Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Anataka Tufanikiwe

Anataka Tufanikiwe

Mkaribie Mungu

Anataka Tufanikiwe

Yoshua 1:6-9

WAZAZI wenye kujali hutaka sana watoto wao wafanikiwe, waishi maisha yenye kusudi na yenye kuridhisha. Vivyo hivyo, Yehova, Baba yetu wa mbinguni, anataka watoto wake wanaoishi duniani wafanikiwe. Kwa sababu anatujali kwa upendo, yeye hutuambia jinsi ya kufanikiwa. Kwa mfano, fikiria maneno aliyomwambia Yoshua kwenye Yoshua 1:6-9.

Wazia jinsi hali zilivyokuwa kama inavyoonyeshwa katika picha iliyo upande wa kulia. Baada ya Musa kufa, Yoshua ndiye kiongozi mpya wa Israeli, taifa lenye mamilioni ya watu. Waisraeli wanajitayarisha kuingia nchi ambayo Mungu aliwaahidi mababu zao. Mungu ana mashauri anayotaka kumpa Yoshua. Akiyafuata, atafanikiwa. Lakini mashauri hayo si kwa faida ya Yoshua peke yake. Sisi pia tutafanikiwa ikiwa tutayafuata.—Waroma 15:4.

Yehova anamwambia Yoshua awe hodari na mwenye nguvu. Hasemi maneno hayo mara moja tu bali anayarudia mara tatu. (Mstari 6, 7, 9) Ni wazi kwamba Yoshua atahitaji kuwa hodari na mwenye nguvu ili aweze kuliongoza taifa hilo hadi kwenye Nchi ya Ahadi. Lakini, ni nini kitakachomsaidia kuwa na sifa hizo?

Yoshua anaweza kuwa hodari na mwenye nguvu kupitia maandishi yaliyoandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu. Yehova anasema: “Uangalie kufanya kulingana na sheria yote ambayo Musa mtumishi wangu alikuamuru.” (Mstari wa 7) Huenda wakati huo, Yoshua ana vitabu vichache tu vya Biblia vilivyoandikwa. * Hata hivyo, hatafanikiwa kwa sababu tu ana Neno la Mungu. Ili afaidike, Yoshua anapaswa kufanya mambo mawili.

Kwanza, lazima Yoshua aujaze moyo wake neno la Mungu kwa ukawaida. Yehova anasema hivi: “Nawe ukisome kwa sauti ya chini mchana na usiku.” (Mstari wa 8) Kitabu kimoja kinasema: “Mungu alikuwa akimwamuru Yoshua akumbuke Sheria Yake kwa ‘kujisomea kwa sauti ya chini,’ ‘kuifikiria kwa uzito,’ au ‘kuitafakari.’” Kusoma na kutafakari Neno la Mungu kila siku kutamsaidia Yoshua kukabiliana na matatizo yaliyo mbele.

Pili, Yoshua anahitaji kufuata yale anayojifunza kutoka katika Neno la Mungu. Yehova anamwambia hivi: “Upate kuangalia kufanya kulingana na yote ambayo yameandikwa ndani yake; kwa maana ndipo utakapoifanikisha njia yako.” (Mstari wa 8) Yoshua angefanikiwa ikiwa tu angefanya mapenzi ya Mungu. Hakuna njia nyingine. Mapenzi ya Mungu hufanikiwa sikuzote.—Isaya 55:10, 11.

Yoshua alitii mashauri ya Yehova. Kwa sababu hiyo, aliishi maisha yenye kuridhisha akiwa mwabudu mwaminifu wa Yehova.—Yoshua 23:14; 24:15.

Je, unataka kuishi maisha yenye kuridhisha kama Yoshua? Yehova anataka ufanikiwe. Lakini kuwa tu na Neno lake, Biblia, hakutoshi. Mkristo mmoja ambaye amekuwa mwaminifu kwa muda mrefu alitoa dokezo hili: “Usisome Biblia tu, bali tafakari ili kuiingiza moyoni mwako.” Ikiwa utajaza moyo wako Neno la Mungu kwa ukawaida na kulifuata maishani, basi kama Yoshua, ‘utaifanikisha njia yako.’

[Maelezo ya chini]

^ fu. 4 Maandishi yaliyoandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu ambayo Yoshua alikuwa nayo huenda yalitia ndani vile vitabu vitano vya Musa (Mwanzo, Kutoka, Mambo ya Walawi, Hesabu, Kumbukumbu la Torati), kitabu cha Ayubu, na zaburi moja au mbili.