Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Marko ‘Mwenye Faida kwa Ajili ya Huduma’

Marko ‘Mwenye Faida kwa Ajili ya Huduma’

Marko ‘Mwenye Faida kwa Ajili ya Huduma’

KUTANIKO la Antiokia lilikuwa na matatizo fulani, lakini tatizo la kutoelewana kati ya mtume Paulo na Barnaba lilikuwa tofauti. Wanaume hao walikuwa wakipanga safari ya umishonari; hata hivyo, walipokuwa wakiamua mtu ambaye angesafiri pamoja nao, ‘kulitokea hasira kali’ kati yao. (Mdo. 15:39) Walitengana na kila mmoja akaenda njia yake. Waligombana kwa sababu ya mmishonari wa tatu aliyeitwa Marko.

Marko alikuwa nani? Kwa nini mitume hao wawili waligombana kwa sababu yake? Kwa nini kila mmoja wao alishikilia maoni yake? Je, walibadili maoni hayo? Na unaweza kujifunza nini kutokana na masimulizi kumhusu Marko?

Nyumbani Huko Yerusalemu

Marko, ambaye inaonekana kwamba alitoka katika familia tajiri ya Kiyahudi, alilelewa Yerusalemu. Tunapata habari zake kwa mara ya kwanza kutokana na historia ya kutaniko la mapema la Kikristo. Karibu mwaka wa 44 W.K. malaika wa Yehova alipomweka huru kimuujiza mtume Petro kutoka katika gereza la Herode Agripa wa Kwanza, Petro alienda “kwenye nyumba ya Maria mama ya Yohana aliyeitwa Marko, ambamo watu wengi walikuwa wamekusanyika na wakisali.”—Mdo. 12:1-12. *

Basi, inaonekana kwamba kutaniko la Yerusalemu lilifanyia mikutano katika nyumba ya mama ya Marko. Inaonekana kwamba nyumba hiyo ilikuwa kubwa kwa sababu “watu wengi” walikusanyika humo. Maria alikuwa na msichana wa kazi aliyeitwa Roda ambaye alifungua mlango wakati Petro alipopiga hodi “kwenye mlango wa njia ya lango.” Maelezo hayo yanaonyesha kwamba Maria alikuwa mwanamke tajiri kwa kadiri fulani. Na nyumba hiyo inaitwa nyumba ya Maria bali si ya mume wake, kwa hiyo inawezekana kwamba alikuwa mjane na Marko alikuwa mtoto wakati huo.—Mdo. 12:13.

Inaelekea kwamba Marko alikuwa kati ya watu waliokusanyika kwa ajili sala. Ni wazi kwamba aliwafahamu vizuri wanafunzi wa Yesu na watu wengine waliokuwa wameshuhudia mambo yaliyotukia katika huduma ya Yesu. Kwa kweli, huenda Marko ndiye kijana aliyekuwa amevaa vazi la kitani bora ambaye alijaribu kumfuata Yesu alipokamatwa mara ya kwanza na kukimbia walipojaribu kumshika.—Marko 14:51, 52.

Mapendeleo Katika Kutaniko

Bila shaka, kushirikiana na Wakristo wakomavu kulikuwa na uvutano mzuri juu ya Marko. Alifanya maendeleo ya kiroho ambayo yalionwa na ndugu wenye madaraka. Karibu mwaka wa 46 W.K. Paulo na Barnaba walipopeleka “huduma ya misaada” huko Yerusalemu kutoka Antiokia ili kukabiliana na njaa, walipendezwa na Marko. Paulo na Barnaba waliporudi Antiokia, walimchukua Marko na wakasafiri pamoja naye.—Mdo. 11:27-30; 12:25.

Mtu asiposoma masimulizi hayo kwa uangalifu anaweza kufikiri kwamba watu hao watatu walikuwa tu na uhusiano wa kiroho. Pia, anaweza kufikiri kwamba Paulo na Barnaba walimchagua Marko kwa sababu tu ya uwezo wake. Lakini barua moja ya Paulo inafunua kwamba Marko alikuwa binamu ya Barnaba. (Kol. 4:10) Hilo linaweza kutusaidia kuelewa matukio mengine yaliyofuata ambayo yalimhusisha Marko.

Baada ya mwaka mmoja hivi kupita, roho takatifu ilielekeza kwamba Paulo na Barnaba waende safari ya umishonari. Walitoka Antiokia na kuelekea Kipro. Yohana Marko alisafiri pamoja nao “akiwatumikia.” (Mdo. 13:2-5) Labda Marko alishughulikia mahitaji yao wakati wa safari ili mitume hao wakazie fikira mambo ya kiroho.

