Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unapaswa Kushika Sabato ya Kila Juma?

Je, Unapaswa Kushika Sabato ya Kila Juma?

Je, Unapaswa Kushika Sabato ya Kila Juma?

MWISHONI mwa miaka ya 1980, vikundi vidogo vya Wamethodisti vilivamia Suva, mji mkuu wa Fiji. Wanaume, wanawake, na watoto—wote wakiwa wamevalia mavazi ya kidini waliweka vizuizi 70 barabarani. Walisimamisha magari yote na kuzuia ndege zote za kimataifa na za ndani ya nchi zisisafiri. Kwa nini walifanya hivyo? Walitaka sheria kali iwekwe inayomlazimisha kila mtu nchini humo kushika Sabato.

Kuanzia mwaka wa 2001, kila jengo jipya la ghorofa ambalo linajengwa nchini Israel ni lazima liwe na angalau lifti moja ambayo inasimama yenyewe kwenye kila ghorofa. Kwa nini? Ili Wayahudi ambao wanashika sana Sabato kuanzia Ijumaa (Siku ya 5) jioni mpaka Jumamosi (Siku ya Posho) jioni, wasifanye “kazi” ya kubonyeza vitufe vya lifti.

Huko Tonga, nchi iliyo Pasifiki ya Kusini ambayo inatawaliwa na mfalme, ni marufuku kufanya kazi ya aina yoyote siku ya Jumapili (Siku ya Yenga). Ndege haziruhusiwi kutua, na meli haziruhusiwi kutia nanga bandarini. Mikataba yoyote inayofanywa siku hiyo haionwi kuwa halali. Katiba ya nchi ya Tonga inasema kwamba watu wote wanapaswa kuiona Jumapili “kuwa takatifu,” bila kujali imani yao ya kidini. Kwa nini? Ili kuhakikisha kwamba taifa lote linashika Sabato.

Kama mifano iliyotajwa inavyoonyesha, watu wengi wanahisi kwamba Mungu anataka washike siku ya Sabato kila juma. Kwa kweli, watu fulani wanasema kwamba kushika Sabato ni jambo la maana sana, wanaamini kwamba wokovu wetu wa milele unategemea jambo hilo. Wengine wanahisi kwamba amri ya maana zaidi kutoka kwa Mungu ni kushika Sabato. Sabato ni nini? Na je, Biblia inawahimiza Wakristo washike Sabato ya kila juma?

Sabato Ni Nini?

Neno la Kiswahili “Sabato” limetafsiriwa kutokana na neno la Kiebrania linalomaanisha “pumzika, koma, acha.” Ingawa masimulizi ya kitabu cha Mwanzo yanasema kwamba Yehova Mungu alipumzika siku ya saba kutokana na kazi zake za uumbaji, watu wa Mungu waliagizwa wawe na siku ya saa 24 ya pumziko au Sabato kuanzia siku za Musa. (Mwanzo 2:2) Baada ya Waisraeli kuondoka Misri mwaka wa 1513 K.W.K., Yehova aliwaandalia mana kimuujiza wakiwa nyikani. Waliagizwa hivi kuhusu kukusanya mana: “Siku sita mtakiokota, lakini siku ya saba ni sabato. Siku hiyo hakuna chochote kitakachofanyizwa.” (Kutoka 16:26) Kisha tunaambiwa kwamba “watu wakaishika sabato siku ya saba,” kuanzia Ijumaa jioni baada ya jua kutua mpaka Jumamosi jioni.—Kutoka 16:30.

Muda mfupi tu baada ya maagizo hayo kutolewa, Yehova aliweka sheria kuhusu kushika Sabato, na ilikuwa kati ya zile Amri Kumi ambazo Musa alipewa. (Kutoka 19:1) Amri ya nne ilisema hivi kwa sehemu: “Kwa kuikumbuka siku ya sabato ili kuiona kuwa takatifu, utafanya utumishi nawe uifanye kazi yako yote kwa siku sita. Lakini siku ya saba ni sabato kwa Yehova Mungu wako.” (Kutoka 20:8-10) Hivyo, kushika Sabato kukawa jambo la maana katika maisha ya Waisraeli.—Kumbukumbu la Torati 5:12.

