Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unapaswa Kuwa Mnyoofu Nyakati Zote?

Je, Unapaswa Kuwa Mnyoofu Nyakati Zote?

Je, Unapaswa Kuwa Mnyoofu Nyakati Zote?

KILA mtu ni mnyoofu nyakati nyingine; huenda wengi wanakuwa wanyoofu mara nyingi. Hata hivyo, unajua watu wangapi ambao wanajitahidi kuwa wanyoofu nyakati zote?

Leo, watu si wanyoofu katika mambo mengi. Lakini tunajua vizuri maoni ya Mungu kuhusu unyoofu. Kwa mfano, watu wengi wanajua kwamba amri ya nane kati ya zile Amri Kumi inasema hivi: “Usiibe.” (Kutoka 20:15) Hata hivyo, wengi wanafikiri kwamba nyakati nyingine wanaweza kuiba au kukosa kuwa wanyoofu kwa sababu ya hali fulani. Acheni tuzungumzie sababu tatu ambazo wengi wanaona kwamba zinawaruhusu kuiba.

Je, Ni Sawa Kuiba kwa Sababu ya Umaskini?

Mtawala mmoja wa Roma alisema hivi: “Umaskini ndio chanzo cha uhalifu.” Mtu maskini anaweza kufikiri kwamba ana haki ya kuiba. Huenda watazamaji wakaona kwamba ni sawa kwa maskini kuiba. Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu jambo hilo? Aliwatendea maskini kwa huruma. ‘Aliwasikitikia.’ (Mathayo 9:36) Hata hivyo, hakuunga mkono kamwe wizi kwa sababu yoyote. Basi, mtu maskini anapaswa kufanya nini?

Mungu anawahurumia wale ambao wanajitahidi kwa unyoofu kumtii, naye atabariki jitihada zao za kutosheleza mahitaji yao. (Zaburi 37:25) Biblia inaahidi hivi: “Yehova hataiacha nafsi ya mwadilifu iteswe na njaa, lakini atasukumia mbali tamaa ya waovu.” (Methali 10:3) Je, mtu maskini anaweza kuamini ahadi hiyo? Victorine anaamini kwamba ni ahadi ya kweli.

Maisha ya Victorine ni magumu kwa sababu ni mjane aliye na watoto watano wanaoenda shuleni. Anaishi katika nchi inayositawi ambamo hawapati msaada wa kutosha kutoka kwa serikali. Kuna nafasi nyingi za kuiba kwa sababu wengi wanafanya kazi katika mitaa. Hata hivyo, Victorine hakubali kamwe kushawishiwa kuiba. Badala yake, anajitahidi kupata mahitaji yake kwa unyoofu kwa kuuza vitu kando ya barabara. Kwa nini anaendelea kuwa mnyoofu?

“Kwanza, ninaamini kwamba Mungu ni mnyoofu na atanitendea kwa unyoofu ikiwa nitamwiga. Pili, watoto wangu watajifunza kuwa wanyoofu ikiwa tu wataniona nikiwa mnyoofu.”

Matokeo yamekuwa nini? Anasema hivi: “Tuna chakula, mavazi, na makao. Hata hivyo, nyakati nyingine ninalazimika kuwaomba marafiki wanisaidie, kwa mfano, ninapohitaji pesa za kulipia matibabu ya ugonjwa wa ghafula. Sijawahi kamwe kukosa ninachohitaji. Kwa nini? Kwa sababu marafiki wangu wanajua kwamba siwadanganyi ninapowaeleza hali zangu na sijaribu kujipatia faida.

“Watoto wangu wanajifunza kuwa wanyoofu wanapoendelea kukua. Hivi karibuni, jirani mmoja aliona sarafu chache kwenye meza yetu akaniuliza kwa nini sikuogopa kwamba watoto wangu watazichukua. Hakuamini kamwe nilipomwambia kwamba watoto wangu hawawezi kufanya hivyo. Aliamua kuwajaribu bila mimi kujua. Kwa siri aliweka sarafu mbili zenye thamani ya faranga 100 katika nyumba yetu mahali ambapo watoto wangeweza kuziona kwa urahisi. Aliporudi siku iliyofuata, alishangaa sana kuona kwamba bado sarafu hizo zilikuwapo. Kuwa na watoto wanyoofu ni jambo bora zaidi kuliko kuwa na vitu vingi vya kimwili.”

