Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unamfuata Kristo kwa Ukamili?

Je, Unamfuata Kristo kwa Ukamili?

Je, Unamfuata Kristo kwa Ukamili?

“Kwa kweli kama vile mnavyotembea, . . . mwendelee kufanya hivyo kwa ukamili zaidi.”—1 THE. 4:1.

1, 2. (a) Watu wengi walioishi katika siku za Yesu walishuhudia mambo gani makubwa? (b) Kwa nini wakati wetu pia ni wa pekee?

JE, UMEWAHI kufikiria jinsi ilivyokuwa vizuri kuishi wakati ambapo Yesu alikuwa duniani? Huenda ungetazamia kuponywa na Yesu na hivyo kuacha kuteseka kwa sababu ya ugonjwa fulani unaokusumbua. Au unaweza kuwazia furaha kubwa ambayo ungepata ikiwa ungemwona na kumsikia Yesu akizungumza, na hivyo kujifunza kutoka kwake au kumwona akifanya miujiza. (Marko 4:1, 2; Luka 5:3-9; 9:11) Lingekuwa pendeleo kubwa kama nini kuwapo wakati Yesu alipokuwa akifanya mambo hayo yote! (Luka 19:37) Tangu wakati huo hakuna kizazi ambacho kimeona mambo kama hayo, na jambo ambalo Yesu alitimiza duniani “kupitia dhabihu yake mwenyewe” halitarudiwa tena.—Ebr. 9:26; Yoh. 14:19.

2 Hata hivyo, wakati wetu pia ni wa pekee. Kwa nini? Kwa sababu tunaishi wakati ambao Maandiko yalitabiri kuwa “wakati wa mwisho” na “siku za mwisho.” (Dan. 12:1-4, 9; 2 Tim. 3:1) Katika kipindi hiki, Shetani alitupwa kutoka mbinguni. Hivi karibuni, atafungwa na kutupwa “ndani ya abiso.” (Ufu. 12:7-9, 12; 20:1-3) Katika kipindi hiki, sisi pia tuna pendeleo kubwa la kutangaza “habari njema ya ufalme” ulimwenguni pote, na kuwaambia watu kuhusu tumaini la Paradiso inayokuja. Kazi hiyo haitarudiwa tena.—Mt. 24:14.

3. Muda mfupi kabla ya kupanda mbinguni, Yesu aliwaambia wafuasi wake wafanye nini, na hilo lingetia ndani nini?

3 Muda mfupi kabla ya kupanda mbinguni, Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Kazi hiyo ya kufundisha ingefanywa ulimwenguni pote. Kusudi lingekuwa nini? Kufanya wanafunzi, yaani, wafuasi zaidi wa Kristo, kabla ya ule mwisho kuja. (Mt. 28:19, 20) Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunataka kufanikiwa kutimiza kazi tuliyopewa na Kristo?

4. (a) Maneno ya Petro katika 2 Petro 3:11, 12 yanakazia uhitaji gani? (b) Tunahitaji kujilinda na nini?

4 Ona maneno haya ya mtume Petro: “Ninyi mnapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu, mkingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova!” (2 Pet. 3:11, 12) Maneno ya Petro yanakazia uhitaji wa kuendelea kujichunguza katika siku hizi za mwisho ili kuhakikisha kwamba tunatanguliza matendo ya ujitoaji-kimungu katika maisha yetu. Matendo hayo yanatia ndani kuhubiri habari njema. Kwa hiyo, tunafurahi sana kuona ndugu zetu ulimwenguni pote wakijitahidi kutimiza kazi ya kuhubiri tuliyopewa na Kristo. Vilevile, tunatambua kwamba tunahitaji kuwa waangalifu ili mikazo ya kila siku kutoka katika ulimwengu wa Shetani na mielekeo tuliyorithi ya dhambi isipunguze bidii yetu ya kumtumikia Mungu. Basi, acheni tuchunguze jinsi tunavyoweza kuhakikisha kwamba tunaendelea kumfuata Kristo.

