Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Ujiweke Wakfu kwa Yehova?

Kwa Nini Ujiweke Wakfu kwa Yehova?

Kwa Nini Ujiweke Wakfu kwa Yehova?

‘Usiku huu malaika wa Mungu ambaye mimi ni mali yake alisimama karibu nami.’—MDO. 27:23.

1. Wale wanaojitoa ili wabatizwe tayari wamechukua hatua gani, na hilo linatokeza maswali gani?

“KWA msingi wa dhabihu ya Yesu Kristo, je, umetubu dhambi zako na kujiweka wakfu kwa Yehova ili kufanya mapenzi yake?” Swali hilo ni kati ya maswali mawili ambayo wale wanaotaka kubatizwa wanajibu mwishoni mwa hotuba ya ubatizo. Kwa nini Wakristo wanahitaji kujiweka wakfu kwa Yehova? Tunapata faida gani tunapojiweka wakfu kwa Mungu? Kwa nini mtu hawezi kumwabudu Mungu kwa njia inayokubalika ikiwa hajajiweka wakfu kwake? Ili kupata majibu ya maswali hayo, tunahitaji kwanza kuelewa maana ya wakfu.

2. Kujiweka wakfu kwa Yehova kunamaanisha nini?

2 Kujiweka wakfu kwa Mungu kunamaanisha nini? Ona jinsi mtume Paulo alivyoeleza kuhusu uhusiano wake na Mungu. Akiwa pamoja na watu waliosafiri naye kwenye mashua iliyokumbwa na hatari ya tufani, Paulo alimwita Yehova, “Mungu ambaye mimi ni mali yake.” (Soma Matendo 27:22-24.) Wakristo wote wa kweli ni mali ya Yehova. Lakini ulimwengu kwa ujumla “unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yoh. 5:19) Wakristo wanakuwa mali ya Yehova wanapojiweka wakfu kwa njia inayofaa katika sala. Wakfu huo ni nadhiri ambayo mtu mwenyewe anaweka. Baada ya kujiweka wakfu, anabatizwa katika maji.

3. Ubatizo wa Yesu ulionyesha nini, na wafuasi wake wanaweza kuiga mfano wake jinsi gani?

3 Yesu alituwekea mfano alipofanya uamuzi wake binafsi wa kufanya mapenzi ya Mungu. Tayari alikuwa wakfu kwa Mungu kwa sababu alizaliwa katika taifa la Israeli ambalo lilikuwa wakfu. Hata hivyo, alipobatizwa alifanya jambo fulani ambalo halikuagizwa katika Sheria. Neno la Mungu linaonyesha kwamba alisema hivi: “Tazama! Nimekuja . . . ili kufanya mapenzi yako, Ee Mungu.” (Ebr. 10:7; Luka 3:21) Kwa hiyo, ubatizo wa Yesu ulionyesha kwamba alijitoa mwenyewe kwa Mungu ili kufanya mapenzi ya Baba yake. Wafuasi wake wanaiga mfano wake wanapojitoa wenyewe ili wabatizwe. Hata hivyo, wafuasi wake wanapobatizwa katika maji wanaonyesha hadharani kwamba wamejiweka wakfu kwa Mungu kupitia sala.

Faida za Kujiweka Wakfu

4. Urafiki kati ya Daudi na Yonathani unatuonyesha nini kuhusu kuwajibika?

4 Wakfu wa Kikristo ni jambo zito. Ni zaidi ya kutimiza wajibu tu. Hata hivyo, tunapata faida gani tunapojiweka wakfu? Kwa mfano, hebu tuone faida za kuwajibika katika mahusiano ya kibinadamu, kama vile uhusiano kati ya marafiki. Ili ufurahie pendeleo la kuwa na rafiki, ni lazima ukubali daraka la kuwa rafiki. Hilo linahusisha kujitoa kabisa, yaani, kuhisi kwamba una daraka au wajibu wa kumjali rafiki yako. Urafiki kati ya Daudi na Yonathani ni kati ya urafiki wa pekee sana katika Biblia. Hata walifanya agano la urafiki kati yao. (Soma 1 Samweli 17:57; 18:1, 3.) Ingawa si rahisi kupata marafiki wanaojitoa kufikia hatua hiyo, mara nyingi urafiki unasitawi wakati watu wanapojitoa kabisa, au kuhisi kwamba wana wajibu au daraka kuelekea marafiki wao.—Met. 17:17; 18:24.

