Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wamishonari Watumwa “Mpaka Sehemu ya Mbali Zaidi ya Dunia”

Wamishonari Watumwa “Mpaka Sehemu ya Mbali Zaidi ya Dunia”

Kuhitimu kwa Darasa la 127 la Gileadi

Wamishonari Watumwa “Mpaka Sehemu ya Mbali Zaidi ya Dunia”

YESU aliwaamuru wanafunzi wake wawe mashahidi “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8) Mashahidi wa Yehova wanatii kabisa amri hiyo.

Kwa zaidi ya miaka 65, wamishonari waliozoezwa kwenye Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) wamesaidia kuongoza kazi hii ya kuhubiri katika nchi zaidi ya 200. Mnamo Jumamosi, Septemba 12, 2009, wahubiri wengine 56 wenye uzoefu walihitimu baada ya kuzoezwa kwa miezi mitano kwenye shule hiyo ya wamishonari huko Patterson, New York, Marekani.

Nguvu za Kufikiri

Stephen Lett, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova na ambaye alikuwa mwenyekiti wa programu hiyo ya kuhitimu, alitoa hotuba yenye kichwa “Tumia kwa Hekima Nguvu Zako za Kufikiri.” Kwanza aliwaonya wahitimu kuhusu mambo manne ambayo hawapaswi kufikiria. Mambo matatu ya kwanza yalikuwa: (1) Usifikiri kwamba vitu vya kimwili vinaweza kuleta ulinzi wa kudumu; (2) epuka kufikiria matendo mapotovu kiadili; na (3) epuka kuhangaika kupita kiasi, ukifikiri kwamba mambo yatakuwa mabaya sana kesho. (Methali 18:11; Mathayo 5:28; 6:34) Kuhusu jambo la tatu, msemaji alisema kwamba mtu anayehangaika kupita kiasi anaongeza mahangaiko ya jana kwenye mahangaiko ya leo, kisha analeta mahangaiko ya kesho na kuyaongeza kwenye mahangaiko ya leo. Ndugu Lett alisema: “Huo ni mzigo mzito sana kubeba.” Jambo la nne lilihusu nini? Wahitimu walionywa wasifikirie kwamba maisha yao yalikuwa mazuri zaidi kabla ya kuwa wamishonari. Ikiwa watafikiria hivyo, hawatapata shangwe inayoweza kupatikana katika maeneo yao mapya.

Kisha Ndugu Lett akawatia moyo wahitimu watumie nguvu zao za kufikiri kwa njia nne zinazofaa. Alisema: (1) Tambua mapema hali ambazo zinaweza kuwa hatari kimwili na kiroho, na uepuke msiba huo; (2) wazia akilini masimulizi unayosoma katika Biblia, na uwazie kwamba unashiriki katika mambo hayo; (3) wazia kwamba kila mtu unayezungumza naye katika mgawo wako mpya anaweza kuwa mwabudu wa Yehova; na (4) sitawisha huruma kwa kujiwazia ukiwa katika hali za wale unaowahubiria.—Methali 22:3.

Faida ya Kuwazoeza Wengine

David Splane, mshiriki mwingine wa Baraza Linaloongoza, alitoa hotuba iliyotegemea andiko la 2 Timotheo 2:2 yenye kichwa: “Mambo Hayo Uwakabidhi Watu Waaminifu.” Mtume Paulo alipomwagiza Timotheo awazoeze wanaume waaminifu, Paulo hakutaka Timotheo awafundishe tu wanaume hao kweli zilizojulikana bali pia alitaka awatie moyo wawazoeze wengine. Msemaji aliwaambia wahitimu hao kwamba kuna uhitaji mkubwa sana wa wanaume wenye kuongoza katika utendaji wa Kikristo. Wanaume hao watazoezwa jinsi gani na wakati gani? Ndugu Splane aliwatia moyo wamishonari hao waanze kuwazoeza wanaume hao mara tu wanapoanza kujifunza Biblia pamoja nao.

