Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Moyo Uliovunjika na Kupondwa” Unapotafuta Msamaha

“Moyo Uliovunjika na Kupondwa” Unapotafuta Msamaha

Mkaribie Mungu

“Moyo Uliovunjika na Kupondwa” Unapotafuta Msamaha

2 Samweli 12:1-14

SISI sote tunatenda dhambi mara nyingi. Hata tukiomba msamaha kadiri gani, huenda tukajiuliza: ‘Je, Mungu anasikia sala zangu za unyoofu za kutubu? Atanisamehe?’ Biblia inafundisha ukweli huu wenye kufariji: Ingawa Yehova haachilii tu dhambi, yuko tayari kumsamehe mtenda-dhambi anayetubu. Ukweli huo ulionekana wazi zaidi katika kisa cha Mfalme Daudi wa Israeli la kale, ambacho kinasimuliwa katika 2 Samweli sura ya 12.

Hebu wazia kile kilichotukia. Daudi ana hatia ya kutenda dhambi nzito. Alifanya uzinzi na Bath-sheba, na aliposhindwa kuficha dhambi hiyo, alipanga njama ili mume wake auawe. Kisha, Daudi akanyamaza kuhusu dhambi zake, huku akionekana kuwa asiye na hatia kwa miezi fulani. Hata hivyo, Yehova alikuwa akitazama. Aliona dhambi za Daudi. Lakini pia aliona kwamba Daudi alikuwa na mtazamo wa kutubu katika moyo wake. (Methali 17:3) Yehova angefanya nini?

Yehova anamtuma nabii Nathani kwa Daudi. (Mstari wa 1) Akiongozwa na roho takatifu, Nathani anazungumza na mfalme kwa busara, huku akijua kwamba anapaswa kuchagua maneno yake kwa uangalifu. Atamwonyesha Daudi jinsi gani kwamba anajidanganya na kumfanya aone uzito wa dhambi zake?

Ili kumzuia Daudi asijitetee, Nathani anasimulia hadithi ambayo bila shaka ingegusa moyo wa Daudi ambaye zamani alikuwa mchungaji wa kondoo. Ni hadithi ya wanaume wawili, mmoja ni tajiri na yule mwingine ni maskini. Yule mwanamume tajiri alikuwa na “kondoo na ng’ombe wengi sana,” lakini yule mwanamume maskini “hakuwa na chochote isipokuwa mwana-kondoo jike mmoja.” Yule mwanamume tajiri alimkaribisha mgeni na alitaka kumtayarishia chakula. Badala ya kuchukua mmoja kati ya kondoo wake, alichukua yule mwana-kondoo jike mmoja wa mwanamume maskini. Inaelekea Daudi anafikiri kwamba hadithi hiyo ni ya kweli, naye anakasirika sana na kusema hivi bila kufikiri: “Mtu huyo aliyefanya hivyo anastahili kufa!” Kwa nini? Daudi anaeleza: “Kwa sababu hakuwa na huruma.” *Mstari wa 2-6.

Hadithi ambayo Nathani anasimulia imetimiza kusudi lake. Ni wazi kwamba Daudi amejishtaki. Sasa Nathani anamwambia hivi waziwazi: “Wewe mwenyewe ndiye yule mwanamume!” (Mstari wa 7) Kwa kuwa Nathani anamwakilisha Mungu, ni wazi kwamba Yehova anachukua kwa uzito sana matendo ya Daudi. Kwa kuvunja sheria za Mungu, Daudi ameonyesha kwamba hamheshimu Mungu ambaye ni Mpaji-Sheria. Mungu anasema: “Ulinidharau mimi.” (Mstari wa 10) Moyo wa Daudi ukiwa umechomwa na karipio hilo kali, anaungama hivi: “Nimemtendea Yehova dhambi.” Nathani anamhakikishia Daudi kwamba Yehova amemsamehe, lakini Daudi atalazimika kuishi na matokeo mabaya ya matendo yake.—Mstari wa 13, 14.

Baada ya dhambi yake kufunuliwa, Daudi aliandika maneno ambayo sasa ni Zaburi ya 51. Katika Zaburi hiyo, Daudi anamwaga mambo yaliyo katika moyo wake, akifunua jinsi alivyotubu kikweli. Daudi alipotenda dhambi, alimdharau Yehova. Lakini mara tu mfalme huyo mwenye toba alipoona jinsi msamaha wa Yehova unavyofurahisha sana, alimwambia Yehova hivi: “Moyo uliovunjika na kupondwa, Ee Mungu, hutaudharau.” (Zaburi 51:17) Maneno hayo yanamtia moyo sana mtenda-dhambi mwenye toba anayetafuta msamaha wa Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Mtu aliyemtayarishia mgeni mwana-kondoo wa kula alionyesha sifa ya ukaribishaji-wageni. Lakini mtu aliyeiba mwana-kondoo alifanya uhalifu, na hivyo aliadhibiwa kwa kulipa kondoo wanne. (Kutoka 22:1) Kwa maoni ya Daudi, mtu huyo tajiri ambaye alichukua mwana-kondoo wa maskini hakuwa na huruma. Kwa hiyo, tajiri huyo aliiba mnyama wa yule mwanamume maskini ambaye huenda angeandalia familia yake maziwa na manyoya na ambaye hata angezaa kundi kubwa la kondoo.