Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasaidie Watoto Wako Wakabiliane na Matatizo

Wasaidie Watoto Wako Wakabiliane na Matatizo

Wasaidie Watoto Wako Wakabiliane na Matatizo

VIJANA wetu wanakabili matatizo makubwa sana. Wanakabiliana na roho ya ulimwengu mwovu wa Shetani, na wanalazimika kupambana na “tamaa zinazotukia ujanani.” (2 Tim. 2:22; 1 Yoh. 5:19) Zaidi ya hayo, kwa sababu wanajitahidi ‘kumkumbuka Muumba wao Mkuu,’ wanalazimika kukabiliana na dhihaka au hata wanateswa na wale wanaopinga imani yao. (Mhu. 12:1) Anapokumbuka siku zake za ujana, ndugu mmoja anayeitwa Vincent anasema: “Kila wakati nilionewa, niliteswa au kuchokozwa kwa sababu tu nilikuwa Shahidi. Mara nyingi mateso hayo yalikuwa makali sana hivi kwamba sikutaka kwenda shuleni.” *

Mbali na kushinikizwa na ulimwengu, huenda vijana au mabinti wetu wanapambana na tamaa ya kuwaiga marafiki wao. Cathleen, dada mwenye umri wa miaka 16 anasema kwamba “si rahisi kukabiliana na hali ya kuonekana kwamba uko tofauti.” Ndugu mmoja kijana aitwaye Alan anakiri hivi: “Mara nyingi wanafunzi wenzangu waliniomba niende nao kustarehe mwishoni mwa juma, na kwa kweli nilitamani sana kwenda nao.” Zaidi ya hayo, vijana wana tamaa kubwa ya kutaka kushiriki michezo shuleni, jambo linalofanya iwe rahisi kwao kushirikiana na marafiki wabaya. Dada kijana anayeitwa Tanya anasema hivi: “Ninapenda michezo, walimu wa michezo walitaka sana nichezee timu ya shule. Haikuwa rahisi kukataa.”

Unaweza kuwasaidia jinsi gani vijana wako wakabiliane na matatizo mbalimbali? Yehova amewapa wazazi daraka la kuwaongoza watoto wao. (Met. 22:6; Efe. 6:4) Lengo la wazazi wanaomhofu Mungu ni kusitawisha ndani ya mioyo ya watoto wao tamaa ya kumtii Yehova. (Met. 6:20-23) Kwa njia hiyo, watoto watachochewa kupinga vishawishi vya ulimwengu hata wakiwa peke yao.

Si rahisi kwa wazazi kutafuta riziki, kutunza familia, na wakati huohuo kutimiza migawo mbalimbali kutanikoni. Wengine wanafanya hivyo wakiwa wazazi wasio na wenzi au wanakabili upinzani kutoka kwa wenzi wao wasio waamini. Hata hivyo, Yehova anataka wazazi watenge wakati ili kuwasaidia watoto wao. Hivyo basi, unaweza kufanya nini ili kuwasaidia watoto wako washinde shinikizo la marafiki, vishawishi, na mateso wanayokabili siku kwa siku?

Uhusiano wa Karibu Pamoja na Yehova

Kwanza kabisa, vijana wetu wanahitaji kujua kwamba Yehova ni Mtu halisi. Wanahitaji kusaidiwa ‘kumwona Yeye asiyeonekana.’ (Ebr. 11:27) Vincent, aliyetajwa awali, anakumbuka jinsi wazazi wake walivyomsaidia kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Anasema: “Walinifundisha umuhimu wa sala. Ninakumbuka kwamba nikiwa mtoto mdogo sana nilikuwa nikisali kwa Yehova kila usiku kabla ya kulala. Yehova alikuwa halisi kwangu.” Je, unasali pamoja na watoto wako? Mbona usisikilize kile wanachomwambia Yehova katika sala zao? Je, wanarudia-rudia maneno fulani? Au wanaposali wanaeleza jinsi wanavyohisi kumhusu Yehova? Ukisikiliza sala zao, unaweza kutambua maendeleo yao ya kiroho.

Kusoma Neno la Mungu ni njia nyingine muhimu inayoweza kuwasaidia vijana kumkaribia Yehova. Cathleen, aliyetajwa awali, anasema: “Kusoma Biblia nzima nikiwa na umri mdogo kulinisaidia. Kwa hiyo, nilikuwa na hakika kwamba hata watu wakinipinga, Yehova atanitegemeza.” Je, watoto wako wana ratiba yao ya kusoma Biblia?—Zab. 1:1-3; 77:12.

