Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuendelea Kuwa na Kibali cha Mungu Hali Zinapobadilika

Kuendelea Kuwa na Kibali cha Mungu Hali Zinapobadilika

Kuendelea Kuwa na Kibali cha Mungu Hali Zinapobadilika

JE, UNAKABILIANA na mabadiliko katika maisha yako? Je, unashindwa kukubali mabadiliko hayo? Wengi wetu wamekabiliana na mabadiliko au watakabiliana nayo wakati ujao. Mifano ya watu fulani walioishi zamani inaweza kutusaidia kutambua sifa ambazo zitatusaidia.

Kwa mfano, mfikirie Daudi na mabadiliko mengi aliyokabili. Alikuwa kijana mchungaji tu Samweli alipomtia mafuta ili awe mfalme baadaye. Alipokuwa kijana mdogo, alijitolea kupigana na lile jitu la Wafilisti, Goliathi. (1 Sam. 17:26-32, 42) Kijana Daudi alialikwa kuishi katika makao ya Mfalme Sauli, akachaguliwa kuwa mkuu wa jeshi. Daudi hangeweza hata kuwazia kwamba angekabiliana na mabadiliko hayo yote katika maisha yake; wala hakujua mambo ambayo yangetokea baadaye.

Uhusiano wa Daudi na Sauli uliharibika kabisa. (1 Sam. 18:8, 9; 19:9, 10) Ili kuokoa uhai wake, Daudi alilazimika kuishi akiwa mkimbizi kwa miaka mingi. Hata alipokuwa akitawala akiwa mfalme wa Israeli, hali zake zilibadilika kabisa, hasa baada ya kufanya uzinzi na kuua alipokuwa akijaribu kuficha dhambi hiyo. Kwa sababu ya dhambi zake, Daudi alipatwa na misiba katika familia yake. Kwa mfano, Absalomu, mwana wa Daudi aliasi. (2 Sam. 12:10-12; 15:1-14) Lakini baada ya Daudi kutubu dhambi yake ya kuua na kufanya uzinzi, Yehova alimsamehe na akapata tena kibali cha Mungu.

Hali zako zinaweza pia kubadilika. Matatizo ya kiafya, kiuchumi, au ya familia, hata matendo yetu wenyewe, yanaweza kubadili kabisa maisha yetu. Ni sifa gani ambazo zinaweza kutusaidia kukabiliana vizuri na hali hizo ngumu?

Unyenyekevu Unatusaidia

Unyenyekevu unatia ndani kuwa na mtazamo wa kujitiisha. Unyenyekevu wa kweli unatuwezesha kujua kabisa jinsi tulivyo na jinsi wengine walivyo. Tusipopuuza sifa nzuri za wengine na mambo mazuri wanayotimiza, tutawathamini zaidi na pia mambo wanayofanya. Vivyo hivyo, unyenyekevu unaweza kutusaidia kuelewa kwa nini tumepatwa na hali fulani na jinsi ya kuishughulikia.

Yonathani, mwana wa Sauli, ni mfano mzuri. Hali zake zilibadilika kwa sababu ya matukio ambayo hangeweza kuzuia. Samweli alipomwambia Sauli kwamba Yehova angeuchukua ufalme kutoka kwake, hakusema kwamba Yonathani angekuwa mfalme. (1 Sam. 15:28; 16:1, 12, 13) Mungu alimchagua Daudi awe mfalme wa Israeli baada ya Sauli, lakini hakumchagua Yonathani. Kwa njia fulani, kutotii kwa Sauli kulikuwa na matokeo mabaya kwa Yonathani. Hata ingawa hakuchangia makosa ya Sauli, Yonathani hangetawala baada ya baba yake. (1 Sam. 20:30, 31) Yonathani alikabiliana jinsi gani na hali hiyo? Je, alikuwa na kinyongo kwa sababu ya kupoteza nafasi ya kutawala, na kumwonea Daudi wivu? Hapana. Hata ingawa Yonathani alikuwa na umri mkubwa zaidi na uzoefu kuliko Daudi, alishikamana na Daudi. (1 Sam. 23:16-18) Unyenyekevu ulimsaidia Yonathani kuelewa ni nani aliyechaguliwa na Mungu, naye ‘hakujifikiria mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.’ (Rom. 12:3) Yonathani alijua mambo ambayo Yehova alimtazamia afanye na akakubali uamuzi wa Yehova.

