Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtazamo Unaofaa Kuhusu Pombe

Mtazamo Unaofaa Kuhusu Pombe

Mtazamo Unaofaa Kuhusu Pombe

TONY anayetajwa katika makala ya kwanza angaliweza kufurahia maisha kama angalikubali ana tatizo la kunywa kupita kiasi. Lakini, kwa sababu aliweza kunywa pombe nyingi bila dalili yoyote iliyoonekana wazi, alifikiri kwamba hakuwa na tatizo lolote. Kwa nini maoni yake yalikuwa yenye kupotoka sana?

Ni kwa sababu maoni yake yalikuwa yamepotoshwa na zoea lake la kunywa pombe kupita kiasi. Hatujui kama Tony alitambua kwamba ubongo wake ulioongoza mwili, akili, na hisia zake, haukufanya kazi sawasawa alipokuwa amelewa. Kadiri alivyokunywa, ndivyo ubongo wake ulivyoshindwa kutambua hali yake.

Sababu nyingine iliyofanya Tony asiweze kutambua tatizo lake ni tamaa yake ya kuendelea kunywa. Allen, anayetajwa katika makala zinazotangulia, alikuwa akikana kwamba anakunywa pombe kupita kiasi. Anasema hivi: “Nilificha zoea langu la kunywa, nilitoa udhuru, na kusisitiza kwamba sikuwa nikinywa pombe nyingi. Nilikuwa na lengo moja tu—kuendelea kunywa.” Ijapokuwa wengine waliona kwamba pombe ilianza kutawala Tony na Allen, wote wawili waliendelea kujisadikishia kwamba mambo ni shwari. Wote wawili walihitaji kuchukua hatua ili kudhibiti zoea lao la kunywa. Lakini wangechukua hatua gani?

Chukua Hatua!

Wengi ambao wameacha kunywa kupita kiasi, wamefanya kama Yesu alivyohimiza: “Ikiwa, sasa, hilo jicho lako la kuume linakufanya ukwazike, ling’oe ulitupilie mbali nawe. Kwa maana kuna faida zaidi kwako kimoja cha viungo vyako kipotee kuliko mwili wako wote utupwe ndani ya Gehena.”—Mathayo 5:29.

Ni wazi kwamba Yesu hakuwashauri watu wakate viungo halisi vya mwili, bali alikazia kwa njia ya mfano kwamba tunapaswa kuwa tayari kuondoa katika maisha yetu chochote kinachoweza kutudhuru kiroho. Ni kweli kwamba linaweza kuwa jambo gumu na lenye kuumiza sana kuchukua hatua kama hiyo. Lakini tutaepuka mawazo na hali zinazoweza kufanya tunywe pombe kupita kiasi. Kwa hiyo, ikiwa watu wengine wametaja kwamba unakunywa pombe kupita kiasi, chukua hatua ya kudhibiti zoea lako la kunywa. * Ikiwa unatambua kwamba huwezi kunywa pombe kwa kiasi, uwe tayari kuacha pombe kabisa. Ijapokuwa hilo linaweza kuwa jambo gumu na lenye kuumiza sana, ni afadhali kufanya hivyo kuliko kuharibu maisha yako.

Hata kama wewe si mlevi sugu, je, unakunywa kupita kiasi mara kwa mara? Ikiwa ndivyo, unaweza kuchukua hatua gani ili uwe na mtazamo unaofaa kuhusu pombe?

Unaweza Kupata Msaada

1. Tegemea nguvu zinazopatikana kwa kusali mara nyingi kwa moyo wote. Biblia inawashauri hivi wote wanaotaka kumpendeza Yehova Mungu: “Katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Unaweza kusali kuhusu mambo gani ili upate amani hiyo ya akili?

Taja wazi kwamba una tatizo la kunywa pombe kupita kiasi, tatizo ambalo umejiletea mwenyewe. Mwambie Mungu kile unachotaka kufanya kuhusu tatizo lako, naye atabariki jitihada zako za kupata suluhisho na kuepuka matatizo makubwa zaidi. “Anayefunika makosa yake hatafanikiwa, lakini yeye anayeyaungama na kuyaacha ataonyeshwa rehema.” (Methali 28:13) Yesu alitufundisha kusali hivi: “Usituingize katika jaribu, bali utukomboe na maovu.” (Mathayo 6:13; maelezo ya chini katika NW yenye marejeo) Unaweza kutenda kupatana na sala kama hizo jinsi gani, na unaweza kupata wapi majibu kwa sala zako?

