Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Masihi! Njia ya Mungu ya Wokovu

Masihi! Njia ya Mungu ya Wokovu

Masihi! Njia ya Mungu ya Wokovu

“Kwa maana kama vile katika Adamu wote wanakufa, vivyo hivyo pia katika Kristo wote watafanywa kuwa hai.”—1 KOR. 15:22.

1, 2. (a) Andrea na Filipo walitenda jinsi gani walipokutana na Yesu? (b) Kwa nini tunasema kwamba leo tuna uthibitisho mwingi kuliko Wakristo wa karne ya kwanza kwamba Yesu ndiye yule Masihi?

“TUMEMPATA Masihi,” hivyo ndivyo Andrea alivyomwambia ndugu yake Petro. Andrea alisadiki kabisa kwamba Yesu wa Nazareti alikuwa ndiye Mtiwa-Mafuta wa Mungu. Filipo alisadikishwa naye akamtafuta rafiki yake Nathanaeli, na kumwambia hivi: “Tumempata yule ambaye Musa, katika Sheria, na Manabii, aliandika juu yake, Yesu, mwana wa Yosefu, kutoka Nazareti.”—Yoh. 1:40, 41, 45.

2 Je, unasadiki kabisa kwamba Yesu ndiye yule Masihi aliyeahidiwa, “Wakili Mkuu [wa Yehova] wa wokovu”? (Ebr. 2:10) Leo, tofauti na wafuasi wake wa karne ya kwanza, tuna uthibitisho mwingi ambao unaonyesha kwamba Yesu ndiye yule Masihi. Tangu Yesu alipozaliwa mpaka alipofufuliwa, Neno la Mungu ambalo limeongozwa na roho linatoa uthibitisho ulio wazi kabisa kwamba alikuwa ndiye Kristo. (Soma Yohana 20:30, 31.) Pia, Biblia inaonyesha kwamba akiwa mbinguni, Yesu angeendelea kutimiza daraka lake akiwa Masihi. (Yoh. 6:40; soma 1 Wakorintho 15:22.) Leo, wewe pia unaweza kusema kwamba ‘umempata yule Masihi’ kwa njia ya kiroho. Lakini chunguza kwanza jinsi wanafunzi hao wa awali walivyokata kauli iliyo sahihi kwamba walikuwa wamempata yule Masihi.

“Siri Takatifu” Kumhusu Masihi Ilifunuliwa Hatua kwa Hatua

3, 4. (a) Wanafunzi wa karne ya kwanza wangeweza ‘kumpata yule Masihi’ jinsi gani? (b) Kwa nini unaweza kusema kwamba ni Yesu tu ndiye aliyetimiza unabii wote kumhusu Masihi?

3 Kwa nini wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza walisema kwa uhakika kwamba Yesu alikuwa ndiye yule Masihi? Kupitia manabii, Yehova alifunua hatua kwa hatua ishara za kumtambulisha Masihi aliyetarajiwa. Msomi mmoja wa Biblia alilinganisha hatua hizo na kazi ya kuunganisha vipande mbalimbali vya sanamu ya mawe ya marumaru. Hebu wazia ikiwa wanaume wengi ambao hawajawahi kamwe kuonana wangeleta kila mmoja wao kipande kimoja cha sanamu hiyo. Ikiwa vipande vya sanamu hiyo vingeunganishwa na kufanyiza sanamu kamili, bila shaka ungekata kauli kwamba kuna mtu fulani ambaye aliitengeneza na kumpa kila mmoja wa wanaume hao kipande kimoja cha sanamu hiyo. Sawa na kila kipande cha sanamu hiyo, kila unabii ambao unamhusu Masihi ungetoa habari fulani ya maana sana kumhusu Masihi.

4 Hivyo basi, kuna uwezekano gani kwamba unabii wote kumhusu Masihi ungetimizwa kimuujiza tu na mtu mmoja? Mtafiti mmoja alisema kwamba haingewezekana kamwe kwa mtu mmoja kutimiza kimuujiza tu unabii wote kumhusu Masihi! “Ni Yesu tu katika historia yote, ndiye aliyetimiza unabii wote kumhusu Masihi.”

