Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Alikuwa Mshikamanifu Alipokabili Majaribu

Alikuwa Mshikamanifu Alipokabili Majaribu

Igeni Imani Yao

Alikuwa Mshikamanifu Alipokabili Majaribu

PETRO alitazama kwa wasiwasi nyuso za watu waliokuwa wakimsikiliza Yesu. Walikuwa katika sinagogi la Kapernaumu. Petro aliishi katika mji huu; alifanya biashara yake ya kuvua samaki hapa kwenye fuo za Bahari ya Galilaya; wengi wa marafiki wake, watu wa ukoo, na watu aliofanya biashara pamoja nao waliishi hapa. Bila shaka, Petro alitamani watu wa mji wao wawe na maoni sawa na yake kumhusu Yesu, wasisimke kama yeye kujifunza kuhusu Ufalme wa Mungu kutoka kwa yule mwalimu mkuu zaidi kushinda wote. Lakini inaonekana mambo yangekuwa tofauti siku hii.

Wengi walikuwa wameacha kumsikiliza. Baadhi yao walikuwa wakinung’unika kwa sauti, wakipinga ujumbe wa Yesu. Lakini, kilichomsumbua Petro zaidi ni jinsi baadhi ya wanafunzi wa Yesu mwenyewe walivyofanya waliposikia ujumbe wake. Nyuso zao hazikuonyesha msisimko wowote unaotokana na kujifunza jambo jipya, shangwe ya kujifunza kweli. Sasa walionekana wenye hasira, hata wenye uchungu. Baadhi yao walisema kwamba maneno ya Yesu yalikuwa yenye kushtua. Walikataa kuendelea kumsikiliza, wakatoka kwenye sinagogi, na hata wakaacha kumfuata.

Ulikuwa wakati mgumu kwa Petro na kwa mitume wenzake. Petro hakuelewa vizuri yale ambayo Yesu alisema siku hiyo. Kwa kweli, aliona kwa nini maneno ya Yesu yangeweza kuudhi yasipofafanuliwa vizuri. Petro angefanya nini? Hii haikuwa mara ya kwanza kwa ushikamanifu wake kwa Bwana wake kujaribiwa, wala haingekuwa ya mwisho. Hebu tuone jinsi imani ya Petro ilivyomsaidia kukabili majaribu hayo na kudumisha ushikamanifu wake.

Petro Adumisha Ushikamanifu Wengine Wanaposhindwa

Mara nyingi, Yesu alimshangaza Petro. Tena na tena, Bwana wake alitenda na kusema kinyume cha matarajio ya watu. Siku moja tu kabla ya hapo, Yesu alikuwa amewalisha kimuujiza maelfu ya watu, nao wakajaribu kumfanya mfalme. Lakini aliwashangaza wengi alipoondoka na kuwaagiza wanafunzi wake wapande mashua kwenda Kapernaumu. Wanafunzi wake walipokuwa wakisafiri kwa mashua usiku, Yesu aliwashangaza tena kwa kutembea juu ya Bahari ya Galilaya yenye dhoruba. Wakati huo Petro alijifunza jambo muhimu kuhusu imani. *

Asubuhi, walikuta kwamba wale watu walikuwa wamepanda mashua kwenda kuwatafuta. Lakini, ni wazi kwamba watu hao walikuwa wanasukumwa na tamaa ya kuona Yesu akitokeza chakula tena kimuujiza, bali si tamaa ya kujifunza kweli. Yesu aliwakemea kwa sababu ya mtazamo wao wa kupenda vitu vya kimwili. Aliendelea kuwafundisha katika sinagogi mjini Kapernaumu, ambapo kwa mara nyingine tena, Yesu alitenda kinyume cha matarajio ya watu alipojaribu kuwafunza kweli muhimu, lakini ngumu kueleweka.

Yesu alitaka watu hao wasimwone tu kuwa mwandalizi wa chakula cha kimwili, bali wamwone kuwa yule ambaye Mungu ameandaa ili kupitia maisha na kifo chake akiwa mwanadamu, wengine waweze kupata uzima wa milele. Kwa hiyo, akawapa mfano kwa kujilinganisha na mana, mkate uliotoka mbinguni wakati wa Musa. Baadhi ya watu walipopinga, alitumia mfano ulio wazi zaidi na kuwaeleza kwamba ilikuwa lazima wale mwili na damu yake ili wapate uzima. Wakati huo ndipo watu walipokazana kumpinga. Wengine walisema: “Maneno hayo yanashtua; ni nani ambaye anaweza kuyasikiliza?” Wengi wa wanafunzi wa Yesu waliamua kumwacha. *Yohana 6:48-60, 66.