5. Mtumwa angefanya nini ili aendelee kuwa mali ya bwana mzuri?

5 Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli inaeleza kuhusu uhusiano mwingine ambao uliwanufaisha watu walipojitoa kabisa. Ikiwa mtumwa alitaka kuendelea kuwa mali ya bwana wake mzuri, angeweza kufanya makubaliano ya kudumu yenye masharti pamoja na bwana huyo. Sheria hiyo inasema hivi: “Ikiwa mtumwa huyo atasisitiza kusema, ‘Nampenda bwana wangu kwelikweli, mke wangu na wanangu; sitaki kuondoka kama mtu aliyewekwa huru,’ basi bwana wake atamleta karibu na Mungu wa kweli naye atamleta kwenye mlango au kwenye mwimo wa mlango; naye bwana wake atalichoma sikio lake na kulitoboa kwa sindano, naye atakuwa mtumwa wake mpaka wakati usio na kipimo.”—Kut. 21:5, 6.

6, 7. (a) Watu wanapata faida gani wanapowajibika? (b) Hilo linaonyesha nini kuhusu uhusiano wetu pamoja na Yehova?

6 Ndoa ni uhusiano ambao unahitaji watu wajitoe kabisa au kuwajibika kwa kadiri kubwa sana. Mtu anawajibika kwa mtu mwingine bali si kwa mkataba au makubaliano. Mwanamume na mwanamke ambao wanaishi pamoja bila kufunga ndoa hawawezi kamwe kuwa na usalama wa kweli; wala watoto wao hawawezi kuwa salama. Lakini wenzi wa ndoa ambao wamejitoa kabisa kwa mmoja na mwenzake katika ndoa inayoheshimika wana sababu ya Kimaandiko inayowachochea wajitahidi kusuluhisha matatizo kwa njia ya upendo.—Mt. 19:5, 6; 1 Kor. 13:7, 8; Ebr. 13:4.

7 Katika nyakati za Biblia, watu walifaidika kwa kufanya makubaliano yenye masharti katika biashara na katika kazi. (Mt. 20:1, 2, 8) Ndivyo ilivyo leo. Kwa mfano, tunafaidika tunapoandika mkataba au makubaliano yenye masharti, kabla ya kuanza biashara au kufanya kazi katika kampuni fulani. Hivyo, ikiwa kujitoa au kuwajibika kunaboresha mahusiano kati ya marafiki, wenzi wa ndoa, na wafanyakazi wenzako, bila shaka utapata faida hata zaidi ukijiweka wakfu bila masharti katika uhusiano wako pamoja na Yehova! Acheni sasa tuone jinsi ambavyo watu walifaidika kwa kujiweka wakfu kwa Yehova Mungu wakati uliopita na jinsi walivyofanya mengi zaidi kuliko tu kujitoa kwake.

Jinsi Waisraeli Walivyofaidika kwa Kujiweka Wakfu kwa Mungu

8. Kujiweka wakfu kwa Mungu kulimaanisha nini kwa Waisraeli?

8 Kwa ujumla, taifa la Israeli lilijiweka wakfu kwa Yehova lilipoweka nadhiri kwa Mungu. Yehova aliwaagiza wakusanyike karibu na Mlima Sinai, kisha akawaambia hivi: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kabisa na kulishika kwa kweli agano langu, ndipo hakika mtakapokuwa mali yangu ya pekee kutoka kati ya vikundi vingine vyote vya watu.” Watu wote wakajibu hivi kwa pamoja: “Yote ambayo Yehova amesema tuko tayari kuyafanya.” (Kut. 19:4-8) Waisraeli walipojiweka wakfu, walihitaji kufanya mengi zaidi ya kujitoa tu kufanya jambo fulani. Ilimaanisha kwamba walikuwa mali ya Yehova, na Yehova aliwatendea kama ‘mali yake ya pekee.’

