Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mfalme Daudi na Muziki

Mfalme Daudi na Muziki

Mfalme Daudi na Muziki

MTU ambaye hutukumbusha kuhusu muziki wa nyakati za Biblia ni Daudi, mwanamume wa pekee aliyeishi miaka 3,000 iliyopita. Kwa kweli, mambo mengi ambayo tunajua kuhusu muziki wa nyakati hizo unatokana na rekodi ya Biblia ya maisha ya Daudi—kutoka wakati alipokuwa kijana mchungaji hadi alipokuwa mfalme mwenye uwezo wa kupanga mambo.

Kuna mambo mengi ambayo tunaweza kujifunza kutokana na muziki wa nyakati za Biblia kupitia Daudi. Kwa mfano, ni ala gani za muziki walizotumia, na waliimba nyimbo gani? Muziki ulikuwa na sehemu gani katika maisha ya Daudi na kwa taifa la Israeli kwa ujumla?

Muziki Katika Israeli la Kale

Unapotamka maneno ya wimbo fulani, mara moja unakumbuka jinsi muziki huo unavyoimbwa. Biblia ina maneno ya nyimbo mbalimbali, ingawa haijulikani jinsi nyimbo hizo zilivyokuwa zikiimbwa. Lazima ziwe zilikuwa zenye kupendeza, na zenye kuchochea. Ubora wa kishairi ulio kwenye Zaburi unaonyesha kuwa muziki wake ulikuwa maridadi sana.

Biblia inaeleza mambo machache sana kuhusu ala za muziki zilizotumiwa. (Ona sanduku lenye kichwa  “Ala za Muziki Zilizotumiwa Nyakati za Biblia.”) Hata haijulikani Daudi alitumia kinubi cha aina gani. Lakini, ni muhimu kutambua kwamba Waisraeli walivumbua ala kadhaa za muziki, kama vile vinubi vya mbao vyenye thamani sana ambavyo havikupatikana kwa urahisi.—2 Mambo ya Nyakati 9:11; Amosi 6:5.

Hata hivyo, jambo moja ni hakika. Muziki ulikuwa na sehemu muhimu katika ya maisha ya Waisraeli, hasa katika ibada yao kwa Mungu. Muziki ulichezwa wakati wa kutawazwa kwa wafalme, katika sherehe za kidini, na pia wakati wa vita. Muziki ulichezwa katika makao ya kifalme, ulifanya sherehe za arusi au mikusanyiko ya kifamilia iwe yenye furaha, na kufanya sherehe za mavuno ya zabibu na nafaka kuwa zenye kuvutia. Kwa kusikitisha, muziki ulihusianishwa pia na maeneo yenye sifa mbaya. Mwishowe, mtu alipokufa muziki uliwaliwaza waliofiwa.

Katika Israeli muziki ulikuwa na fungu lingine. Muziki ulikuwa na uwezo wa kusisimua akili na kuwafanya manabii wapate maono. Elisha aliposikia sauti ya kinanda alipokea maagizo kutoka kwa Yehova. (2 Wafalme 3:15) Muziki ulitumiwa pia kutangaza matukio muhimu. Mwezi mpya na sherehe zote zilitangazwa kwa tarumbeta mbili za fedha. Siku ya Yubile, baragumu ilitangaza kuwekwa huru kwa watumwa na kurudishwa kwa mashamba na nyumba zilizokuwa zimechukuliwa. Lazima maskini wawe walifurahi sana kusikia muziki uliotangaza kurudishwa kwa mali na uhuru wao!—Mambo ya Walawi 25:9; Hesabu 10:10.

Huenda Waisraeli fulani walikuwa wanamuziki wazuri. Kulingana na mchongo wa Kiashuru, Mfalme Senakeribu alimwambia Mfalme Hezekia amlipe wanamuziki wa kiume na wa kike kama ushuru. Inaonekana kuwa walikuwa waimbaji stadi sana. Lakini Daudi alikuwa mmoja kati ya waimbaji wenye ujuzi mwingi sana.