“Kila Mtu Anaiba”

Watu wengi wanaiba kazini. Kwa hiyo, wengi wanasema, “Ikiwa kila mtu anaiba, kwa nini nisiibe?” Hata hivyo, Biblia inasema hivi: “Usiufuate umati kwa ajili ya makusudio maovu.” (Kutoka 23:2) Victoire ametii shauri hilo. Je, amepata matokeo mazuri?

Alipokuwa na umri wa miaka 19, Victoire alipata kazi katika kiwanda cha kutengeneza mafuta ya mawese. Muda si muda, aligundua kwamba wanawake 40 wanaofanya kazi katika kiwanda hicho walikuwa wakitumia vikapu vyao kuiba mbegu za mafuta hayo na kwenda nazo nyumbani. Kila mwisho-juma, waliuza mbegu hizo na kupata pesa zilizolingana na mshahara wa siku tatu au nne. Victoire anasema hivi: “Kwa kweli, kila mtu alikuwa akifanya hivyo. Walitazamia kwamba nitajiunga nao, lakini nilikataa, na kuwaambia kwamba kuwa mnyoofu ni njia yangu ya maisha. Walinidhihaki, wakidai kwamba ningepata hasara.

“Siku moja tulipokuwa tukiondoka kwenye kiwanda, meneja alitokea kwa ghafula. Alichunguza kikapu cha kila mtu na kupata mbegu nyingi katika kila kikapu isipokuwa changu. Wote waliopatwa na mbegu hizo waliambiwa kwamba wachague kufutwa kazi papo hapo au kufanya kazi kwa majuma mawili bila mshahara. Katika majuma hayo mawili, wanawake hao waliona wazi kwamba sikupata hasara.”

“Kuokota Si Kuiba”

Unafanya nini unapookota kitu chenye thamani ambacho mtu amepoteza? Watu wengi wanafurahi sana kukichukua na hawafikirii hata kidogo kumrudishia mwenyewe. Wanaamini kwamba “kuokota si kuiba.” Huenda wengine wakafikiri kwamba hakuna madhara ya kufanya hivyo. Wanadai kwamba mwenyewe anajua kimepotea. Wengine wanasema kwamba si daraka lao kumtafuta mwenyewe, kwa sababu huenda ikawa vigumu kumpata.

Mungu ana maoni gani kuhusu jambo hilo? Andiko la Kumbukumbu la Torati 22:1-3 linasema kwamba mtu aliyepata kitu kilichopotea hakupaswa kukaa nacho tu bali alipaswa kukaa nacho ‘mpaka mwenyewe adai kitu hicho, kisha amrudishie.’ (The New English Bible) Ikiwa mtu hakutangaza kwamba amepata kitu kilichopotea, angeshtakiwa kwamba ameiba. (Kutoka 22:9) Je, sheria hiyo inafaa leo? Christine anasadiki kwamba inafaa.

Christine ni msimamizi wa shule fulani. Jumatano moja (Siku ya 3) alichukua mshahara wake wa mwezi. Kama watu wengi wanavyofanya huko Afrika Magharibi, alifunga noti hizo pamoja na kuzitia ndani ya mfuko wake. Kisha akapanda pikipiki ya abiria na mara moja akapelekwa kwenye mkutano. Alipofika, alitafuta-tafuta ndani ya mfuko wake sarafu za kumlipa mwendeshaji wa pikipiki. Tayari giza lilikuwa limeingia na bila kujua, pesa alizokuwa nazo zilianguka chini.

Muda mfupi baadaye, Blaise, mwenye umri wa miaka 19, ambaye si mkaaji wa eneo hilo alipitia njia hiyo. Alikuwa amepanga kukutana na rafiki yake kwenye mkutano ambao Christine alikuwa anahudhuria. Aliona bunda la noti akazitia ndani ya mfuko wake. Mkutano ulipokwisha, alimwambia rafiki yake kwamba alikuwa ameokota kitu fulani nje na mtu yeyote aliyepoteza kitu angeweza kumpigia simu na kusema alichopoteza.

