, mbele ya umati wa watu uliokusanyika huko Yerusalemu kwa ajili ya kuzinduliwa kwa hekalu la Yehova katika mwaka wa 1026 K.W.K. Baada ya sanduku la agano kuwekwa katika Patakatifu Zaidi na wingu la Yehova kulijaza hekalu, Sulemani alimsifu Mungu.

10 Ichunguze sala ya Sulemani na uone mambo anayotaja kuhusu moyo. Sulemani alitambua kwamba Yehova peke yake ndiye anayeujua moyo wa mwanadamu. (1 Fal. 8:38, 39) Sala hiyohiyo inaonyesha kwamba kuna tumaini kwa mtenda-dhambi ‘anayerudi kwa Mungu kwa moyo wake wote.’ Ikiwa adui angewateka nyara watu wa Mungu, maombi yao yangesikiwa ikiwa mioyo yao ilikuwa kamili kwa Yehova. (1 Fal. 8:48, 58, 61) Hivyo basi, sala zako zinapaswa kutoka moyoni.

Jinsi Zaburi Zinavyoweza Kuboresha Sala Zako

11, 12. Umejifunza nini kutokana na sala ya Mlawi mmoja ambaye kwa muda fulani hangeweza kwenda patakatifu pa Mungu?

11 Kujifunza Zaburi kunaweza kuboresha sala zako na kukusaidia kumngojea Mungu ajibu sala hizo. Fikiria subira ambayo ilionyeshwa na Mlawi mmoja aliyekuwa uhamishoni. Ingawa kwa muda fulani hangeweza kwenda patakatifu pa Yehova, aliimba hivi: “Kwa nini umekata tamaa, Ee nafsi yangu, na kwa nini una msukosuko ndani yangu? Mngojee Mungu, kwa maana bado nitamsifu kuwa ndiye wokovu wangu mkuu na kuwa ndiye Mungu wangu.”—Zab. 42:5, 11; 43:5.

12 Unaweza kujifunza nini kutokana na Mlawi huyo? Ikiwa kufungwa gerezani kwa ajili ya uadilifu kungekuzuia kwa muda fulani kuwa pamoja na waamini wenzako mahali pa ibada, mngojee Mungu kwa subira ili atende kwa ajili yako. (Zab. 37:5) Tafakari juu ya shangwe uliyopata wakati uliopita katika utumishi wa Mungu, na usali ili uweze kuvumilia ‘unapomngojea Mungu’ akufungulie njia ya kuendelea kushirikiana na watu wake.

Sali kwa Imani

13. Kulingana na Yakobo 1:5-8, kwa nini unapaswa kusali kwa imani?

13 Hata uwe unakabili hali gani, sali sikuzote kwa imani. Ikiwa unakabili jaribu la utimilifu, fuata shauri la mwanafunzi Yakobo. Sali kwa Yehova, na usiwe na shaka kamwe kwamba anaweza kukupa hekima unayohitaji ili uvumilie jaribu lako. (Soma Yakobo 1:5-8.) Mungu anajua mahangaiko yote yanayokusumbua, naye anaweza kukuongoza na kukufariji kupitia roho yake. Mfungulie moyo wako ukiwa na imani kamili, “bila kutia shaka hata kidogo,” na ukubali mwongozo wa roho yake na mashauri ya Neno lake.

14, 15. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Hana alisali na kutenda kwa imani?

14 Hana, mmoja kati ya wake wawili wa Mlawi aliyeitwa Elkana, alisali na kutenda kwa imani. Hana ambaye hakuwa amezaa mtoto alidhihakiwa na mke mwenzake, Penina, ambaye alizaa watoto wengi. Kwenye maskani, Hana aliweka nadhiri kwamba ikiwa angezaa mwana, angemtoa kwa Yehova. Kwa kuwa midomo ya Hana ilikuwa ikitetemeka alipokuwa akisali, Kuhani Mkuu Eli alifikiri kwamba alikuwa mlevi. Lakini Eli alipojua kwamba Hana hakuwa mlevi, alimwambia hivi: “Mungu wa Israeli akupe ombi lako ambalo umemwomba.” Ingawa Hana hakujua matokeo yangekuwa nini, alikuwa na imani kwamba sala yake ingejibiwa. Kwa hiyo, “uso wake haukuonyesha tena kuhangaika.” Hakuendelea kuhuzunika au kuvunjika moyo.—1 Sam. 1:9-18.

