Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kubatizwa Katika Jina la Nani na kwa Nini?

Kubatizwa Katika Jina la Nani na kwa Nini?

Kubatizwa Katika Jina la Nani na kwa Nini?

“Nendeni mkafanye wanafunzi . . . , mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.”—MT. 28:19.

1, 2. (a) Ni nini kilichotukia Yerusalemu siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K.? (b) Kwa nini watu wengi walichochewa kubatizwa?

JIJI la Yerusalemu lilijaa watu kutoka katika nchi nyingi siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Kulikuwa na sherehe ya maana sana na wageni wengi walikuwa wakiisherehekea. Lakini jambo fulani lisilo la kawaida lilitukia, na baadaye mtume Petro akatoa hotuba yenye kusisimua ambayo ilikuwa na matokeo ya ajabu. Watu 3,000 hivi, Wayahudi na watu waliogeuzwa imani waliguswa mioyo na maneno yake, wakatubu, na kubatizwa katika maji. Hivyo, wakajiunga na kutaniko jipya la Kikristo ambalo lilikuwa limeanzishwa. (Mdo. 2:41) Ni wazi kwamba ubatizo huo wa watu wengi ndani ya vidimbwi au matangi karibu na Yerusalemu ulisababisha msisimuko mkubwa!

2 Ni nini kilichofanya watu wengi hivyo wabatizwe? Mapema siku hiyo, ‘kulitokea kutoka mbinguni kelele kama ile ya upepo wenye nguvu unaovuma.’ Katika chumba cha juu cha nyumba moja, wanafunzi 120 hivi wa Yesu walijazwa roho takatifu. Baadaye, wanaume na wanawake wenye kumwogopa Mungu walikusanyika na walishangaa kuwasikia wanafunzi hao ‘wakisema katika lugha tofauti.’ Baada ya kusikiliza mambo ambayo Petro alisema, kutia ndani maelezo yake ya waziwazi kuhusu kifo cha Yesu, wengi “walichomwa moyoni.” Walipaswa kufanya nini? Petro alijibu: “Tubuni, na acheni kila mmoja wenu abatizwe katika jina la Yesu Kristo . . . , nanyi mtapokea zawadi ya bure ya roho takatifu.”—Mdo. 2:1-4, 36-38.

3. Siku ya Pentekoste, Wayahudi na watu waliogeuzwa imani waliotubu walihitaji kufanya nini?

3 Fikiria hali ya kiroho ya Wayahudi hao na watu waliogeuzwa imani ambao walimsikiliza Petro. Tayari walikuwa wamemkubali Yehova kuwa Mungu wao. Na kutokana na Maandiko ya Kiebrania, walijua kwamba roho takatifu ni nguvu ya utendaji ya Mungu ambayo alitumia wakati wa uumbaji na baadaye. (Mwa. 1:2; Amu. 14:5, 6; 1 Sam. 10:6; Zab. 33:6) Lakini walihitaji jambo fulani zaidi. Lilikuwa jambo la maana sana kwao kuelewa na kukubali njia ya Mungu ya wokovu, yaani, yule Masihi, Yesu. Hivyo, Petro alikazia kwamba walihitaji ‘kubatizwa katika jina la Yesu Kristo.’ Siku chache kabla ya hapo, Yesu aliyefufuliwa alimwamuru Petro na wengine wawabatize watu “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.” (Mt. 28:19, 20) Jambo hilo lilikuwa na maana sana katika karne ya kwanza, na bado lina maana sana leo. Ni maana gani hiyo?

Katika Jina la Baba

4. Ni mabadiliko gani yaliyotokea kuhusu watu ambao walikuwa na uhusiano pamoja na Yehova?

4 Kama tulivyoona, wale waliochochewa na hotuba ya Petro walikuwa wakimwabudu Yehova na kabla ya hapo walikuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Walikuwa wakijitahidi kufuata Sheria yake, na ndiyo sababu walitoka nchi nyingine na kuja Yerusalemu. (Mdo. 2:5-11) Hata hivyo, Mungu alikuwa amebadili njia yake ya kushughulika na wanadamu. Aliwakataa Wayahudi kuwa taifa lake la pekee; na ili kupata kibali cha Mungu haikuwa tena lazima kwa watu hao kushika Sheria. (Mt. 21:43; Kol. 2:14) Ikiwa wasikilizaji hao walitaka kuwa na uhusiano wa kudumu pamoja na Yehova, walihitaji kitu kingine.