Petro angefanya nini? Yeye pia alitatanishwa na maneno ya Yesu. Bado hakuelewa ni lazima Yesu afe ili atimize mapenzi ya Mungu. Je, Petro alishawishiwa kuacha kumfuata Yesu kama wanafunzi hao wasio na msimamo waliomwacha siku hiyo? Hapana; Petro alikuwa na sifa muhimu iliyomfanya awe tofauti na watu hao. Sifa gani hiyo?

Yesu aliwageukia mitume wake na kuwauliza: “Je, ninyi pia mnataka kwenda?” (Yohana 6:67) Aliwauliza mitume wote 12, lakini Petro ndiye aliyeongea. Petro alifanya hivyo mara nyingi. Huenda Petro ndiye aliyekuwa na umri mkubwa kati yao. Vyovyote vile, Petro kwa hakika ndiye aliyeongea waziwazi kati ya mitume, na mara nyingi hakusita kusema yaliyokuwa akilini mwake. Wakati huo, alikuwa na maneno haya mazuri akilini ambayo yanastahili kukumbukwa: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele.”—Yohana 6:68.

Maneno hayo yanagusa moyo sana. Petro alimwamini Yesu, na imani yake ilimsaidia kuwa na sifa fulani nzuri sana—ushikamanifu. Petro alielewa wazi kwamba hakuna Mwokozi mwingine ila Yesu, na kwamba Yesu aliwaokoa watu kupitia mafundisho yake kuhusu Ufalme wa Mungu. Petro alijua kwamba hata kama kulikuwa na mambo ambayo hakuelewa, hakuna mahali pengine ambapo angeweza kwenda kama angetaka kukubaliwa na Mungu na kupata uzima wa milele.

Je, unahisi hivyo? Inasikitisha kwamba watu wengi ulimwenguni leo wanadai wanampenda Yesu, lakini wanashindwa kuwa washikamanifu kwake. Ushikamanifu wa kweli kwa Kristo unamaanisha kuwa na maoni kama ya Petro kuhusu mafundisho ya Yesu. Tunahitaji kuyajua, kuelewa maana yake, na kuyafuata—hata yanapokuwa kinyume cha matarajio yetu au mapendezi yetu. Tunaweza kuwa na tumaini la kupata uzima wa milele ambao Yesu anataka tuufurahie, ikiwa tu tutakuwa washikamanifu.

Adumisha Ushikamanifu Anaporekebishwa

Muda mfupi baada ya wakati huo wenye shughuli nyingi, Yesu aliongoza mitume wake na baadhi ya wanafunzi wake, katika safari ndefu kuelekea kaskazini. Nyakati nyingine, kilele chenye theluji cha Mlima Hermoni, uliokuwa upande wa kaskazini zaidi mwa Nchi ya Ahadi, kilionekana kutoka kwenye Bahari ya Galilaya yenye maji ya bluu. Hatua kwa hatua, sehemu kubwa ya mlima huo ilionekana kadiri walivyoukaribia, wakipanda eneo lenye mwinuko kuelekea kwenye vijiji fulani karibu na Kaisaria Filipi. * Wakiwa katika mandhari hii yenye kuvutia, ambapo wangeweza kuona sehemu kubwa ya Nchi ya Ahadi upande wa kusini, Yesu aliwauliza wafuasi wake swali fulani muhimu.

Aliwauliza hivi: “Umati unasema mimi ni nani?” Tunaweza kuwazia Petro akiyatazama macho ya Yesu yenye utambuzi, na kwa mara nyingine akatambua jinsi Bwana wake alivyokuwa mwenye fadhili na akili nyingi. Yesu alitaka kujua maoni ya wasikilizaji wake kuhusu mambo waliyoona na kusikia. Wanafunzi wa Yesu walijibu swali hilo kwa kutaja baadhi ya maoni yenye makosa kuhusu utambulisho wa Yesu, ambayo watu wengi walikuwa nayo. Lakini Yesu alitaka kujua mengi zaidi. Alitaka kujua kama wafuasi wake wa karibu zaidi walikuwa na maoni kama hayo yenye makosa. Hivyo akawauliza, “Ninyi mnasema mimi ni nani?”—Luka 9:18-22.

