Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Ambayo Yesu Alifundisha Kumhusu Mungu

Mambo Ambayo Yesu Alifundisha Kumhusu Mungu

Mambo Ambayo Yesu Alifundisha Kumhusu Mungu

‘Hakuna amjuaye Baba ila Mwana, na yeyote yule ambaye Mwana atapenda kumfunulia.’—LUKA 10:22, BIBLIA HABARI NJEMA.

ALIPOISHI mbinguni kabla ya kuja duniani, Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu alikuwa na uhusiano wa karibu na Baba yake kwa muda mrefu sana. (Wakolosai 1:15) Kwa hiyo, Mwana huyo alipata kuelewa mawazo, hisia, na njia za Baba yake. Baadaye, Mwana huyo alipokuja duniani kama mwanadamu na kuitwa Yesu, alikuwa na hamu ya kufundisha ukweli kumhusu Baba yake. Tunaweza kujifunza mengi kumhusu Mungu kwa kusikiliza mambo ambayo Mwana huyu alisema.

Jina la Mungu Yesu aliliona jina la Mungu, Yehova, kuwa muhimu sana. Mwana huyo mpendwa alitaka wengine walijue jina la Baba yake na kulitumia. Jina la Yesu linamaanisha “Yehova ni Wokovu.” Usiku uliotangulia kifo chake, Yesu alisali hivi kwa Yehova: “Nimewajulisha jina lako.” (Yohana 17:26) Haishangazi kwamba Yesu alilitumia jina la Mungu na kuwaeleza wengine kulihusu. Wasikilizaji wake hawangeweza kuelewa ukweli kumhusu Yehova kama hawangejua jina Lake na maana ya jina hilo. *

Upendo mkuu wa Mungu Yesu alisema hivi aliposali: “Baba, . . . ulinipenda kabla ya kuwekwa kwa msingi wa ulimwengu.” (Yohana 17:24) Yesu alikuwa amejionea upendo wa Mungu mbinguni, kwa hiyo, alipokuwa duniani alitaka watu wajue jinsi Mungu anavyoonyesha upendo huo kwa njia nyingi mbalimbali.

Yesu alionyesha kwamba watu wengi sana wanaweza kunufaika na upendo wa Yehova. Yesu alisema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Katika andiko hili, neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa “ulimwengu” halimaanishi “dunia.” Katika muktadha huu, neno hili linarejelea wanadamu, kwa kweli, wanadamu wote. Upendo wa Mungu ni mwingi sana hivi kwamba alimtoa Mwana wake mpendwa ili wanadamu waaminifu waweze kuwekwa huru kutokana na dhambi na kifo, na hivyo, wawe na tumaini la kuishi milele. Hatuwezi kuelewa kabisa kina cha upendo wa Mungu.—Waroma 8:38, 39.

Yesu alikazia ukweli mmoja unaotia moyo sana: Yehova anampenda sana kila mmoja wa waabudu wake. Yesu alifundisha kwamba Yehova ni kama mchungaji anayemjua na kumpenda kila kondoo katika kundi lake. (Mathayo 18:12-14) Yesu alisema kwamba hata shomoro mmoja hawezi kuanguka chini bila Yehova kujua. Yesu aliongeza hivi: “Nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote.” (Mathayo 10:29-31) Iwapo Yehova ana uwezo wa kujua kama shomoro mmoja ameanguka kutoka katika kiota chake, ni wazi kwamba anamwona na kumjali hata zaidi kila mtu anayemwabudu. Iwapo Yehova anajua na anaweza kuhesabu kila unywele kichwani mwako, basi, je, kuna mambo yoyote kutuhusu, kama vile mahitaji yetu, matatizo yetu, au mahangaiko yetu, ambayo hajui?

Baba wa mbinguni Kama habari zilizotangulia zinavyoonyesha, Yesu ni Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu. Si ajabu basi, mara nyingi Mwana huyo mpendwa alimrejelea na kumwita Yehova, “Baba.” Alipokuwa hekaluni akiwa na miaka 12, Yesu alimwita Yehova, “Baba yangu.” Hayo ni kati ya maneno ya kwanza ya Yesu yanayotajwa katika Biblia. (Luka 2:49) Neno “Baba” linatajwa mara 190 hivi katika vitabu vya Injili. Yesu alimwita Yehova “Baba yenu,” “Baba yetu,” na “Baba yangu.” (Mathayo 5:16; 6:9; 7:21) Kwa kumwita Yehova “Baba” mara nyingi hivyo, Yesu alionyesha kwamba wanadamu wenye dhambi na wasio wakamilifu wanaweza kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova.

Mwenye rehema na tayari kusamehe Yesu alijua kwamba watu wasio wakamilifu wanahitaji sana rehema ya Yehova. Katika mfano wake kumhusu mwana mpotevu, Yesu alimlinganisha Yehova na baba mwenye rehema ambaye yu tayari kumsamehe mwana wake mwenye kutubu. (Luka 15:11-32) Maneno ya Yesu yanatuhakikishia kwamba Yehova anatafuta mabadiliko yoyote katika mioyo ya wanadamu wenye dhambi ili awe na msingi wa kuwaonyesha rehema. Yehova ana hamu sana ya kumsamehe mtenda dhambi anayetubu. Yesu alieleza: “Ninawaambia ninyi kwamba ndivyo kutakavyokuwa na shangwe zaidi mbinguni juu ya mtenda-dhambi mmoja anayetubu kuliko juu ya waadilifu 99 ambao hawahitaji kutubu.” (Luka 15:7) Bila shaka, tunataka kumkaribia Mungu huyu mwenye rehema!

Msikiaji wa sala Alipokuwa mbinguni kabla ya kuja duniani, Yesu alijionea mwenyewe kwamba Yehova ni “msikiaji wa sala” na kuwa anafurahia kusikia sala za watumishi wake waaminifu. (Zaburi 65:2) Kwa hiyo, wakati wa huduma yake, Yesu aliwafundisha wasikilizaji wake jinsi ya kusali na mambo yanayofaa kutajwa katika sala. Alitoa shauri hili: “Msiseme mambo yaleyale tena na tena.” Aliwahimiza wasikilizaji wake waombe mapenzi ya Mungu “yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” Tunaweza pia kuomba tupate chakula cha kila siku, msamaha wa dhambi, na nguvu za kusimama imara tunaposhawishiwa. (Mathayo 6:5-13) Yesu alifundisha kwamba Yehova anajibu sala za watumishi Wake wanaosali kwa imani, kama ambavyo baba angemjibu mtoto wake.—Mathayo 7:7-11.

Yesu alijitahidi kuwafundisha watu ukweli kumhusu Yehova na sifa zake. Lakini kulikuwa na jambo lingine ambalo Yesu alitaka kufundisha kumhusu Yehova—jinsi ambavyo Yehova ataleta mabadiliko ulimwenguni pote ili atimize kusudi Lake kuhusu dunia na wanadamu. Hiyo ndiyo habari kuu katika mahubiri ya Yesu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Jina Yehova linapatikana mara 7,000 hivi katika hati za awali za Biblia. Maana ya jina hilo ni, “nitakuwa kile nitakachokuwa.” (Kutoka 3:14) Mungu anaweza kuwa chochote anachotaka ili kutimiza kusudi lake. Jina hilo ni hakikisho kwamba siku zote Mungu atatenda kupatana na kusudi lake na kwamba atatimiza ahadi zake zote.