5, 6. Wayahudi wengi na watu waliogeuzwa imani katika karne ya kwanza walifanya nini ili kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu?

5 Bila shaka, hilo halikumaanisha kumwacha Yehova, Mpaji-Uhai wao. (Mdo. 4:24) Hapana, wale ambao wangekubali maelezo ya Petro wangetambua kuliko wakati mwingine wowote kwamba Yehova alikuwa Baba mwenye upendo. Alimtuma Masihi kuwakomboa na alikuwa tayari kuwasamehe hata wale ambao Petro alisema hivi kuwahusu: “Acha nyumba yote ya Israeli ijue kwa hakika kwamba Mungu alimfanya Bwana na pia Kristo, Yesu huyu ambaye ninyi mlimtundika mtini.” Kwa kweli, wale ambao wangekubali maneno ya Petro wangekuwa sasa na sababu nzuri hata zaidi ya kuthamini yale ambayo Mungu ambaye ni Baba alikuwa amefanya kwa ajili ya wale ambao walitaka kuwa na uhusiano pamoja Naye!—Soma Matendo 2:30-36.

6 Kwa kweli, Wayahudi hao na watu waliogeuzwa imani wangeona sasa kwamba kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova kulitia ndani kumtambua yeye kuwa Mpaji wa wokovu kupitia Yesu. Hivyo, unaweza kuelewa kwa nini walitubu dhambi zao, kutia ndani dhambi ya kushiriki kumuua Yesu iwe walijua au hawakujua. Na inaeleweka pia kwa nini katika siku zilizofuata ‘waliendelea kujitoa wenyewe kwa fundisho la mitume.’ (Mdo. 2:42) Wangeweza na walitaka ‘kukikaribia, wakiwa na uhuru wa kusema, kiti cha ufalme cha fadhili zisizostahiliwa.’—Ebr. 4:16.

7. Watu wengi leo wamebadili maoni yao juu ya Mungu jinsi gani na kubatizwa katika jina la Baba?

7 Leo, mamilioni ya watu wenye malezi mbalimbali wamejifunza ukweli kumhusu Yehova kutoka katika Biblia. (Isa. 2:2, 3) Wengine wao walikuwa watu wasioamini kwamba kuna Mungu au waliamini kuna Mungu lakini hapendezwi na uumbaji wake, lakini baadaye walisadiki kabisa kwamba kuna Muumba ambaye wanaweza kuwa na uhusiano mzuri pamoja naye. Wengine waliabudu mungu wa utatu au sanamu mbalimbali. Walijifunza kwamba Yehova peke yake ndiye Mungu mweza-yote, na sasa wanasali kwake wakitumia jina lake binafsi. Hilo linapatana na ukweli wa kwamba Yesu alisema kuwa wanafunzi wake wanapaswa kubatizwa katika jina la Baba.

8. Wale ambao hawakujua kuhusu dhambi ya Adamu walihitaji kujua nini kumhusu Baba?

8 Wamejifunza pia kwamba walirithi dhambi kutoka kwa Adamu. (Rom. 5:12) Hilo lilikuwa jambo jipya ambalo walipaswa kukubali kuwa la kweli. Watu hao wanaweza kulinganishwa na mwanamume mgonjwa ambaye hakujua kwamba ni mgonjwa. Huenda alikuwa na dalili fulani, kama vile maumivu ya mara kwa mara. Lakini, kwa kuwa hakufanyiwa uchunguzi wa ugonjwa fulani hususa, huenda alifikiri kwamba afya yake ni nzuri. Hata hivyo, uchunguzi ulionyesha kwamba ni mgonjwa. (Linganisha na 1 Wakorintho 4:4.) Namna gani ikiwa alifanyiwa uchunguzi ulio sahihi wa ugonjwa wake? Je, halingekuwa jambo la hekima kutafuta na kukubali matibabu yanayojulikana, yaliyothibitishwa, na mazuri? Vivyo hivyo, baada ya kujifunza ukweli kuhusu dhambi tuliyorithi, watu wengi wamekubali maelezo ya Biblia ya kwamba dhambi ni kama “ugonjwa” na wamekuja kuelewa kwamba Mungu anaweza “kuponya” ugonjwa huo. Ndiyo, wote ambao wametengwa mbali na Baba wanahitaji kumrudia Yule ambaye anaweza “kuwaponya.”—Efe. 4:17-19.