Je, Yesu Alishika Sabato ya Kila Juma?

Ndiyo, Yesu alishika Sabato. Tunaambiwa hivi kumhusu: “Wakati kamili ulipofika, Mungu alimtuma Mwana wake, aliyezaliwa na mwanamke na aliyekuja kuwa chini ya sheria.” (Wagalatia 4:4) Yesu alizaliwa akiwa Mwisraeli na hivyo alikuwa chini ya Sheria, ambayo ilitia ndani sheria ya Sabato. Agano la Sheria lilifutiliwa mbali baada ya kifo cha Yesu. (Wakolosai 2:13, 14) Tukijua mambo hayo yalitukia wakati gani tutaelewa maoni ya Mungu kuhusu jambo hilo.—Angalia chati kwenye  ukurasa wa 15.

Ni kweli kwamba Yesu alisema hivi: “Msifikiri nilikuja kuharibu Sheria au Manabii. Sikuja kuharibu, bali kutimiza.” (Mathayo 5:17) Lakini neno “kutimiza” linamaanisha nini? Kwa mfano: Mjenzi anatimiza mkataba wa kujenga nyumba, si kwa kuvunja mkataba huo, bali kwa kukamilisha ujenzi wa jengo hilo. Hata hivyo, mara tu anapomaliza kazi hiyo kama mwenye nyumba alivyotaka, mkataba unakuwa umetimizwa na hivyo mjenzi hana tena wajibu wa kufanya kazi hiyo. Vivyo hivyo, Yesu hakuvunja au kukiuka ile Sheria; badala yake, aliitimiza kwa kuishika kwa ukamilifu. Mara tu alipoitimiza, watu wa Mungu hawakuwa tena na wajibu wa kutimiza “mkataba” huo wa Sheria.

Je, Sabato Ni Takwa la Kikristo?

Kwa kuwa Kristo alitimiza Sheria, je, Wakristo wana wajibu au daraka la kushika Sabato ya kila juma? Akiongozwa na roho ya Mungu, mtume Paulo anajibu hivi: “Kwa hiyo mtu yeyote asiwahukumu ninyi katika kula na kunywa au kuhusu sherehe au kuhusu kushika mwezi mpya au sabato; kwa maana mambo hayo ni kivuli cha mambo yanayokuja, bali uhalisi ni wa Kristo.”—Wakolosai 2:16, 17.

Maneno hayo yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanaonyesha kwamba matakwa ambayo Mungu aliwapa watumishi wake yalibadilika sana. Kwa nini yalibadilika? Kwa sababu Wakristo wako chini ya sheria mpya, “sheria ya Kristo.” (Wagalatia 6:2) Agano la zamani la Sheria ambalo Mungu aliwapa Waisraeli kupitia Musa lilifikia mwisho wake wakati kifo cha Yesu kilipotimiza agano hilo. (Waroma 10:4; Waefeso 2:15) Je, amri ya kushika Sabato ilifikia mwisho pia? Ndiyo. Baada ya kusema kwamba “tumefunguliwa kutoka katika Sheria,” Paulo alitaja amri moja kati ya zile Amri Kumi. (Waroma 7:6, 7) Kwa hiyo, zile Amri Kumi, kutia ndani sheria ya Sabato, ni sehemu ya ile Sheria ambayo ilifikia mwisho. Kwa hiyo, waabudu wa Mungu, hawako chini ya takwa la kushika Sabato ya kila juma.

Mfano unaofuata unaweza kutusaidia kuelewa badiliko kutoka katika ibada ya Waisraeli kuingia katika ibada ya Kikristo: Nchi inaweza kubadili katiba yake. Baada ya katiba mpya kukubaliwa kisheria, watu hawatakiwi tena kufuata katiba ya zamani. Hata ingawa huenda sheria fulani katika katiba hiyo mpya zikafanana na sheria fulani za katiba ya zamani, sheria nyingine zinaweza kuwa tofauti. Kwa hiyo, mtu angehitaji kujifunza katiba mpya kwa uangalifu ili aone sheria ambazo zinatumika sasa. Kwa kuongezea, raia mshikamanifu angependa kujua katiba hiyo mpya ilianza kutumika wakati gani.