Timiza Madaraka Unayopewa na Mungu

5, 6. (a) Paulo aliwapongeza waamini wenzake huko Yerusalemu kwa sababu gani, na aliwaonya kuhusu nini? (b) Kwa nini tunapaswa kuchukua kwa uzito madaraka tunayopewa na Mungu?

5 Katika barua yake kwa Wakristo huko Yerusalemu, mtume Paulo aliwasifu waamini wenzake kwa sababu walivumilia mateso kwa uaminifu. Alisema hivi: “Endeleeni kuzikumbuka zile siku za zamani ambazo, baada ya kutiwa nuru, mlivumilia shindano kubwa chini ya mateso.” Ndiyo, Yehova alikumbuka uaminifu wao. (Ebr. 6:10; 10:32-34) Bila shaka, maneno ya Paulo ya pongezi yaliwatia moyo sana Wakristo hao Waebrania. Hata hivyo, katika barua hiyohiyo, Paulo alionya pia kuhusu mwelekeo fulani wa kibinadamu ambao unaweza kupunguza bidii yetu ya kumtumikia Mungu ikiwa hautazuiwa. Alisema kwamba Wakristo wanapaswa kuwa waangalifu ili ‘wasikatae,’ au kutoa visingizio vya kutotii amri za Mungu.—Ebr. 12:25.

6 Onyo hilo kuhusu mwelekeo wa ‘kukataa’ kutimiza madaraka tunayopewa na Mungu linawahusu pia Wakristo leo. Tunatambua kwamba tunahitaji kuazimia kuchukua kwa uzito madaraka yetu ya Kikristo na kutoruhusu bidii yetu ya kumtumikia Mungu ipungue. (Ebr. 10:39) Kwa kweli, kutimiza utumishi mtakatifu kunamaanisha uhai au kifo.—1 Tim. 4:16.

7, 8. (a) Ni nini kitakachotusaidia kuendelea kumtumikia Mungu kwa bidii? (b) Ikiwa bidii tuliyokuwa nayo imepungua, tunapaswa kukumbuka nini kuhusu Yehova na Yesu?

7 Ni nini kitakachotusaidia kuepuka kutoa visingizio vya kutotimiza wajibu wetu mbele za Mungu? Njia moja muhimu ya kushinda mwelekeo huo ni kutafakari kwa ukawaida kuhusu maana ya nadhiri yetu ya kujiweka wakfu kwa Mungu. Kwa kweli, tulimwahidi Yehova kwamba tutatanguliza mapenzi yake katika maisha yetu, na tunataka kutimiza ahadi hiyo. (Soma Mathayo 16:24.) Kwa hiyo, tunahitaji kujiuliza hivi mara kwa mara: ‘Je, bado nimeazimia kuishi kulingana na wakfu wangu kwa Mungu kama nilivyoazimia wakati nilipobatizwa? Au je, bidii yangu imepungua kadiri ambavyo miaka imepita?’

8 Ikiwa baada ya kujichunguza kwa unyoofu tunaona kwamba kwa njia fulani mikono yetu imelegea, tunapaswa kukumbuka maneno yenye kuchochea yaliyosemwa na nabii Sefania. Alisema hivi: “Mikono yako isilegee. Yehova Mungu wako yupo katikati yako. Kama Mwenye nguvu, ataokoa. Atakufurahia kwa shangwe.” (Sef. 3:16, 17) Maneno hayo yanayotia moyo yaliwahusu kwanza Waisraeli wa zamani waliorudi Yerusalemu kutoka utekwani huko Babiloni. Hata hivyo, maneno hayo yanawatia moyo pia watu wa Mungu leo. Kwa kuwa kazi tunayofanya ni ya Yehova, tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova na Mwana wake wanatutegemeza na kututia nguvu ili tutimize kwa ukamili madaraka tunayopewa na Mungu. (Mt. 28:20; Flp. 4:13) Tukijitahidi kuendelea kufanya kazi ya Mungu kwa bidii, atatubariki na kutusaidia kufanya maendeleo ya kiroho.