Mwanamuziki wa Kipekee

Daudi alikuwa mwanamuziki wa kipekee kwa kuwa alikuwa mwimbaji na pia mtungaji wa mashairi. Inasemekana kwamba zaidi ya nusu ya Zaburi zilitungwa na Daudi. Alipokuwa mvulana, alikuwa mchungaji na akili yake yenye utambuzi na ufahamu wa hali ya juu ilihifadhi habari nyingi kuhusu maeneo ya malisho ya Bethlehemu. Alikuwa amefurahia kusikia sauti ya vibubujiko vya maji na sauti ya wana-kondoo wanapojibu anapowaita. Akivutiwa na umaridadi wa sauti hizo zilizomzunguka, alichukua kinubi chake na kuanza kumsifu Mungu kwa sauti. Lazima iwe ilipendeza kusikia muziki wa Daudi alipoimba Zaburi ya 23.

Akiwa kijana, Daudi alicheza kinubi vizuri sana hata akapendekezwa kwenda kumchezea Mfalme Sauli. Sauli alipokuwa amefadhaika sana na kusumbuka kiakili, Daudi alicheza muziki mzuri kwa kinubi chake ulioutuliza moyo wa Sauli. Mawazo mabaya aliyokuwa nayo yaliondoka na akaacha kusumbuka kiakili.—1 Samweli 16:16.

Muziki, ambao Daudi alipenda sana na uliomletea furaha, wakati mwingine ulimletea matatizo. Siku moja, Daudi na Sauli waliporudi kutoka vitani baada ya kuwashinda Wafilisti, mfalme muziki wa ushindi na wenye furaha. Wanawake walikuwa wakiimba hivi: “Sauli amepiga maelfu yake, na Daudi makumi ya maelfu yake.” Jambo hilo lilimkasirisha Sauli sana na kumfanya awe na wivu hivi kwamba “akawa akimtilia Daudi shaka tangu siku hiyo na kuendelea.”—1 Samweli 18:7-9.

Muziki Ulimchochea Daudi

Muziki wa Daudi ulioongozwa na roho takatifu, ulikuwa bora katika njia nyingi. Nyimbo zake zinatia ndani zaburi za mambo aliyokuwa ametafakari na maisha ya uchungaji. Zinatia ndani sifa na hadithi, shangwe ya mavuno ya zabibu na shamrashamra za kuwekwa wakfu kwa makao ya mfalme, kumbukumbu na nyimbo za tumaini, maombi na sihi. (Ona Zaburi 32, 23, 145, 8, 30, 38, 72, 51, 86 na maandishi ya utangulizi ya zaburi hizi.) Sauli na mwana wake Yonathani walipokufa, Daudi alitunga wimbo wa kuomboleza ulioitwa: “Upinde,” ulioanza kwa maneno haya: “Ee Israeli, uzuri umeuawa katika mahali pako pa juu.” Wimbo huo uliimbwa kwa sauti ya huzuni. Daudi alijua jinsi ya kueleza hisia mbalimbali, kwa maneno na pia kwa kinubi.—2 Samweli 1:17-19.

Kwa sababu ya utu wake mchangamfu, Daudi alipenda nyimbo zenye furaha zinazochangamsha na miziki yenye midundo yenye kupendeza. Alipoleta sanduku la agano hadi Sayuni, Daudi alirukaruka na kucheza dansi kwa nguvu zake zote ili kusherehekea pindi hiyo. Simulizi hilo la Biblia linaonyesha kuwa huenda muziki huo ulikuwa wenye kusisimua sana. Je, unaweza kuwazia pindi hiyo? Mke wake Mikali alianza kumdhihaki. Daudi hakujali jambo hilo. Alimpenda Yehova, na muziki huo uliomfanya awe na shangwe nyingi sana, ulimchochea arukeruke mbele ya Mungu wake.—2 Samweli 6:14, 16, 21.

