Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kundi Moja, Mchungaji Mmoja

Kundi Moja, Mchungaji Mmoja

Kundi Moja, Mchungaji Mmoja

“Ninyi ambao mmenifuata mtaketi pia juu ya viti vya ufalme kumi na viwili, mkiyahukumu yale makabila kumi na mawili ya Israeli.”—MT. 19:28.

1. Yehova alishughulika jinsi gani na wazao wa Abrahamu, na kwa nini hilo halimaanishi kwamba aliwapuuza kabisa watu wengine wote?

YEHOVA alimpenda Abrahamu, ndiyo sababu aliwaonyesha wazao wa Abrahamu upendo mshikamanifu. Kwa karne zaidi ya 15, aliliona taifa la Israeli, ambalo lilitokana na Abrahamu, kuwa watu ambao aliwachagua, ‘mali yake ya pekee.’ (Soma Kumbukumbu la Torati 7:6.) Je, hilo lilimaanisha kwamba Yehova aliwapuuza kabisa watu wa mataifa mengine? Hapana. Wakati huo, watu wasio Waisraeli ambao walitaka kumwabudu Yehova waliruhusiwa kujiunga na taifa lake la pekee. Watu hao waliogeuzwa imani walionwa kuwa sehemu ya taifa hilo. Waisraeli walipaswa kuwatendea kama ndugu zao. (Law. 19:33, 34) Na watu hao walipaswa kutii sheria zote za Yehova.—Law. 24:22.

2. Yesu alitoa tangazo gani lenye kushangaza, na linatokeza maswali gani?

2 Hata hivyo, Yesu aliwatangazia Wayahudi wa siku zake jambo hili lenye kushangaza: “Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu na kupewa taifa lenye kuzaa matunda yake.” (Mt. 21:43) Ni nani wangekuwa washiriki wa taifa hilo jipya, na badiliko hilo linatuhusu namna gani leo?

Taifa Jipya

3, 4. (a) Mtume Petro alilitambulisha jinsi gani taifa hilo jipya? (b) Ni nani wanaofanyiza taifa hilo jipya?

3 Mtume Petro alilitambulisha waziwazi taifa hilo jipya. Aliwaandikia hivi Wakristo wenzake: “Ninyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa kuwa mali ya pekee, ili mtangaze kotekote sifa bora’ zake yeye aliyewaita ninyi kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.” (1 Pet. 2:9) Kama ilivyotabiriwa, Wayahudi wa asili ambao walimkubali Yesu kuwa ndiye Masihi ndio waliokuwa washiriki wa kwanza wa taifa hilo jipya. (Dan. 9:27a; Mt. 10:6) Baadaye, watu wengi ambao hawakuwa Waisraeli waliingizwa katika taifa hilo, kwa sababu Petro aliendelea kusema hivi: “Wakati mmoja ninyi mlikuwa si watu, lakini sasa ninyi ni watu wa Mungu.”—1 Pet. 2:10.

4 Petro alikuwa akizungumza na nani katika andiko hilo? Mwanzoni mwa barua yake anasema hivi: “[Mungu] alituzaa sisi upya kwenye tumaini lililo hai kupitia ufufuo wa Yesu Kristo kutoka kwa wafu, kwenye urithi usioharibika na usiotiwa unajisi na usiofifia. Huo umewekwa akiba mbinguni kwa ajili yenu.” (1 Pet. 1:3, 4) Kwa hiyo, taifa hilo jipya limefanyizwa na Wakristo watiwa-mafuta, ambao wana tumaini la kwenda mbinguni. Wao ni “Israeli wa Mungu.” (Gal. 6:16) Katika maono, mtume Yohana aliona kwamba hesabu ya Waisraeli hao wa kiroho ni 144,000. ‘Wamenunuliwa kutoka kati ya wanadamu wakiwa matunda ya kwanza kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo’ ili watumike wakiwa “makuhani” na ‘watawale wakiwa wafalme pamoja na [Yesu] ile miaka elfu.’—Ufu. 5:10; 7:4; 14:1, 4; 20:6; Yak. 1:18.