“Kuutafuta Kwanza Ufalme” kwa Bidii

9, 10. Mfano wa Yesu wa karamu kubwa ya jioni unakazia jambo gani, na ni somo gani tunalojifunza kutokana na mfano huo?

9 Alipokuwa akila chakula katika nyumba ya mtawala mmoja wa Mafarisayo, Yesu alitoa mfano kuhusu karamu kubwa ya jioni. Katika mfano huo, alieleza kuhusu nafasi ya kuingia katika Ufalme wa mbinguni ambayo watu mbalimbali walipewa. Alitoa pia mfano unaoonyesha maana ya “kutoa visingizio.” (Soma Luka 14:16-21.) Wageni walioalikwa katika mfano huo wa Yesu walitoa visingizio ili wasihudhurie karamu hiyo. Mmoja wao alisema kwamba alihitaji kwenda kuchunguza shamba ambalo alikuwa ametoka tu kununua. Mwingine alisema kuwa alinunua ng’ombe na alitaka kuwachunguza. Na mwingine akasema hivi: ‘Nimeoa mke sasa hivi na kwa hiyo siwezi kuja.’ Hizo zilikuwa sababu zisizofaa. Kwa kawaida, mtu anayenunua shamba au wanyama wa kufugwa anachunguza vitu hivyo kabla ya kuvinunua, kwa hiyo hahitaji sana kuvichunguza baadaye. Na kwa nini kufunga ndoa hivi karibuni kungemzuia mtu asikubali mwaliko huo wa maana? Haishangazi kwamba mwenye nyumba katika mfano huo alikasirika sana!

10 Watu wote wa Mungu wanaweza kujifunza somo fulani kutokana na mfano wa Yesu. Somo gani? Hatupaswi kamwe kuruhusu mambo ya kibinafsi, kama yale yanayotajwa katika mfano wa Yesu, yawe ya maana sana kwetu hivi kwamba tunayatanguliza badala ya utumishi wetu kwa Mungu. Mkristo akitanguliza mambo ya kibinafsi katika maisha yake, bidii yake katika huduma itapungua hatua kwa hatua. (Soma Luka 8:14.) Ili bidii yetu isipungue, tunafuata shauri hili la Yesu: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake.” (Mt. 6:33) Inatia moyo kama nini kuona kwamba watumishi wa Mungu, vijana kwa wazee, wanafuata shauri hilo la maana sana! Kwa kweli, watu wengi wamerahisisha mtindo wao wa maisha ili watumie wakati mwingi zaidi katika huduma. Wanajifunza kutokana na maisha yao kwamba kuutafuta kwanza Ufalme kwa bidii kunaleta furaha ya kweli na uradhi mkubwa.

11. Ni simulizi gani la Biblia linaloonyesha faida ya kuwa na bidii na kumtumikia Mungu kwa moyo wote?

11 Ili kuonyesha faida ya kumtumikia Mungu kwa bidii, ona jambo lililotukia katika maisha ya Mfalme Yehoashi wa Israeli. Akiwa na wasiwasi kwamba Siria ingeishambulia na kuishinda Israeli, Yehoashi alienda kumwona Elisha huku akilia. Nabii huyo alimwagiza Yehoashi apige mshale nje kupitia dirisha kuelekea Siria, ili kuonyesha jinsi ambavyo Yehova angewasaidia kushinda taifa hilo. Bila shaka, jambo hilo lilipaswa kumtia nguvu mfalme huyo. Kisha, Elisha akamwambia Yehoashi achukue mishale yake na kuipiga chini. Yehoashi alipiga chini mara tatu tu. Hilo lilimkasirisha sana Elisha, kwa kuwa kupiga mishale chini mara tano au sita kungeonyesha kwamba ‘Siria ingepigwa kufikia hatua ya kuimaliza.’ Sasa Yehoashi angeshinda mara tatu tu. Kwa kuwa hakuonyesha bidii, Yehoashi hakufanikiwa sana. (2 Fal. 13:14-19) Tunajifunza somo gani kutokana na simulizi hilo? Yehova atatubariki sana ikiwa tu tutafanya kazi yake kwa moyo wote na kwa bidii.