9. Yehova alifanya nini ili tuweze kuwa na uhusiano mzuri pamoja naye?

9 Ikiwa tayari umeweka maisha yako wakfu kwa Yehova Mungu na umekuwa Mkristo aliyebatizwa, unajua kwamba ni jambo zuri ajabu kuwa na uhusiano mzuri pamoja naye. Unaweza sasa kuthamini jinsi Baba yako, Yehova, alivyo mwenye upendo. (Soma Waroma 5:8.) Ingawa Adamu na Hawa walimtendea dhambi, Mungu alichukua hatua ili wazao wao, kutia ndani sisi, wawe na uhusiano mzuri pamoja naye. Kwa kufanya hivyo, Mungu alilazimika kuvumilia uchungu wa kuona Mwana wake mpendwa akiteseka na kufa. Je, kujua jambo hilo hakutusaidii kutambua mamlaka ya Mungu na kutii kwa upendo amri zake? Ikiwa bado hujajiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa, una sababu nzuri ya kufanya hivyo.

Katika Jina la Mwana

10, 11. (a) Kwa nini unapaswa kumshukuru Yesu? (b) Unahisi jinsi gani kuhusu Yesu kufa akiwa fidia au dhabihu ya ukombozi?

10 Hata hivyo, fikiria tena yale ambayo Petro aliambia ule umati. Alikazia wazo la kumkubali Yesu, ambalo linahusiana moja kwa moja na kubatizwa “katika jina . . . la Mwana.” Kwa nini hilo lilikuwa jambo la maana sana wakati huo, na kwa nini ni la maana sana leo? Kumkubali Yesu na kubatizwa katika jina lake kunamaanisha kutambua daraka lake katika uhusiano wetu pamoja na Muumba. Yesu alipaswa kutundikwa kwenye mti wa mateso ili kuwaondolea Wayahudi laana ya Sheria; hata hivyo, kifo chake kilikuwa na faida nyingine kubwa zaidi. (Gal. 3:13) Alitoa fidia au dhabihu ya ukombozi ambayo wanadamu wote walihitaji. (Efe. 2:15, 16; Kol. 1:20; 1 Yoh. 2:1, 2) Ili kutimiza hilo, Yesu alivumilia ukosefu wa haki, matusi, mateso, na mwishowe kifo. Unathamini dhabihu yake kwa kadiri gani? Wazia kwamba wewe ni kijana wa kiume mwenye umri wa miaka 12 na unasafiri ndani ya meli ya Titanic, ambayo iligonga barafu na kuzama baharini mwaka wa 1912. Unajaribu kuruka ndani ya mashua ndogo ya kuokoa watu, lakini imejaa. Kisha mwanamume mmoja aliye ndani ya mashua hiyo anambusu mke wake, anaruka na kurudi ndani ya meli, halafu anakutia ndani ya mashua ya kuokoa. Unahisi namna gani? Bila shaka unamshukuru sana. Unaweza kuelewa jinsi kijana mmoja alivyohisi baada ya kuokolewa kwa njia hiyohiyo. * Hata hivyo, Yesu alikufanyia mengi zaidi. Alikufa ili uweze kupata tena uzima usio na mwisho.