Vivyo hivyo, Yehova Mungu aliwapa Waisraeli sheria zaidi ya 600, pamoja na zile amri 10 za msingi. Sheria hizo zilitia ndani sheria kuhusu maadili, dhabihu, mambo ya kiafya, na kushika Sabato. Hata hivyo, Yesu alisema kwamba wafuasi wake watiwa-mafuta wangekuwa “taifa” jipya. (Mathayo 21:43) Kuanzia mwaka wa 33 W.K. na kuendelea, taifa hilo limekuwa na “katiba” mpya ambayo inategemea sheria mbili za msingi, yaani, kumpenda Mungu na kumpenda jirani. (Mathayo 22:36-40) Ingawa “sheria ya Kristo” inatia ndani maagizo mengi ambayo yanalingana na sheria ambazo Waisraeli walipewa, hata hivyo, Sheria fulani ni tofauti kabisa na sheria nyingine hazihitajiwi tena. Sheria ya kushika Sabato ya kila juma ni moja kati ya sheria ambazo hazitumiki tena.

Je, Mungu Amebadili Viwango Vyake?

Je, badiliko hilo la kuacha Sheria ya Musa na kufuata sheria ya Kristo linamaanisha kwamba Mungu amebadili viwango vyake? Hapana. Yehova amebadili sheria ambazo watu wake wanapaswa kutii kama vile tu mzazi anavyobadili sheria anazowawekea watoto wake ikitegemea umri na hali zao. Mtume Paulo anaeleza hivi jambo hilo: “Kabla ya ile imani kufika, tulikuwa tukilindwa chini ya sheria, tukiwekwa pamoja kifungoni, tukiitazamia imani iliyokusudiwa kufunuliwa. Kwa sababu hiyo Sheria imekuwa mtunzaji wetu kutuongoza kwa Kristo, ili tutangazwe kuwa waadilifu kutokana na imani. Lakini sasa kwa kuwa imani imefika, sisi hatuko tena chini ya mtunzaji.”—Wagalatia 3:23-25.

Hoja hizo za Paulo zinahusu Sabato jinsi gani? Fikiria mfano huu: Mwanafunzi anaweza kuagizwa ajifunze somo fulani shuleni, kama vile useremala, siku fulani ya juma. Hata hivyo, anapoanza kufanya kazi, huenda akahitaji kutumia ustadi aliojifunza, kila siku ya juma badala ya kuutumia siku moja tu. Vivyo hivyo, Waisraeli walipokuwa chini ya Sheria walitakiwa watenge siku moja kila juma ya kupumzika na kuabudu. Hata hivyo, Wakristo wanatakiwa wamwabudu Mungu kila siku badala ya siku moja tu kwa juma.

Basi je, ni kosa kutenga siku moja kila juma ili kupumzika na kuabudu? Hapana. Neno la Mungu linamruhusu kila mtu ajiamulie jambo hilo, linasema hivi: “Mtu mmoja anaamua kwamba siku moja ni takatifu kuliko nyingine. Mtu mwingine anaamua kwamba siku zote ni sawa. Ni lazima kila mtu afanye uamuzi wake mwenyewe.” (Waroma 14:5, tafsiri ya God’s Word) Ingawa huenda watu fulani wakaamua kuona siku moja kuwa takatifu kuliko siku nyingine, Biblia inaonyesha waziwazi kwamba Mungu hatarajii Wakristo washike Sabato ya kila juma.

