Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Ufalme Wako Hakika Utakuwa Imara’

‘Ufalme Wako Hakika Utakuwa Imara’

Mkaribie Mungu

‘Ufalme Wako Hakika Utakuwa Imara’

2 Samweli 7:1-16

TANGU zamani, watawala wa kibinadamu wamekuwa wakiondolewa mamlakani. Baadhi yao wameondolewa kupitia upigaji wa kura, huku wengine wakiondolewa kwa nguvu. Namna gani Yesu Kristo, Mfalme wa Ufalme wa mbinguni wa Mungu? Je, kuna chochote kinachoweza kumzuia asitawale akiwa Mfalme aliyewekwa na Mungu? Tunapata jibu katika maneno ya Yehova kwa Mfalme Daudi wa Israeli la kale, yaliyo katika 2 Samweli sura ya 7.

Katika mistari ya kwanza ya sura hiyo, tunasoma kwamba Daudi anaona aibu, kwa kuwa, yeye ni mfalme wa kibinadamu tu, lakini anaishi katika jumba maridadi la kifalme, huku sanduku la Mungu likikaa katika hema. * Daudi anasema angependa kumjengea Yehova nyumba, au hekalu zuri. (Mstari wa 2) Lakini si Daudi atakayejenga nyumba hiyo. Kupitia nabii Nathani, Yehova anamwambia Daudi kwamba mwana wake ndiye atakayejenga hekalu hilo.—Mistari 4, 5, 12, 13.

Yehova anapendezwa na tamaa ya Daudi ya moyoni. Kwa hiyo, kupatana na unabii, na pia kwa sababu ya kujitolea kwa Daudi, Mungu anafanya agano naye kwamba atainua mtu fulani katika ukoo wa kifalme wa Daudi ambaye atatawala milele. Nathani anamjulisha Daudi ahadi hii yenye uzito kutoka kwa Mungu: “Nyumba yako na ufalme wako hakika zitakuwa imara mpaka wakati usio na kipimo mbele yako; nacho kiti chako cha ufalme kitafanywa imara mpaka wakati usio na kipimo.” (Mstari wa 16) Ni nani aliye Mrithi wa kudumu wa agano hilo—Yule atakayetawala milele?—Zaburi 89:20, 29, 34-36.

Yesu wa Nazareti alikuwa wa uzao wa Daudi. Alipotangaza kuzaliwa kwa Yesu, malaika alisema: “Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, naye atatawala akiwa mfalme juu ya nyumba ya Yakobo milele, na ufalme wake hautakuwa na mwisho.” (Luka 1:32, 33) Kwa hiyo, agano kati ya Mungu na Daudi linatimizwa katika Yesu Kristo. Hivyo, anatawala, si kwa kuchaguliwa na wanadamu, bali kupitia ahadi ya Mungu yenye uzito ambayo inampa haki ya kutawala milele. Na tukumbuke kwamba sikuzote ahadi za Mungu zinatimia.—Isaya 55:10, 11.

Kuna mambo mawili muhimu tunayojifunza katika 2 Samweli sura ya 7. Kwanza, tunaweza kuwa na hakika kwamba hakuna chochote wala yeyote anayeweza kumzuia Yesu Kristo asitawale. Kwa hiyo, hatuna shaka kwamba atatekeleza jambo alilosema angetekeleza katika utawala wake, yaani, kutimiza kikamili mapenzi ya Mungu duniani kama ilivyo mbinguni.—Mathayo 6:9, 10.

Pili, masimulizi haya yanatufunza jambo lenye kuchangamsha kumhusu Yehova. Kumbuka kwamba Yehova aliona na kuthamini kile ambacho Daudi alinuia kufanya. Inatia moyo kujua kwamba Yehova anathamini tunapojitolea kwa ajili ya ibada yake. Katika visa fulani, hali tusizoweza kuepuka, kama vile afya inayoendelea kuzorota au uzee, zinaweza kutuzuia kutimiza yale ambayo moyo wetu unatamani kufanya katika kumtumikia Mungu. Ikiwa ndivyo, tunaweza kufarijika kujua kwamba Yehova anaona hata nia ya moyo ambao umejitolea kabisa kwa ajili ya ibada yake.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Sanduku la agano lilikuwa takatifu na lilitengenezwa jinsi Yehova alivyotaka na kupatana na mwelekezo wake. Sanduku hilo liliwakilisha kuwapo kwa Yehova katika Israeli la kale.—Kutoka 25:22.