Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Yafika Kwenye Kisiwa Kikubwa Chekundu

Biblia Yafika Kwenye Kisiwa Kikubwa Chekundu

Biblia Yafika Kwenye Kisiwa Kikubwa Chekundu

KISIWA cha Madagaska kiko umbali wa kilomita 400 hivi kutoka kusini mashariki ya pwani ya Afrika, na ndicho kisiwa cha nne kwa ukubwa duniani. Watu wanaoishi huko Madagaska wamelifahamu jina Yehova kwa muda mrefu, kwa sababu tafsiri ya Biblia ya Kimalagasi ambayo ina jina la Mungu imekuwapo kwa zaidi ya miaka 170. Uvumilivu na kujitoa kabisa kulihitajiwa ili kutokeza tafsiri ya Biblia katika Kimalagasi.

Juhudi za kutafsiri Biblia katika Kimalagasi zilianzia kwenye kisiwa kilicho karibu cha Mauritius. Mwaka wa 1813, Sir Robert Farquhar, gavana Mwingereza wa kisiwa cha Mauritius, alianzisha kazi ya kutafsiri vitabu vya Injili katika Kimalagasi. Baadaye, alimtia moyo Radama wa Kwanza, mfalme wa Madagaska, awaalike walimu kutoka kwa Shirika la Wamishonari la London (LMS) kwenye Kisiwa Kikubwa Chekundu, yaani Madagaska.

Mnamo Agosti 18, 1818 (18/8/1818), wamishonari wawili kutoka Wales, David Jones na Thomas Bevan, waliwasili kwenye mji wenye bandari wa Toamasina kutoka Mauritius. Huko Madagaska, walikuta watu waliopenda sana ibada, wengine wao waliabudu mababu waliokufa na walifuata sana mapokeo katika maisha yao ya kila siku. Watu wa Madagaska walizungumza lugha yenye kupendeza sana na yenye asili ya Malaysia na Polinesia.

Muda mfupi baada ya kufungua shule ndogo, Jones na Bevan walihamisha wake na watoto wao kutoka Mauritius hadi Toamasina. Hata hivyo, kwa kusikitisha, kila mtu katika kikundi hicho alishikwa na malaria, na mke na mtoto wa Jones wakafa Desemba (Mwezi wa 12) 1818. Miezi miwili baadaye, ugonjwa huo uliua familia yote ya Bevan. Katika kikundi hicho, David Jones ndiye tu aliyebaki.

Jones hakuruhusu msiba huo umzuie kuendelea. Alikuwa ameazimia kuwasaidia watu wa Madagaska kupata Neno la Mungu. Baada ya kurudi Mauritius ili apate matibabu, Jones alianza kazi ngumu ya kujifunza Kimalagasi. Muda mfupi baadaye alianza kazi ya kutafsiri Injili ya Yohana.

Oktoba 1820, Jones alirudi tena Madagaska. Alienda kwenye mji mkuu Antananarivo, na baada ya muda mfupi akaanzisha shule ya kimishonari. Hali zilikuwa mbaya sana. Hakukuwa na vitabu vya kusoma, ubao, wala meza za kuandikia. Lakini masomo yalikuwa mazuri sana na watoto walitamani kujifunza.

Baada ya kufanya kazi akiwa peke yake kwa miezi saba, Jones alipata mfanyakazi mwingine ambaye angechukua mahali pa Bevan, mmishonari aliyeitwa David Griffiths. Wamishonari hao wawili walifanya kazi ya kutafsiri Biblia katika Kimalagasi kwa bidii sana.

Kazi ya Kutafsiri Yaanza

Mwanzoni mwa miaka ya 1820, Kimalagasi kiliandikwa kwa kutumia sorabe, yaani, maneno ya Kimalagasi yaliyoandikwa kwa kutumia herufi za Kiarabu. Ni watu wachache sana ambao wangeweza kusoma maandishi hayo. Hivyo, baada ya wamishonari hao kushauriana na Mfalme Radama wa Kwanza, mfalme huyo aliwaruhusu kutumia herufi za Kiroma badala ya sorabe.

Kazi ya kutafsiri ilianza Septemba 10, 1823 (10/9/1823). Jones alianza kutafsiri vitabu vya Mwanzo na Mathayo, naye Griffiths akaanza kutafsiri vitabu vya Kutoka na Luka. Wanaume hao wawili walifanya kazi kwa bidii sana. Mbali na kufanya kazi ya kutafsiri wakiwa peke yao, waliendelea kufundisha shuleni wakati wa asubuhi na alasiri. Pia, walitayarisha na kuongoza ibada za kanisani kwa lugha tatu tofauti. Lakini bado waliona kazi ya kutafsiri kuwa ya maana kuliko kazi nyingine zote.

