Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni Mafundisho ya Uwongo Au ya Kweli?—Ukweli Kumhusu Yesu

Je, Ni Mafundisho ya Uwongo Au ya Kweli?—Ukweli Kumhusu Yesu

Je, Ni Mafundisho ya Uwongo Au ya Kweli?—Ukweli Kumhusu Yesu

MAONI YAKO NI NINI? HABARI ZIFUATAZO NI ZA KWELI AU NI ZA UWONGO?

Yesu alizaliwa Desemba 25.

Mamajusi watatu walimtembelea Yesu baada tu ya kuzaliwa kwake.

Yesu hakuwa na ndugu wala dada.

Yesu alikuwa Mungu katika mwili wa binadamu.

Yesu hakuwa mtu mwema tu.

WATU wengi wangesema kwamba habari hizi zote ni za kweli. Huenda wengine wangesema kwamba ni vigumu na hata haiwezekani kujua ukweli wa mambo. Labda wanafikiri kwamba mradi tu mtu anamwamini Yesu, si lazima ajue majibu ya maswali hayo.

Hata hivyo, Biblia inatutia moyo tuwe “na ujuzi sahihi juu ya Bwana wetu Yesu Kristo.” (2 Petro 1:8) Tunaweza kupata ujuzi huo kwa kuchunguza vitabu vya Injili. Vinafunua ukweli kumhusu Yesu, na hivyo kutusaidia kutofautisha ukweli na uwongo. Kwa hiyo, acheni tuone yale ambayo vitabu vya Injili vinaonyesha kuhusu mafundisho yaliyo juu.

FUNDISHO: Yesu alizaliwa Desemba 25.

NI UWONGO.

Biblia haitaji mwezi wala siku ambayo Yesu alizaliwa. Hivyo basi, tarehe ya Desemba 25 ilitoka wapi? Kitabu kimoja cha marejeo (The Encyclopædia Britannica) kinasema kwamba watu fulani waliojiita Wakristo “walitaka tarehe hiyo ilingane na sherehe ya kipagani ya Waroma ya kuadhimisha . . . siku ambapo mchana unaanza kuwa mrefu na jua linaanza kupaa juu zaidi angani.” Kitabu hicho kinasema pia kwamba desturi nyingi za Krismasi zilitokana na “sherehe za kipagani zilizohusu ukulima na ibada ya jua katikati ya majira ya baridi kali.”

Je, Yesu angekubali watu washerehekee kuzaliwa kwake siku ya Desemba 25? Fikiria hili: Siku ambayo Yesu alizaliwa haijulikani. Biblia haitoi maagizo yoyote kwamba tunapaswa kusherehekea kuzaliwa kwa Yesu, wala hakuna uthibitisho wowote kwamba Wakristo wa mapema walifanya hivyo. Kinyume cha hilo, Biblia inataja siku hususa ambayo Yesu alikufa, naye aliwaamuru wafuasi wake waikumbuke siku hiyo. * (Luka 22:19) Basi ni wazi kwamba Yesu alitaka watu wazingatie zaidi umuhimu wa kifo chake cha kidhabihu wala si kuzaliwa kwake.—Mathayo 20:28.

FUNDISHO: Mamajusi watatu (au wafalme watatu kulingana na mafundisho fulani) walimtembelea Yesu baada tu ya kuzaliwa kwake.

NI UWONGO.

Labda umeona michoro au mandhari inayoonyesha kitoto Yesu kikiwa kimelazwa kwenye hori huku kimezungukwa na mamajusi watatu walioleta zawadi. Hata hivyo, hiyo ni mandhari ya kubuniwa tu, si ya kweli.

Ni kweli kwamba watu fulani kutoka Mashariki walimtembelea mtoto Yesu. Hata hivyo, watu hao waliomtembelea walikuwa wanajimu, au wataalamu wa nyota. (Mathayo 2:1, Biblia Habari Njema) Je, walimpata Yesu akiwa amelazwa horini? Hapana; walimtembelea ndani ya nyumba. Yaelekea walifika miezi kadhaa baada ya Yesu kuzaliwa.—Mathayo 2:9-11.