9. Waisraeli walifaidika jinsi gani kwa sababu ya kujiweka wakfu kwa Mungu?

9 Waisraeli walifaidika kwa sababu ya kuwa mali ya Yehova. Yehova alikuwa mshikamanifu naye aliwatunza kama vile mzazi mwenye upendo anavyomtunza mtoto wake. Mungu aliwaambia hivi Waisraeli: “Je, mke anaweza kumsahau mtoto wake anayenyonya hivi kwamba asimhurumie mwana wa tumbo lake? Hata hawa wanawake wanaweza kusahau, lakini mimi mwenyewe sitakusahau wewe.” (Isa. 49:15) Yehova aliwapa Sheria ili iwaongoze, aliwatia moyo kupitia manabii, na akawalinda kwa kutumia malaika. Mtunga-zaburi mmoja aliandika hivi: “Anamtangazia Yakobo neno lake, na Israeli masharti yake na maamuzi yake ya hukumu. Hajafanya hivyo kwa taifa lingine lolote.” (Zab. 147:19, 20; soma Zaburi 34:7, 19; 48:14.) Kama Yehova alivyolitunza taifa ambalo lilikuwa mali yake zamani, ndivyo atakavyowatunza wale wanaojiweka wakfu kwake leo.

Kwa Nini Tunapaswa Kujiweka Wakfu kwa Mungu?

10, 11. Je, tumezaliwa katika familia ya Mungu ya ulimwenguni pote? Eleza.

10 Watu fulani wanapofikiria kuhusu wakfu na ubatizo wa Kikristo, huenda wakauliza, ‘Je, ni lazima nijiweke wakfu kwa Mungu ili nimwabudu?’ Tutaelewa wazi jambo hilo tukifikiria msimamo wetu wa sasa mbele za Mungu. Kumbuka kwamba kwa sababu ya dhambi ya Adamu, sote tumezaliwa nje ya familia ya Mungu. (Rom. 3:23; 5:12) Kujiweka wakfu kwa Mungu ni takwa la maana sana ili tukubaliwe katika familia yake ya ulimwenguni pote. Hebu tuone kwa nini hilo ni takwa la maana.

11 Hakuna yeyote kati yetu aliyezaliwa na baba ambaye angeweza kumpitishia uhai ambao Mungu alikusudia tuwe nao—uhai mkamilifu. (1 Tim. 6:19) Hatukuzaliwa tukiwa wana wa Mungu kwa sababu wenzi wawili wa kwanza walipofanya dhambi, jamii yote ya wanadamu ilitengwa mbali na Baba yao mwenye upendo, Muumba wao. (Linganisha na Kumbukumbu la Torati 32:5.) Kuanzia wakati huo na kuendelea, wanadamu wamekuwa wakiishi nje ya familia ya Yehova ya ulimwenguni pote, wakiwa wametengwa mbali na Mungu.

12. (a) Wanadamu wasio wakamilifu wanaweza jinsi gani kuwa washiriki wa familia ya Mungu? (b) Ni lazima tuchukue hatua gani kabla ya kubatizwa?