Wamishonari wanaweza kuwazoeza jinsi gani wanafunzi wa Biblia wawe mifano mizuri ya uaminifu? Msemaji alitaja njia mbalimbali. Wamishonari wanahitaji kuwazoeza kujitayarisha vizuri kwa ajili funzo lao la Biblia. Kisha, wanafunzi hao wanapoanza kuhudhuria mikutano ya kutaniko, wanahitaji kujifunza jinsi ya kutayarisha wakiwa peke yao habari inayotegemea Biblia ambayo itazungumziwa katika mikutano. Msemaji alisema kwamba “ikiwa mtu hawezi kujifunza Biblia akiwa peke yake, hawezi kamwe kuwafundisha wengine.” Ndugu Splane alisema pia kwamba wamishonari wanaweza kuwasaidia wapya kufika kwa wakati kwenye mikutano, kutoa michango ya kutegemeza kazi ya kuhubiri, na kuwatii wale ambao wanaongoza. Alisema kwamba njia bora ya kufundisha mambo hayo ni kuwawekea mfano mzuri.

Pendeleo la Kuwa Mashahidi

Guy Pierce, ambaye pia ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitoa hotuba ambayo ilitegemea maneno ya Yesu kwenye Matendo 1:8, “Mtakuwa Mashahidi Wangu.” Aliwakumbusha wahitimu hao kwamba katika karne ya kwanza W.K., taifa la Israeli lilipoteza pendeleo la kuwa mashahidi wa Yehova. Taifa linalozaa matunda ya Ufalme ndilo lililopewa pendeleo hilo. (Mathayo 21:43) Kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta lilithibitika kuwa taifa hilo. Msemaji alimnukuu mtume Petro ambaye alisema kwamba “taifa takatifu” la Wakristo watiwa-mafuta ‘lingetangaza kotekote’ sifa bora za Yehova. (1 Petro 2:6-9) Hivyo, Yesu hakuwa akisema kwamba Wakristo wangekuwa tu mashahidi wake na si mashahidi wa Yehova. Hata Yesu mwenyewe anaitwa “Shahidi Mwaminifu.” (Ufunuo 1:5; 3:14) Yeye ndiye Shahidi wa kwanza kabisa wa Yehova na tunaiga mfano wake.—1 Peter 2:21.

Msemaji aliwaambia wahitimu kwamba leo, maneno ya Yesu kwenye Matendo 1:8 yana maana kubwa zaidi. Kwa nini? Unabii wa maana sana ambao umerekodiwa kwenye Ufunuo 11:15, umetimizwa! Ufalme wa Kimasihi wa Mungu umesimamishwa. Leo, kwa njia halisi, kazi ya kutoa ushahidi inatimizwa “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8) Ndugu Pierce alikazia kwamba wamishonari wanatoa ushahidi kuhusu Yehova na Ufalme wake, na si kujihusu wenyewe au kuhusu maisha waliyokuwa wanaishi zamani, kuhusu utamaduni, au nchi yao. Aliwatia moyo wahitimu wawafundishe “watu wengi iwezekanavyo katika muda uliobaki.”

Mambo Mengine Makuu ya Programu

Alex Reinmueller, ambaye ni msaidizi wa Halmashauri ya Utangazaji, alitoa hotuba yenye kichwa “Yehova Atakupa Ujasiri.” Alisema kwamba ikiwa wamishonari hao watategemea nguvu za Yehova, atawasaidia kutumia uwezo wao kikamili, kukubali udhaifu wao, kukabiliana na woga wao, na kumtolea Mungu utumishi bora zaidi.

Walimu wawili wa Idara ya Shule za Kitheokrasi, Sam Roberson na William Samuelson walitoa hotuba pia. Ndugu Roberson alizungumzia kichwa “Mimi Nipo Pamoja Nawe,” kinachotegemea Isaya 41:10. Alisema kwamba wamishonari hao watapata shangwe nyingi. Watakuwa pia na matatizo. Wanaweza kukabiliana na matatizo hayo wakimwiga Mfalme Daudi ambaye alimlilia Baba yake mwenye upendo katika sala. (Zaburi 34:4, 6, 17, 19) Hotuba ya Ndugu Samuelson ilikazia kwa nini ni jambo la maana kuendelea kusitawisha uwezo wa kufikiri. Wamishonari wanaositawisha uwezo huo wanaepuka kutenda isivyofaa watu wanaposema mambo mabaya kuwahusu na hawakasiriki haraka.—Methali 2:10, 11.