15 Baada ya Samweli kuzaliwa na kuachishwa kunyonya, Hana alimtoa kwa Yehova ili afanye utumishi mtakatifu kwenye maskani. (1 Sam. 1:19-28) Kutafakari kuhusu sala ya Hana katika pindi hiyo kunaweza kuboresha sala zako na kukusaidia kuona kwamba unaweza kushinda hata huzuni inayosababishwa na tatizo lenye kufadhaisha, ukisali ukiwa na imani ya kwamba Yehova atajibu sala yako.—1 Sam. 2:1-10.

16, 17. Ni nini kilichotukia baada ya Nehemia kusali na kutenda kwa imani?

16 Mwanamume mnyoofu Nehemia aliyeishi katika karne ya tano K.W.K. alisali na kutenda kwa imani. Alisihi hivi: “Ah, tafadhali, Yehova, tega sikio lako kwa sala ya mtumishi wako na kwa sala ya watumishi wako wanaofurahia kuliogopa jina lako; na, tafadhali, mpe mafanikio mtumishi wako leo na kumfanya ahurumiwe mbele ya mtu huyu.” “Mtu huyu” alikuwa nani? Alikuwa Mfalme Artashasta wa Uajemi, ambaye Nehemia alimtumikia akiwa mnyweshaji.—Neh. 1:11.

17 Nehemia alisali kwa imani kwa siku nyingi baada ya kupata habari kwamba Wayahudi ambao waliachiliwa huru kutoka utekwani Babiloni walikuwa “katika hali mbaya sana na katika aibu; na ukuta wa Yerusalemu [ulikuwa] umebomoka.” (Neh. 1:3, 4) Sala za Nehemia zilijibiwa kupita alivyotazamia wakati Mfalme Artashasta alipomruhusu kwenda kujenga upya ukuta wa Yerusalemu. (Neh. 2:1-8) Baada ya muda mfupi, ukuta ulikuwa umejengwa. Sala za Nehemia zilijibiwa kwa sababu zilikazia ibada ya kweli na zilitolewa kwa imani. Je, ndivyo sala zako zilivyo?

Kumbuka Kumsifu na Kumshukuru Mungu

18, 19. Kwa nini mtumishi wa Yehova anapaswa kumsifu na kumshukuru?

18 Kumbuka kumsifu na kumshukuru Yehova katika sala. Kuna sababu nyingi sana za kufanya hivyo! Kwa mfano, Daudi alikuwa na hamu kubwa ya kuusifu ufalme wa Yehova. (Soma Zaburi 145:10-13.) Je, sala zako zinaonyesha kwamba unathamini pendeleo la kutangaza Ufalme wa Yehova? Maneno ya watunga-zaburi yanaweza pia kukusaidia kusali kwa Mungu kutoka moyoni na kumshukuru kwa ajili ya mikutano ya Kikristo na makusanyiko yote.—Zab. 27:4; 122:1.

19 Kuthamini uhusiano wako mzuri pamoja na Mungu kunaweza kukuchochea usali kutoka moyoni ukitumia mawazo kama haya: “Nitakusifu katikati ya vikundi vya watu, Ee Yehova; nitakupigia muziki katikati ya vikundi vya mataifa. Kwa maana fadhili zako zenye upendo ni kuu kufika mbinguni, na ukweli wako mpaka angani. Utukuzwe juu ya mbingu, Ee Mungu; utukufu wako na uwe juu ya dunia yote.” (Zab. 57:9-11) Ni maneno yenye kutia moyo kama nini! Je, hukubali kwamba maneno hayo yenye kugusa moyo ya Zaburi yanaweza kuwa na uvutano mzuri juu yako na kuboresha sala zako?

Msihi Mungu kwa Heshima

20. Maria alionyesha jinsi gani ujitoaji wake kwa Mungu?

20 Sala zako zinapaswa kuonyesha wazi kwamba unamheshimu Mungu. Maneno ya heshima ambayo Maria alisema muda mfupi baada ya kujulishwa kwamba angekuwa mama ya Masihi yanalingana na yale ambayo Hana alisema alipokuwa akimpeleka kijana Samweli kwenye utumishi wa maskani. Maneno yafuatayo yaliyosemwa na Maria yanaonyesha wazi kwamba alimheshimu Mungu: “Nafsi yangu inamtukuza Yehova, na roho yangu haiwezi kuacha kumfurahia Mungu Mwokozi wangu.” (Luka 1:46, 47) Je, unaweza kuboresha sala zako na maneno kama hayo yenye hisia? Haishangazi kwamba Maria aliyemwogopa Mungu alichaguliwa kuwa mama ya Yesu yule Masihi!