5, 6. (a) Hukumu juu ya Shetani ingetekelezwa jinsi gani? (b) Mungu alifunua jinsi gani hatua kwa hatua ukoo wa “uzao” ulioahidiwa?

5 Unabii mbalimbali kumhusu Masihi ni “siri takatifu” yenye mambo mengi ambayo ni ya maana sana kwa ulimwengu wote. (Kol. 1:26, 27; Mwa. 3:15) Hukumu juu ya Shetani Ibilisi, “yule nyoka wa zamani,” ambaye aliwaingiza wanadamu katika dhambi na kifo, ni sehemu ya siri hiyo takatifu. (Ufu. 12:9) Hukumu hiyo ingetekelezwa jinsi gani? Yehova alitabiri kwamba “uzao” ambao ungetokezwa na “mwanamke” ungemponda Shetani kichwa. “Uzao” huo uliotabiriwa ungemponda nyoka kichwa, na hivyo kumwondoa yule anayesababisha uasi, magonjwa, na kifo. Hata hivyo, Mungu angemruhusu kwanza Shetani atie “uzao” wa mwanamke jeraha la mfano kwenye kisigino.

6 Yehova alifunua hatua kwa hatua ni nani angekuwa ule “uzao” ulioahidiwa. Mungu alimwapia Abrahamu hivi: “Kupitia kwa uzao wako mataifa yote ya dunia hakika yatajibariki.” (Mwa. 22:18) Musa alitabiri kwamba Yule ambaye angekuwa uzao huo angekuwa “nabii” mkuu kuliko yeye. (Kum. 18:18, 19) Daudi alihakikishiwa, na baadaye manabii wakathibitisha kwamba Masihi angetoka katika ukoo wa Daudi na angerithi milele kiti cha ufalme cha Daudi.—2 Sam. 7:12, 16; Yer. 23:5, 6.

Sifa za Yesu Akiwa Masihi

7. Yesu alitokana na “mwanamke” wa Mungu katika njia gani?

7 Mungu alimtuma Mwana wake, uumbaji wake wa kwanza, kutoka katika tengenezo lake la viumbe wa roho mbinguni ambalo ni kama mke Wake, ili awe “uzao” ulioahidiwa. Hilo lilihitaji Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu ‘ajiondolee mwenyewe’ uhai wake wa kimbingu na kuzaliwa akiwa mwanadamu mkamilifu. (Flp. 2:5-7; Yoh. 1:14) ‘Kufunikwa’ kwa Maria na roho takatifu kulihakikisha kwamba kile ambacho kingezaliwa ‘kingeitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu.’—Luka 1:35.

8. Yesu alitimiza jinsi gani unabii kumhusu Masihi alipojitokeza ili abatizwe katika maji?

8 Unabii kumhusu Masihi ulionyesha mahali na wakati ambapo Yesu angetokea. Yesu alizaliwa Bethlehemu kama ilivyotabiriwa. (Mika 5:2) Katika karne ya kwanza, Wayahudi walikuwa na matarajio makubwa sana. Huku wakitarajia kutokea kwa Masihi, wengine waliuliza hivi kumhusu Yohana Mbatizaji: “Je, labda yeye ndiye Kristo?” Lakini Yohana akajibu: “Mwenye nguvu kuliko mimi anakuja.” (Luka 3:15, 16) Alipomwendea Yohana mwishoni mwa mwaka wa 29 W.K. ili abatizwe akiwa na umri wa miaka 30, Yesu alijitokeza mwenyewe kwa wakati unaofaa akiwa yule Masihi. (Dan. 9:25) Kisha alianza huduma yake yenye matukio mengi, akisema: “Wakati uliowekwa umetimizwa, na ufalme wa Mungu umekaribia.”—Marko 1:14, 15.