Je, Taifa Hilo Linatia Ndani Watu Wengine?

5. (a) Maneno “Israeli wa Mungu” yanawahusu nani? (b) Kwa nini neno “Israeli” sikuzote halimaanishi watiwa-mafuta peke yao?

5 Basi, ni wazi kwamba maneno “Israeli wa Mungu” katika Wagalatia 6:16 yanawahusu Wakristo watiwa-mafuta peke yao. Hata hivyo, je, nyakati nyingine Yehova anatumia taifa la Israeli kama mfano, kuwahusu Wakristo wengine ambao si watiwa-mafuta? Jibu linapatikana katika maneno haya ambayo Yesu aliwaambia mitume wake waaminifu: “Nami ninafanya agano pamoja nanyi, sawa na vile Baba yangu alivyofanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme, ili mpate kula na kunywa mezani pangu katika ufalme wangu, na kuketi juu ya viti vya ufalme kuyahukumu makabila kumi na mawili ya Israeli.” (Luka 22:28-30) Hilo litatukia wakati wa “uumbaji-mpya,” au wakati wa kufanya upya vitu vyote, wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo.—Soma Mathayo 19:28.

6, 7. Maneno “makabila kumi na mawili ya Israeli” yanawahusu nani katika Mathayo 19:28 na Luka 22:30?

6 Wale 144,000 watatumika wakiwa wafalme, makuhani, na mahakimu mbinguni wakati wa ule Utawala wa Miaka Elfu. (Ufu. 20:4) Watahukumu nani na watatawala nani? Katika andiko la Mathayo 19:28 na Luka 22:30, tunaambiwa kwamba watayahukumu “yale makabila kumi na mawili ya Israeli.” “Yale makabila kumi na mawili ya Israeli” yanafananisha nani katika maandiko hayo? Yanafananisha watu wote wenye tumaini la kuishi duniani, wale ambao wanaonyesha imani katika dhabihu ya Yesu lakini si sehemu ya jamii ya makuhani wa kifalme. (Kabila la Lawi halikuhesabiwa kati ya yale makabila 12 ya Waisraeli wa asili.) Wale wanaofananishwa na yale makabila 12 ya Israeli katika maandiko hayo ni wale ambao watafaidika kiroho kupitia utumishi wa kikuhani wa wale 144,000. Watu hao wanaofaidika kiroho ambao si makuhani, wao pia ni watu wa Mungu, anawapenda na kuwakubali. Kwa kufaa, wanalinganishwa na watu wake wa zamani.

7 Baada ya mtume Yohana kuona wale Waisraeli wa kiroho 144,000 wakitiwa muhuri wa kudumu kabla ya dhiki kuu, aliona pia “umati mkubwa” usio na hesabu, “kutoka mataifa yote.” (Ufu. 7:9) Watu hao wataokoka dhiki kuu na kuingia katika Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. Mabilioni ya watu watakaofufuliwa watajiunga nao. (Yoh. 5:28, 29; Ufu. 20:13) Watu wote hao watafanyiza “makabila kumi na mawili ya Israeli,” ya mfano ambayo yatahukumiwa na Yesu na watawala wenzake 144,000.—Mdo. 17:31; 24:15; Ufu. 20:12.

8. Mambo yaliyotukia katika Siku ya Upatanisho kila mwaka yalionyesha jinsi gani uhusiano kati ya wale 144,000 na wanadamu wengine?