2. Jiimarishe kwa kusoma Neno la Mungu. “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu . . . nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.” (Waebrania 4:12) Watu wengi waliokuwa wakinywa kupita kiasi wamesaidiwa kwa kusoma na kutafakari kila siku kuhusu maandiko ya Biblia. Mtunga-zaburi aliyemcha Mungu aliandika hivi: “Mwenye furaha ni mtu ambaye hakutembea katika shauri la waovu, . . . bali mapendezi yake ni katika sheria ya Yehova, naye huisoma sheria yake kwa sauti ya chini mchana na usiku. . . . Kila jambo analofanya litafanikiwa.”—Zaburi 1:1-3.

Allen alipata nguvu ya kuacha ulevi kwa kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Anasema hivi: “Nina hakika kwamba mimi niko hai leo kwa sababu Biblia na kanuni za Biblia zilinisaidia kuacha ulevi.”

3. Sitawisha sifa ya kujizuia. Biblia inaonyesha kwamba watu katika kutaniko la Kikristo waliokuwa walevi hapo awali walioshwa na wakawa safi “kwa roho ya Mungu wetu.” (1 Wakorintho 6:9-11) Jinsi gani? Walikuwa wamesaidiwa kuacha ulevi na karamu za kupindukia kwa kusitawisha sifa ya kujizuia kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu. “Msiwe mkilewa divai, ambayo ina upotovu ndani yake, bali endeleeni kujazwa na roho.” (Waefeso 5:18; Wagalatia 5:21-23) Yesu Kristo aliahidi kwamba ‘Baba aliye mbinguni angewapa roho takatifu wale wanaomwomba.’ Kwa hiyo, ‘endelea kuomba, nawe utapewa.’—Luka 11:9, 13.

Watu wanaotaka kumwabudu Yehova kwa njia anayokubali wanaweza kusitawisha sifa ya kujizuia kwa kusoma na kujifunza Biblia, na pia kwa kusali mara nyingi kwa moyo. Usivunjike moyo, bali tegemea ahadi hii katika Neno la Mungu: “Anayepanda kwa roho atavuna uzima wa milele kutokana na roho. Kwa hiyo na tusife moyo katika kufanya yaliyo mema, kwa maana katika majira yanayofaa tutavuna ikiwa hatuchoki kabisa.”—Wagalatia 6:8, 9.

4. Chagua marafiki wazuri. “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” (Methali 13:20) Waambie marafiki wako kwamba umeazimia kudhibiti zoea lako la kunywa pombe. Hata hivyo, Neno la Mungu linasema kwamba baadhi ya wale waliokuwa marafiki wako hapo awali ‘watashangaa na kuendelea kukutukana’ unapoacha kunywa “divai kupita kiasi,” au kushirikiana nao katika “karamu za kupindukia, [na] mashindano ya kunywa.” (1 Petro 4:3, 4) Uwe tayari kuvunja urafiki pamoja na wale wanaotaka kukuvunja moyo usishikilie azimio lako la kudhibiti zoea lako la kunywa.

5. Weka mipaka. “Acheni kufanyizwa kulingana na mfumo huu wa mambo [au, ulimwengu huu], bali mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu, ili mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Waroma 12:2) Ukiruhusu kanuni za Neno la Mungu zikusaidie kuweka mipaka badala ya kuwaruhusu marafiki au ulimwengu huu kufanya hivyo, utakuwa na maisha yanayompendeza Mungu. Lakini unaweza kujua jinsi gani kiasi cha pombe kinachokufaa?

Kiasi chochote cha pombe kinachopunguza au kudhoofisha uwezo wako wa kufikiri, kimepita kiasi kwako. Kwa hiyo, ukiamua kunywa pombe, ni jambo la hekima kuweka mpaka ulio wazi kabisa. Unapochunguza zoea lako la kunywa, usipuuze dalili zinazoonyesha wazi hali yako. Weka mpaka ulio wazi na utakaokulinda, yaani, mpaka ambao hautakuruhusu kunywa kupita kiasi au kulewa.

6. Jifunze kukataa. “Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, Siyo yenu, Siyo.” (Mathayo 5:37) Jifunze jinsi ya kukataa bila kumwudhi mtu anayekukaribisha kwa fadhili unywe. “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.”—Wakolosai 4:6.