Yesu alitembelewa na watu wangapi? Je, walikuwa 2, 3, au 30? Biblia haisemi. Huenda wengi wanaamini kwamba ni watatu kwa sababu Biblia inataja aina tatu za zawadi. * (Mathayo 2:11) Hata watu fulani wamedokeza kwamba kila moja ya zawadi hizo inawakilisha jamii tofauti ya wanadamu. Lakini wazo hilo halipatikani katika Biblia. Badala yake, kitabu kimoja kinachofafanua vitabu vya Injili kinasema kwamba wazo hilo lilibuniwa na “mwanahistoria mbunifu sana wa karne ya nane.”

FUNDISHO: Yesu hakuwa na ndugu wala dada.

NI UWONGO.

Vitabu vya Injili vinaonyesha wazi kwamba Yesu alikuwa na ndugu na dada. Injili ya Luka inamwita Yesu “mzaliwa wa kwanza” wa Maria, kuonyesha kwamba alizaa watoto wengine baadaye. * (Luka 2:7) Injili ya Marko inataja kwamba watu fulani katika jiji la Nazareti walimwona Yesu kuwa mtu wa kawaida tu, aliyekuwa sawa na ndugu na dada zake. Waliuliza hivi: “Je, Yakobo, Yosefu, Yuda na Simoni si ndugu zake? Je, si dada zake wanaishi hapa katika mji wetu?”—Marko 6:3, Contemporary English Version; Mathayo 12:46; Yohana 7:5.

Tofauti na yale ambayo vitabu vya Injili vinasema, wanatheolojia wengi wanadai kwamba Yesu alikuwa mzaliwa wa pekee wa Maria. Baadhi yao wanasema kwamba ndugu na dada za Yesu wanaotajwa katika Biblia ni binamu zake. * Wengine hufikiri kwamba ndugu na dada hao wa Yesu ni watoto wa kambo wa Maria. Lakini fikiri hili: Ikiwa Yesu hakuwa na ndugu au dada, je, watu hao wa Nazareti wangesema maneno waliyosema? Kinyume chake, yaelekea baadhi yao walimwona Maria alipokuwa na mimba za watoto wale wengine. Walijionea kwa macho yao kwamba Yesu alikuwa mmoja kati ya watoto wengi ambao Maria alizaa.

FUNDISHO: Yesu alikuwa Mungu katika mwili wa binadamu.

NI UWONGO.

Wazo kwamba Mungu alikuja duniani na kuishi kama mwanadamu Yesu, limekuwako kwa muda mrefu, na ndilo msingi wa fundisho la Utatu. Hata hivyo, fundisho hilo halikuwapo wakati wa Yesu, kama vile tu kitabu kimoja cha marejeo (The Encyclopædia Britannica) kinavyosema: “Neno Utatu, wala fundisho la wazi kama hilo, halionekani katika Agano Jipya . . . Fundisho hilo lilisitawishwa hatua kwa hatua kwa muda wa karne kadhaa na kwa mabishano mengi.”

Kwa kweli, dini zinamshushia Yesu heshima kwa kufundisha kwamba yeye ni Mungu katika mwili wa binadamu. * Kwa njia gani? Fikiria mfano huu. Wafanyakazi fulani wanamwomba msimamizi wao awafanyie jambo fulani, lakini msimamizi huyo anasema hana mamlaka ya kufanya hivyo. Ikiwa msimamizi huyo anasema kweli, anaonyesha kwa hekima kwamba anatambua mipaka yake. Lakini kama ana uwezo na anakataa kuwasaidia wafanyakazi hao, yeye ni mdanganyifu.

Yesu alifanya nini wakati wawili kati ya mitume wake walipojitakia vyeo vya umashuhuri? Aliwaambia: “Kuketi upande wangu wa kuume na upande wangu wa kushoto sina haki ya kutoa, bali wataketi wale ambao Baba yangu amewatayarishia.” (Mathayo 20:23) Ikiwa kwa kweli Yesu alikuwa Mungu, je, si angekuwa amesema uwongo? Badala ya hivyo, kwa kumrejelea Yule aliye na mamlaka zaidi, Yesu alituwekea mfano bora wa kuwa wenye kiasi na akaonyesha kwamba yeye si sawa na Mungu.