12 Hata hivyo, kila mmoja wetu anaweza kumwomba Mungu amruhusu ajiunge na familia Yake ya watumishi ambao amewakubali. * Hilo linawezekana jinsi gani kwa watenda-dhambi kama sisi? Mtume Paulo aliandika hivi: “Tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kupitia kifo cha Mwana wake.” (Rom. 5:10) Tunapobatizwa tunatoa ombi kwa Mungu la kupata dhamiri njema ili tuweze kukubalika kwake. (1 Pet. 3:21) Hata hivyo, kabla ya kubatizwa kuna hatua ambazo tunapaswa kuchukua. Ni lazima tumjue Mungu, tujifunze kumwamini, tutubu, na kubadili njia zetu. (Yoh. 17:3; Mdo. 3:19; Ebr. 11:6) Na kuna jambo lingine ambalo linahitajiwa ili tukubaliwe katika familia ya Mungu. Ni jambo gani hilo?

13. Kwa nini ni jambo linalofaa kwa mtu kuweka nadhiri ya wakfu kwa Mungu ili awe sehemu ya familia Yake ya waabudu anaowakubali?

13 Ili mtu ambaye ametengwa mbali na Mungu aweze kuwa mshiriki wa familia ya Mungu ya watumishi anaowakubali, anahitaji kwanza kutoa ahadi rasmi mbele za Yehova. Ili kuelewa kwa nini anahitaji kufanya hivyo, hebu fikiria baba mwenye heshima anayemjali sana kijana yatima. Baba huyo angependa kumchukua kijana huyo ili awe mshiriki wa familia yake. Baba huyo anajulikana kuwa mtu mzuri. Hata hivyo, kabla ya kumkubali kijana huyo kuwa mwana wake, anataka kijana huyo atoe ahadi. Kwa hiyo, anasema, “Kabla sijakubali uwe mwana wangu, ninataka kujua ikiwa utanipenda na kuniheshimu nikiwa baba yako.” Atakubali kijana huyo ajiunge na familia yake ikiwa tu kijana huyo yuko tayari kutoa ahadi hiyo rasmi. Takwa hilo linapatana na akili, sivyo? Vivyo hivyo, watu ambao Yehova anakubali wajiunge na familia yake ni wale tu ambao wako tayari kuweka nadhiri ya kujiweka wakfu kwake. Biblia inasema hivi: “Jitoeni ninyi wenyewe kwake: dhabihu iliyo hai, iliyo wakfu na ambayo anaweza kukubali.”—Rom. 12:1, The New English Bible.

Kujiweka Wakfu Ni Tendo la Upendo na Imani

14. Kujiweka wakfu kunaonyesha upendo katika njia gani?

14 Kuweka nadhiri ya wakfu kwa Mungu kunaonyesha kwamba tunampenda Yehova kutoka moyoni. Kwa njia fulani hiyo ni kama nadhiri ya ndoa. Bwana-arusi Mkristo anaonyesha upendo wake kwa kuweka nadhiri ya kwamba atakuwa mshikamanifu kwa bibi-arusi wake chini ya hali yoyote ile. Ni ahadi inayotolewa kwa mtu bali si ahadi tu ya kufanya jambo fulani. Bwana-arusi Mkristo anaelewa kwamba hawezi kupata pendeleo la kuishi na bibi-arusi wake asipoweka nadhiri ya ndoa. Vivyo hivyo, hatuwezi kufurahia kikamili faida za kuwa washiriki wa familia ya Yehova tusipoweka nadhiri ya wakfu. Kwa hiyo, tunajiweka wakfu kwa Mungu kwa sababu, hata ingawa sisi si wakamilifu, tunatamani kuwa mali yake na tumeazimia kuwa washikamanifu kwake, chini ya hali yoyote ile.—Mt. 22:37.

15. Kwa nini kujiweka wakfu ni tendo la imani?

15 Kujiweka wakfu kwa Mungu, ni tendo la imani. Kwa nini? Imani yetu katika Yehova inatufanya tuwe na uhakika kwamba kumkaribia Mungu ni jambo jema kwetu. (Zab. 73:28) Tunajua kwamba si rahisi sikuzote kutembea na Mungu tunapoishi katikati ya “kizazi kilicho kombo na kilichopotoka,” lakini tunaamini ahadi ya Mungu ya kwamba atatutegemeza katika jitihada zetu. (Flp. 2:15; 4:13) Tunajua kwamba sisi si wakamilifu, lakini tuna hakika kwamba Yehova atatuonyesha rehema hata tukikosea. (Soma Zaburi 103:13, 14; Waroma 7:21-25.) Tuna imani kwamba Yehova atabariki azimio letu la kudumisha utimilifu wetu.—Ayu. 27:5.

