Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumia Kila Siku ya Maisha Yako kwa Utukufu wa Mungu

Tumia Kila Siku ya Maisha Yako kwa Utukufu wa Mungu

Tumia Kila Siku ya Maisha Yako kwa Utukufu wa Mungu

MTUNGA-ZABURI Daudi alisali hivi: “Asubuhi unifanye nisikie fadhili zako zenye upendo, unijulishe njia ninayopaswa kuitembea.” (Zab. 143:8) Unapoamka asubuhi na kumshukuru Yehova kwa sababu umeona siku nyingine, je, unamsihi Yehova akuongoze kufanya maamuzi mazuri, kama Daudi alivyofanya? Bila shaka, unafanya hivyo.

Tukiwa watumishi waliojiweka wakfu kwa Yehova, ‘iwe tunakula au tunakunywa au tunafanya jambo lingine lolote,’ tunajitahidi ‘kufanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu.’ (1 Kor. 10:31) Tunatambua kwamba maisha yetu ya kila siku yanaweza kumletea Yehova sifa au kumwaibisha. Pia, tunakumbuka kwamba Neno la Mungu linasema kuwa Shetani anawashtaki “mchana na usiku” ndugu za Kristo—na kwa kweli, anawashtaki watumishi wote wa Mungu duniani. (Ufu. 12:10) Kwa hiyo, tumeazimia kuthibitisha kwamba mashtaka ya Shetani ni ya uwongo na kuufanya moyo wa Yehova ushangilie kwa kutoa utumishi mtakatifu kwa Baba yetu wa mbinguni “mchana na usiku.”—Ufu. 7:15; Met. 27:11.

Acheni tuzungumzie kwa ufupi njia mbili muhimu ambazo tunaweza kutumia kila siku ya maisha yetu kwa utukufu wa Mungu. Kwanza, tunapaswa kujua mambo ya kutanguliza, na pili, tunapaswa kuwajali wengine.

Kuishi Kulingana na Ahadi Yetu

Tunapojiweka wakfu kwa Yehova, tunaonyesha kutoka moyoni kwamba tunataka sana kumtumikia. Pia, tulimwahidi Yehova kwamba tutatembea katika njia zake “siku baada ya siku.” (Zab. 61:5, 8) Basi, tunaweza jinsi gani kuishi kulingana na ahadi hiyo? Tunaweza kuonyesha jinsi gani kila siku kwamba tunampenda Yehova kwa moyo wetu wote?

Neno la Mungu linaeleza waziwazi mambo ambayo Yehova anatutarajia tutimize. (Kum. 10:12, 13) Mambo kadhaa yameorodheshwa kwenye sanduku lenye kichwa  “Mambo Ambayo Mungu Anataka Tufanye,” kwenye ukurasa wa 22. Mambo hayo yote ambayo Mungu anataka tutimize ni ya maana. Tunaweza kuamua jinsi gani jambo la kutanguliza ikiwa tuna mambo mawili au zaidi ya kufanya?

Tunatanguliza utumishi wetu mtakatifu, unaotia ndani kujifunza Biblia, sala, mikutano ya Kikristo, na huduma. (Mt. 6:33; Yoh. 4:34; 1 Pet. 2:9) Lakini hatuwezi kufanya mambo ya kiroho siku nzima. Tunahitaji pia kufanya mambo mengine kama vile kazi, kusoma, na shughuli mbalimbali za nyumbani. Hata hivyo, tunajitahidi kabisa kupanga kazi na shughuli zetu nyingine kwa njia ya kwamba hazivurugi utumishi wetu mtakatifu, kama vile kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Kwa mfano, tunapopanga kwenda likizo, tunahakikisha kwamba hatukosi ziara ya mwangalizi wa mzunguko, kusanyiko la pekee na la mzunguko, au kusanyiko la wilaya. Wakati mwingine, tunaweza kuunganisha shughuli zetu pamoja. Kwa mfano, tunaweza kuamua kusafisha Jumba la Ufalme tukiwa familia au kutumia wakati wa chakula cha mchana kazini au shuleni kuwahubiria wafanyakazi au wanafunzi wenzetu. Kwa kweli, tunapohitaji kufanya uamuzi wowote maishani—kama vile kutafuta kazi, kuchagua shule, au kuchagua marafiki—tungependa maamuzi yetu yote yategemee jambo muhimu zaidi katika maisha yetu—yaani, kumwabudu Yehova, Baba yetu mwenye upendo.—Mhu. 12:13.

Wajali Wengine

Yehova anataka tuwajali wengine na kuwatendea mema. Lakini, Shetani anataka tuwe na ubinafsi. Ulimwengu wake umejaa watu ambao ‘wanajipenda wenyewe’ na “wanaopenda raha” na pia wale ‘wanaopanda kwa mwili wao.’ (2 Tim. 3:1-5; Gal. 6:8) Wengi hawafikirii matokeo ya mambo wanayowatendea wengine. “Matendo ya mwili” yanaonekana kila mahali.—Gal. 5:19-21.