FUNDISHO: Yesu hakuwa mtu mwema tu.

NI KWELI.

Yesu alisema waziwazi kwamba hakuwa mtu mwema tu. Alisema: “Mimi ni Mwana wa Mungu.” (Yohana 10:36) Bila shaka, mtu yeyote anaweza kudai kuwa Mwana wa Mungu. Lakini kama madai hayo ya Yesu si ya kweli, basi yeye si mtu mwema bali mdanganyifu mkubwa!

Ushuhuda wenye kutegemeka zaidi kwamba Yesu alikuwa Mwana wa Mungu ulitoka kwa Mungu mwenyewe. Yehova alisema hivi mara mbili kumhusu Yesu: “Huyu ni Mwanangu.” (Mathayo 3:17; 17:5) Ebu fikiria hili: Kuna visa vichache tu katika Biblia ambapo sauti ya Mungu ilisikika duniani—na viwili kati ya hivyo ni wakati Yehova alipothibitisha kwamba Yesu ni Mwana wake! Huo ndio uthibitisho bora kabisa kwamba Yesu alikuwa Mwana wa Mungu kama alivyosema.

Je, umejifunza mambo yoyote kumhusu Yesu ambayo hukujua hapo awali? Ikiwa ndivyo, unaweza kuchunguza zaidi vitabu vya Injili vilivyoandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu. Uchunguzi huo unaweza kuwa wenye kufurahisha na kunufaisha. Hata Yesu mwenyewe alisema kwamba kujifunza kweli kumhusu yeye na Baba yake kunamaanisha “uzima wa milele.”—Yohana 17:3.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Yesu alikufa Siku ya Pasaka, au Nisani 14, kulingana na kalenda ya Wayahudi.—Mathayo 26:2.

^ fu. 18 Mathayo anasema kwamba wageni hao “wakafungua hazina zao” na kumtolea dhahabu, ubani, na manemane. Hata hivyo, huenda familia ya Yesu—ambayo haikuwa tajiri—ilipata zawadi hizo zenye thamani kubwa wakati unaofaa kwa sababu ililazimika kukimbia nchi yao muda mfupi baadaye.—Mathayo 2:11-15.

^ fu. 21 Ingawa Maria alichukua mimba ya Yesu kimuujiza, alichukua mimba za watoto wale wengine kwa njia ya kawaida kupitia mume wake Yosefu.—Mathayo 1:25.

^ fu. 22 Wazo hili lililoungwa mkono na Jerome yapata mwaka wa 383 W.K. linapendwa na watu wengi wanaoamini kwamba Maria alibaki bikira maisha yake yote. Ingawa baadaye Jerome alitilia shaka wazo hili, watu wengi bado wanaliamini. Huo pia ndio msimamo wa Kanisa Katoliki.

^ fu. 26 Kwa habari zaidi kuhusu fundisho la Utatu, ona broshua Je! Uamini Utatu? iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 14]

Mambo Mengine Yanayoweza Kukushangaza Kumhusu Yesu

Yesu alikuwa mtu wa aina gani? Je, alikuwa mtu mwenye kujinyima raha, mgumu na mwenye kujitenga na watu hivi kwamba hangeweza kuwa na urafiki na watu wa kawaida? Huenda wengine wakafikiri hivyo. Labda hiyo ndiyo sababu inayofanya washangae kujua kwamba Yesu . . .

• alijiunga na wengine wakati wa matukio yenye shangwe.—Yohana 2:1-11.

• aliwapongeza wengine.—Marko 14:6-9.

• alifurahia kuwa pamoja na watoto.—Marko 10:13, 14.

• alilia hadharani.—Yohana 11:35.

• aliwahurumia watu.—Marko 1:40, 41.