Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Habari Njema” Inahubiriwa Kwenye Visiwa vya Mbali Kaskazini Mwa Australia

“Habari Njema” Inahubiriwa Kwenye Visiwa vya Mbali Kaskazini Mwa Australia

“Habari Njema” Inahubiriwa Kwenye Visiwa vya Mbali Kaskazini Mwa Australia

YESU alisema: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.” (Mathayo 24:14) Mashahidi wa Yehova wanatii amri ya Yesu na wanajaribu kuwapelekea watu ujumbe wa Biblia kila mahali wanapoishi. (Mathayo 28:19, 20) Wanafanya kazi hiyo kwa kujitolea, na nyakati nyingine wanakabiliana na hali ngumu na kutumia pesa zao wenyewe.

Kwa mfano, Nathan na Carly, walifanya mabadiliko katika maisha yao ili wawahubirie watu wanaoishi mbali kwenye Visiwa vya Mlango-Bahari wa Torres. Mwaka wa 2003, mwakilishi wa ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Australia aliwaomba wahamie kwenye Kisiwa cha Thursday ili wahubiri pamoja na kutaniko la huko. Kisiwa hicho ni moja kati ya visiwa vingi vyenye rangi ya kijani ambavyo viko katikati ya maji ya rangi ya bluu ya Bahari ya Pasifiki, kati ya nchi ya Australia na New Guinea.

Mwaka wa 2007, familia hiyo ilinunua mashua ya mbao iliyokuwa imezeeka ambayo ilitumiwa kuvua lulu. Mashua hiyo iliitwa Teisan-Y. Waliirekebisha mashua hiyo wakitumia pesa zao wenyewe na wakaanza kwenda katika safari za kuwahubiria wakaaji wa visiwa kumi vilivyo mbali zaidi, huku wakiishi kwenye Kisiwa cha Thursday. Zifuatazo ni safari fulani walizofunga.

Januari (Mwezi wa 1) 2008: Leo, niliendesha boti mpaka Bamaga, umbali wa kilomita 80 kwenda na kurudi, ili kuwachukua Mashahidi sita wanaoishi katika eneo hilo. Sasa tuko ndani ya mashua ya Teisan-Y tukielekea kwenye visiwa vya Warraber na Poruma. Matangi ya mashua yamejaa lita 5,500 za mafuta yanayogharimu dola mbili kwa kila lita. Mashua inaenda polepole sana, mwendo wa kilomita kumi tu kwa saa. Lakini hali ya hewa ni nzuri, maji ya bahari yametulia kabisa.

Tunapofika, tunatia nanga kwenye ufuo, tunashuka pamoja na watu fulani tuliosafiri pamoja nao ambao wana watu wa ukoo kwenye kisiwa cha Warraber, na tunasafiri kwa boti ili kwenda kumwona chifu wa kisiwa hicho ili aturuhusu kuhubiri. Yeye ni kasisi katika kanisa fulani kwenye kisiwa hicho lakini anaturuhusu tuzungumze na wakaaji. Tunafanya vivyo hivyo tunapofika huko Poruma na tunaruhusiwa pia kuhubiri. Watu ni wenye urafiki sana na wanatamani kusoma vitabu vyetu. Tunaanzisha mafunzo mengi ya Biblia.

Aprili (Mwezi wa 4) 2008: Tunapanga safari ya kufika kwenye visiwa vitatu vilivyo mbali zaidi, Dauan, Saibai, na Boigu, karibu na mpaka wa Papua New Guinea (PNG). Hali ya hewa inakuwa mbaya sana na hivyo tunaelekea kwenye Kisiwa cha Mabuiag. Kisiwa cha Mabuiag kiko umbali wa kilomita 70 tu kutoka kwenye bandari ya kisiwa ambako tunaishi, lakini tutasafiri kilomita 140 tukizunguka-zunguka miamba mingi ya baharini.

