Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Utawala wa Yehova Umethibitika Kuwa Bora!

Utawala wa Yehova Umethibitika Kuwa Bora!

Utawala wa Yehova Umethibitika Kuwa Bora!

“Aliye Juu Zaidi ni Mtawala katika ufalme wa wanadamu.”—DAN. 4:17.

1, 2. Taja sababu fulani ambazo zimefanya utawala wa wanadamu ushindwe.

UTAWALA wa wanadamu umeshindwa! Hakuna shaka yoyote kuhusu hilo. Sababu kuu ambayo imefanya ushindwe ni kwamba wanadamu hawana hekima ya kutawala kwa mafanikio. Leo ni wazi zaidi kwamba utawala wa wanadamu umeshindwa kwa kuwa watawala wengi ‘wanajipenda wenyewe, wanapenda pesa, wanajidai, wana majivuno, si washikamanifu, hawataki makubaliano yoyote, ni wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, na wenye kujivuna kwa kiburi.’—2 Tim. 3:2-4.

2 Hapo zamani, wazazi wetu wa kwanza walikataa utawala wa Mungu. Walipofanya hivyo, huenda walifikiri kwamba wanachagua uhuru. Hata hivyo, ukweli ni kwamba walikuwa wanajitiisha chini ya utawala wa Shetani. Utawala mbaya wa wanadamu ambao umekuwapo kwa miaka elfu sita chini ya uvutano wenye nguvu wa “mtawala wa ulimwengu huu,” Shetani, umesababisha hali iliyopo leo ambayo ni mbaya zaidi katika historia yote ya wanadamu. (Yoh. 12:31) Kikizungumza kuhusu hali ya wanadamu leo, kitabu kimoja (The Oxford History of the Twentieth Century) kinasema kwamba, ni kazi bure “kutafuta ulimwengu ulio mkamilifu.” Kinaeleza hivi: “Mbali na kwamba hauwezi kupatikana, jitihada hizo zinasababisha misiba, utawala wa kimabavu, na vita vibaya zaidi.” Maelezo hayo manyoofu yanaonyesha wazi kwamba utawala wa wanadamu umeshindwa!

3. Tunaweza kusema Mungu angetawala jinsi gani ikiwa Adamu na Hawa hawangefanya dhambi?

3 Basi, inasikitisha kwamba wazazi wetu wa kwanza walikataa utawala pekee ambao unafaa, yaani, utawala wa Mungu! Bila shaka, hatujui vizuri kabisa jinsi ambavyo Yehova angeitawala dunia ikiwa Adamu na Hawa wangeendelea kuwa waaminifu kwake. Hata hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba utawala wa Mungu ambao ungekubaliwa na wanadamu wote ungetawala kwa upendo na haungekuwa na ubaguzi. (Mdo. 10:34; 1 Yoh. 4:8) Kwa sababu Mungu ana hekima isiyo na kifani, tunaweza pia kuwa na hakika kwamba ikiwa wanadamu wangeendelea kujitiisha chini ya utawala wa Yehova, makosa yote ambayo yamefanywa na watu ambao wameunga mkono utawala wa wanadamu yangeepukwa. Utawala wa Mungu, yaani, theokrasi, ungefanikiwa “kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.” (Zab. 145:16) Kwa ufupi, ungekuwa utawala mkamilifu. (Kum. 32:4) Inasikitisha kwamba wanadamu walikataa utawala huo!

4. Shetani ameruhusiwa kutawala kwa kadiri gani?

4 Hata hivyo, ni vizuri kukumbuka kwamba hata ingawa Yehova aliwaruhusu wanadamu wajitawale, hakupoteza kamwe haki yake ya kuwatawala viumbe wake. Hata mfalme mwenye nguvu wa Babiloni alilazimika kukiri kwamba kwa hakika “Aliye Juu Zaidi ni Mtawala katika ufalme wa wanadamu.” (Dan. 4:17) Mwishowe, Ufalme wa Mungu utafanya mapenzi ya Mungu yatendeke. (Mt. 6:10) Ni kweli kwamba Yehova amemruhusu Shetani awe “mungu wa mfumo huu wa mambo” kwa kipindi kifupi ili masuala ambayo yalitokezwa na mpinzani huyo yajibiwe kikamili. (2 Kor. 4:4; 1 Yoh. 5:19) Hata hivyo, Shetani hana uwezo wa kuvuka mipaka ambayo amewekewa na Yehova. (2 Nya. 20:6; linganisha na Ayubu 1:11, 12; 2:3-6.) Sikuzote kumekuwa na watu ambao wamechagua kujitiisha kwa Mungu hata ingawa wameishi katika ulimwengu ambao unatawaliwa na Adui mkuu wa Mungu.