11 Ulihisi jinsi gani ulipojifunza kuhusu yale ambayo Mwana wa Mungu alifanya kwa ajili yako? (Soma 2 Wakorintho 5:14, 15.) Inaelekea kwamba ulikuwa na shukrani nyingi sana. Hilo lilikuchochea kuweka maisha yako wakfu kwa Mungu na ‘kuishi si kwa ajili yako tena, bali kwa ajili ya yeye aliyekufa kwa ajili yako.’ Kubatizwa katika jina la Mwana kunamaanisha kutambua yale ambayo Yesu amefanya kwa ajili yako na kukubali mamlaka yake akiwa “Wakili Mkuu wa uzima.” (Mdo. 3:15; 5:31) Zamani, hukuwa na uhusiano pamoja na Muumba, na kwa wazi hukuwa na tumaini la kweli. Lakini kwa kuwa una imani katika damu iliyomwagwa ya Yesu Kristo na umebatizwa, sasa una uhusiano mzuri pamoja na Baba. (Efe. 2:12, 13) Mtume Paulo aliandika hivi: “Ninyi ambao hapo zamani mlikuwa mmetengwa, nanyi mlikuwa adui kwa sababu akili zenu zilikuwa zimekazwa juu ya matendo maovu, [Mungu] sasa amewapatanisha tena kwa njia ya mwili wenye nyama wa huyo kupitia kifo chake [Yesu], ili awatoe ninyi mkiwa watakatifu na wasio na dosari.”—Kol. 1:21, 22.

12, 13. (a) Kubatizwa katika jina la Mwana kunapaswa kukuchochea kufanya nini mtu fulani anapokukosea? (b) Ukiwa Mkristo aliyebatizwa katika jina la Yesu, una wajibu gani?

12 Ingawa ulibatizwa katika jina la Mwana, unatambua vizuri kwamba una mielekeo ya dhambi. Ni jambo la maana sana kutambua hilo kila siku. Kwa mfano, ikiwa mtu fulani anakukosea, je, unakumbuka kwamba nyote wawili ni watenda-dhambi? Nyote wawili mnahitaji msamaha wa Mungu, na mnapaswa kusameheana. (Marko 11:25) Yesu alitoa mfano ili kukazia uhitaji huo: Bwana wa mtumwa fulani alifuta deni la mtumwa huyo la talanta elfu kumi (dinari milioni 60). Baadaye, mtumwa huyo hakumsamehe mtumwa mwenzake aliyekuwa na deni lake la dinari 100. Yesu akakata kauli hii: Yehova hatamsamehe yule ambaye anakataa kumsamehe ndugu yake. (Mt. 18:23-35) Ndiyo, kubatizwa katika jina la Mwana kunamaanisha kutambua mamlaka ya Yesu na kujitahidi kufuata mfano na mafundisho yake, kutia ndani, fundisho la kuwa tayari kuwasamehe wengine.—1 Pet. 2:21; 1 Yoh. 2:6.

13 Kwa kuwa wewe si mkamilifu, huwezi kumwiga Yesu kwa ukamilifu. Hata hivyo, kwa kuwa ulijiweka wakfu kwa Mungu kwa moyo wako wote, unapaswa kumwiga Yesu kwa uwezo wako wote. Hilo linatia ndani kuendelea kujitahidi kuvua utu wa zamani na kuvaa utu mpya. (Soma Waefeso 4:20-24.) Unapomheshimu rafiki fulani, inaelekea unajitahidi kuiga mfano na sifa zake nzuri. Vivyo hivyo, unataka sana kujifunza kutoka kwa Kristo na kumwiga.

14. Unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba unatambua mamlaka ya Yesu akiwa Mfalme wa kimbingu?

14 Kuna njia nyingine ya kuonyesha kwamba unaelewa kile kinachomaanishwa na kubatizwa katika jina la Mwana. Mungu “alivitiisha pia vitu vyote chini ya miguu yake [Yesu], na kumfanya kuwa kichwa juu ya vitu vyote kuhusiana na kutaniko.” (Efe. 1:22) Hivyo, unahitaji kuheshimu njia ambayo Yesu anatumia kuwaongoza wale waliojiweka wakfu kwa Yehova. Kristo anawatumia wanadamu wasio wakamilifu katika kutaniko lenu, hasa wanaume wazee kiroho, yaani, wazee waliowekwa rasmi. Mpango wa kuwa na wanaume hao waliowekwa rasmi ni “kwa kusudi la kuwarekebisha upya watakatifu, . . . kwa ajili ya kuujenga mwili wa Kristo.” (Efe. 4:11, 12) Hata mwanadamu asiye mkamilifu akikosea, Yesu akiwa Mfalme wa Ufalme wa kimbingu anaweza kushughulikia jambo hilo kwa wakati wake na kwa njia yake. Je, unaamini hilo?