8 Uhusiano kati ya wale 144,000 na wanadamu wengine ulionyeshwa mapema na mambo yaliyotukia katika Siku ya Upatanisho kila mwaka. (Law. 16:6-10) Kwanza, kuhani mkuu alipaswa kutoa dhabihu ya ng’ombe-dume kuwa toleo la dhambi “kwa ajili yake mwenyewe na nyumba yake.” Hivyo, dhabihu ya Yesu inatumika kwanza kwa ajili ya nyumba yake ya makuhani wa cheo cha chini, wale ambao watatumika pamoja naye mbinguni. Pia, zamani katika Siku ya Upatanisho, mbuzi wawili walitolewa kwa ajili ya dhambi za Waisraeli wengine. Katika mazungumzo haya, kabila la makuhani linafananisha wale 144,000, na Waisraeli wengine wanafananisha wote walio na tumaini la kuishi duniani. Hilo linaonyesha kwamba maneno “makabila kumi na mawili ya Israeli” katika Mathayo 19:28 hayamaanishi makuhani wa cheo cha chini wa Yesu waliozaliwa kwa roho bali watu wengine wote ambao wanaonyesha imani katika dhabihu ya Yesu. *

9. Katika maono ya hekalu la Ezekieli, makuhani wanafananisha nani, na Waisraeli wasio makuhani wanafananisha nani?

9 Fikiria mfano mwingine. Nabii Ezekieli alipata maono yenye mambo mengi kuhusu hekalu la Yehova. (Eze., sura ya 40-48) Katika maono hayo, makuhani walitumika katika hekalu hilo, wakifundisha, kurekebishwa, na kupokea mashauri kutoka kwa Yehova. (Eze. 44:23-31) Watu wa makabila mbalimbali walikuja kuabudu na kutoa dhabihu katika hekalu hilohilo. (Eze. 45:16, 17) Hivyo basi, katika maono hayo, makuhani wanafananisha watiwa-mafuta, nao Waisraeli wa makabila yasiyo ya kikuhani wanafananisha watu walio na tumaini la kuishi duniani. Maono hayo yanakazia kwamba vikundi hivyo viwili vinafanya kazi pamoja kwa umoja, huku jamii ya makuhani ikiongoza katika ibada safi.

10, 11. (a) Tumeona maneno ya Yesu yakitimizwa kwa njia gani yenye kutia nguvu imani? (b) Ni swali gani linalotokea kuhusu kondoo wengine?

10 Yesu alisema kuhusu “kondoo wengine,” ambao hawangekuwa katika “zizi” la “kundi dogo” la wafuasi wake watiwa-mafuta. (Yoh. 10:16; Luka 12:32) Alisema hivi: “Hao pia nitawaleta, nao wataisikiliza sauti yangu, nao watakuwa kundi moja, mchungaji mmoja.” Imani yetu imetiwa nguvu kama nini kuona maneno hayo yakitimizwa! Vikundi viwili vya watu vimeunganishwa pamoja, yaani, kikundi kidogo cha watiwa-mafuta na umati mkubwa wa kondoo wengine. (Soma Zekaria 8:23.) Ingawa kondoo wengine hawatumiki kwa njia ya mfano katika ua wa ndani wa hekalu la kiroho, wanatumika katika ua wa nje wa hekalu hilo.

11 Kwa kuwa nyakati nyingine Yehova analinganisha kondoo wengine na washiriki wasio makuhani wa taifa la kale la Israeli, je, wale ambao wana tumaini la kuishi duniani wanapaswa pia kula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho? Sasa tutazungumzia swali hilo.

Agano Jipya

12. Yehova alitabiri mpango gani mpya?

12 Yehova alitabiri kwamba kungekuwa na mpango mpya kwa ajili ya watu wake aliposema hivi: “Hili ndilo agano nitakalofanya pamoja na nyumba ya Israeli baada ya siku hizo. . . . Nitaitia sheria yangu ndani yao, nami nitaiandika katika moyo wao. Nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.” (Yer. 31:31-33) Kupitia agano hilo jipya, ahadi ya Yehova kwa Abrahamu ingetimizwa kwa njia tukufu na yenye kudumu.—Soma Mwanzo 22:18.

13, 14. (a) Ni nani washiriki wa agano jipya? (b) Ni nani wanaofaidika na agano hilo, nao ‘wanalishika’ jinsi gani agano hilo jipya?