9. Ingawa hawakuwa na habari kamili, wanafunzi wa Yesu walikuwa na usadikisho gani ulio imara?

9 Hata hivyo, matarajio ya watu, yalihitaji kurekebishwa. Yesu alitukuzwa kwa kufaa kama Mfalme, lakini watu wangeelewa kikamili baadaye kwamba angetawala wakati ujao na angetawala kutoka mbinguni. (Yoh. 12:12-16; 16:12, 13; Mdo. 2:32-36) Kwa hiyo, Yesu alipouliza, “Ninyi mnasema mimi ni nani?” Petro alijibu hivi bila kusitasita: “Wewe ndiye Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.” (Mt. 16:13-16) Petro alijibu vivyo hivyo wengi walipokwazika na kumwacha Yesu kwa sababu ya fundisho fulani.—Soma Yohana 6:68, 69.

Kumsikiliza Masihi

10. Kwa nini Yehova alikazia uhitaji wa kumsikiliza Mwana wake?

10 Huko mbinguni, Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu alikuwa mtu wa roho mwenye nguvu. Duniani, Yesu alikuwa “mwakilishi wa Baba.” (Yoh. 16:27, 28) Alisema hivi: “Yale ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma.” (Yoh. 7:16) Akithibitisha kwamba Yesu ni Masihi, Yehova alisema hivi kumhusu Yesu wakati wa kugeuka sura: “Msikilizeni.” (Luka 9:35) Ndiyo, msikilize, au mtii, Mchaguliwa huyo. Hilo lilihitaji imani na matendo mazuri, na yote mawili ni mambo ya maana sana ili kumpendeza Mungu na kupata uzima wa milele.—Yoh. 3:16, 35, 36.

11, 12. (a) Taja sababu zilizowafanya Wayahudi wa karne ya kwanza wamkatae Yesu kuwa yule Masihi. (b) Ni nani waliomwamini Yesu?

11 Ingawa Yesu alikuwa na sifa nyingi za kuthibitisha kwamba ndiye Masihi, Wayahudi wengi wa karne ya kwanza hawakumkubali. Kwa nini? Kwa sababu walikuwa na mawazo yao wenyewe kumhusu Masihi, kutia ndani mawazo ya kwamba masihi angekuwa mwanasiasa ambaye angewakomboa kutoka chini ya ukandamizaji wa Waroma. (Soma Yohana 12:34.) Hivyo, hawangemkubali Masihi ambaye alitimiza unabii ambao ulisema kwamba masihi angedharauliwa, angeepukwa na watu, angekuwa mtu aliyekusudiwa maumivu, na aliyezoeana na ugonjwa, na kwamba mwishowe angeuawa. (Isa. 53:3, 5) Hata wanafunzi fulani washikamanifu wa Yesu walivunjika moyo kwa sababu hakuwakomboa kisiasa. Lakini waliendelea kuwa washikamanifu, na kwa wakati unaofaa, walisaidiwa kuelewa mambo kwa usahihi.—Luka 24:21.

12 Sababu nyingine iliyofanya watu wamkatae Yesu kuwa Masihi aliyeahidiwa ni mafundisho yake, ambayo wengi waliona vigumu kuyakubali. Ili kuingia katika Ufalme, mtu alipaswa ‘kujikana mwenyewe,’ ‘kula’ mwili na kunywa damu ya Yesu, ‘kuzaliwa tena,’ na ‘kutokuwa sehemu ya ulimwengu.’ (Marko 8:34; Yoh. 3:3; 6:53; 17:14, 16) Wenye kiburi, matajiri, na wanafiki waliona matakwa hayo kuwa magumu sana kutimiza. Hata hivyo, Wayahudi wanyenyekevu walimkubali Yesu kuwa Masihi, kama walivyofanya Wasamaria fulani waliosema: “Mtu huyu kwa hakika ndiye mwokozi wa ulimwengu.”—Yoh. 4:25, 26, 41, 42; 7:31.