Tulipokuwa baharini, wimbi kubwa sana lilikata kamba iliyokuwa ikivuta boti kutoka kwa Teisan-Y. Ingawa bahari ilikuwa imechafuka, tuligeuza mashua yetu na kurudi kuitafuta boti hiyo na tukaipata. Wengi tunaosafiri nao wana kichefuchefu.

Tunapofika Mabuiag, tunaruhusiwa kuhubiri kwenye kisiwa hicho, na wakaaji wanatusalimu kwa uchangamfu sana hivi kwamba baada ya muda mfupi tunasahau matatizo tuliyokabili. Mwanamke mmoja anafurahi sana kusikia ujumbe wetu hivi kwamba anachukua vitabu zaidi ili aviweke kwenye maktaba ya kisiwa hicho, ambako anafanya kazi.

Mei (Mwezi wa 5) mpaka Oktoba (Mwezi wa 10) 2008: Kwa sababu ya hali ya hewa, tunashindwa kwenda kwenye visiwa vingine. Tunatumia muda huo kuhubiri katika kisiwa chetu, kufanya kazi, na kuirekebisha mashua.

Mashua inahitaji kufanyiwa marekebisho makubwa, hivyo tunasafiri mpaka kwenye bandari ya Weipa na tunavuta mashua hiyo kutoka ndani ya maji na kuiweka juu ya trela kubwa. Huenda likaonekana kuwa jambo rahisi lakini sivyo! Mashahidi wa kutaniko la eneo hilo wanajitolea kutusaidia kufanya kazi hiyo, ambayo inahusisha, kurekebisha mabomba, kupaka rangi, na kazi za mbao. Wengine wanaleta vyakula. Na wengine wanatuletea vyakula ambavyo tutatumia katika safari yetu inayofuata ya kuhubiri. Tunathamini sana ukarimu na msaada wao.

Desemba 2008: Tunaanza tena safari kuelekea Dauan, Saibai, na Boigu. Tunaepuka dhoruba za kitropiki kwa kutumia mfumo wetu wa rada, na tunapita katikati ya miamba tukitumia kifaa cha kielektroniki cha kusafiri baharini. Tunasafiri baharini kwa saa 12 kabla ya kufika Dauan. Hatujawahi kamwe kuona kisiwa maridadi zaidi kama hicho. Vilima virefu vilivyo kwenye kisiwa hicho vimefunikwa na mawingu. Wakaaji wa Dauan wanatusikiliza kwa makini na tunafanya mpango ili tuendelee na mazungumzo ya Biblia kupitia simu tutakaporudi nyumbani.

Mkaaji mmoja mwanamke anayeitwa Lettie, alikuwa amepokea magazeti yetu na akatuma ombi la kupata vichapo zaidi. Ofisi ya tawi huko Australia ilikuwa imetuma barua katika kutaniko letu ikiomba tumtembelee ikiwezekana. Mwishowe, tunampata Lettie na tunafurahi sana kutimiza sehemu ndogo katika kutosheleza mahitaji yake ya kiroho.

Chifu wa kisiwa cha Saibai anakataa kuturuhusu tuwahubirie wakaaji wa kisiwa hicho. Lakini anawaruhusu wale tunaosafiri nao ambao wana watu wa ukoo kwenye kisiwa hicho wawatembelee na kuzungumza nao. Serikali imenipa kazi ya kupaka rangi nyumba fulani huko Saibai, na kazi hiyo inatusaidia kupata pesa za kulipia gharama zetu.