7. Omba msaada. Waombe msaada marafiki wanaokuunga mkono ambao wanaweza kuimarisha azimio lako la kutokunywa kupita kiasi na kukusaidia kiroho. “Wawili ni afadhali kuliko mmoja, kwa maana wana thawabu nzuri kwa ajili ya kazi yao ngumu. Kwa maana mmoja wao akianguka, yule mwingine anaweza kumwinua mwenzake.” (Mhubiri 4:9, 10; Yakobo 5:14, 16) Taasisi ya Kitaifa ya Ulevi na Ulevi Sugu ya Marekani inashauri hivi: “Huenda ikawa vigumu kupunguza kiasi cha pombe unachokunywa. Hivyo, waombe watu wa familia na marafiki wakusaidie ili ufikie lengo lako.”

8. Shikilia azimio lako. “Iweni watendaji wa neno, na si wasikiaji tu, mkijidanganya wenyewe kwa mawazo yasiyo ya kweli. Lakini yeye anayechunguza ndani ya sheria kamilifu iliyo ya uhuru na ambaye hudumu katika hiyo, mtu huyo, kwa sababu amekuwa, si msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, atakuwa mwenye furaha katika kuitenda.”—Yakobo 1:22, 25.

Kuacha Ulevi

Si kila mtu anayekunywa pombe kupita kiasi anayekuwa mlevi sugu. Lakini baadhi ya watu wanaokunywa kwa ukawaida pombe nyingi, wanakuwa walevi sugu. Kwa kuwa mwili na akili za walevi sugu zimezoea sana pombe, watu hao hawawezi kuacha ulevi kwa kujidhibiti tu au kwa kupata msaada wa kiroho. Allen anasema: “Nilipokuwa nikijitahidi kuacha pombe, nilipatwa na maumivu makali sana. Ndipo nilipotambua kwamba ingawa nilikuwa nikipata msaada wa kiroho, nilihitaji pia matibabu.”

Walevi wengi wanahitaji matibabu ili kuwasaidia katika pigano lao la kiroho la kuacha ulevi na kuepuka kuurudia. * Baadhi yao wanahitaji kulazwa hospitalini ili waweze kupambana na maumivu makali yanayowapata wanapoacha kunywa pombe, au ili wapate dawa za kupunguza tamaa ya pombe na kuwasaidia wasirudie ulevi tena. Mwana wa Mungu aliye na nguvu za kufanya miujiza alisema hivi: “Wale walio na nguvu hawahitaji tabibu, bali wale walio wagonjwa wanamhitaji.”—Marko 2:17.

Manufaa ya Kufuata Mwongozo wa Mungu

Mashauri ya Biblia yenye hekima kuhusu pombe yanatoka kwa Mungu wa kweli, anayetaka tufurahie maisha sasa na milele. Miaka 24 baada ya kuacha pombe, Allen anasema hivi: “Nilifurahi sana nilipojua kwamba ninaweza kubadilika, na kujua kwamba Yehova alitaka kunisaidia kurekebisha mambo yaliyokuwa yameenda kombo maishani mwangu, na kwamba yeye . . . ” Allen anatua ili kuzuia machozi yanayotaka kububujika anapokumbuka mambo ya zamani. “Yaani, . . . ni jambo zuri sana kujua kwamba Yehova anaelewa, anajali, na anasaidia.”

Kwa hiyo, ikiwa unakunywa pombe kupita kiasi au wewe ni mlevi sugu, usikate tamaa haraka, wala usiamue kwamba hakuna tumaini. Allen pamoja na wengine wengi wamekuwa katika hali ambayo unakabili sasa, nao wamefaulu kupunguza kiasi cha pombe wanachokunywa au wameacha kunywa kabisa. Hawajuti hata kidogo; nawe hutajuta.

Iwe unaamua kunywa pombe kwa kiasi au la, fanya kama Mungu anavyohimiza kwa upendo: “Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto, na uadilifu wako kama mawimbi ya bahari.”—Isaya 48:18.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ona sanduku  “Je, Pombe Inanitawala?” kwenye ukurasa wa 8.