Mungu Atawala Israeli

5. Waisraeli walimwahidi Mungu nini?

5 Kuanzia wakati wa Abeli mpaka wakati taifa la Israeli lilipoanzishwa, watu fulani waaminifu walimwabudu Yehova na kutii amri zake. (Ebr. 11:4-22) Katika siku za Musa, Yehova alifanya agano na wazao wa mzee Yakobo, nao wakawa taifa la Israeli. Mwaka wa 1513 K.W.K., Waisraeli pamoja na wazao wao walimkubali Yehova awe Mtawala wao, wakasema hivi: “Yote ambayo Yehova amesema tuko tayari kuyafanya.”—Kut. 19:8.

6, 7. Utawala wa Mungu katika Israeli ulionyesha nini?

6 Yehova aliwachagua Waisraeli wawe watu wake kwa kusudi fulani. (Soma Kumbukumbu la Torati 7:7, 8.) Yehova hakuwachagua Waisraeli kwa faida yao. Jina la Mungu na enzi yake kuu ilihusika pia, na hayo yalikuwa mambo ya maana zaidi. Waisraeli wangetumiwa kutoa ushahidi kwamba Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli. (Isa. 43:10; 44:6-8) Kwa hiyo, Yehova aliliambia hivi taifa hilo: “Ninyi ni watu watakatifu kwa Yehova Mungu wenu, naye Yehova amewachagua ninyi muwe watu wake, mali ya pekee, kutoka kati ya vikundi vyote vya watu vilivyo kwenye uso wa nchi.”—Kum. 14:2.

7 Yehova alipowatawala Waisraeli alikumbuka kwamba hawakuwa wakamilifu. Wakati huohuo, sheria zake zilikuwa kamilifu na zilionyesha sifa za yule Aliyezitoa. Amri za Yehova ambazo Musa alipewa zilionyesha utakatifu wa Mungu, jinsi anavyopenda haki, jinsi alivyo tayari kusamehe, na subira yake. Baadaye, katika siku za Yoshua na kizazi kilichoishi wakati huo, taifa hilo lilitii amri za Yehova na likapata amani na baraka za kiroho. (Yos. 24:21, 22, 31) Kipindi hicho cha historia ya taifa la Israeli kilionyesha mafanikio ya utawala wa Yehova.

Matokeo Mabaya ya Utawala wa Wanadamu

8, 9. Ni ombi gani lisilo la hekima ambalo Waisraeli walitoa, na lilikuwa na matokeo gani?

8 Hata hivyo, baada ya muda, Waisraeli waliasi tena na tena utawala wa Mungu na wakapoteza ulinzi wake. Mwishowe, kupitia nabii Samweli, Waisraeli waliomba wawe na mfalme wa kibinadamu ambaye wangeweza kumwona. Yehova alimwambia Samweli awape mfalme kama walivyoomba. Hata hivyo, Yehova aliongezea hivi: “Hawakukukataa wewe, bali wamenikataa mimi nisiwe mfalme juu yao.” (1 Sam. 8:7) Ingawa Yehova aliwaruhusu Waisraeli wawe na mfalme ambaye wangeweza kumwona, aliwaonya kwamba utawala wa mfalme wa kibinadamu ungekuwa na matokeo mabaya.—Soma 1 Samweli 8:9-18.

9 Historia ilionyesha ukweli wa onyo ambalo Yehova alitoa. Waisraeli walipata matatizo makubwa walipotawaliwa na mfalme wa kibinadamu, hasa mfalme alipokosa kuwa mwaminifu. Tukifikiria mfano huo wa Waisraeli, haishangazi kwamba katika historia yote serikali zinazoongozwa na wanadamu ambao hawamjui Yehova zimeshindwa kuleta mafanikio yenye kudumu. Ni kweli kwamba wanasiasa fulani wanamwomba Mungu abariki jitihada zao za kupata amani na usalama, lakini Mungu anaweza jinsi gani kuwabariki wale ambao hawajitiishi chini ya utawala wake?—Zab. 2:10-12.

