Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yesu Kristo—Ujumbe Wake Unavyokuhusu

Yesu Kristo—Ujumbe Wake Unavyokuhusu

Yesu Kristo—Ujumbe Wake Unavyokuhusu

“Nimekuja ili wapate kuwa na uzima na wapate kuwa nao kwa wingi.”—YOHANA 10:10.

YESU KRISTO alikuja duniani ili kutoa wala si kupokea. Katika huduma yake, aliwapa wanadamu zawadi yenye thamani kubwa, yaani, ujumbe unaofunua ukweli kumhusu Mungu na mapenzi Yake. Kama maisha ya mamilioni ya Wakristo wa kweli yanavyoonyesha, watu wanaokubali ujumbe huu wanaweza kuwa na maisha bora leo. * Hata hivyo, ujumbe wa Yesu unategemea dhabihu ya uhai mkamilifu ambayo ni zawadi yenye thamani sana kutoka kwake. Wakati wetu ujao unategemea jinsi tunavyochagua kutenda kuhusiana na sehemu hii muhimu ya ujumbe wake.

Mungu na Kristo walitoa nini? Yesu alijua kwamba adui zake wangemtesa sana na kumuua. (Mathayo 20:17-19) Hata hivyo, katika Yohana 3:16, alisema maneno haya maarufu: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” Pia, Yesu alisema kwamba alikuja “kutoa nafsi yake [au, uhai wake] kuwa fidia badala ya wengi.” (Mathayo 20:28) Kwa nini alisema kwamba angetoa uhai wake badala ya kusema kwamba angeuawa?

Kwa upendo usio na kifani, Mungu alifanya mpango ili kuwaweka wanadamu huru kutokana na dhambi waliyorithi, na matokeo yake ya kutokamilika na kifo. Mungu alifanya hivyo kwa kumtuma duniani Mwana wake mzaliwa-pekee ili atoe uhai wake kama dhabihu. Yesu alikubali kwa hiari kutoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kwa ajili yetu. Huo ndio mpango wa fidia au dhabihu ya ukombozi, nayo ndiyo zawadi kubwa zaidi kutoka kwa Mungu. * Zawadi hiyo inawawezesha wanadamu kupata uzima wa milele.

Unahitaji kufanya nini? Je, fidia ni zawadi kwako binafsi? Hilo linategemea wewe. Wazia kwamba mtu anataka kukupa zawadi iliyofungwa vizuri kwa karatasi maridadi. Zawadi hiyo haitakuwa yako usipoichukua na kuikubali. Vivyo hivyo, Yehova anataka kukupa wewe zawadi ya fidia, lakini usipoichukua na kuikubali haiwezi kuwa yako. Unaweza kuichukua na kuikubali zawadi hiyo jinsi gani?

Yesu alisema kwamba ni wale tu “wanaomwamini” ambao watapata uzima wa milele. Imani inahusisha matendo yako maishani. (Yakobo 2:26) Kumwamini Yesu kunamaanisha kuishi kupatana na mambo aliyofundisha na kufanya. Ili kufanya hivyo ni lazima umjue Yesu na Baba yake vizuri. Yesu alisema hivi: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.

Miaka 2,000 hivi iliyopita, Yesu Kristo alihubiri ujumbe ambao umebadili maisha ya mamilioni ya watu duniani kote. Je, ungependa kujua ujumbe huo vizuri zaidi na jinsi wewe na wapendwa wako mnavyoweza kunufaika kutokana nao, leo na hata milele? Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia.

Makala zinazofuata zinazungumzia mambo mengine mengi kumhusu Yesu Kristo, mtu ambaye alihubiri ujumbe unaoweza kubadili maisha yako kabisa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Si kila mtu anayejidai kuwa Mkristo, ambaye ni mfuasi wa kweli wa Kristo. Wafuasi wa kweli wa Yesu wanaishi kupatana na kweli ambazo alifundisha kumhusu Mungu na mapenzi Yake.—Mathayo 7:21-23.

^ fu. 5 Ili kupata habari zaidi kuhusu fundisho la Biblia juu ya fidia, ona sura ya 5, “Fidia—Zawadi Bora Zaidi Kutoka kwa Mungu,” ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.