Jim Mantz, msaidizi wa Halmashauri ya Uandikaji, alimhoji mshiriki wa Halmashauri ya Tawi kutoka Jamhuri ya Georgia, na mwingine kutoka Honduras, na mshiriki wa Halmashauri ya Nchi kutoka Jamhuri ya Tajikistan. Ndugu hao wenye uzoefu waliwashauri wamishonari kuhusu jinsi ya kufanya urafiki na watu ambao wanaweza kuwapinga kwa “kuushinda uovu kwa wema.” (Waroma 12:21) Mark Noumair, ambaye pia ni mwalimu, aliongoza kipindi chenye kuchangamsha cha mazungumzo kuhusu mambo ambayo wanafunzi walijionea katika mahubiri wakati wa mazoezi yao ya Gileadi. Sehemu hiyo ilikuwa na kichwa hiki chenye kuchochea fikira: “Ndiyo, Nikusaidie Jinsi Gani?”

Mwenyekiti alimalizia programu hiyo kwa kutaja maneno ya wimbo mpya “Jiwazie Wakati Vitu Vyote Vitakuwa Vipya.” Watu 6,509 waliohudhuria walienda nyumbani wakiwa wameazimia hata zaidi kutoa ushahidi kumhusu Yehova na Mwana wake “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”

[Chati/Ramani katika ukurasa wa 31]

TAKWIMU ZA DARASA

8 nchi zilizowakilishwa

56 wanafunzi

28 wenzi wa ndoa

33.6 wastani wa umri

18.3 wastani wa miaka tangu kubatizwa

13.6 wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote

[Ramani]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Wahitimu walitumwa katika nchi 22 zilizoonyeshwa hapa chini

MIGAWO YA WAMISHONARI

JAMAIKA

NIKARAGUA

KOSTA RIKA

PANAMA

PERU

CHILE

HAITI

KURASAO

GUYANA

CÔTE D’IVOIRE

BOLIVIA

PARAGUAI

SERBIA

ALBANIA

KONGO, JAM. YA KIDEM.

MOLDOVA

UGANDA

BURUNDI

TANZANIA

MSUMBIJI

NEPAL

KAMBODIA

[Picha katika ukurasa wa 31]

Darasa la 127 Lililohitimu la Shule ya Gileadi

Katika orodha iliyo chini, nambari za safu zinaanza mbele kwenda nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kwenda kulia katika kila safu.

(1) Marshall, T.; Prudent, L.; Mashburn, A.; Rosenström, S.; Testa, A.; Takeyama, M.; Sisk, M.

(2) Grooms, K.; Miura, S.; Camacho, M.; Rozas, S.; Burch, M.; Meza, I.; Young, G.; Geraghty, S.

(3) Bonilla, C.; Knaller, D.; Parrales, R.; Hotti, S.; Takada, A.; Tournade, M.; Sopel, C.

(4) Miura, Y.; Parrales, K.; Prudent, K.; Colburn, S.; Willis, L.; Vääränen, A.; Sisk, B.; Takada, R.

(5) Grooms, J.; Vääränen, M.; Geraghty, B.; Stackhouse, R.; Wilson, A.; Bonell, E.; Camacho, D.; Meza, R.; Bonell, M.

(6) Takeyama, S.; Testa, G.; Colburn, T.; Mashburn, C.; Willis, W.; Tournade, L.; Burch, J.; Stackhouse, J.

(7) Wilson, J.; Young, J.; Marshall, E.; Rozas, M.; Knaller, J.; Hotti, N.; Rosenström, A.; Sopel, J.; Bonilla, O.