13. Yesu alitiwa jeraha la mfano kwenye kisigino jinsi gani?

13 Yesu alitabiri kwamba wakuu wa makuhani wangemhukumu na Watu wa Mataifa wangemtundika mtini, lakini siku ya tatu, angefufuka. (Mt. 20:17-19) Waliona kwamba anakufuru alipokubali mbele ya Sanhedrini kwamba alikuwa “ndiye Kristo Mwana wa Mungu.” (Mt. 26:63-66) Pilato hakumpata Yesu na jambo “lolote linalostahili kifo,” lakini kwa sababu Wayahudi walimshtaki pia kwa kosa la uchochezi, Pilato “akamtia Yesu mikononi mwao wamtendee wanavyopenda.” (Luka 23:13-15, 25) Kwa hiyo, ‘walimkana’ na kupanga njama ya kumuua “Wakili Mkuu wa uzima,” ingawa kulikuwa na uthibitisho mwingi ulioonyesha kwamba alitumwa na Mungu. (Mdo. 3:13-15) Yule Masihi ‘alikatiliwa mbali’ kama ilivyotabiriwa, akatundikwa kwenye mti Siku ya Pasaka ya mwaka wa 33 W.K. (Dan. 9:26, 27; Mdo. 2:22, 23) Kwa kufa kifo hicho cha kikatili, alitiwa jeraha kwenye “kisigino” kama ilivyotabiriwa kwenye Mwanzo 3:15.

Kwa Nini Masihi Alipaswa Kufa?

14, 15. (a) Taja sababu mbili zilizomfanya Yehova aruhusu Yesu afe. (b) Yesu alifanya nini baada ya kufufuliwa?

14 Yehova aliruhusu Yesu afe kwa sababu mbili kuu. Kwanza, uaminifu wa Yesu mpaka kifo ulitimiza sehemu ya maana sana ya ile “siri takatifu.” Yesu alithibitisha kwa ukamili kabisa kwamba mwanadamu mkamilifu anaweza kudumisha “ujitoaji-kimungu” na kuunga mkono enzi kuu ya Mungu hata akijaribiwa vikali na Shetani. (1 Tim. 3:16) Pili, kama Yesu alivyosema, ‘Mwana wa binadamu alikuja kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.’ (Mt. 20:28) Dhabihu hiyo ya ukombozi au “fidia inayolingana” ililipia adhabu ya dhambi ambayo wazao wa Adamu walirithi na iliwapa wote ambao wanakubali kwamba Yesu ni njia ya Mungu ya wokovu nafasi ya kupata uzima wa milele.—1 Tim. 2:5, 6.

15 Baada ya kukaa kaburini kwa siku tatu, Kristo alifufuliwa, na kwa siku 40 aliwatokea wanafunzi wake ili kuthibitisha kwamba alikuwa hai, kisha akawapa maagizo zaidi. (Mdo. 1:3-5) Halafu akapanda mbinguni ili kumtolea Yehova thamani ya dhabihu yake bora zaidi na kungoja wakati uliowekwa ambapo kuwapo kwake akiwa Mfalme wa Kimasihi kungeanza. Wakati huo, alikuwa na mambo mengi ya kufanya.

Kukamilisha Daraka Lake Akiwa Masihi

16, 17. Eleza daraka la Yesu akiwa Masihi baada ya yeye kupanda mbinguni.

16 Katika karne zote tangu kufufuliwa kwake, Yesu amesimamia kwa uaminifu kazi mbalimbali za kutaniko la Kikristo ambalo amekuwa akilitawala akiwa Mfalme. (Kol. 1:13) Kwa wakati uliowekwa, angeanza kutumia nguvu zake akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Unabii mbalimbali wa Biblia na matukio ya ulimwengu yanathibitisha kwamba kuwapo kwake akiwa Mfalme kulianza mwaka wa 1914, na pia “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 24:3; Ufu. 11:15) Muda mfupi baadaye, aliongoza malaika wake watakatifu kumtupa Shetani na roho wake waovu kutoka mbinguni.—Ufu. 12:7-10.

17 Kazi ya kuhubiri na kufundisha ambayo Yesu alianzisha mwaka wa 29 W.K. inakaribia kilele chake chenye utukufu. Hivi karibuni, atawahukumu wote wanaoishi. Kisha, atawaambia wale walio mfano wa kondoo wanaomkubali kuwa njia ambayo Yehova anatumia kuwaokoa wanadamu ‘warithi ufalme uliotayarishwa kwa ajili yao tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu.’ (Mt. 25:31-34, 41) Wote wanaomkataa Yesu kuwa Mfalme wataharibiwa wakati atakapoongoza majeshi ya kimbingu katika kuondoa uovu wote. Kisha Yesu atamfunga Shetani na roho wake waovu na kuwatupa ndani ya “abiso.”—Ufu. 19:11-14; 20:1-3.