Kwa mara nyingine, Petro alikuwa mwepesi kujibu. Alitaja wazi na kwa ujasiri maoni ya wengi waliokuwa pale. Alisema: “Wewe ndiye Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.” Tunaweza kuwazia Yesu akitabasamu na kumpongeza Petro kwa shauku. Yesu alimkumbusha Petro kwamba Yehova Mungu—bali si mwanadamu—ndiye aliyefunua kweli hiyo muhimu kwa wale wenye imani ya kweli. Petro alikuwa amewezeshwa kutambua mojawapo ya kweli muhimu zaidi ambazo Yehova alikuwa amefunua hadi wakati huo, yaani, utambulisho wa Masihi, au Kristo, aliyeahidiwa zamani!—Mathayo 16:16, 17.

Unabii wa kale ulimwita Kristo huyo jiwe ambalo wajenzi wangelikataa. (Zaburi 118:22; Luka 20:17) Akiwa na unabii huo akilini, Yesu alifunua kwamba Yehova angeanzisha kutaniko juu ya jiwe hilo au mwamba, ambao Petro alikuwa ametoka tu kuutambulisha. * Kisha akampa Petro mapendeleo muhimu sana katika kutaniko hilo. Hakumpa Petro mamlaka makubwa kuliko mitume wengine, kama watu wengine wanavyofikiri, lakini alimpa majukumu mbalimbali. Alimpa Petro “funguo za ufalme wa mbinguni.” (Mathayo 16:19) Lingekuwa jukumu la Petro kufungulia makundi matatu ya wanadamu tumaini la kuingia katika Ufalme wa Mungu—kwanza Wayahudi, kisha Wasamaria, na mwishowe Watu wa Mataifa, au watu wasio Wayahudi.

Lakini, baadaye Yesu alisema kwamba wale wanaopewa mengi wanadaiwa mengi, na ukweli wa maneno hayo unaonekana katika kisa cha Petro. (Luka 12:48) Yesu aliendelea kufunua kweli muhimu kumhusu Masihi. Kwa mfano, alifunua kwamba karibuni ingekuwa lazima Masihi ateseke na kufa jijini Yerusalemu. Mambo hayo yalimtia Petro wasiwasi. Alimchukua Yesu kando na kumkemea akisema: “Jitendee kwa fadhili, Bwana; wewe hutapatwa hata kidogo na jambo hili.”—Mathayo 16:21, 22.

Petro hakuwa na nia mbaya, lakini bila shaka jibu la Yesu lilimshangaza. Yesu alimgeuzia Petro mgongo na kuwatazama wanafunzi wale wengine—ambao labda walikuwa na maoni kama ya Petro—na kusema: “Nenda nyuma yangu, Shetani! Wewe ni kikwazo kwangu, kwa sababu wewe unafikiri, si fikira za Mungu, bali za wanadamu.” (Mathayo 16:23; Marko 8:32, 33) Maneno ya Yesu yana ushauri mzuri kwetu sote. Ni rahisi sana kutanguliza maoni ya kibinadamu kuliko maoni ya Mungu. Tukifanya hivyo, hata kama tuna nia ya kusaidia, tunaweza kuwa tunaendeleza kusudi la Shetani bila kujua, badala ya kuendeleza kusudi la Mungu. Petro aliitikia jinsi gani?

Bila shaka, Petro alijua kwamba Yesu hakumaanisha yeye ni Shetani Ibilisi. Yesu hakuzungumza na Petro jinsi alivyozungumza na Shetani. Yesu alimwambia Shetani: “Nenda zako”; na kumwambia Petro: “Nenda nyuma yangu.” (Mathayo 4:10) Yesu hakumkataa mtume huyo ambaye alijua alikuwa na sifa nyingi nzuri, lakini alirekebisha tu maoni yake yenye makosa kuhusu jambo hilo. Si vigumu kuona kwamba Petro alihitaji kuacha kuwa kama jiwe la kukwaza mbele ya Bwana wake, na badala yake, kuwa mfuasi wake mshikamanifu.