Dada yetu mmoja anayeitwa Tassie anatoka kwenye kijiji kimoja huko PNG, ambacho kiko kilomita nne hivi kutoka Saibai. Kwa sababu ya makubaliano yaliyofanywa pamoja na serikali ya Australia, wakaaji wa PNG wanaweza kuja Saibai kufanya biashara. Tassie anakutana na watu wengi kutoka kwenye kijiji chao lakini hana vichapo vya kutosha kuwapa wote. Hii ni mara ya kwanza kwa Tassie kukutana na watu kutoka kwenye kijiji chao tangu alipokuwa Shahidi wa Yehova. Tunarudi kwenye mashua na kumletea katoni lililojaa vichapo, vingi vikiwa vya lugha ya Pijini ya PNG, lugha ambayo inaitwa Tok Pisin. Tassie anahubiri ujumbe wa Biblia kwa kikundi cha watu zaidi ya 30 kutoka PNG, na wale wanaopendezwa wanachukua vichapo vyote alivyo navyo. Kijiji chao kinaweza kufikiwa tu kwa mashua na huenda hakijawahi kutembelewa na Mashahidi wa Yehova.

Ni vigumu sana kufika kwenye kisiwa cha mwisho, Boigu. Tuko umbali wa kilomita nne hivi kutoka kwenye ufuo wa bahari lakini kina cha maji ni mita mbili na nusu tu. Mashua inafikia kina cha karibu mita mbili. Mimi na mtu mmoja kati ya watu tunaosafiri nao tunatumia ile boti kutafuta njia ya kufika kwenye kisiwa hicho. Mvua inanyesha na tunaloa! Tunapata njia baada ya muda wa saa mbili.

Tunapofika, tunashangaa wakati wakaaji wa kisiwa hicho wanapotuambia kwamba ramani niliyo nayo si sahihi na kwamba hata walinzi wa pwani na wanajeshi hawaingii katika eneo hilo. Chifu wa kisiwa hicho anatunyima ruhusa ya kuhubiri lakini anawaruhusu wale tunaosafiri nao ambao wana watu wa ukoo kwenye kisiwa hicho wawatembelee na kuwahubiria. Tunatii agizo la chifu huyo na kuwatembelea tu watu wa ukoo. Mwanamume mmoja anachukua kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?, * mara moja anakisoma, naye anaanza kuandika maswali upande wa nyuma wa Biblia yake. Mwanamume huyohuyo anahubiriwa tena na Mashahidi anapotembelea Kisiwa cha Thursday.

Januari 2009: Tunarudi tena kwenye visiwa vya Moa na Mabuiag ili kuzungumza tena na watu waliopendezwa na ujumbe wa Biblia. Tunakaribishwa kwa uchangamfu sana kwenye visiwa vyote viwili. Wengi katika kijiji cha St. Paul na wengine kwenye Kisiwa cha Moa wanatuambia kwamba tusikae sana kabla ya kuwatembelea tena. Chifu anasema kwamba tunakaribishwa kuhubiri katika kijiji hicho wakati wowote.

Kuna visiwa 17 vilivyo na wakaaji kwenye Mlango-Bahari wa Torres. Hatujui kama tutafaulu kuzungumza na kila mtu anayeishi kwenye visiwa hivyo. Lakini sote katika kutaniko lililo kwenye visiwa vilivyo mbali zaidi kaskazini mwa Australia tunafurahi kufanya yote tunayoweza ili kumletea sifa Muumba wetu Mkuu, Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Ramani katika ukurasa wa 23]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

AUSTRALIA

Weipa

Bamaga

VISIWA VYA MLANGO-BAHARI WA TORRES

PAPUA NEW GUINEA

[Hisani]

Based on NASA/Visible Earth imagery

[Ramani katika ukurasa wa 24, 25]

Bamaga

Kisiwa cha Thursday

Kisiwa cha Moa

Kisiwa cha Warraber

Kisiwa cha Poruma

Kisiwa cha Mabuiag

Kisiwa cha Saibai

Kisiwa cha Dauan

Kisiwa cha Boigu

PAPUA NEW GUINEA

[Hisani]

Based on NASA/Visible Earth imagery

[Picha katika ukurasa wa 24]

Tunawasili kwenye Kisiwa cha Thursday

[Picha katika ukurasa wa 24]

Tukienda kuwahubiria watu kwenye Kisiwa cha Saibai

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kuhubiri habari njema katika lugha ya Tok Pisin