Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Anafanya Nini?

Mungu Anafanya Nini?

Mungu Anafanya Nini?

“Ee Yehova, kwa nini unaendelea kusimama mbali? Kwa nini unaendelea kujificha nyakati za taabu?” *ZABURI 10:1.

UKITUPIA jicho vichwa vikuu vya habari utaona wazi kwamba tunaishi katika “nyakati za taabu.” Na sisi wenyewe tunapokabili msiba, yaani, tunapotendewa uhalifu, tunapopata aksidenti mbaya, au mpendwa wetu anapokufa, huenda tukajiuliza, Je, Mungu anaona? Je, anajali? Na je, kweli yuko?

Hata hivyo, je, umefikiria uwezekano wa kwamba mambo ambayo tunatarajia Mungu afanye hayana msingi mzuri? Kwa mfano: Wazia mtoto mchanga ambaye amekasirika kwa sababu baba yake ameenda kazini. Mtoto huyo anamkosa sana baba yake na anatamani arudi nyumbani. Mtoto huyo anahisi kwamba ameachwa. Siku nzima, anauliza hivi tena na tena: “Baba yuko wapi?”

Tunaona wazi kasoro katika njia ya kufikiri ya mtoto huyo. Kwa kweli, wakati huo, baba yake anafanya kazi ili kutosheleza mahitaji ya familia yote. Je, njia yetu ya kufikiri inaweza kuwa na kasoro kama ya mtoto huyo wakati tunapolia, “Mungu yuko wapi”?

Kwa mfano, huenda wengine wakataka Mungu awe mtekelezaji wa hukumu ambaye daraka lake kuu ni kumwadhibu papo hapo mtu yeyote anayefanya makosa fulani. Wengine wanamwona Mungu kama Baba Krismasi aliye mbinguni, ambaye kazi yake ni kuwapa watu zawadi, kama vile, kazi, mke au mume, au hata tikiti ya kushinda mchezo wa bahati nasibu.

Maoni hayo mawili yanaonyesha kwamba ikiwa Mungu hatekelezi haki papo hapo au ikiwa hatupatii mambo tunayoomba, basi hajali tunapoteseka na hajui mahitaji yetu. Hata hivyo, yote hayo si kweli! Ukweli ni kwamba Yehova Mungu anafanya kazi sasa hivi ili kutimiza mahitaji ya familia yote ya wanadamu, hata hivyo si katika njia ambayo wengi wanamwomba.

Hivyo basi, Mungu anafanya nini sasa? Ili kujibu swali hilo, tunahitaji kurudi mwanzoni mwa historia ya wanadamu wakati uhusiano kati ya Mungu na wanadamu ulipoharibika kabisa—lakini mambo yangerekebishwa baadaye.

Matokeo Mabaya ya Dhambi

Fikiria nyumba ambayo imeharibika kwa miaka mingi. Paa limebomoka, milango imeng’oka, na sehemu ya nje imeharibiwa. Wakati fulani, nyumba hiyo ilikuwa katika hali nzuri, lakini kwa sasa imeharibika. Tunapofikiria jinsi ambavyo nyumba hiyo imeharibika, bila shaka si kazi rahisi kuirekebisha na haiwezi kufanywa kwa siku moja.

Sasa fikiria madhara ambayo wanadamu walipata miaka 6,000 hivi iliyopita wakati kiumbe wa roho asiyeonekana, Shetani, alipowashawishi Adamu na Hawa wamwasi Mungu. Kabla ya tukio hilo, wenzi hao wawili wa kwanza walifurahia afya kamilifu wakiwa na tumaini la kuishi milele pamoja na vizazi vya wakati ujao vya wazao wao. (Mwanzo 1:28) Hata hivyo, Adamu na Hawa walipotenda dhambi, ni kana kwamba waliharibu familia ya kibinadamu ambayo ilikuwa haijazaliwa.

Usipuuze matokeo mabaya ya uasi huo. Biblia inasema hivi: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi.” (Waroma 5:12) Zaidi ya kutuletea kifo, dhambi iliharibu uhusiano wetu pamoja na Muumba wetu na imekuwa na matokeo mabaya juu ya miili, akili, na hisia zetu. Kwa sababu hiyo, hali yetu ni kama ya ile nyumba iliyoharibika. Mwanamume mwadilifu Ayubu alieleza waziwazi hali yetu aliposema kwamba “siku [za mwanadamu] za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu.”—Ayubu 14:1, Union Version.