Bila shaka, mara nyingi mabadiliko yanasababisha matatizo fulani. Pindi moja, Yonathani alishughulika na wanaume wawili ambao walikuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. Mmoja wao alikuwa Daudi, rafiki yake ambaye alichaguliwa na Yehova ili awe mfalme baada ya Sauli. Mwingine alikuwa Sauli, baba yake, ambaye alikuwa amekataliwa na Yehova lakini bado alikuwa akitawala akiwa mfalme. Bila shaka, hali hiyo ilimuumiza Yonathani hisia ambaye alikuwa akijitahidi kumpendeza Yehova. Huenda tukahangaika na kuwa na wasiwasi tunapokabiliana na mabadiliko katika maisha yetu. Lakini tukijitahidi kuelewa maoni ya Yehova, tutaendelea kumtumikia kwa ushikamanifu huku tukikabiliana na mabadiliko hayo.

Sifa ya Kiasi Ni ya Maana

Mtu mwenye kiasi anatambua mipaka yake. Hatupaswi kufikiri kwamba sifa ya kiasi ni sawa na sifa ya unyenyekevu. Mtu mnyenyekevu anaweza kukosa kutambua kikamili mipaka yake.

Daudi alikuwa mwenye kiasi. Ingawa Yehova alikuwa amemchagua kuwa mfalme, kwa miaka mingi Daudi hakuweza kuchukua utawala. Biblia haisemi kwamba Yehova alimweleza Daudi sababu ya kutompa ufalme haraka. Hata hivyo, Daudi hakuhangaishwa na hali hiyo, hata ingawa ilionekana kuwa yenye kuvunja moyo. Alitambua mipaka yake, na alielewa kwamba Yehova, ambaye aliruhusu hali hiyo itukie, alikuwa akiongoza mambo. Kwa hiyo, Daudi hangemuua Sauli, hata kama ni kwa sababu ya kuokoa uhai wake, na alimzuia mwandamani wake Abishai kufanya hivyo.—1 Sam. 26:6-9.

Nyakati nyingine, hali fulani inaweza kutokea katika kutaniko letu ambayo hatuelewi au ambayo kwa maoni yetu, haijashughulikiwa kwa njia bora au inayofaa zaidi. Je, tutakuwa wenye kiasi na kutambua kwamba Yesu ndiye Kichwa cha kutaniko na kwamba anatumia baraza la wazee waliowekwa rasmi kuongoza? Je, tutaonyesha sifa ya kiasi, huku tukitambua kwamba ili tuendelee kuwa na kibali cha Yehova tunahitaji kumngojea ili aongoze mambo kupitia Yesu Kristo? Je, tutakuwa wenye kiasi na kungojea hata ingawa si rahisi kufanya hivyo?—Met. 11:2.

Upole Unatusaidia Kuwa na Mtazamo Mzuri

Upole unamaanisha kutokasirika haraka. Upole unatusaidia kuvumilia kwa subira tunapokosewa na kuepuka kukasirika, kuwa na kinyongo, au kulipiza kisasi. Si rahisi kukuza sifa ya upole. Jambo la kupendeza ni kwamba katika andiko moja la Biblia, “wapole wa dunia” wanahimizwa ‘watafute upole.’ (Sef. 2:3) Sifa ya upole inahusiana na unyenyekevu na kiasi, lakini pia inatia ndani sifa nyingine, kama vile wema na wororo. Mtu mpole anaweza kukua kiroho kwa kuwa anakubali kufundishwa na kufinyangwa.

Upole unaweza kutusaidia namna gani kukabiliana na mabadiliko katika maisha yetu? Huenda umegundua kwamba watu wengi wana maoni mabaya kuhusu mabadiliko. Ukweli ni kwamba mabadiliko yanaweza kutupatia nafasi ya kuzoezwa na Yehova. Maisha ya Musa yanaonyesha hivyo.