Isitoshe, Daudi alijulikana kwa kutengeneza ala mpya za muziki. (2 Mambo ya Nyakati 7:6) Kwa ujumla, Daudi alikuwa msanii mwenye kipawa, kwa kuwa alikuwa mtengenezaji wa ala za muziki, mshairi, mtungaji, na mtumbuizaji. Hata hivyo, Daudi alifanya mambo makubwa hata zaidi.

Muziki na Uimbaji Katika Hekalu

Daudi hukumbukwa kwa kuwa yeye ndiye aliyepanga uimbaji na muziki katika nyumba ya Yehova. Alikuwa na waimbaji na wanamuziki 4,000 waliosimamiwa na Asafu, Hemani, na Yeduthuni (ambaye pia huenda aliitwa Ethani). Daudi aliwaweka chini ya wataalamu 288 ambao waliwafunza na kuwaongoza. Wanamuziki na waimbaji hao 4,000 walikuwepo wakati wa sherehe tatu kubwa zilizofanywa kila mwaka. Hebu wazia kwaya hiyo kubwa yenye kuvutia!—1 Mambo ya Nyakati 23:5; 25:1, 6, 7.

Ni wanaume peke yake walioimba hekaluni. Maneno “juu ya Wanawali” yanayopatikana katika maandishi ya utangulizi ya Zaburi 46, huashiria sauti nyembamba na iliyo ya juu sana ya mtu au ya ala fulani ya muziki. Waliimba kwa umoja, kama inavyoonyeshwa kwenye 2 Mambo ya Nyakati 5:13: ‘Waimbaji walikuwa kama mtu mmoja.’ Huenda nyimbo hizo zilikuwa muziki, kama vile Zaburi 3 na zaburi nyingine nyingi za Daudi, na nyakati nyingine zilikuwa na korasi, kama inavyoonyeshwa katika Zaburi 42:5, 11 na 43:5. Nyimbo za majibizano, iwe ziliimbwa katika kwaya na/au ziliimbwa na watu wawili waliojibizana, zilipendwa sana. Mfano mmoja ni ule wa Zaburi 24, ambayo bila shaka ilitungwa Daudi alipoleta sanduku la agano Sayuni.—2 Samweli 6:11-17.

Hata hivyo, si Walawi peke yao walioimba. Watu wa kawaida ndio walioimba walipokuwa wakipanda kwenda Yerusalemu wakati wa sherehe za kila mwaka. Huenda hilo ndilo linalomaanishwa na maneno “Wimbo wa Mipando.” (Zaburi 120 hadi 134) Kwa mfano, katika Zaburi 133, Daudi anaimba kuhusu udugu ambao Waisraeli walifurahia katika pindi hizo. Anaanza kwa maneno haya: “Tazama! Jinsi ilivyo vyema na jinsi inavyopendeza ndugu kukaa pamoja kwa umoja!” Jaribu kuwazia muziki ulioambatanishwa na wimbo huo!

Muziki na Ibada ya Yehova

Asilimia kumi ya Biblia imefanyizwa na nyimbo kama hizo, na kitabu cha Zaburi kinawatia moyo wanadamu wote wamsifu Yehova. (Zaburi 150) Muziki unaweza kumfanya mtu asahau matatizo ya maisha, na kuimba kunaweza kuponya mioyo iliyoumia. Hata hivyo, Biblia inapendekeza kwamba wale walio na roho changamfu waimbe zaburi.—Yakobo 5:13.

Kuimba ni njia moja ambayo mtu anaweza kuonyesha ana imani na anampenda Mungu. Usiku kabla ya Yesu kuuawa, yeye na mitume walimalizia mlo wao kwa kuimba. (Mathayo 26:30) Lazima Mwana wa Daudi awe alikuwa na sauti yenye kupendeza kwani alikuwa anajua uimbaji wenye utukufu unaosikika katika ua wa kimbingu wa Mungu! Huenda waliimba Haleli, yaani, Zaburi 113 hadi 118. Ikiwa ndivyo, basi akiwa pamoja na mitume ambao walikuwa hawajui mambo yaliyokuwa karibu kutukia, huenda Yesu aliimba kwa sauti ya juu: “Ninajawa na upendo, kwa sababu Yehova husikia sauti yangu, kusihi kwangu. . . . Kamba za kifo zilinizunguka na hali zenye kutaabisha za Kaburi zikanipata. . . . ‘Ah, Yehova, uiokoe nafsi yangu!’”—Zaburi 116:1-4.