Wakisaidiwa na wanafunzi 12, wamishonari hao walitafsiri Maandiko yote ya Kigiriki na vitabu vingi vya Maandiko ya Kiebrania kwa miezi 18 tu. Mwaka uliofuata, kwa mara ya kwanza, kazi ya kutafsiri Biblia nzima ilikuwa imekamilika. Bila shaka, walihitaji kusahihisha na kuboresha tafsiri hiyo. Hivyo, wataalamu wawili wa lugha, David Johns na Joseph Freeman, walitumwa kutoka Uingereza ili wasaidie.

Kukabiliana na Vizuizi

Wakati kazi ya kutafsiri Biblia katika Kimalagasi ilipokamilika, shirika la LMS lilimtuma Charles Hovenden aunganishe mashini ya kwanza ya kuchapisha nchini Madagaska. Hovenden alifika Novemba 21, 1826 (21/11/1826). Hata hivyo, alishikwa na malaria na akafa mwezi mmoja tu baada ya kufika na hakuna mtu ambaye angeweza kutumia mashini hiyo ya kuchapisha. Mwaka uliofuata, James Cameron, fundi mwenye ustadi kutoka Scotland, alifaulu kuunganisha mashini hiyo ya kuchapisha akitumia kitabu cha maagizo ambacho alipata katikati ya visehemu vya mashini hiyo. Baada ya kujaribu-jaribu mara nyingi, Cameron alifaulu kuchapisha sehemu ya kitabu cha Mwanzo sura ya 1 mnamo Desemba 4, 1827. *

Kizuizi kingine kilitokea Julai 27, 1828 (27/7/1828), baada ya kifo cha Radama wa Kwanza. Mfalme Radama alikuwa ameunga mkono sana kazi hiyo ya kutafsiri. Wakati huo David Jones alisema hivi: “Mfalme Radama ni mchangamfu na mwenye fadhili kwelikweli. Anapenda sana elimu kuliko Dhahabu na Fedha, na anaheshimu sana mafundisho ambayo watu wake wanapata kuhusu mambo ya ustaarabu.” Hata hivyo, baada ya kifo cha mfalme huyo, mke wake, Ranavalona wa Kwanza alianza kutawala, na punde si punde ikawa wazi kwamba hangeunga mkono kazi ya kutafsiri kama mume wake alivyofanya.

Muda mfupi baada ya malkia huyo kutawazwa, mgeni fulani kutoka Uingereza aliomba kuzungumza naye kuhusu kazi ya kutafsiri. Hakupewa ruhusa. Pindi nyingine, wamishonari walipomwambia malkia huyo kwamba bado walikuwa na mambo mengi ya kuwafundisha watu, kutia ndani lugha ya Kigiriki na Kiebrania, aliwaambia hivi: “Mimi sijali sana kuhusu Kigiriki na Kiebrania, lakini ningependa kujua ikiwa mnaweza kuwafundisha watu wangu jambo linaloweza kuwasaidia zaidi, kama vile kutengeneza sabuni.” Akitambua kwamba huenda wangelazimika kuondoka kabla ya Biblia ya Kimalagasi kukamilika, Cameron aliomba juma moja ili ayafikirie maneno ya malkia.

Juma lililofuata, Cameron aliwapa wajumbe wa kifalme wa malkia vipande viwili vidogo vya sabuni iliyotengenezwa kwa vitu vilivyopatikana katika eneo hilo. Jambo hilo pamoja na kazi nyingine ambazo zilifanywa na wamishonari wenye ustadi mbalimbali zilimtuliza malkia kwa muda ambao ulitosha kumaliza kuchapisha karibu vitabu vyote vya Maandiko ya Kiebrania.

Habari Njema, Kisha Jambo Lenye Kuvunja Moyo

Ingawa mwanzoni malkia aliwapinga wamishonari, mnamo Mei 1831 alitoa amri yenye kusisimua. Angewaruhusu raia wake wabatizwe na kuwa Wakristo! Lakini uamuzi huo haukudumu kwa muda mrefu. Kulingana na kitabu kimoja (A History of Madagascar), “idadi ya watu waliokuwa wakibatizwa iliwashtua watu walioishi katika makao ya mfalme ambao hawakutaka mabadiliko, na wakamsadikisha malkia kwamba ibada ya ushirika ilikuwa sawa na kula kiapo cha utii kwa Uingereza.” Hivyo, kibali cha ubatizo wa Kikristo kilifutiliwa mbali mwishoni mwa mwaka wa 1831, baada ya muda wa miezi sita tu.