Ni kweli kwamba watoto wanapokea maagizo ya wazazi wao kwa njia tofauti-tofauti. Pia, maendeleo yao ya kiroho yanategemea umri wao. Hata hivyo, bila mwelekezo haitakuwa rahisi kwa vijana kumwona Yehova kuwa Mtu halisi. Wazazi wanapaswa kuwafundisha watoto wao maneno ya Mungu ili wamwone Yehova kuwa halisi mahali popote walipo. (Kum. 6:6-9) Watoto wako wanapaswa kuamini kwamba Yehova anawajali.

Jinsi ya Kuwasiliana Vizuri

Njia nyingine muhimu ya kumsaidia mtoto wako ni kuwasiliana naye. Bila shaka, mawasiliano mazuri yanatia ndani mengi zaidi ya kuongea tu na watoto wako. Yanatia ndani kuuliza maswali na kusikiliza kwa subira majibu yao—hata ikiwa ni mambo ambayo hupendi kusikia. Anne, mama ya wavulana wawili anasema hivi: “Ninawauliza maswali ili niweze kuelewa wanachofikiri na mambo wanayokabiliana nayo maishani.” Je, watoto wako wanahisi kwamba unawasikiliza? Tanya, aliyenukuliwa awali anasema: “Wazazi wangu walinisikiliza kwa makini na kukumbuka mambo tuliyozungumza. Walijua majina ya wanafunzi wenzangu darasani. Mara nyingi waliuliza kuwahusu na kuhusu hali nyingine tulizozungumzia wakati uliopita.” Kusikiliza na kukumbuka ni mambo ya maana sana katika mawasiliano mazuri.

Familia nyingi zimegundua kwamba wakati wa chakula ni pindi inayofaa ya kuwa na mazungumzo mazuri. Vincent, anasema: “Kula pamoja lilikuwa jambo la maana katika familia yetu. Ilipowezekana familia nzima ilitarajiwa kuwa mezani. Hatukuruhusiwa kutazama televisheni, kusikiliza redio, au kusoma wakati wa mlo. Kwa kuwa mara nyingi mazungumzo hayo yalikuwa ya kawaida tu, yalinisaidia kutulia na kujitayarisha kukabiliana na vurugu na mikazo shuleni.” Anaongezea hivi: “Pia, kwa kuwa nilizoea kuzungumza na wazazi wangu wakati wa mlo nilijihisi huru kuzungumza nao nilipohitaji msaada wa kukabiliana na mambo mazito zaidi.”

Jiulizeni hivi: ‘Ni mara ngapi katika juma tunapokula pamoja tukiwa familia?’ Je, mkifanya mabadiliko fulani mnaweza kupata nafasi zaidi ya kuwasiliana na watoto wenu?

Vipindi vya Mazoezi Ni Vyenye Thamani Sana

Pia, jioni ya Ibada ya Familia ya kila juma inawasaidia wote katika familia kuwasiliana kwa uhuru na inawasaidia vijana kuwa tayari kukabiliana na matatizo fulani hususa. Alan, aliyetajwa awali, anasema: “Wazazi wangu walitumia funzo la familia kutuchochea tuseme yaliyo mioyoni mwetu. Walichagua habari zilizohusu mambo tuliyokuwa tukikabili.” Mama ya Alan anasema: “Tulitumia muda fulani wa funzo la familia kwa ajili ya vipindi vya mazoezi. Vipindi hivyo viliwasaidia watoto wetu kujifunza jinsi ya kuitetea imani yao na kuthibitisha kwamba yale wanayoamini ni ya kweli. Hilo liliwapa ujasiri waliohitaji ili kupambana na matatizo waliyokabili.”

Bila shaka, wanaposhawishiwa na marafiki, watoto wanahitaji kufanya mengi zaidi ya kusema tu hapana na kuondoka. Wanapaswa kuwa na uwezo wa kueleza kwa nini wanafanya au kutofanya mambo fulani. Wanahitaji pia kujua kwa uhakika jambo la kufanya wanapodhihakiwa kwa sababu ya imani yao. Ikiwa hawawezi kutetea yale wanayoamini, itakuwa vigumu kwao kutetea kwa ujasiri ibada ya kweli. Vipindi vya mazoezi vinaweza kuwasaidia kuwa na ujasiri huo.

 Sanduku lililo kwenye ukurasa wa 18 linaorodhesha hali fulani ambazo zinaweza kuigizwa wakati wa jioni ya Ibada ya Familia. Fanyeni vipindi hivyo kuwa halisi kwa kuwaomba waeleze majibu yao. Wakati wa vipindi hivyo vya mazoezi, zungumzieni pia masomo fulani muhimu tunayojifunza kutokana na watu wanaotajwa kwenye Biblia. Bila shaka, watoto wakizoezwa hivyo nyumbani, watakuwa tayari kukabiliana na matatizo shuleni au mahali pengine popote.

Je, Nyumba Yako Ni Mahali Penye Kuburudisha?