Christine alipofika nyumbani jioni hiyo, alishtuka sana kugundua kwamba mshahara wake wa mwezi mzima ulikuwa umepotea. Baada ya juma moja, alipomwambia rafiki yake Josephine, aliambiwa kwamba mgeni fulani aliyehudhuria mkutano alikuwa ameokota kitu fulani. Christine alimpigia simu Blaise na kumwambia kiasi cha pesa alichokuwa amepoteza. Christine alifurahi sana Blaise alipomrudishia pesa hizo. Namna gani Blaise? Alikaa na pesa hizo kwa juma moja, lakini alisema hivi: “Baada ya kurudisha pesa hizo nilipata shangwe nyingi ambayo singepata ikiwa singezirudisha.”

Kwa Nini Wanajitahidi Kuwa Wanyoofu Nyakati Zote?

Victorine, Victoire, na Blaise wanaishi katika maeneo mbalimbali na hawafahamiani. Hata hivyo, kuna jambo moja linalowaunganisha. Wao ni Mashahidi wa Yehova, ambao wanafuata mashauri ya Biblia kuhusu unyoofu. Wanangojea wakati ambapo Mungu atatimiza ahadi yake ya kuleta ulimwengu mpya. “Kulingana na ahadi yake tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.” Watu wote ambao watakuwa wakiishi wakati huo watakuwa waadilifu na wanyoofu.—2 Petro 3:13.

Victorine anajua kwamba matatizo yake ya kifedha yatakwisha kabisa wakati ambapo Mungu atabadili mambo. Hata hivyo, ana utajiri wa kiroho ambao hauwezi kununuliwa kwa pesa. Watoto wake ni wanyoofu na wana tabia nzuri. Kila Jumapili (Siku ya Yenga) ‘wanabubujikwa na maneno’ wanapozungumza na majirani wao kuhusu wema wa Mungu na jinsi atakavyowatosheleza “wote wanaomwitia yeye katika ukweli” na kwamba atawalinda “wale wote wanaompenda.”—Zaburi 145:7, 18, 20.

Baada ya muda, Victoire alitoka kwenye kile kiwanda cha kutengeneza mafuta. Alianza biashara yake ya kuuza garri (unga wa mhogo) sokoni. Watu wengi wanapenda kununua unga wake kwa sababu ya unyoofu wake. Baada ya muda, alipunguza muda aliokaa katika soko na kutumia muda zaidi akizungumza na wengine kuhusu tumaini la kuishi katika ulimwengu ambao hautakuwa kamwe na ukosefu wa unyoofu. Baadaye aliolewa, na sasa yeye pamoja na mume wake wanatumika wakiwa wahubiri wa wakati wote.

Christine aliangusha pesa zake mbele ya Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Blaise hakuwafahamu watu wengi kwenye mkutano huo, lakini alijua kwamba wao ni ndugu na dada zake Wakristo, ambao wanajitahidi kuwa wanyoofu nyakati zote.

Unawajua watu wangapi wanaojitahidi kikweli kuwa wanyoofu nyakati zote? Hebu jiwazie ukiwa pamoja na watu 50, 100, au 200 wanyoofu. Hiyo ndiyo furaha ambayo Mashahidi wa Yehova wanapata katika Majumba yao ya Ufalme. Kwa nini usihudhurie mikutano yao na kuwafahamu?

[Blabu katika ukurasa wa 12]

“Kuwa na watoto wanyoofu ni jambo bora zaidi kuliko kuwa na vitu vingi vya kimwili.”—VICTORINE

[Sanduku katika ukurasa wa 14]

Je, Andiko la Methali 6:30 Linaunga Mkono Kuiba?

Andiko la Methali 6:30 linasema hivi: “Watu hawamdharau mwizi kwa sababu tu anaiba ili kushibisha nafsi yake akiwa na njaa.” Je, maneno hayo yanaunga mkono kuiba? Hapana. Mistari mingine katika kitabu hicho inaonyesha kwamba Mungu anamwona mwizi kuwa na hatia kwa sababu ya kosa lake. Mstari unaofuata unasema hivi: “Lakini, akipatikana, atalipa mara saba ya kiasi hicho; atatoa vitu vyote vyenye thamani vya nyumba yake.” (Methali 6:31) Ingawa mtu anayeiba kwa sababu ya njaa huenda asionekane kuwa mbaya kama yule anayeiba kwa sababu ya pupa au ili kumuumiza mwingine, bado anapaswa ‘kulipa’ au kurudisha. Wale wanaotaka kumpendeza Mungu hawapaswi kuwa na hatia ya kuiba kwa sababu yoyote.