13 Yesu alizungumzia agano hilo jipya usiku uliotangulia kifo chake aliposema hivi: “Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa msingi wa damu yangu, ambayo itamwagwa kwa ajili yenu.” (Luka 22:20; 1 Kor. 11:25) Je, Wakristo wote wanatiwa ndani ya agano hilo jipya? Hapana. Wakristo fulani, kama wale mitume ambao walikunywa kikombe hicho jioni hiyo, ni washiriki katika hilo agano jipya. * Yesu alifanya nao agano lingine ili watawale pamoja naye katika Ufalme wake. (Luka 22:28-30) Watashiriki pamoja na Yesu katika Ufalme wake.—Luka 22:15, 16.

14 Namna gani wale ambao wataishi duniani chini ya Ufalme wake? Wao wanafaidika na agano hilo jipya. (Gal. 3:8, 9) Hata ingawa wao si washiriki wa agano hilo, ‘wanalishika’ agano hilo kwa kutii matakwa yake, kama ilivyotabiriwa na nabii Isaya: “Wageni ambao wamejiunga na Yehova ili kumhudumia na kulipenda jina la Yehova, ili kuwa watumishi wake, wale wote wanaoishika sabato ili wasiitie unajisi na kulishika agano langu, mimi pia nitawaleta katika mlima wangu mtakatifu na kuwafanya washangilie ndani ya nyumba yangu ya sala.” Kisha, Yehova anasema: “Kwa maana nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa ajili ya vikundi vyote vya watu.”—Isa. 56:6, 7.

Ni Nani Wanaopaswa Kula Mkate na Kunywa Divai ya Ukumbusho?

15, 16. (a) Mtume Paulo anahusianisha agano jipya na nini? (b) Kwa nini wale walio na tumaini la kuishi duniani hawapaswi kula mkate wala kunywa divai ya Ukumbusho?

15 Wale ambao wako katika agano jipya ‘wana ujasiri wa njia ya kuingia katika mahali patakatifu.’ (Soma Waebrania 10:15-20.) Hawa ndio ‘watakaopokea ufalme ambao hauwezi kutikiswa.’ (Ebr. 12:28) Hivyo basi, ni wale tu ambao watakuwa wafalme na makuhani mbinguni pamoja na Yesu Kristo wanaopaswa kunywa “kikombe” ambacho kinafananisha agano jipya. Washiriki hao wa agano jipya ndio wameahidiwa kufunga ndoa na Mwana-Kondoo. (2 Kor. 11:2; Ufu. 21:2, 9) Watu wengine wote wanaohudhuria Ukumbusho wa kila mwaka wanatazama kwa heshima, hawanywi divai wala kula mkate wa Ukumbusho.

16 Paulo anatusaidia pia kuelewa kwamba wale walio na tumaini la kuishi duniani hawanywi divai wala kula mkate wa Ukumbusho. Aliwaambia hivi Wakristo watiwa-mafuta: “Kwa maana kila mara mnapokula mkate huu na kunywa kikombe hiki, mnaendelea kukitangaza kifo cha Bwana, mpaka atakapofika.” (1 Kor. 11:26) Bwana ‘atafika’ wakati gani? Atafika wakati atakapokuja kuwachukua washiriki wa mwisho watiwa-mafuta wa jamii yake ya bibi-arusi na kuwapeleka katika makao yao ya mbinguni. (Yoh. 14:2, 3) Ni wazi kwamba ukumbusho wa kila mwaka wa Chakula cha Jioni cha Bwana hautaendelea milele. “Wale waliobaki” duniani wa uzao wa mwanamke wataendelea kushiriki chakula hicho mpaka wote watakapopokea thawabu yao ya kimbingu. (Ufu. 12:17) Hata hivyo, ikiwa wale watakaoishi milele duniani wangehitaji kushiriki mifano hiyo, basi chakula cha Ukumbusho kingehitaji kuendelea kuwapo milele.

“Nao Watakuwa Watu Wangu”

17, 18. Unabii ulio katika Ezekieli 37:26, 27 umetimizwa jinsi gani?