[Blabu katika ukurasa wa 12]

“Siku sita mtakiokota, lakini siku ya saba ni sabato. Siku hiyo hakuna chochote kitakachofanyizwa.”—KUTOKA 16:26

[Blabu katika ukurasa wa 14]

“Sheria imekuwa mtunzaji wetu kutuongoza kwa Kristo, ili tutangazwe kuwa waadilifu kutokana na imani. Lakini sasa kwa kuwa imani imefika, sisi hatuko tena chini ya mtunzaji.”—WAGALATIA 3:24, 25

[Sanduku/Mchoro katika ukurasa wa 13]

Mstari wa Kimataifa wa Tarehe na Sabato

Mstari wa kimataifa wa tarehe unawatatanisha wale wanaoamini kwamba ni lazima washike Sabato ya kila juma siku ileile kila mahali. Mstari huo wa tarehe si mstari halisi na sehemu kubwa ya mstari huo inapita kwenye Bahari ya Pasifiki kwenye mstari wa meridiani wa 180. Nchi ambazo ziko upande wa magharibi wa mstari huo ziko mbele ya nchi za mashariki kwa siku moja.

Kwa mfano, inapokuwa siku ya Jumapili huko Fiji na Tonga, inakuwa siku ya Jumamosi huko Samoa na Niue. Kwa hiyo, ikiwa mtu anashika Sabato nchini Fiji siku ya Jumamosi, washiriki wa dini yake huko Samoa, umbali wa kilomita 1,145 tu, wanafanya kazi kwa sababu ni siku ya Ijumaa nchini humo.

Waumini wa Kanisa la Sabato huko Tonga wanashika Sabato yao siku ya Jumapili, wakifikiri kwamba kwa kufanya hivyo, wanashika Sabato wakati uleule na washiriki wa kanisa lao nchini Samoa, umbali wa kilomita 850 hivi. Hata hivyo, wakati uleule, waumini wa Kanisa la Sabato nchini Fiji, umbali usiozidi kilomita 800, hawapumziki kwa sababu ni siku ya Jumapili nchini humo, na hivyo wanashika Sabato siku ya Jumamosi!

[Mchoro]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

\

\

\

\ SAMOA

\

— ― ― ― ― ― ― ―

FIJI \

Jumapili \ Jumamosi

\

\

TONGA \

\

\

\

[Chati katika ukurasa wa 15]

 (Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Mambo ya Kukumbuka Kuhusu Sabato:

Hata ingawa huenda andiko fulani la Biblia likataja uhitaji wa kushika Sabato ya kila juma, tunapaswa kujua maneno hayo yalisemwa wakati gani.

4026 K.W.K. KABLA YA SIKU ZA MUSA

ADAMU AUMBWA Sheria ya Sabato haikutolewa

kabla ya siku za Musa na Waisraeli.

Kumbukumbu la Torati 5:1-3, 12-14.

1513 K.W.K. SHERIA YA MUNGU KWA WAISRAELI

WAISRAELI WAPEWA SHERIA Mataifa mengine hayakupewa sheria

ya Sabato. (Zaburi 147:19, 20)

Sheria hiyo ilitolewa kuwa

“ishara” kati ya Yehova na wana

wa Israeli.—Kutoka 31:16, 17.

Sabato ya kila juma ilikuwa mojawapo

ya sabato nyingi ambazo Waisraeli

waliamuriwa washike.—Mambo ya Walawi

16:29-31; 23:4-8; 25:4, 11; Hesabu 28:26.

33 W.K. SHERIA YA KRISTO

SHERIA AMBAYO WAISRAELI Mitume na wanaume wazee huko Yerusalemu

WALIPEWA YAFIKIA MWISHO walipoamua kuhusu matakwa ya Mungu kwa

Wakristo katika mwaka wa 49 W.K., hawakutaja

kwamba Wakristo wanahitaji kushika

Sabato ya kila juma.—Matendo 15:28, 29.

Mtume Paulo alikuwa na wasiwasi

kuhusu Wakristo ambao

walisisitiza kushika siku

fulani za pekee.—Wagalatia 4:9-11.

2010 W.K.

[Picha katika ukurasa wa 11]

Magazeti yaliyozungumza kuhusu vizuizi vya barabarani vilivyowekwa na Wamethodisti waliotaka kila mtu katika nchi ya Fiji aanze tena kushika Sabato

[Hisani]

Courtesy of the Fiji Times