Paulo, Barnaba, na Marko walisafiri katika nchi yote ya Kipro, wakihubiri njiani; kisha wakaenda Asia Ndogo. Wakiwa huko, Yohana Marko alifanya uamuzi ambao ulimkasirisha Paulo. Masimulizi hayo yanasema kwamba walipofika Perga, “Yohana akawaacha na kurudi Yerusalemu.” (Mdo. 13:13) Biblia haisemi kwa nini alifanya hivyo.

Miaka michache baadaye, Paulo, Barnaba, na Marko walirudi Antiokia. Mitume hao wawili walikuwa wakipanga safari ya pili ya umishonari ya kuwatia moyo watu waliowahubiria katika safari yao ya kwanza. Barnaba alitaka kumchukua binamu yake, lakini Paulo alikataa kabisa kwa sababu Marko aliwaacha katika safari ya kwanza. Jambo hilo lilisababisha ugomvi ambao unatajwa mwanzoni mwa habari hii. Barnaba aliyekuwa mzaliwa wa Kipro alimchukua Marko na kwenda kuhubiri huko, naye Paulo akaenda Siria. (Mdo. 15:36-41) Ni wazi kwamba Paulo na Barnaba walikuwa na maoni tofauti kuhusu uamuzi ambao Marko alikuwa amefanya mapema.

Walipatana

Bila shaka, jambo hilo lilimhuzunisha sana Marko. Hata hivyo, aliendelea kuwa mhudumu mwaminifu. Miaka 11 au 12 hivi baada ya kukosana na Paulo, Marko anatajwa tena katika utendaji wa Wakristo wa mapema. Akiwa na nani? Akiwa na mtu ambaye hungetazamia kamwe, Paulo!

Katika mwaka wa 60-61 W.K., Paulo alipokuwa gerezani huko Roma, alituma barua fulani ambazo sasa ni sehemu ya Maandiko Matakatifu. Katika barua kwa Wakolosai, aliandika hivi: “Aristarko mateka mwenzangu anawatumia ninyi salamu zake, na pia Marko binamu ya Barnaba, (ambaye mlipokea amri kumhusu yeye ili mkamkaribishe ikiwa atakuja kwenu) . . . Ni hawa tu walio wafanyakazi wenzangu kwa ajili ya ufalme wa Mungu, na hawa ndio wamekuwa msaada wenye kunitia nguvu.”—Kol. 4:10, 11.

Hilo lilikuwa badiliko kubwa kama nini! Mwanzoni Marko alimkasirisha sana Paulo, lakini sasa Paulo alimthamini sana akiwa mfanyakazi mwenzake. Inaonekana Paulo aliwajulisha Wakolosai kwamba huenda Marko angewatembelea. Ikiwa Marko angewatembelea, angekuwa mwakilishi wa Paulo.

Je, inawezekana kwamba Paulo alimchambua Marko kupita kiasi miaka iliyotangulia? Je, Marko alifaidika na nidhamu aliyopata? Au labda mambo hayo mawili yalihusika? Vyovyote vile, Paulo na Marko walionyesha kwamba walikuwa wakomavu kwa sababu walipatana tena. Walisahau jambo lililotukia kati yao zamani nao wakatumika tena pamoja. Ni mfano mzuri kama nini kwa mtu yeyote ambaye amekosana na Mkristo mwenzake!

Marko Alisafiri Sana

Ukisoma kuhusu safari mbalimbali za Marko, utatambua kwamba alisafiri sana. Alitoka Yerusalemu, akahamia Antiokia, kisha akasafiri kwa mashua mpaka Kipro na Perga. Halafu akaenda Roma. Akiwa huko, Paulo alitaka kumtuma Kolosai. Alisafiri sehemu nyingine nyingi!

Mtume Petro aliandika barua yake ya kwanza kati ya mwaka wa 62 na 64 W.K. Aliandika hivi: “Mwanamke aliye katika Babiloni . . . anawatumia ninyi salamu zake, na vilevile Marko mwanangu.” (1 Pet. 5:13) Kwa hiyo, Marko alisafiri mpaka Babiloni ili kutumika pamoja na mtume Petro ambaye miaka iliyotangulia alihudhuria mikutano ya Kikristo katika nyumba ya mama ya Marko.