Je, watoto wako wana hamu ya kurudi nyumbani wanapotoka shuleni? Ikiwa ni mahali penye kuburudisha, patawasaidia watoto kukabiliana na matatizo ya kila siku. Dada ambaye sasa ni Mwanabetheli anasema: “Nilipokuwa mtoto, moja ya mambo yaliyonisaidia sana ni kwamba nyumba yetu ilikuwa mahali penye kuburudisha. Hata iwe mambo yalikuwa mabaya kadiri gani shuleni, nilijua kwamba kila niliporudi nyumbani mambo yangekuwa sawa.” Kuna hali gani nyumbani mwenu? Je, ni mahali ambapo “milipuko ya hasira, magomvi, [na] migawanyiko” ni mambo ya kawaida, au inajulikana kwamba kuna “upendo, shangwe, [na] amani?” (Gal. 5:19-23) Ikiwa mara nyingi hakuna amani, je, mnajitahidi kadiri mwezavyo kujua ni mabadiliko gani mnayohitaji kufanya ili nyumba yenu iwe mahali panapowaburudisha watoto wenu?

Njia nyingine ya kuwasaidia watoto wenu kukabiliana na matatizo ni kuwatafutia marafiki wazuri. Kwa mfano, je, mnaweza kuwakaribisha ndugu na dada wa kiroho wa kutaniko lenu katika tafrija ya familia yenu? Au mnaweza kuwakaribisha waangalizi wanaosafiri na watumishi wengine wa wakati wote kwa ajili ya chakula chepesi nyumbani mwenu? Je, mnawafahamu wamishonari au Wanabetheli wowote ambao watoto wenu wanaweza kuanzisha urafiki nao, hata ikiwa ni kupitia kuandika barua, barua-pepe, au kwa kuwapigia simu mara kwa mara? Urafiki kama huo unaweza kuwasaidia watoto wenu kufanya maendeleo na kuwa na miradi ya kiroho. Fikiria jinsi mtume Paulo alivyomsaidia kijana Timotheo. (2 Tim. 1:13; 3:10) Urafiki huo ulimsaidia Timotheo kukazia fikira miradi ya kiroho.—1 Kor. 4:17.

Wapongeze Watoto Wako

Yehova anafurahi anapowaona vijana wakisimama imara na kutenda yaliyo sawa wanaposhawishiwa na ulimwengu wa Shetani. (Zab. 147:11; Met. 27:11) Bila shaka, wewe pia unafurahi kuona watoto wako wakitenda kwa hekima. (Met. 10:1) Waeleze watoto wako jinsi unavyowathamini, na uwapongeze kwa upendo. Yehova amewawekea wazazi kielelezo kizuri. Yesu alipokuwa akibatizwa, Yehova alisema: “Wewe ni Mwanangu, mpendwa; nimekukubali wewe.” (Marko 1:11) Bila shaka, maneno hayo ya pongezi kutoka kwa Baba yake yalimwimarisha sana Yesu kukabiliana na majaribu mengi yaliyokuwa mbele yake. Vivyo hivyo, waambie watoto wako kwamba unawapenda, na uwapongeze kwa yale wanayofanya.

Bila shaka, huwezi kuwalinda watoto wako kutokana na kila tatizo, mateso na dhihaka. Hata hivyo, unaweza kufanya mengi ili kuwasaidia. Kwa njia gani? Wasaidie kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Andaa mazingira yatakayochochea mazungumzo mazuri. Ifanye jioni ya Ibada ya Familia iwe yenye kunufaisha na uifanye nyumba yako iwe yenye kuburudisha. Bila shaka, ukifanya hivyo utawatayarisha watoto wako kukabiliana na matatizo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 18]

 VIPINDI VYA MAZOEZI VINAWEZA KUSAIDIA

Zifuatazo ni hali fulani ambazo watoto wetu wanakabili. Kwa nini msijizoeze mambo hayo wakati wa jioni ya Ibada ya Familia?

▸ Mwalimu wa michezo anamtaka binti yako ajiunge na timu ya shule.

▸ Baada ya shule, mwana wako anashawishiwa kuvuta sigareti.

▸ Wavulana fulani wanamtisha kijana wako kwamba watampiga wakimwona tena akihubiri.

▸ Binti yako anahubiri nyumba kwa nyumba, anakutana na mwanafunzi mwenzake.

▸ Binti yako anasimamishwa mbele ya darasa na kuulizwa kwa nini haisalimu bendera.

▸ Kijana fulani anamdhihaki daima mwana wako kwa sababu ni Shahidi.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Je, watoto wako wana ratiba yao ya usomaji wa Biblia?

[Picha katika ukurasa wa 19]

Je, unawakaribisha ndugu na dada wa kiroho katika tafrija ya familia yenu?