Lakini je, Mungu aliiacha jamii ya wanadamu baada ya Adamu na Hawa kutenda dhambi? Hapana! Kwa kweli, kuanzia wakati huo mpaka sasa, Baba yetu wa mbinguni amekuwa akifanya kazi kwa faida ya familia ya wanadamu. Ili kuthamini vizuri zaidi kile ambacho anafanya kwa ajili yetu, fikiria hatua tatu ambazo ni za lazima ili kuirekebisha nyumba iliyoharibika na jinsi kila hatua inavyohusiana na kile ambacho Mungu amefanya ili kuwarudishia wanadamu hali yao ya kwanza.

1 Baada ya kuichunguza nyumba iliyoharibika, ni lazima mwenye nyumba hiyo aamue ikiwa atairekebisha au kuibomoa.

Mara tu baada ya uasi katika Edeni, Yehova Mungu alitangaza kusudi lake la kuwarudishia wanadamu hali yao ya kwanza. Alimwambia hivi yule kiumbe wa roho asiyeonekana ambaye alichochea uasi huo: “Nitaweka uadui kati yako na yule mwanamke na kati ya uzao wako na uzao wake. Yeye atakuponda kichwa nawe utamtia jeraha kwenye kisigino.”—Mwanzo 3:15.

Kwa maneno hayo, Yehova aliahidi kumharibu yule aliyeanzisha uasi katika Edeni. (Waroma 16:20; Ufunuo 12:9) Zaidi ya hayo, Yehova alitabiri kwamba “uzao” ambao ungetokea wakati ujao ungewakomboa wanadamu kutoka katika dhambi. * (1 Yohana 3:8) Ahadi hizo zilifunua ukweli wa maana sana: Mungu angerekebisha, wala si kubomoa, uumbaji wake. Lakini kuwarudishia wanadamu hali yao ya kwanza kungehitaji muda.

2 Mtaalamu anachora ramani ya nyumba inayoonyesha jinsi kazi ya kurekebisha itakavyofanywa.

Yehova Mungu aliwapa Waisraeli mfumo wa sheria na maagizo ya kujenga hekalu ambamo wangemwabudu. Biblia inasema hivi: “Mambo hayo ni kivuli cha mambo yanayokuja.” (Wakolosai 2:17) Kama ramani ya nyumba, mambo hayo yalifananisha jambo fulani kubwa zaidi.

Kwa mfano, Waisraeli walitoa dhabihu za wanyama ili wasamehewe dhambi zao. (Walawi 17:11) Zoea hilo lilifananisha kimbele dhabihu kubwa zaidi ambayo ingetolewa karne nyingi baadaye, dhabihu ambayo ingeandaa ukombozi wa kweli kwa wanadamu. * Muundo wenyewe wa hema na hekalu ambamo Waisraeli waliabudu ulifananisha hatua mbalimbali ambazo Masihi aliyeahidiwa angechukua, kuanzia kifo chake cha kidhabihu mpaka kupanda kwake mbinguni.—Ona  chati kwenye ukurasa wa 7.

3 Mjenzi ambaye atafuata ramani na kuirekebisha nyumba iliyoharibika anachaguliwa.

Yesu alikuwa ndiye Masihi aliyechaguliwa ambaye angefuata kielelezo ambacho kiliwekwa na dhabihu za Waisraeli na angetoa uhai wake mwenyewe ili kuwakomboa wanadamu. Kwa kweli, Yohana Mbatizaji alimwita Yesu, “Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu.” (Yohana 1:29) Yesu alikubali kwa kupenda mgawo huo. Alisema hivi: “Nimeshuka kutoka mbinguni kufanya, si mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenituma.”—Yohana 6:38.

Mapenzi ambayo Mungu alitaka Yesu atimize yalitia ndani “kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi” na pia kufanya agano pamoja na wafuasi wake kwa ajili ya Ufalme. (Mathayo 20:28; Luka 22:29, 30) Mungu atatumia Ufalme huo ili kutimiza kusudi lake kwa ajili ya wanadamu. Ujumbe kuhusu Ufalme wa Mungu unaitwa “habari njema” kwa sababu unaeleza kwamba Mungu amesimamisha serikali mbinguni ambayo itasimamia mambo ya dunia!—Mathayo 24:14; Danieli 2:44. *

Kazi ya Kurudishwa Inaendelea

Kabla ya kupanda mbinguni, Yesu aliwaamuru hivi wafuasi wake: ‘Fanyeni wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu. Na, tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.’—Mathayo 28:19, 20.