Paulo alipofungwa gerezani kwa mara ya pili huko Roma karibu mwaka wa 65 W.K., alimwandikia Timotheo huko Efeso na kuongezea hivi: “Umchukue Marko na uje pamoja naye.” (2 Tim. 4:11) Kwa hiyo, wakati huo Marko alikuwa Efeso. Hatuna shaka yoyote kwamba alikubali ombi la Paulo la kurudi Roma pamoja na Timotheo. Safari zilikuwa ngumu wakati huo, lakini Marko alifunga safari hizo kwa kupenda.

Pendeleo Lingine Kubwa

Marko alipata pendeleo lingine kubwa la kuongozwa na roho ya Yehova kuandika kitabu kimoja cha Injili. Ingawa kitabu cha pili cha Injili hakimtaji mwandikaji, mapokeo ya zamani yanadai kwamba Marko ndiye aliyeandika kitabu hicho na alipata habari kutoka kwa Petro. Kwa kweli, Petro alishuhudia karibu kila jambo ambalo Marko aliandika.

Wachunguzi wa Injili ya Marko wanaamini kwamba Marko aliandika kitabu hicho kwa ajili ya wasomaji wasio Wayahudi kwa kuwa alitaja maelezo ya maana sana kuhusu mazoea ya Kiyahudi. (Marko 7:3; 14:12; 15:42) Marko anatafsiri maneno ya Kiaramu ambayo huenda watu wasio Wayahudi hawangeweza kuelewa. (Marko 3:17; 5:41; 7:11, 34; 15:22, 34) Anatumia maneno mengi ya Kilatini na hata anaeleza maneno ya kawaida ya Kigiriki kwa kutumia Kilatini. Anataja thamani ya sarafu za Wayahudi kwa kutumia thamani ya pesa za Kiroma. (Marko 12:42) Inaonekana mambo hayo yote yanapatana na mapokeo ambayo yamekuwapo kwa muda mrefu ya kwamba Marko aliandika Injili yake huko Roma.

“Mwenye Faida Kwangu kwa Ajili ya Huduma”

Zaidi ya kuandika Injili yake, Marko alifanya mambo mengine huko Roma. Kumbuka maneno ambayo Paulo alimwambia Timotheo: “Umchukue Marko na uje pamoja naye.” Kwa nini Paulo alisema hivyo? “Kwa maana yeye ni mwenye faida kwangu kwa ajili ya huduma.”—2 Tim. 4:11.

Uhakika wa kwamba Marko anatajwa katika vitabu vya Maandiko vilivyoandikwa mwisho unafunua mengi kumhusu. Katika masimulizi yote kuhusu utendaji wake kutanikoni, Marko hatajwi popote kuwa mtume, kiongozi, au nabii. Alikuwa mhudumu, yaani, aliwahudumia na kuwatumikia wengine. Na muda mfupi kabla ya kifo cha Paulo, bila shaka Marko alimsaidia sana mtume huyo.

Tunapochunguza habari mbalimbali ambazo tunazo kumhusu Marko tunajifunza kwamba alikuwa mwanamume mwenye bidii katika kutangaza habari njema katika maeneo mbalimbali ya ulimwengu, naye alifurahia kuwatumikia wengine. Kwa kweli, Marko alipata mapendeleo yenye kuthawabisha sana kwa sababu ya kutovunjika moyo!

Leo, tukiwa watumishi wa Mungu tumeazimia kama Marko kutangaza habari njema ya Ufalme. Wengine wetu wanaweza kuhamia maeneo mengine, hata nchi za mbali, ili kutangaza habari njema huko kama Marko alivyofanya. Ingawa wengi wetu hawawezi kuhama, sote tunaweza kumwiga Marko katika njia nyingine ya maana. Kama Marko alivyojitolea kabisa kuwahudumia ndugu zake Wakristo, sisi pia tuko tayari kujitolea kabisa kuwasaidia waamini wenzetu katika njia zinazofaa ili waendelee kumtumikia Mungu. Tunapofanya hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba tutaendelea kupata baraka za Yehova.—Met. 3:27; 10:22; Gal. 6:2.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Katika siku za Marko ilikuwa kawaida kwa watu kukubali au kuwa na jina la pili la Kiebrania au la kigeni. Jina la Kiyahudi la Marko lilikuwa Yohanan, yaani, Yohana katika Kiswahili. Jina lake la Kilatini lilikuwa Marcus, au Marko.—Mdo. 12:25.

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 8, 9]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Majiji Fulani Ambayo Marko Alitembelea

Roma

Efeso

Kolosai

Perga

Antiokia (ya Siria)

Kipro

BAHARI YA MEDITERANIA

Yerusalemu

Babiloni