21. Sala za Yesu zilionyesha jinsi gani heshima na imani?

21 Yesu alisali kwa heshima akiwa na imani kabisa. Kwa mfano, kabla ya kumfufua Lazaro, ‘Yesu aliinua macho yake kuelekea mbinguni na kusema: “Baba, ninakushukuru kwamba umenisikia. Kweli, nilijua kwamba sikuzote wewe hunisikia.”’ (Yoh. 11:41, 42) Je, sala zako zinaonyesha imani na heshima kama hiyo? Ukichunguza sala ya Yesu ya kielelezo yenye heshima, utaona kwamba mambo makuu katika sala hiyo hasa ni kutakaswa kwa jina la Yehova, kuja kwa Ufalme wake, na kutimizwa kwa mapenzi yake. (Mt. 6:9, 10) Fikiria kuhusu sala zako mwenyewe. Je, zinaonyesha kwamba unapendezwa sana na Ufalme wa Mungu, kufanya mapenzi yake, na kutakaswa kwa jina lake takatifu? Sala zako zinapaswa kuonyesha hivyo.

22. Kwa nini unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atakupa ujasiri wa kutangaza habari njema?

22 Kwa sababu ya mateso au majaribu mengine, mara nyingi sala inatia ndani kumsihi Yehova atusaidie kumtumikia kwa ujasiri. Wakati Sanhedrini ilipowaamuru Petro na Yohana waache ‘kufundisha juu ya msingi wa jina la Yesu,’ kwa ujasiri mitume hao walikataa kufanya hivyo. (Mdo. 4:18-20) Baada ya kuachiliwa huru, waliwaeleza waamini wenzao yale yaliyotukia. Kisha, wote walimwomba Mungu awasaidie kusema neno lake kwa ujasiri. Lilikuwa jambo lenye kusisimua kama nini sala hiyo ilipojibiwa, kwa kuwa ‘walijazwa roho takatifu na wakawa wakisema neno la Mungu kwa ujasiri’! (Soma Matendo 4:24-31.) Kwa sababu hiyo, watu wengi wakawa waabudu wa Yehova. Sala inaweza pia kukutia nguvu ili utangaze habari njema kwa ujasiri.

Endelea Kuboresha Sala Zako

23, 24. (a) Taja mifano mingine inayoonyesha jinsi funzo la Biblia linavyoweza kuboresha sala zako. (b) Utafanya nini ili uboreshe sala zako?

23 Tunaweza kutoa mifano mingine mingi inayoonyesha kwamba kusoma Biblia na kujifunza kunaweza kuboresha sala zako. Kwa mfano, katika sala yako unaweza kukiri kama Yona kwamba “wokovu ni wa Yehova.” (Yona 2:1-10) Ikiwa dhamiri inakusumbua kwa sababu ya dhambi nzito na umepata msaada kutoka kwa wazee, maneno ambayo Daudi alisema katika sala yanaweza kukusaidia kuonyesha toba katika sala zako za kibinafsi. (Zab. 51:1-12) Katika sala nyingine, unaweza kumsifu Yehova kama Yeremia alivyofanya. (Yer. 32:16-19) Ikiwa unatafuta mwenzi wa ndoa, kuchunguza sala iliyo katika Ezra sura ya 9 na kusali kibinafsi, kunaweza kutia nguvu azimio lako la kumtii Mungu kwa ‘kuoa katika Bwana tu.’—1 Kor. 7:39; Ezra 9:6, 10-15.

24 Endelea kusoma, kujifunza, na kuichunguza Biblia. Tafuta mambo unayoweza kutia ndani ya sala zako. Unaweza kutumia mawazo fulani ya Kimaandiko katika dua na sala zako za kumshukuru na kumsifu Mungu. Ukifanya hivyo, bila shaka utamkaribia zaidi Yehova Mungu unapoendelea kuboresha sala zako kupitia funzo la Biblia.

Ungesema Nini?

• Kwa nini tunapaswa kutafuta na kufuata mwongozo wa Mungu?

• Ni nini kinachopaswa kutuchochea kusali ili tupewe hekima?

• Kitabu cha Zaburi kinaweza kuboresha jinsi gani sala zetu?

• Kwa nini tunapaswa kusali kwa imani na heshima?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8]

Mtumishi wa Abrahamu alisali ili aongozwe na Mungu. Je, unafanya hivyo?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Ibada ya Familia inaweza kuboresha sala zako