15. Ikiwa bado hujabatizwa, ni baraka gani unazoweza kutazamia baada ya kubatizwa?

15 Tena, wengine bado hawajajiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Ikiwa hujafanya hivyo, je, unaweza kuona kutokana na yale yanayosemwa hapo juu kwamba kumtambua Mwana ni jambo la hekima linaloonyesha kwamba unathamini yale aliyofanya kwa ajili yako? Ukibatizwa katika jina la Mwana utapata baraka nyingi sana.—Soma Yohana 10:9-11.

Katika Jina la Roho Takatifu

16, 17. Kubatizwa katika jina la roho takatifu kunamaanisha nini kwako?

16 Kubatizwa katika jina la roho takatifu kunamaanisha nini? Kama ilivyotajwa mapema, wale ambao walimsikiliza Petro siku ya Pentekoste walijua kuhusu roho takatifu. Kwa kweli, wangeweza kuona uthibitisho ulio wazi kwamba Mungu aliendelea kutumia roho takatifu. Petro alikuwa mmoja wa wale ‘waliojazwa roho takatifu na ambao walianza kusema katika lugha tofauti.’ (Mdo. 2:4, 8) Maneno “katika jina la” hayamaanishi kwamba ni jina la mtu. Leo, mambo mengi yanafanywa “katika jina la serikali,” ambayo si mtu. Mambo hayo yanafanywa kwa mamlaka ya serikali. Vivyo hivyo, mtu anayebatizwa katika jina la roho takatifu anatambua kwamba roho takatifu si mtu, bali ni nguvu ya utendaji ya Yehova. Na kubatizwa katika jina la roho takatifu kunamaanisha kwamba mtu anatambua kazi ambayo roho takatifu inatimiza katika kusudi la Mungu.

17 Je, si kweli kwamba kupitia funzo la Biblia umejua roho takatifu ni nini? Kwa mfano, umeelewa kwamba Maandiko yaliandikwa chini ya mwongozo wa roho takatifu. (2 Tim. 3:16) Kadiri ulivyofanya maendeleo ya kiroho, inaelekea ulielewa kwa undani kwamba ‘Baba aliye mbinguni anawapa roho takatifu wale wanaomwomba,’ kutia ndani wewe. (Luka 11:13) Inawezekana kwamba umeona roho takatifu ikitenda kazi katika maisha yako. Kwa upande mwingine, ikiwa bado hujabatizwa katika jina la roho takatifu, uhakikisho wa Yesu wa kwamba Baba anawapa watu roho takatifu unamaanisha kuwa kadiri unavyopokea roho hiyo ndivyo utakavyopata baraka kwelikweli.

18. Wale ambao wanabatizwa katika jina la roho takatifu wanapata baraka gani?

18 Ni wazi kwamba leo pia, Yehova analiongoza kutaniko la Kikristo kupitia roho yake. Roho hiyo inamsaidia pia kila mmoja wetu katika utendaji mbalimbali wa kila siku. Kubatizwa katika jina la roho takatifu kunamaanisha kwamba tunaelewa daraka ambalo roho hiyo inatimiza katika maisha yetu na tunaonyesha shukrani kwa kushirikiana nayo. Huenda wengine wakajiuliza jinsi tunavyoweza kuishi kulingana na wakfu wetu kwa Yehova na jinsi roho takatifu inavyohusika. Tutazungumzia jambo hilo katika habari inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Ona gazeti la Amkeni! la Kiingereza la Oktoba 22, 1981 (22/10/1981), ukurasa wa 3-8, au la Januari 22, 1982 (22/1/1982), ukurasa 3-8, la Kifaransa.

Je, Unakumbuka?

• Kubatizwa katika jina la Baba kunatia ndani nini?

• Inamaanisha nini kubatizwa katika jina la Mwana?

• Unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba unathamini umuhimu wa kubatizwa katika jina la Baba na la Mwana?

• Kubatizwa katika jina la roho takatifu kunamaanisha nini?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

By permission of the Israel Museum, Jerusalem

[Hisani]

Baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., wanafunzi waliingia katika uhusiano gani pamoja na Baba?