18, 19. Yesu anatimiza nini katika kutekeleza daraka lake akiwa yule Masihi, naye anawaletea nini wanadamu watiifu?

18 Wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu, Yesu atatumia kikamili vyeo vyake vyote, kama vile “Mshauri wa Ajabu, Mungu Mwenye Nguvu, Baba wa Milele, Mkuu wa Amani.” (Isa. 9:6, 7) Chini ya utawala wake wa Ufalme, wanadamu watakuwa wakamilifu, kutia ndani wafu watakaofufuliwa. (Yoh. 5:26-29) Masihi atawaongoza wanadamu wenye nia nzuri kwenye “chemchemi za maji ya uzima,” na hivyo kuwawezesha wanadamu watiifu kuwa na uhusiano wenye amani pamoja na Yehova. (Soma Ufunuo 7:16, 17.) Baada ya jaribu la mwisho, waasi wote, kutia ndani Shetani na roho wake waovu, ‘watatupwa ndani ya lile ziwa la moto,’ yaani, watapata pigo la kifo la kumponda kichwa yule “nyoka.”—Ufu. 20:10.

19 Yesu anatimiza kwa njia nzuri ajabu na kamilifu kama nini daraka lake akiwa yule Masihi! Dunia paradiso itajaa wanadamu waliokombolewa, ambao wataishi milele wakiwa wenye furaha na afya kamilifu. Jina takatifu la Yehova litaondolewa suto kabisa, na haki yake ya kutawala ulimwengu wote itatetewa kikamili. Hivi karibuni sana, wote ambao wanamtii huyo Mtiwa-Mafuta wa Mungu watapata urithi mkubwa kama nini!

Je, Umempata Yule Masihi?

20, 21. Una sababu gani za kuzungumza na wengine kumhusu yule Masihi?

20 Kuanzia mwaka wa 1914 tumekuwa tukiishi katika kipindi cha pa·rou·siʹa, au kuwapo kwa Kristo. Ingawa kuwapo kwake akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu hakuonekani kihalisi, kunaonekana wazi kupitia utimizo wa unabii mbalimbali. (Ufu. 6:2-8) Hata hivyo, leo watu wengi wanapuuza uthibitisho wa kuwapo kwa Masihi kama walivyofanya Wayahudi wa karne ya kwanza. Wao pia wanataka masihi wa kisiasa au angalau yule ambaye atatawala kupitia wanadamu ambao ni watawala wa kisiasa. Lakini wewe unajua kwamba Yesu anatawala sasa akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Je, hukusisimka kujua hilo? Kama wanafunzi wa karne ya kwanza, ulichochewa kutangaza hivi: “Tumempata Masihi.”

21 Leo, unapozungumza na watu kuhusu kweli, je, unakazia daraka la Yesu akiwa Masihi? Kufanya hivyo kutakusaidia kuthamini zaidi mambo ambayo tayari amekufanyia, yale anayofanya sasa, na yale ambayo atafanya baadaye. Kama Andrea na Filipo, bila shaka wewe pia tayari umezungumza na marafiki na watu wako wa ukoo kumhusu yule Masihi. Kwa nini usizungumze nao tena kwa bidii zaidi na kuwaonyesha kwamba Yesu Kristo kwa kweli ndiye yule Masihi aliyeahidiwa, njia ya Mungu ya kuwaokoa wanadamu?

Je, Unaweza Kueleza?

• Wanafunzi wa karne ya kwanza wangeweza jinsi gani kumpata yule Masihi?

• Yesu alikufa kwa sababu gani mbili kuu?

• Yesu atafanya nini wakati ujao ili kutimiza daraka lake akiwa yule Masihi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Watu katika karne ya kwanza wangeweza kujua jinsi gani kwamba Yesu ndiye yule Masihi aliyeahidiwa?

[Picha katika ukurasa wa 23]

Unapozungumza na wengine, je, unakazia daraka la Yesu akiwa Masihi?