Kwa kuwa malkia alikuwa kigeugeu, na pia kwa sababu ya uvutano uliokuwa unaongezeka kutoka kwa watu waliopenda utamaduni ambao walikuwa katika serikali, wamishonari walijitahidi sana kumaliza kazi ya kuchapisha Biblia. Tayari Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yalikuwa yamechapishwa, na maelfu ya nakala zilikuwa zinasambazwa. Hata hivyo, kizuizi kingine kilitokea Machi 1, 1835, wakati Malkia Ranavalona wa Kwanza alipopiga marufuku Ukristo na akaamuru kwamba vitabu vyote vya Kikristo vipelekwe kwa wenye mamlaka.

Pia, amri ya malkia ilimaanisha kwamba wanafunzi wa Malagasi hawangeendelea na kazi ya kuchapisha. Hivyo, wamishonari wachache tu ambao wangemaliza kazi hiyo waliendelea na kazi mchana na usiku na mwishowe, Juni (Mwezi wa 6) 1835, Biblia nzima ilichapishwa. Ndiyo, hatimaye kulikuwa na Biblia ya Kimalagasi!

Kwa sababu ya marufuku, Biblia ziligawanywa haraka haraka, na nakala 70 za Maandiko zikazikwa ili kuzihifadhi zisiharibiwe. Hatua hiyo ilichukuliwa wakati uliofaa kwa sababu katika kipindi kisichozidi mwaka mmoja, wamishonari wengi waliondoka kwenye kisiwa hicho na wawili tu ndio waliobaki. Lakini neno la Mungu lilikuwa linasambaa kwenye Kisiwa Kikubwa Chekundu.

Jinsi Watu wa Madagaska Wanavyopenda Biblia

Watu wa Madagaska walifurahi sana kuweza kusoma Neno la Mungu kwa lugha yao wenyewe! Tafsiri hiyo ina makosa mengi, na lugha iliyotumiwa ni tofauti na ile inayozungumzwa leo. Lakini bado, si rahisi kupata nyumba ambayo haina Biblia, na watu wengi wa Madagaska wanaisoma kwa ukawaida. Jambo moja ambalo linaonekana wazi katika tafsiri hiyo ni jinsi ambavyo jina la Mungu, Yehova, limetumiwa sana katika Maandiko ya Kiebrania. Katika nakala za awali, jina la Mungu linapatikana pia katika Maandiko ya Kigiriki. Hivyo basi, watu wengi wa Madagaska wanafahamu jina la Mungu.

Kwa kweli, wakati nakala za kwanza za Maandiko ya Kigiriki zilipochapishwa, Bw. Baker, ambaye alikuwa anafanya kazi kwenye mashini ya uchapishaji aliona shangwe ya watu wa Madagaska na akasema hivi: “Sitaki kutoa unabii, lakini siwezi kuamini kwamba siku moja neno la Mungu litaondolewa kabisa katika nchi hii!” Maneno yake yamethibitika kuwa ya kweli. Wala malaria, wala tatizo la kujifunza lugha ngumu, au hata amri kali ya mtawala haingeweza kuzuia Neno la Mungu lisienee nchini Madagaska.

Sasa hali imekuwa bora zaidi. Jinsi gani? Mnamo 2008, Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kimalagasi ilitolewa. Tafsiri hiyo ni hatua kubwa sana ya maendeleo kwa sababu imeandikwa kwa lugha ya kisasa ambayo inaeleweka kwa urahisi. Hivyo, Neno la Mungu limetia mizizi hata zaidi kwenye Kisiwa Kikubwa Chekundu.—Isa. 40:8.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 14 Sehemu za kwanza kabisa za Biblia zilizochapishwa katika Kimalagasi ni Amri Kumi, na Sala ya Bwana, sehemu hizo zilichapishiwa huko Mauritius kati ya Aprili (Mwezi wa 4) na Mei 1826. Hata hivyo, familia ya Mfalme Radama na maofisa fulani wa serikali ndio tu waliopewa nakala hizo.

[Picha katika ukurasa wa 31]

“Tafsiri ya Ulimwengu Mpya” katika Kimalagasi inaheshimu jina la Mungu, Yehova