Taifa Jipya Chini ya Utawala wa Mungu

10. Kwa nini Yehova aliwakataa Waisraeli wasiwe taifa lake lililochaguliwa?

10 Taifa la Israeli halikutaka kumtumikia Mungu kwa uaminifu. Mwishowe, walimkataa Masihi aliyechaguliwa na Mungu, naye Yehova akawakataa na kuchagua kikundi kingine ambacho kingekuwa taifa jipya na kuchukua nafasi ya taifa la Israeli. Hivyo, kutaniko la Kikristo la waabudu wa Yehova waliotiwa mafuta lilianzishwa mwaka wa 33 W.K. Kwa kweli, kutaniko hilo lilikuwa taifa jipya ambalo lilitawaliwa na Yehova. Paulo aliliita taifa hilo “Israeli wa Mungu.”—Gal. 6:16.

11, 12. Taifa la Israeli linafanana jinsi gani na “Israeli wa Mungu” katika usimamizi?

11 Kuna mambo fulani yanayotofautiana na mengine yanayofanana kati ya taifa la Israeli na taifa jipya la “Israeli wa Mungu.” Tofauti na Israeli la kale, kutaniko la Kikristo halina mfalme wa kibinadamu na halihitaji kutoa dhabihu za wanyama kwa ajili ya watenda-dhambi. Mpango wa kuwa na wazee au wanaume wazee, ambao ulikuwapo katika taifa la Israeli upo pia katika kutaniko la Kikristo. (Kut. 19:3-8) Wazee hao Wakristo hawatawali kundi. Badala yake, wanalichunga kutaniko na wanajitoa kabisa katika kuongoza utendaji wa Kikristo. Wanashughulika kwa upendo na kila mtu kutanikoni, nao wanawaheshimu wote.—2 Kor. 1:24; 1 Pet. 5:2, 3.

12 Wanapotafakari kuhusu jinsi Mungu alivyoshughulika na taifa la Israeli, washiriki wa “Israeli wa Mungu” na waandamani wao, “kondoo wengine,” wanachochewa kumthamini zaidi Yehova na utawala wake. (Yoh. 10:16) Kwa mfano, historia inaonyesha kwamba watawala katika Israeli walikuwa na uvutano mkubwa sana juu ya raia wao, iwe ni uvutano mzuri au uvutano mbaya. Hilo linapaswa kuwakumbusha wale wanaoongoza kati ya Wakristo kwamba ingawa wao si watawala kama wafalme wa zamani, ni lazima sikuzote waweke mfano mzuri katika kuonyesha imani.—Ebr. 13:7.

Jinsi Yehova Anavyotawala Leo

13. Ni jambo gani la maana sana lililotukia mwaka wa 1914?

13 Leo, Wakristo wanautangazia ulimwengu kwamba utawala wa wanadamu unakaribia kukoma. Mwaka wa 1914, Yehova aliusimamisha Ufalme wake mbinguni chini ya Mfalme aliyemweka rasmi, Yesu Kristo. Wakati huo, alimpa Yesu mamlaka ya kwenda “akishinda na kukamilisha ushindi wake.” (Ufu. 6:2) Mfalme huyo mpya aliyetawazwa aliambiwa hivi: “Nenda ukitiisha katikati ya adui zako.” (Zab. 110:2) Inasikitisha kwamba mataifa yameendelea kukataa kujitiisha chini ya utawala wa Yehova. Yameendelea kutenda kana kwamba “hakuna Yehova.”—Zab. 14:1.

14, 15. (a) Ufalme wa Mungu unatutawala jinsi gani leo, na hivyo, tunapaswa kujiuliza maswali gani? (b) Ubora wa utawala wa Mungu unaonekana jinsi gani hata leo?

14 Leo, kuna washiriki wachache waliotiwa mafuta wa “Israeli wa Mungu,” na wakiwa ndugu za Yesu, wanaendelea kutenda wakiwa “mabalozi walio badala ya Kristo.” (2 Kor. 5:20) Wamewekwa rasmi kuwa jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara ili kutunza na kuwaandalia chakula cha kiroho watiwa-mafuta na umati unaoongezeka wa mamilioni ya Wakristo walio na tumaini la kuishi milele duniani. (Mt. 24:45-47; Ufu. 7:9-15) Ufanisi wa kiroho ambao waabudu wa kweli wanafurahia leo unaonyesha kwamba Yehova amebariki mpango huo.

