Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuhusu Ibada ya Kweli

Kuhusu Ibada ya Kweli

Tunayojifunza Kutoka kwa Yesu

Kuhusu Ibada ya Kweli

Je, Mungu anakubali ibada yoyote ile?

▪ Yesu aliwasikitikia watu ambao walikuwa wamedanganywa na dini ya uwongo. Alionya kwamba ‘manabii wa uwongo wangekuja katika mavazi ya kondoo, lakini ndani ni mbwa-mwitu wenye kunyafua.’ (Mathayo 7:15) Je, umegundua kwamba watu fulani wanatumia dini ili kufanya mambo maovu?

Yesu alisema hivi katika sala kwa Mungu: “Neno lako ni kweli.” (Yohana 17:17) Kwa hiyo, Mungu hakubali ibada ambayo inapingana na kweli ya Biblia. Ndiyo sababu Yesu alitaja maneno haya ya Mungu aliposema kuhusu wanafiki fulani wa kidini: “Wao huniabudu bure, kwa sababu wao hufundisha amri za wanadamu kuwa mafundisho.”—Mathayo 15:9.

Je, kuna dini ya kweli?

▪ Alipokutana na mwanamke fulani huko Samaria ambaye alikuwa amedanganywa na dini ya uwongo, Yesu alimwambia hivi: “Ninyi mnaabudu msichokijua . . . Waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli, kwa maana, kwa kweli, Baba anawatafuta watu wa namna hiyo wamwabudu.” (Yohana 4:22, 23) Ni wazi kwamba ibada ya kweli inaweza kupatikana.

Yesu alisema hivi: “Sifanyi jambo lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe; bali kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema mambo haya.” Kwa hiyo, Yesu alijua kwamba dini aliyofundisha ndiyo iliyokuwa dini pekee ya kweli. (Yohana 8:28) Hivyo, alisema: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia kwangu.” (Yohana 14:6) Kwa kuwa waabudu wa kweli wanamfikia Baba kupitia njia moja, ni lazima waungane katika dini moja ya kweli.

Unaweza kuwatambua jinsi gani waabudu wa kweli?

▪ Mkristo ni mtu anayemfuata Yesu Kristo. Chunguza njia nne zinazowatambulisha wafuasi wa Yesu ambao wanaiga mfano wake.

1. Yesu Kristo alisali hivi kwa Yehova: “Nimewajulisha jina lako.” (Yohana 17:26) Wakristo wa kweli wanafanya vivyo hivyo.

2. Yesu alihubiri kuhusu Ufalme wa Yehova, naye aliwatuma wanafunzi wake pia kuhubiri nyumba kwa nyumba. Alisema hivi: “Katika jiji lolote lile au kijiji chochote kile mtakapoingia, tafuteni ni nani humo anayestahili.” Baadaye, aliwaambia hivi wafuasi wake: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” (Mathayo 10:7, 11; 28:19) Ni rahisi kuwatambua Wakristo wa kweli leo kwa sababu wanaendelea kufanya kazi hiyohiyo.

3. Yesu alikataa kuunga mkono upande wowote katika siasa. Kwa hiyo, alisema hivi kuhusu wafuasi wake: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:14) Waabudu wa kweli wanapaswa kujulikana waziwazi kwa sababu ya kutounga mkono upande wowote katika siasa.

4. Yesu aliwaonyesha wengine upendo wa kujidhabihu. Alisema hivi: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Wakristo wa kweli wanawajali wenzao na hawashiriki katika vita.

Ibada ya kweli inaweza kukunufaisha jinsi gani?

▪ Ili uabudu kwa njia inayokubalika, kwanza unahitaji kumjua Yehova vizuri. Ujuzi kumhusu Mungu utakuwezesha kufuatia njia bora zaidi ya maisha na utakuchochea kumpenda Mungu kwa moyo wako wote. Yehova ameahidi kwamba wale wanaompenda watapata uzima wa milele. Hivyo, Yesu alisema hivi: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli.”—Yohana 17:3.

Kwa habari zaidi, ona sura ya 15 ya kitabu hiki, Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 16]

“Jihadharini na manabii wa uwongo ambao wanakuja kwenu katika mavazi ya kondoo, lakini ndani wao ni mbwa-mwitu wenye kunyafua.”—Mathayo 7:15