Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Rebeka Alikuwa Tayari Kumpendeza Yehova

Rebeka Alikuwa Tayari Kumpendeza Yehova

Wafundishe Watoto Wako

Rebeka Alikuwa Tayari Kumpendeza Yehova

REBEKA ni jina la kawaida katika sehemu nyingi leo. Je, unamjua mtu yeyote anayeitwa hivyo?— * Rebeka ni mtu wa maana sana katika kitabu maarufu zaidi ulimwenguni, Biblia. Unajua nini kumhusu?— Tunapaswa kujifunza kumhusu Rebeka kwa sababu mfano wake unaweza kutusaidia kumtumikia Mungu wa kweli, Yehova.

Rebeka ndiye mwanamke wa pili kutajwa katika Biblia kuwa mwabudu wa kweli wa Yehova. Je, unajua mwanamke wa kwanza aliyemwabudu Yehova alikuwa nani?— Ni Sara mke wa Abrahamu. Alipozeeka, Sara alimzaa mwana wake wa pekee Isaka. Acheni sasa tuone jinsi Rebeka alivyokuwa tayari kumpendeza Yehova na jinsi alivyokutana na Isaka.

Miaka zaidi ya 60 imepita tangu Mungu alipowaambia Abrahamu na Sara wahame Harani na kwenda nchi ya Kanaani. Abrahamu na Sara wanapokuwa wazee sana, Mungu anawaahidi kwamba watapata mtoto ambaye ataitwa Isaka. Kama unavyowazia, Isaka anapendwa sana na wazazi wake. Sara anapokufa akiwa na umri wa miaka 127, Isaka, mwana wake, ni mtu mzima na anahuzunishwa sana na kifo cha mama yake. Abrahamu hataki Isaka amwoe mwanamke kutoka Kanaani kwa sababu watu hao hawamwabudu Yehova. Kwa hiyo, anamtuma mtumishi wake, yaelekea Eliezeri, akamtafutie Isaka mke kati ya watu wa ukoo wa Abrahamu huko Harani, umbali wa kilomita zaidi ya 800!—Mwanzo 12:4, 5; 15:2; 17:17, 19; 23:1.

Baada ya muda, Eliezeri akiwa na ngamia kumi waliobeba mizigo na zawadi za bibi-arusi, anafika Harani na watumishi wengine wa Abrahamu. Wanasimama karibu na kisima kwa sababu Eliezeri anajua kwamba wakati wa alasiri, watu wanakuja kuteka maji kwa ajili ya wanyama na familia zao. Sasa Eliezeri anasali kwamba yule atakayemchagua kuwa mke wa Isaka atajibu hivi Eliezeri akimwomba maji ya kunywa: “Kunywa, na pia nitanywesha ngamia zako.”

Hivyo ndivyo inavyotukia! Kijana Rebeka “mwenye sura ya kuvutia sana” anakuja kisimani. Baada ya Eliezeri kumwomba maji ya kunywa, anajibu hivi: “Nitateka maji pia kwa ajili ya ngamia zako.” Anapokimbia “tena na tena kisimani ili kuteka maji,” Eliezeri anamkazia macho “kwa kustaajabu.” Hebu fikiria! Ili atosheleze ngamia kumi wenye kiu, Rebeka anahitaji kuteka lita 1,000 za maji!

Eliezeri anampa Rebeka zawadi nzuri sana, na anatambua kwamba Rebeka ni binti ya Bethueli, mtu wa ukoo wa Abrahamu. Rebeka anamkaribisha Eliezeri na marafiki wake nyumbani kwao ili ‘wakae usiku’ huo. Kisha anakimbia nyumbani ili awaambie kuhusu wageni ambao Abrahamu amewatuma kutoka Kanaani.

Labani, ndugu ya Rebeka, anapoona zawadi zenye thamani ambazo dada yake amepewa na baada ya kujua Eliezeri ni nani, anamkaribisha. Lakini Eliezeri anasema: “Mimi sitakula mpaka nitakapokuwa nimesema mambo yangu.” Kwa hiyo, anaeleza kwa nini Abrahamu alimtuma. Bethueli, mke wake, na Labani wanafurahi na kukubali ndoa hiyo.

Baada ya kula, Eliezeri na wale aliokuwa nao wanalala. Asubuhi inayofuata Eliezeri anasema: “Mniache niende kwa bwana wangu.” Lakini mama ya Rebeka na ndugu yake wanataka waendelee kukaa nao “angalau kwa siku kumi.” Rebeka anapoulizwa ikiwa ataenda bila kukawia, anajibu, “Mimi niko tayari kwenda.” Mara moja anaondoka pamoja na Eliezeri. Wanapofika, anakuwa mke wa Isaka.—Mwanzo 24:1-58, 67.

Je, unafikiri kwamba ilikuwa rahisi kwa Rebeka kuacha familia na marafiki na kwenda nchi ya mbali, huku akijua kwamba huenda hangewaona tena?— Hapana, haikuwa rahisi. Hata hivyo, Rebeka alibarikiwa kwa sababu ya kuwa tayari kufanya mambo yanayompendeza Yehova. Kupitia kwake, Mwokozi wetu Yesu Kristo alizaliwa. Sisi pia tutabarikiwa ikiwa, kama yeye, tutakuwa tayari kufanya mambo yanayompendeza Yehova.—Waroma 9:7-10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Ikiwa unasoma pamoja na mtoto, kistari kirefu kinakukumbusha kwamba unapaswa kutua na kumtia moyo ajieleze.

MASWALI:

▪ Rebeka alikuwa nani, na alikutana wapi na Eliezeri?

▪ Kwa nini Abrahamu hakutaka Isaka amwoe mwanamke Mkanaani?

▪ Rebeka alionyesha jinsi gani kwamba atakuwa mke mzuri?

▪ Tunaweza kufanya nini ili tuwe kama Rebeka?