Hivyo, kazi ya kuwarudisha wanadamu katika hali yao ya kwanza haingekoma baada ya kifo cha Yesu. Ingeendelea mpaka “umalizio wa mfumo wa mambo,” yaani, wakati ambapo Ufalme wa Mungu ungeanza kutawala dunia yetu. Wakati huo umefika. Tunajua hilo kwa sababu ishara ambayo Yesu alitabiri kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo” inatimia sasa. *Mathayo 24:3-14; Luka 21:7-11; 2 Timotheo 3:1-5.

Leo, katika nchi 236, Mashahidi wa Yehova wanatii amri ya Yesu ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. Kwa kweli, gazeti hili ambalo unasoma limekusudiwa kukusaidia kujifunza mengi zaidi kuhusu Ufalme huo na yale ambayo utatimiza. Kwenye ukurasa wa 2 wa kila gazeti la Mnara wa Mlinzi, utapata maelezo haya: “Gazeti hili . . . linawafariji watu kwa habari ya kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu, ambao ni serikali halisi iliyo mbinguni, utakomesha uovu wote na kuigeuza dunia kuwa paradiso. Linawatia watu moyo wamwamini Yesu Kristo, ambaye alikufa ili tupate uzima wa milele na ambaye sasa anatawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu.”

Ni kweli kwamba huenda utaendelea kusikia kuhusu mashambulizi ya kigaidi au misiba ya asili, au huenda ukapatwa na msiba. Lakini kujifunza Biblia kutakusadikisha kwamba Mungu hajawaacha wanadamu. Kinyume chake, “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27) Na ahadi yake ya kuturudishia kile ambacho wazazi wetu wa kwanza walipoteza itatimia.—Isaya 55:11.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Yehova ni jina la Mungu ambalo linafunuliwa katika Biblia.

^ fu. 16 Kwa maelezo zaidi kuhusu Mwanzo 3:15, ona sura ya 19 ya kitabu Mkaribie Yehova, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 19 Kwa maelezo zaidi, ona sura ya 5 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 22 Kwa habari zaidi kuhusu Ufalme wa Mungu, ona sura ya 8 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?

[Chati/Picha katika ukurasa wa 7]

 (Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

“Manno wa Uhalisi”—Maskani Ilifananisha Nini?

MADHABAHU

Utayari wa Mungu wa kukubali dhabihu ya Yesu.—WAEBRANIA 13:10-12.

KUHANI MKUU

Yesu.—WAEBRANIA 9:11.

1 Katika Siku ya Upatanisho, kuhani mkuu alitoa dhabihu kwa ajili ya dhambi za watu.—MAMBO YA WALAWI 16:15, 29-31.

1 Siku ya Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., Yesu alidhabihu uhai wake kwa ajili yetu.—WAEBRANIA 10:5-10; 1 YOHANA 2:1, 2.

PATAKATIFU

Hali ya Yesu akiwa kiumbe aliyezaliwa kwa roho.—MATHAYO 3:16, 17; WAROMA 8:14-17; WAEBRANIA 5:4-6.

PAZIA

Mwili wa kibinadamu wa Yesu, ni kizuizi kilichotenganisha uhai wa kidunia na uhai wa kimbingu.—1 WAKORINTHO 15:44, 50; WAEBRANIA 6:19, 20; 10:19, 20.

2 Kuhani mkuu aliingia upande wa pili wa pazia ambalo lilitenganisha Patakatifu na Patakatifu Zaidi.

2 Baada ya kufufuliwa, Yesu ‘aliingia upande mwingine wa pazia’ kwa kupaa mbinguni ‘ili aonekane mbele za uso wa Mungu kwa ajili yetu.’—WAEBRANIA 9:24-28.

PATAKATIFU ZAIDI

Mbinguni.—WAEBRANIA 9:24.

3 Kuhani mkuu alipoingia Patakatifu Zaidi, alitapanya kiasi fulani cha damu ya dhabihu mbele ya sanduku la agano.—MAMBO YA WALAWI 16:12-14.

3 Kwa kutoa thamani ya damu yake iliyomwagwa, Yesu aliandaa upatanisho wa kweli kwa ajili ya dhambi zetu.—WAEBRANIA 9:12, 24; 1 PETRO 3:21, 22.