^ fu. 24 Kuna vituo vingi vya tiba, hospitali, na mipango mingine ya msaada. Mnara wa Mlinzi halipendekezi matibabu yoyote hususa. Kila mtu anapaswa kuchunguza matibabu mbalimbali na kufanya uamuzi unaopatana na kanuni za Biblia.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]

 Je, Pombe Inanitawala?

Jiulize:

• Je, ninakunywa pombe nyingi sasa kuliko hapo awali?

• Je, ninakunywa mara nyingi sasa kuliko hapo awali?

• Je, ninakunywa pombe kali sasa kuliko hapo awali?

• Je, ninakunywa ili kutuliza mfadhaiko au kusahau matatizo?

• Je, rafiki au mtu wa familia yangu ametaja kwamba ana wasiwasi kuhusu zoea langu la kunywa?

• Je, nimepata matatizo nyumbani, kazini, au safarini kwa sababu ya zoea langu la kunywa?

• Je, ni vigumu kwangu kukaa juma moja bila kunywa pombe?

• Je, ninaona vibaya wengine wasipokunywa pombe?

• Je, ninakunywa kisiri ili wengine wasijue kiasi cha pombe ninachokunywa?

Ukijibu ndiyo kwa swali moja au zaidi kati ya hayo, unahitaji kuchukua hatua ya kupunguza au kuacha kunywa pombe.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Kufanya Maamuzi ya Hekima Kuhusu Pombe

Kabla ya kunywa pombe, jiulize:

Je, ni jambo la hekima kwangu kunywa pombe, au ni afadhali nisinywe?

Inapendekezwa: Mtu ambaye hawezi kunywa kwa kiasi anapaswa kuacha kunywa kabisa.

Ni kiasi gani cha pombe kinachonifaa?

Inapendekezwa: Amua kiasi utakachokunywa kabla pombe haijapotosha uwezo wako wa kufikiri.

Ni wakati gani unaofaa kunywa?

Inapendekezwa: Usinywe kabla ya kuendesha gari, kabla ya kufanya shughuli zinazotaka uwe makini, kabla ya kushiriki katika mambo ya dini, wala unapokuwa na mimba au unapotumia dawa fulani.

Ni mahali gani panapofaa kunywea pombe?

Inapendekezwa: Mazingira yanayofaa ni muhimu; usinywe kisiri ili kuficha kwamba unakunywa, wala usinywe mbele ya watu wanaoudhika kumwona mtu akinywa pombe.

Ninywe pombe pamoja na nani?

Inapendekezwa: Kunywa tu pamoja na marafiki au watu wa familia ambao hawatakupotosha; bali si pamoja na watu walio na tatizo la kunywa kupita kiasi.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

Neno la Mungu Lamsaidia Mtu Aliyekuwa Mlevi

Supot anayeishi nchini Thailand alikuwa mlevi. Mwanzoni alikuwa akinywa jioni tu. Hatimaye alianza kunywa asubuhi na pia wakati wa pumziko la mchana. Mara nyingi alikunywa kusudi tu alewe. Kisha, akaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Supot aliacha kunywa alipojifunza kwamba Yehova Mungu hakubali ulevi. Lakini, baada ya muda akarudia ulevi. Watu wa familia yake walihuzunika sana.

Hata hivyo, Supot bado alimpenda Yehova na alitaka kumwabudu ifaavyo. Marafiki wa Supot waliendelea kumsaidia na kuwatia moyo watu wa familia yake watumie wakati mwingi zaidi pamoja naye, na wasiache kumsaidia. Wakati huo, andiko la 1 Wakorintho 6:10 linalosema wazi kwamba ‘walevi hawataurithi ufalme wa Mungu,’ lilimsaidia Supot kuona umuhimu wa kuacha ulevi. Alitambua kwamba alihitaji kufanya jitihada ya kufa na kupona ili kuacha ulevi.

Supot aliazimia kuacha kabisa kunywa pombe. Hatimaye, kwa nguvu za roho takatifu ya Mungu, mwongozo wa Neno la Mungu, na msaada wa watu wa familia na ndugu kutanikoni, Supot alipata nguvu za kiroho na akashinda tamaa ya pombe. Watu wa familia yake walifurahi sana alipobatizwa ili kuonyesha kwamba alikuwa amejiweka wakfu kwa Mungu. Sasa Supot ana ule uhusiano wa karibu pamoja na Mungu ambao alitamani kuwa nao tangu zamani, na anatumia wakati wake kuwasaidia wengine kiroho.