Kujiweka Wakfu kwa Mungu Kunaleta Furaha

16, 17. Kwa nini kujiweka wakfu kwa Yehova kunaleta furaha?

16 Kujiweka wakfu kwa Yehova kunaleta furaha kwa sababu kunahusisha kujitoa wenyewe. Yesu alisema ukweli huu wa msingi: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Mdo. 20:35) Yesu alipata furaha kamili ya kutoa wakati wa huduma yake hapa duniani. Nyakati nyingine alikosa wakati wa kupumzika, kula, na kujifurahisha ili awasaidie wengine kupata barabara ya uzima. (Yoh. 4:34) Yesu alifurahia kuufanya moyo wa Baba yake ushangilie. Yesu alisema hivi: “Sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza.”—Yoh. 8:29; Met. 27:11.

17 Hivyo, Yesu aliwaonyesha wafuasi wake jinsi ya kuwa na maisha yenye kuridhisha aliposema: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe.” (Mt. 16:24) Tunapofanya hivyo tunamkaribia Yehova zaidi. Je, kuna mtu mwingine yeyote ambaye anaweza kututunza kwa upendo mwingi hivyo tukijiweka mikononi mwake?

18. Kwa nini kuishi kupatana na wakfu wetu kwa Yehova kunaleta furaha zaidi kuliko kujiweka wakfu kwa kitu chochote au mtu mwingine yeyote?

18 Kujiweka wakfu kwa Yehova na kuishi kupatana na wakfu huo kwa kufanya mapenzi yake kunaleta furaha zaidi kuliko kujiweka wakfu kwa kitu chochote au mtu mwingine yeyote. Kwa mfano, watu wengi wanatumia maisha yao yote kutafuta utajiri lakini hawatosheki wala kupata furaha ya kweli. Hata hivyo, wale wanaojiweka wakfu kwa Yehova wanapata furaha ya kudumu. (Mt. 6:24) Wanafurahi kwa sababu wana pendeleo la kuwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu,” hata hivyo, hawajajiweka wakfu kwa kazi fulani bali wamejiweka wakfu kwa Mungu wetu mwenye uthamini. (1 Kor. 3:9) Hakuna mtu mwingine anayeweza kuthamini kujidhabihu kwao kuliko Mungu anavyothamini. Hata atawafanya washikamanifu wake wawe vijana tena ili wafaidike na utunzaji wake milele.—Ayu. 33:25; soma Waebrania 6:10.

19. Wale ambao wamejiweka wakfu kwa Yehova wanafurahia pendeleo gani?

19 Unapoweka wakfu maisha yako kwa Yehova unakuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. Biblia inasema hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yak. 4:8; Zab. 25:14) Katika habari inayofuata, tutaona kwa nini tunaweza kuchagua kwa uhakika kuwa mali ya Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 “Kondoo wengine” wa Yesu wataweza tu kuwa wana wa Mungu mwishoni mwa miaka elfu moja. Hata hivyo, kwa kuwa wamejiweka wakfu kwa Mungu, kwa kufaa wanaweza kumwita Mungu “Baba,” na wanaweza kuonwa kuwa washiriki wa familia ya waabudu wa Yehova.—Yoh. 10:16; Isa. 64:8; Mt. 6:9; Ufu. 20:5.

Ungesema Nini?

• Kujiweka wakfu kwa Mungu kunamaanisha nini?

• Tunapata faida gani tunapojiweka wakfu kwa Mungu?

• Kwa nini Wakristo wanahitaji kujiweka wakfu kwa Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 6]

Tunapata furaha ya kudumu tunapoishi kupatana na wakfu wetu