15 Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, ninajua vizuri madaraka ambayo ninapaswa kutimiza katika kutaniko la Kikristo? Je, ninaunga mkono inavyofaa utawala wa Yehova? Je, ninajivunia kuwa raia wa Ufalme wa Yehova unaotawala? Je, nimeazimia kuendelea kuwaambia wengine kuhusu Ufalme wa Mungu kwa kadiri ninayoweza?’ Tukiwa kikundi, tunajitiisha kwa kupenda chini ya mwongozo unaotolewa na Baraza Linaloongoza na kushirikiana na wazee waliowekwa rasmi kutanikoni. Tunapofanya hivyo, tunaonyesha kwamba tunakubali utawala wa Mungu. (Soma Waebrania 13:17.) Kujitiisha kwa kupenda kunatokeza umoja wa ulimwenguni pote ambao ni wa pekee sana katika ulimwengu huu uliogawanyika. Pia, kunatokeza amani na uadilifu na kunamletea Yehova utukufu, na hivyo kuonyesha kwamba utawala wake ndio utawala bora kabisa.

Utawala wa Yehova Utashinda

16. Ni uamuzi gani ambao kila mtu anapaswa kufanya leo?

16 Wakati unakaribia sana ambapo masuala yaliyotokezwa katika Edeni yatatatuliwa. Kwa hiyo, huu ndio wakati wa watu kufanya uamuzi. Ni lazima kila mtu aamue ikiwa atakubali utawala wa Yehova au ataendelea kuunga mkono utawala wa wanadamu. Tuna pendeleo la kuwasaidia watu wapole wafanye uamuzi unaofaa. Hivi karibuni, wakati wa Har–Magedoni, utawala wa Yehova utaondoa kabisa serikali za wanadamu ambazo zinaongozwa na Shetani. (Dan. 2:44; Ufu. 16:16) Utawala wa wanadamu utakoma, na Ufalme wa Mungu utaitawala dunia yote. Bila shaka, kwa njia kamilifu kabisa, utawala wa Yehova utakuwa umethibitika kuwa bora.—Soma Ufunuo 21:3-5.

17. Ni mambo gani ya hakika ambayo yanawasaidia wapole wafanye uamuzi mzuri kuhusu utawala?

17 Wale ambao bado hawajaamua kuwa upande wa Yehova wanapaswa kusali na kufikiria faida ambazo utawala wa Mungu utawaletea wanadamu. Utawala wa wanadamu umeshindwa kusuluhisha tatizo la uhalifu, kutia ndani ugaidi. Utawala wa Mungu utaondoa waovu wote duniani. (Zab. 37:1, 2, 9) Utawala wa wanadamu umesababisha vita visivyokoma, lakini utawala wa Mungu ‘utakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia.’ (Zab. 46:9) Zaidi ya hayo, utawala wa Mungu utarudisha pia amani kati ya wanadamu na wanyama! (Isa. 11:6-9) Umaskini na njaa ni mambo ya kawaida chini ya utawala wa wanadamu, lakini utawala wa Mungu utayaondoa. (Isa. 65:21) Hata watawala wa kibinadamu wenye nia nzuri wameshindwa kuondoa magonjwa na kifo, lakini chini ya utawala wa Mungu, wazee na wagonjwa watafurahi kurudishiwa nguvu za ujana. (Ayu. 33:25; Isa. 35:5, 6) Kwa kweli, dunia itakuwa paradiso na hata wafu watafufuliwa.—Luka 23:43; Mdo. 24:15.

18. Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunaamini kuwa utawala wa Mungu ndio utawala bora?

18 Ndiyo, utawala wa Mungu utaondoa madhara yote ambayo Shetani alisababisha alipowashawishi wazazi wetu wa kwanza wamwasi Muumba wao. Hebu wazia, Shetani amekuwa akisababisha madhara kwa miaka 6,000 hivi, lakini Mungu, kupitia Kristo, ataondoa madhara hayo katika kipindi cha miaka 1,000! Hilo linathibitisha kwa njia kubwa kama nini kwamba utawala wa Mungu ndio utawala bora zaidi! Tukiwa Mashahidi wa Mungu wetu, tunamkubali kuwa Mtawala wetu. Kwa hiyo, acheni tuonyeshe kila siku, ndiyo, kila saa ya maisha yetu kwamba sisi ni waabudu wa Yehova, raia wa Ufalme wake, na tunajivunia kuwa Mashahidi wake. Na acheni tutumie kila nafasi kumwambia kila mtu ambaye atatusikiliza kwamba utawala wa Yehova ndio utawala bora kabisa.

Tumejifunza Nini Kuhusu Utawala wa Mungu kwa Kusoma . . .

Kumbukumbu la Torati 7:7, 8?

1 Samweli 8:9-18?

Waebrania 13:17?

Ufunuo 21:3-5?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 29]

Yehova amekuwa mtawala sikuzote

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kujitiisha kwa kupenda chini ya utawala wa Yehova kumeleta umoja wa ulimwenguni pote