Wale wanaoongozwa na roho takatifu ya Yehova wako tofauti kabisa, wanaonyesha sifa kama vile upendo, fadhili, na wema wanaposhughulika na wengine. (Gal. 5:22) Neno la Mungu linatuambia tutangulize kwanza mahitaji ya wengine. Hivyo, tunapendezwa kikweli na wengine, ingawa tunakuwa waangalifu kwamba tusiingilie mambo yao ya kibinafsi. (1 Kor. 10:24, 33; Flp. 2:3, 4; 1 Pet. 4:15) Tunawaonyesha ufikirio zaidi waamini wenzetu. Hata hivyo, tunajitahidi pia kuwasaidia wale ambao si waamini. (Gal. 6:10) Je, unaweza kutafuta fursa ya kumtendea kwa fadhili mtu fulani leo?—Ona sanduku  “Wajali Wengine,” kwenye ukurasa wa 23.

Hatupaswi kuwajali wengine pindi fulani au katika hali fulani tu. (Gal. 6:2; Efe. 5:2; 1 The. 4:9, 10) Badala yake, kila siku tunajitahidi kutambua uhitaji wa wengine na kuwa tayari kuwasaidia, hata inapokuwa vigumu kufanya hivyo. Tunataka kuwaonyesha wengine ukarimu kwa chochote tulicho nacho iwe ni wakati wetu, vitu vyetu vya kimwili, uzoefu, au hekima yetu. Yehova anatuhakikishia kwamba tukiwaonyesha wengine ukarimu, atatuonyesha ukarimu pia.—Met. 11:25; Luka 6:38.

Kutoa Utumishi Mtakatifu “Mchana na Usiku”

Je, kweli tunaweza kumtolea Yehova utumishi mtakatifu “mchana na usiku”? Bila shaka, kwa kuwa wa kawaida na wenye bidii katika mambo yote ya ibada yetu. (Mdo. 20:31) Tunaweza kutanguliza utumishi mtakatifu maishani mwetu kwa kusoma na kutafakari kuhusu Neno la Mungu kila siku, kwa kudumu katika sala, kwa kujitahidi kuhudhuria mikutano yote, na kutumia kila nafasi kuhubiri.—Zab. 1:2; Luka 2:37; Mdo. 4:20; 1 The. 3:10; 5:17.

Je, sisi binafsi tunamtolea Yehova utumishi huo mtakatifu? Ikiwa ndivyo, tutaonyesha katika maisha yetu ya kila siku kwamba tunatamani kumfurahisha Yehova na kujibu mashtaka ya Shetani. Katika mambo yote na hali yoyote ile, tunajitahidi kumletea Yehova utukufu. Tunaruhusu kanuni zake ziongoze maneno na mwenendo wetu, nasi tunazitumia tunapofanya maamuzi. Tunaonyesha kwamba tunathamini upendo na utegemezo wake kwa kumwamini kabisa na kutumia nguvu zetu katika utumishi wake. Na tunakubali mashauri na nidhamu yake tunapovunja kanuni zake kwa sababu ya kutokamilika.—Zab. 32:5; 119:97; Met. 3:25, 26; Kol. 3:17; Ebr. 6:11, 12.

Acheni tutumie kila siku ya maisha yetu kwa utukufu wa Mungu. Tukifanya hivyo, tutapata burudisho kwa ajili ya nafsi zetu na Baba yetu wa mbinguni atatutunza milele kwa upendo.—Mt. 11:29; Ufu. 7:16, 17.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 22]

 Mambo Ambayo Mungu Anataka Tufanye

• Kusali kwa kawaida.—Rom. 12:12.

• Kusoma na kujifunza Biblia, na kutumia tunayojifunza.—Zab. 1:2; 1 Tim. 4:15.

• Kumwabudu Yehova kutanikoni.—Zab. 35:18; Ebr. 10:24, 25.

• Kuiandalia familia mahitaji ya kimwili, ya kiroho, na ya kihisia.—1 Tim. 5:8.

• Kuhubiri habari njema ya Ufalme, na kufanya wanafunzi.—Mt. 24:14; 28:19, 20.

• Kutunza afya yetu kimwili, kiroho, na kihisia, na pia kuwa na tafrija inayofaa.—Marko 6:31; 2 Kor. 7:1; 1 Tim. 4:8, 16.

• Kutimiza madaraka yetu kutanikoni.—Mdo. 20:28; 1 Tim. 3:1.

• Kutunza nyumba yetu na Jumba la Ufalme.—1 Kor. 10:32.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 23]

 Wajali Wengine

• Ndugu au dada mzee.—Law. 19:32.

• Mtu mgonjwa au mwenye matatizo ya kihisia.—Met. 14:21.

• Mshiriki wa kutaniko mwenye uhitaji ambao unaweza kutimiza.—Rom. 12:13.

• Mshiriki wa karibu wa familia yako.—1 Tim. 5:4, 8.

• Mwamini mwenzetu ambaye amefiwa na mwenzi wa ndoa.—1 Tim. 5:9.

• Mzee wa kutaniko lenu mwenye bidii.—1 The. 5:12, 13; 1 Tim. 5:17.