17 Yehova alitabiri hivi kuhusu umoja wa watu wake: “Nitafanya agano la amani pamoja nao; watakuwa na agano lenye kudumu mpaka wakati usio na kipimo. Nami nitawaweka na kuwazidisha na kuweka patakatifu pangu katikati yao mpaka wakati usio na kipimo. Na maskani yangu kwa kweli itakuwa juu yao, nami hakika nitakuwa Mungu wao, na wao wenyewe watakuwa watu wangu.”—Eze. 37:26, 27.

18 Watu wote wa Mungu wana pendeleo la kufaidika kutokana na utimizo wa ahadi hiyo nzuri ajabu, agano hilo linalowaletea Wakristo amani. Ndiyo, Yehova amewahakikishia watumishi wote wanaomtii kwamba watapata amani. Matunda ya roho yake yanaonekana wazi kati yao. Patakatifu pake, ambapo panafananisha ibada safi ya Wakristo, pako katikati yao. Kwa kweli, wamekuwa watu wake, kwa sababu wameacha ibada ya sanamu ya kila namna, nao wanamwabudu Yehova akiwa Mungu wa pekee wa kweli.

19, 20. Ni nani wanaohesabiwa kati ya wale ambao Yehova anawaita “watu wangu,” na ni nini kinachowezekana kupitia agano jipya?

19 Tumesisimuka kama nini kuona vikundi hivyo viwili vikiunganishwa katika nyakati zetu! Ingawa washiriki wa umati mkubwa ambao unaendelea kuongezeka hawana tumaini la kwenda mbinguni, wanathamini pendeleo la kushirikiana na wale walio na tumaini hilo. Wameshikamana na Israeli wa Mungu. Kwa kufanya hivyo, wanahesabiwa kati ya wale ambao Yehova anawaita “watu wangu.” Wanatimiza unabii huu: “Mataifa mengi yatajiunga na Yehova siku hiyo, nao watakuwa watu wangu; nami nitakaa katikati yako.”—Zek. 2:11; 8:21; soma Isaya 65:22; Ufunuo 21:3, 4.

20 Yehova ametumia agano jipya kutimiza mambo hayo yote. Mamilioni ya wageni wa kiroho wamejiunga na taifa linalokubaliwa na Yehova. (Mika 4:1-5) Wameazimia kuendelea kulishika agano hilo kwa kukubali maandalizi ya agano hilo na kutii matakwa yake. (Isa. 56:6, 7) Wanapofanya hivyo, wao pamoja na Israeli wa Mungu, wanafurahia baraka kubwa ya kuendelea kuwa na amani. Na ufurahie baraka hiyo sasa na kwa umilele wote!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Vivyo hivyo, watiwa-mafuta ndio hasa wanaoitwa “kutaniko.” (Ebr. 12:23) Hata hivyo, neno “kutaniko” linaweza pia kumaanisha Wakristo wote, iwe wana tumaini la kwenda mbinguni au la kuishi duniani.—Ona gazeti Mnara wa Mlinzi, Aprili 15, 2007 (15/4/2007), ukurasa wa 21-23.

^ fu. 13 Yesu ni Mpatanishi wa agano hilo, yeye si mshiriki. Akiwa Mpatanishi, inaonekana kwamba hakula mkate wala kunywa divai ya Ukumbusho.

Je, Unakumbuka?

• “Yale makabila kumi na mawili ya Israeli” ambayo yatahukumiwa na wale 144,000 ni nani?

• Watiwa-mafuta na kondoo wengine wana uhusiano gani na agano jipya?

• Je, Wakristo wote wanapaswa kula mkate na kunywa divai ya Ukumbusho?

• Unabii ulitabiri kungekuwa na umoja gani katika siku zetu?

[Maswali ya Funzo]

[Grafu/Picha katika ukurasa wa 25]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Watu wengi leo wanatumika pamoja na Israeli wa Mungu

1950 | 373,430

1970 | 1,483,430

1990 | 4,017,213

2009 | 7,313,173