12. (a) Ni nini kitakachotusaidia kuendelea kumtumikia Mungu kwa bidii na kuvumilia matatizo tunayokabili? (b) Eleza jinsi unavyofaidika kwa sababu ya kuhubiri kwa bidii.

12 Matatizo tunayokabili yanajaribu bidii yetu na ujitoaji wetu katika utumishi wa Mungu. Ndugu na dada wengi wanavumilia hali ngumu za kiuchumi. Wengine wanavunjika moyo kwa sababu ugonjwa mbaya unawazuia kutimiza mengi katika utumishi wa Yehova. Hata hivyo, kila mmoja wetu anaweza kuchukua hatua ili kuhakikisha kwamba anaendelea kuhubiri kwa bidii na kumfuata Kristo kwa ukamili. Tafadhali ona mapendekezo na maandiko yaliyoorodheshwa katika sanduku lenye kichwa “Ni Nini Kitakachokusaidia Kuendelea Kumfuata Kristo?” Fikiria jinsi unavyoweza kuyatumia kikamili. Ukifanya hivyo, utapata faida kwelikweli. Tunapohubiri kwa bidii tunapata usawaziko, maisha yetu yanakuwa bora zaidi, na tunapata amani na furaha nyingi zaidi. (1 Kor. 15:58) Zaidi ya hayo, kumtumikia Mungu kwa nafsi yote kunatusaidia “kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.”—2 Pet. 3:12.

Chunguza kwa Unyoofu Hali Zako

13. Tunaweza kujua jinsi gani jambo tunalopaswa kufanya ili tumtumikie Mungu kwa nafsi yote?

13 Hata hivyo, ni vizuri kukumbuka kwamba kumtumikia Mungu kwa nafsi yote hakutegemei muda ambao tunatumia katika huduma. Hali zetu zinatofautiana. Mtu anayehubiri kwa muda wa saa moja au mbili tu kila mwezi huenda anampendeza sana Yehova ikiwa afya yake inamruhusu kuhubiri kwa muda huo. (Linganisha na Marko 12:41-44.) Hivyo, ili kujua jambo tunalopaswa kufanya ili tumtumikie Mungu kwa nafsi yote, tunahitaji kuchunguza kwa unyoofu uwezo wetu na pia hali zetu. Tukiwa wafuasi wa Kristo, tunapaswa pia kuwa na maoni kama yake. (Soma Waroma 15:5; 1 Kor. 2:16) Yesu alitanguliza nini katika maisha yake? Aliuambia umati kutoka Kapernaumu hivi: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu, . . . kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43; Yoh. 18:37) Fikiria jinsi Yesu alivyotimiza huduma yake kwa bidii, na uchunguze hali zako ili uone ikiwa unaweza kupanua huduma yako.—1 Kor. 11:1.

14. Tunaweza kupanua huduma yetu katika njia gani mbalimbali?

14 Tukichunguza kwa uangalifu hali zetu huenda tukaona kwamba tunaweza kuongeza muda tunaotumia katika huduma. (Mt. 9:37, 38) Kwa mfano, maelfu ya vijana wetu ambao wamemaliza shule hivi karibuni wamepanua huduma yao na sasa wanapata shangwe inayotokana na kutumika kwa bidii wakiwa mapainia. Je, ungependa pia kuonja shangwe hiyo? Ndugu na dada fulani wamechunguza hali zao na kuamua kwamba wanaweza kuhamia katika eneo lingine la nchi yao, au hata nchi ya kigeni, ambako kuna uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Wengine wamejifunza lugha nyingine ili kuwasaidia watu wanaozungumza lugha ya kigeni. Ingawa si rahisi kupanua huduma yetu, kufanya hivyo kunaleta baraka nyingi, na huenda tukawasaidia watu wengi “kupata ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Tim. 2:3, 4; 2 Kor. 9:6.