Akiwa na umri wa miaka 40, tayari Musa alikuwa na sifa nzuri sana. Alikuwa ameonyesha kwamba anahangaikia mahitaji ya watu wa Mungu na alionyesha roho ya kujidhabihu. (Ebr. 11:24-26) Hata hivyo, kabla ya kutumwa na Yehova kuwaongoza Waisraeli kutoka Misri, Musa alikabili mabadiliko ambayo yaliboresha upole wake. Alilazimika kukimbia Misri na kuishi katika nchi ya Midiani kwa miaka 40, akiwa mchungaji, bila umaarufu wowote. Matokeo yalikuwa nini? Badiliko hilo lilimfanya kuwa mtu mzuri zaidi. (Hes. 12:3) Alijifunza kutanguliza mambo ya kiroho badala ya mambo yake mwenyewe.

Ili kuonyesha kwamba Musa alikuwa mpole, acheni tuchunguze mambo yaliyotukia wakati Yehova aliposema kwamba Alitaka kukataa taifa la Israeli lisilotii na kuruhusu wazao wa Musa wawe taifa lenye nguvu. (Hes. 14:11-20) Musa alimsihi Mungu asiliangamize taifa hilo. Maneno yake yanaonyesha kwamba hakutaka jina la Mungu lipate suto na pia alihangaikia hali nzuri ya ndugu zake, bali si yake mwenyewe. Daraka la kuwa kiongozi na mpatanishi wa taifa hilo lilihitaji mtu mpole kama Musa. Miriamu na Haruni walinung’unika kumhusu, lakini Biblia inasema kwamba Musa alikuwa “mpole zaidi kuliko watu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi.” (Hes. 12:1-3, 9-15) Inaonekana kwamba kwa upole Musa alivumilia matusi yao. Matokeo yangekuwa nini kama Musa hangekuwa mpole?

Pindi nyingine, roho ya Yehova ilishuka juu ya wanaume fulani, na kuwafanya watoe unabii. Yoshua, mtumishi wa Musa, aliona kwamba Waisraeli hao walikuwa wanatenda isivyofaa. Lakini Musa alionyesha upole na kuona mambo kulingana na maoni ya Yehova naye hakuogopa kupoteza mamlaka yake. (Hes. 11:26-29) Kama Musa hangekuwa mpole, je, angekubali badiliko hilo katika mpango wa Yehova?

Upole ulimwezesha Musa kutumia vizuri mamlaka yake makubwa na daraka ambalo Mungu alikuwa amempa. Yehova alimwambia apande Mlima Horebu na kusimama mbele ya watu. Mungu alizungumza na Musa kupitia malaika na kumweka rasmi kuwa mpatanishi wa agano hilo. Upole wa Musa ulimwezesha kukubali badiliko hilo kubwa la mamlaka na kuendelea kuwa na kibali cha Mungu.

Namna gani sisi? Ikiwa tunataka kukua kiroho, ni lazima tukuze sifa ya upole. Wote ambao wamepewa mapendeleo na madaraka kati ya watu wa Mungu wanahitaji kuwa wapole. Upole unatuzuia kuwa na kiburi tunapokabili mabadiliko na unatuwezesha kushughulikia hali mbalimbali kwa mtazamo unaofaa. Itikio letu ni la maana. Je, tutakubali mabadiliko hayo? Je, tutayaona kuwa nafasi ya kufanya maendeleo? Huenda ikawa nafasi ya pekee ya kukuza sifa ya upole!

Sikuzote tutakabili mabadiliko katika maisha yetu. Nyakati nyingine si rahisi kuelewa kwa nini mambo fulani yanatokea. Udhaifu na mahangaiko yetu yanaweza kufanya iwe vigumu kwetu kuendelea kuyaona mambo kama Yehova anavyoyaona. Hata hivyo, sifa kama vile unyenyekevu, kiasi, na upole zitatusaidia kukubali mabadiliko na kuendelea kuwa na kibali cha Mungu.

[Blabu katika ukurasa wa 4]

Unyenyekevu wa kweli unatuwezesha kujua kabisa jinsi tulivyo

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Ikiwa tunataka kukua kiroho, ni lazima tukuze sifa ya upole

[Picha katika ukurasa wa 5]

Musa alikabili hali ngumu ambazo ziliboresha upole wake