Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Mbali na divai, ni vileo gani vingine vilivyotengenezwa katika nyakati za Biblia?

Mara kwa mara, Biblia inataja “divai na kileo.” (Kumbukumbu la Torati 14:26; Luka 1:15) Hatupaswi kufikiri kwamba neno “kileo” linamaanisha kwamba vinywaji hivyo vilitengenezwa kwa njia ya kutonesha, kwa kuwa njia hiyo iligunduliwa miaka mingi baadaye. Vileo havikutengenezwa tu kutokana na matunda kama vile zabibu, tende, tini, matofaa, na makomamanga bali pia kutokana na asali.

Kwa kweli, neno “kileo” linaweza pia kumaanisha bia au pombe. Neno la Kiebrania linalotafsiriwa kuwa “kileo” linahusiana na neno la Kiakadi ambalo linaweza kumaanisha pombe ya kawaida ya shayiri kutoka Mesopotamia. Pombe hiyo haingeweza kumlewesha mtu haraka lakini mtu angeweza kulewa ikiwa angekunywa kupita kiasi. (Methali 20:1) Sanamu za udongo za viwanda vya pombe na michoro ya watu wanaopika pombe imepatikana katika makaburi ya kale nchini Misri. Huko Babiloni, pombe ilikuwa kinywaji cha kawaida katika makao ya kifalme na vilevile nyumba za watu maskini. Wafilisti pia walikuwa na kinywaji kama hicho. Katika nchi ya Palestina, wachimbaji wa vitu vya kale wamepata vyombo vyenye vichujio. Vyombo hivyo vilichuja pombe ili wanywaji wasimeze machicha ya shayiri yaliyotumiwa kupikia pombe hiyo.

Katika siku za mtume Paulo, kwa nini ilikuwa hatari sana kusafiri baharini nyakati fulani za mwaka?

Kwa sababu ya upepo mkali, mashua ambayo mtume Paulo alitumia kusafiria ilichukua muda mrefu zaidi kuelekea upande wa magharibi kandokando ya pwani ya Asia Ndogo. Masimulizi hayo ya Biblia yanasema kwamba pindi fulani ilikuwa “hatari kusafiri kwa sababu hata kufunga kwa siku ya upatanisho kulikuwa tayari kumepita.” Paulo aliwaambia wasafiri wenzake kwamba ikiwa wangejaribu kuendelea na safari hiyo wangepata hasara “si ya shehena na mashua tu bali pia ya nafsi [zao].”—Matendo 27:4-10.

Kufunga kwa Siku ya Upatanisho kulifanywa mwishoni mwa Septemba (Mwezi wa 9) au mwanzoni mwa Oktoba (Mwezi wa 10). Mabaharia Waroma walijua kwamba kwa kawaida ilikuwa salama kusafiri baharini kuanzia tarehe 27 Mei (Mwezi wa 5) mpaka Septemba 14. Ilisemekana kwamba ilikuwa hatari kusafiri kati ya Septemba 14 na tarehe 11 Novemba (Mwezi wa 11), na kuanzia Novemba 11 mpaka tarehe 10 Machi (Mwezi wa 3), ilikuwa hatari hata zaidi kusafiri baharini. Kama masimulizi ya Paulo yanavyoonyesha waziwazi, sababu moja ni kwamba hali ya hewa ilibadilika-badilika. (Matendo 27:13-44) Mabaharia walikabili hatari ya dhoruba kali na ilikuwa vigumu sana kuendesha mashua. Mawingu yalifunika jua wakati wa mchana na nyota wakati wa usiku. Pia, ukungu na mvua ziliwazuia kuona hatari walizokabili.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Chupa za mbao za pombe kutoka Misri

[Hisani]

Erich Lessing/Art Resource, NY

[Picha katika ukurasa wa 23]

Meli ya Roma ya kubeba mizigo karibu mwaka wa 100-200 W.K.

[Hisani]

Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.