Mifano ya Biblia ya Kuiga

15, 16. Ili tuwe wafuasi wenye bidii wa Kristo tunaweza kuwaiga nani?

15 Watu fulani ambao walikuja kuwa mitume waliitikia jinsi gani Kristo alipowaita wawe wafuasi wake? Biblia inasema hivi kumhusu Mathayo: “Baada ya kuacha kila kitu akaondoka akaanza kumfuata.” (Luka 5:27, 28) Kumhusu Petro na Andrea, ambao walikuwa wavuvi, tunasoma hivi: “Mara moja wakaziacha nyavu, wakamfuata.” Baadaye, Yesu alimwona Yakobo na Yohana, ambao walikuwa wakitengeneza nyavu zao pamoja na baba yao. Waliitikia jinsi gani mwaliko wa Yesu? “Mara moja wakaacha ile mashua na baba yao, wakamfuata.”—Mt. 4:18-22.

16 Mfano mwingine mzuri ni ule wa Sauli, ambaye baadaye alikuja kuwa mtume Paulo. Ingawa aliwatesa sana wafuasi wa Kristo, alibadilika na kuwa “chombo kilichochaguliwa” ili kutangaza jina la Kristo. “[Paulo] akaanza mara moja kumhubiri Yesu katika masinagogi, kwamba Huyu ndiye Mwana wa Mungu.” (Mdo. 9:3-22) Ingawa Paulo alivumilia matatizo na mateso mengi, bidii yake haikupungua kamwe.—2 Kor. 11:23-29; 12:15.

17. (a) Umeazimia kufanya nini unapomfuata Kristo? (b) Tunapata baraka gani tunapofanya mapenzi ya Yehova kwa moyo na nguvu zetu zote?

17 Bila shaka, tungependa kuiga mifano mizuri ya wanafunzi hao na kuchukua hatua ya haraka bila masharti. (Ebr. 6:11, 12) Ni baraka gani ambazo tunafurahia tunapoendelea kujitahidi kumfuata Kristo kwa bidii na kwa ukamili? Tunapofanya mapenzi ya Mungu, tunapata furaha ya kweli na pia tunapata uradhi tunapokubali mapendeleo zaidi ya utumishi na madaraka katika kutaniko. (Zab. 40:8; soma 1 Wathesalonike 4:1.) Ndiyo, tunapojitahidi kumfuata Kristo kwa bidii, tunapata baraka nyingi zinazodumu kama vile amani ya akili, kuridhika, kukubaliwa na Mungu, na tumaini la uzima wa milele.—1 Tim. 4:10.

Je, Unakumbuka?

• Ni kazi gani ya maana ambayo tumepewa, na tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu kazi hiyo?

• Ni mwelekeo gani wa kibinadamu tunaopaswa kuepuka, na kwa nini?

• Tunapaswa kuchunguza nini kwa unyoofu?

• Ni nini kitakachotusaidia kuendelea kumfuata Kristo?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 27]

Ni Nini Kitakachokusaidia Kuendelea Kumfuata Kristo?

▪ Soma Neno la Mungu kila siku, na utafakari kuhusu mambo unayosoma.—Zab. 1:1-3; 1 Tim. 4:15.

▪ Sali mara nyingi ili upate msaada na mwongozo wa roho ya Mungu. —Zek. 4:6; Luka 11:9, 13.

▪ Shirikiana na wale ambao wanahubiri kwa bidii kutoka moyoni.—Met. 13:20; Ebr. 10:24, 25.

▪ Tambua uharaka wa nyakati ambamo tunaishi.—Efe. 5:15, 16.

▪ Tambua matokeo mabaya ya ‘kukataa.’—Luka 9:59-62.

▪ Tafakari mara kwa mara kuhusu nadhiri yako ya wakfu na baraka nyingi ambazo zinatokana na kumtumikia Yehova na kumfuata Kristo kwa moyo wote.—Zab. 116:12-14; 133:3; Met. 10:22.