Si mwanadamu aliyevumbua muziki. Biblia hueleza kuhusu muziki na uimbaji huko mbinguni, ambako viumbe wa kiroho hupiga vinubi vya mfano na kuimba nyimbo za sifa wakiwa wamezunguka kiti cha ufalme cha Yehova. (Ufunuo 5:9; 14:3; 15:2, 3) Yehova Mungu aliwapa wanadamu muziki, na kuweka mioyoni mwao tamaa ya muziki na hamu isiyoweza kuzuiwa ya kueleza hisia zao kwa kucheza ala fulani ya muziki au kwa kuimba. Kwa mtu aliye na imani, muziki ni zawadi kutoka kwa Mungu.—Yakobo 1:17.

[Blabu katika ukurasa wa 27]

“Katika siku ya kushangilia kwenu na katika majira yenu ya sherehe . . . mtapiga tarumbeta”—HESABU 10:10

[Blabu katika ukurasa wa 28]

“Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote. Ananilaza katika malisho yenye majani mengi; ananiongoza kando ya mahali pa kupumzika palipo na maji ya kutosha.”—ZABURI 23:1, 2

[Blabu katika ukurasa wa 29]

“Kulikuwa na . . . watu 4,000 wenye kutoa sifa kwa Yehova kwa vyombo ambavyo Daudi alisema ‘Nimevitengeneza kwa ajili ya kutoa sifa.’”—1 MAMBO YA NYAKATI 23:4, 5

[Blabu katika ukurasa wa 29]

Daudi alieleza hisia mbalimbali kwa maneno na pia kwa kinubi

[Blabu katika ukurasa wa 30]

“Msifuni Yah! Msifuni kwa matari na kwa dansi ya mzunguko. Kila kitu kinachopumua—na kimsifu Yah.”—ZABURI 150:1, 4, 6

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 28]

 Ala za Muziki Zilizotumiwa Nyakati za Biblia

Vinanda vilivyotengenezwa kwa kutumia nyuzi vilitia ndani udi, kinubi, na kinanda cha nyuzi kumi. (Zaburi 92:3) Vinanda hivi viliundwa ili viweze kutoa sauti inayopatana na Alamothi na Sheminithi, maneno ambayo huenda yalitumiwa kuashiria alama nane za muziki za juu au za chini. (1 Mambo ya Nyakati 15:20, 21) Kati ya vyombo vilivyotengenezwa kwa shaba na pia vyombo vya kupulizwa kulikuwa na zumari, filimbi, baragumu, na pia tarumbeta, ‘zilizopigwa kwa sauti kubwa.’ (2 Mambo ya Nyakati 7:6; 1 Samweli 10:5; Zaburi 150:3, 4) Wakati wa kuwekwa wakfu kwa hekalu, ‘sauti moja ilisikika’ kutoka kwa tarumbeta na waimbaji. (2 Mambo ya Nyakati 5:12, 13) Huenda hili lilimaanisha kuwa waliimba kwa upatano na pia hakukuwa na migongano ya sauti. Ala zinazotoa sauti zinapogongwa zilitia ndani matari na matasa, na pia “namna zote za vyombo vya mbao za mberoshi.” Pia kulikuwa na matoazi—madogo-madogo yanayotoa “sauti tamu” na makubwa yanayoitwa “matoazi ya kugonganishwa.”—2 Samweli 6:5; Zaburi 150:5

[Picha]

Juu: Michoro kwenye Tao la Tito, huko Roma, Italia, ikionyesha tarumbeta zilizotolewa katika hekalu la Yerusalemu mwaka wa 70 W.K. Sarafu za mwaka wa 130 W.K., zikionyesha ala za muziki za Wayahudi

[Hisani]

Coins: © 2007 by David Hendin. All rights reserved.