Je, Petro alibishana na Yesu, akakasirika, au akanuna? Hapana; alikubali rekebisho la Yesu kwa unyenyekevu. Hivyo, akaonyesha tena ushikamanifu wake. Mara kwa mara wafuasi wote wa Kristo wanahitaji kurekebishwa. Tunaweza kuendelea kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yesu Kristo na Baba yake, Yehova Mungu, ikiwa tu tutakubali nidhamu kwa unyenyekevu na kujifunza kutokana nayo.—Methali 4:13.

Apata Thawabu kwa Sababu ya Ushikamanifu

Muda si muda, Yesu alitaja jambo jingine lenye kushangaza: “Kwa kweli ninawaambia ninyi kwamba kuna baadhi ya wale wanaosimama hapa ambao hawataonja kifo kamwe mpaka kwanza wamwone Mwana wa binadamu akija katika ufalme wake.” (Mathayo 16:28) Bila shaka, maneno hayo yalimfanya Petro atake kujua mengi zaidi. Yesu alimaanisha nini? Labda Petro aliwaza kwamba hangeweza kupata mapendeleo kama hayo ya pekee kwa sababu muda mfupi uliopita, Yesu alikuwa amemkemea vikali.

Hata hivyo, juma moja hivi baadaye, Yesu alimchukua Yakobo, Yohana, na Petro na kupanda juu “katika mlima mrefu”—labda Mlima Hermoni, ambao haukuwa mbali sana. Yaelekea ilikuwa usiku, kwa kuwa wanaume hao watatu walikuwa wakipambana na usingizi. Lakini Yesu alipokuwa akisali, jambo fulani lilitokea na kuwafanya wawe macho kabisa.—Mathayo 17:1; Luka 9:28, 29, 32.

Yesu alianza kubadilika mbele ya macho yao. Uso wake ulianza kung’aa na kuwa mwangavu kama jua. Mavazi yake pia yalibadilika yakawa meupe na yenye kumetameta. Kisha watu wawili wakatokea na kusimama pamoja naye. Mmoja aliwakilisha Musa na yule mwingine Eliya. Walizungumza naye kuhusu “kuondoka kwake ambako angetimiza huko Yerusalemu,” yaani, kifo na ufufuo wake. Ilikuwa wazi kabisa kwamba Petro alikuwa amekosea kutokubali kuwa karibuni Yesu angeteseka na kufa!—Luka 9:30, 31.

Petro alihisi kwamba alipaswa kushiriki kwa njia fulani katika maono hayo yenye kustaajabisha. Ilionekana kama Musa na Eliya walikuwa wanamwacha Yesu. Kwa hiyo Petro akasema: “Mwalimu, ni vizuri kwetu kuwa hapa, kwa hiyo na tusimamishe mahema matatu, moja lako na moja la Musa na moja la Eliya.” Ni wazi kwamba watu hao wawili ambao katika maono hayo waliwakilisha watumishi wa Yehova waliokufa zamani, hawakuhitaji mahema. Kwa kweli, Petro hakujua alichokuwa akisema. Hata hivyo, tunavutiwa na Petro kwa sababu ya fadhili na shauku yake.—Luka 9:33.

Yeye na Yakobo na Yohana walipokea thawabu nyingine usiku huo. Wingu lilitokea na kukaa juu yao kwenye mlima. Sauti ilitoka katika wingu hilo—ilikuwa sauti ya Yehova Mungu! Alisema: “Huyu ni Mwanangu, ambaye amechaguliwa. Msikilizeni.” Kisha maono hayo yakaisha, nao wakaachwa pamoja na Yesu mlimani.—Luka 9:34-36.

Maono hayo yalikuwa thawabu iliyoje kwa Petro na kwetu pia! Miaka mingi baadaye, Petro aliandika kuhusu pendeleo alilopata usiku huo la kuwa mmoja kati ya “mashahidi wa kujionea fahari yake,” yaani, kumwona Yesu kimbele akiwa Mfalme wa mbinguni mwenye utukufu. Maono hayo yalithibitisha unabii mwingi wa Neno la Mungu na kuimarisha imani ya Petro kwa majaribu ambayo angekabili baadaye. (2 Petro 1:16-19) Imani yetu pia inaweza kuimarishwa ikiwa, kama Petro, tunaendelea kuwa washikamanifu kwa Bwana ambaye Yehova alimweka juu yetu, kujifunza kutoka kwake, kukubali nidhamu na marekebisho yake, na kumfuata kwa unyenyekevu siku baada ya siku.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ona makala “Igeni Imani Yao—Alishinda Woga na Shaka,” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 2009 (1/10/2009).

^ fu. 9 Tunaweza kusema kwamba watu kwenye sinagogi hawakuwa na msimamo tunapolinganisha jinsi walivyotenda kuhusiana na maneno ya Yesu wakati huo, na maneno yao siku iliyotangulia, walipotangaza kwa shauku kwamba Yesu ni nabii wa Mungu.—Yohana 6:14.

^ fu. 15 Katika safari yao ya kilomita 48, Yesu pamoja na wale walioandamana naye walipanda kutoka fuo za Bahari ya Galilaya, ambazo ziko mita 210 hivi chini ya usawa wa bahari na kufika eneo lililo mita 350 hivi juu ya usawa wa bahari. Walipita katika maeneo yenye kuvutia sana.

^ fu. 18 Ona sanduku  “Ni Nani Mwamba?” kwenye ukurasa wa 28.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 28]

 Ni Nani Mwamba?

“Ninakuambia, Wewe ni Petro, na juu ya mwamba huu nitajenga kutaniko langu.” (Mathayo 16:18) Mara nyingi, maneno hayo ambayo Yesu alimwambia mtume wake Petro, yameeleweka kumaanisha kwamba Petro angekuwa msingi wa kutaniko la Kikristo. Kanisa Katoliki linafundisha kwamba Yesu alikuwa anampa Petro mamlaka juu ya wale mitume wengine, na hivyo kumfanya papa wa kwanza. Kwa hiyo, kwenye kanisa linaloitwa Saint Peter’s Basilica jijini Rome, maneno hayo ya Yesu yameandikwa kwa Kilatini kwenye dari ya kanisa hilo. Herufi za maneno hayo ni ndefu kuliko mtu.

Je, Yesu alimaanisha kwamba Petro ndiye mwamba ambao juu yake yeye angejenga kutaniko lake? Hapana. Fikiria sababu tatu zinazofanya tuwe na hakika kuhusu jambo hilo. Kwanza, mitume wengine walikuwapo, na hawakuyaelewa maneno ya Yesu kwa njia hiyo. Ikiwa Yesu alimpa Petro mamlaka mbele yao wote, kwa nini baadaye walibishana tena na tena kuhusu ni nani kati yao aliyeonekana kuwa mkuu zaidi ya wote? (Marko 9:33-35; Luka 22:24-26) Pili, baadaye mtume Paulo alionyesha kwamba mwamba huo si Petro, bali ni Yesu Kristo. (1 Wakorintho 3:11; 10:4) Tatu, miaka mingi baadaye, Petro mwenyewe alionyesha kwamba hakufikiri yeye ndiye mwamba huo. Badala yake, aliandika kwamba Yesu ndiye “jiwe la pembeni la msingi” lililotabiriwa zamani, ambalo lilichaguliwa na Mungu mwenyewe.—1 Petro 2:4-8.

Hata hivyo, watu fulani husisitiza kwamba kwa kuwa jina la Petro linamaanisha “Jiwe,” Yesu alikuwa akimtambulisha Petro kuwa mwamba. Lakini, jina la Petro halina maana sawa na neno “mwamba,” ambalo pia limetumiwa katika mstari huo. Jina Petro linamaanisha “Kipande cha Jiwe,” na ni neno la jinsia ya kiume; lakini “mwamba” ni neno la jinsia ya kike. Hivyo basi, maneno ya Yesu yanamaanisha nini? Kwa maneno mengine Yesu alikuwa akimwambia Petro hivi: “Wewe, ambaye nimekuita Petro, au Jiwe, umetambua kwa usahihi kwamba ‘mwamba’ ni Kristo, ambaye atakuwa msingi wa kutaniko la Kikristo.” Petro alikuwa na pendeleo lililoje kusaidia kufunua ukweli huo muhimu!

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Petro alikuwa mshikamanifu hata aliporekebishwa

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kwa sababu ya kuwa mshikamanifu, Petro alipata thawabu ya kuona maono yenye kusisimua