Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wanaume—Je, Mnajitiisha Chini ya Ukichwa wa Kristo?

Wanaume—Je, Mnajitiisha Chini ya Ukichwa wa Kristo?

Wanaume—Je, Mnajitiisha Chini ya Ukichwa wa Kristo?

“Kichwa cha kila mwanamume ni Kristo.”—1 KOR. 11:3.

1. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova ni Mungu mwenye utaratibu?

ANDIKO la Ufunuo 4:11 linasema hivi: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.” Kwa kuwa Yehova Mungu ni Muumba, yeye ndiye Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote naye ana mamlaka juu ya vitu vyote alivyoumba. Tukiangalia mpangilio wa familia yake ya malaika, tunaona wazi kwamba Yehova “si Mungu wa machafuko, bali ni wa amani.”—1 Kor. 14:33; Isa. 6:1-3; Ebr. 12:22, 23.

2, 3. (a) Yehova alimuumba nani kwanza? (b) Mwana mzaliwa wa kwanza ana cheo gani kikilinganishwa na cheo cha Baba?

2 Mungu aliishi peke yake kwa miaka isiyohesabika kabla hajaumba kitu chochote. Yehova aliumba kwanza kiumbe wa roho anayeitwa “Neno” kwa sababu alikuwa Msemaji wake. Vitu vingine vyote viliumbwa kupitia huyo Neno. Baadaye, msemaji huyo alikuja duniani akawa mwanadamu mkamilifu ambaye aliitwa Yesu Kristo.—Soma Yohana 1:1-3, 14.

3 Maandiko yanasema nini kuhusu cheo cha Mungu kikilinganishwa na cheo cha Mwana wake mzaliwa wa kwanza? Akiandika chini ya mwongozo wa roho takatifu, mtume Paulo anatuambia hivi: “Nataka mjue kwamba kichwa cha kila mwanamume ni Kristo; nacho kichwa cha mwanamke ni mwanamume; nacho kichwa cha Kristo ni Mungu.” (1 Kor. 11:3) Kristo yuko chini ya ukichwa wa Baba yake. Ukichwa na kujitiisha ni mambo ya maana sana ili kuwe na amani na utaratibu kati ya viumbe wenye akili. Hata yule ambaye “kwa njia yake vitu vingine vyote viliumbwa” anatakiwa ajitiishe chini ya ukichwa wa Mungu.—Kol. 1:16.

4, 5. Yesu alihisi namna gani kuhusu cheo chake kikilinganishwa na cheo cha Yehova?

4 Yesu alihisi namna gani kuhusu kujitiisha chini ya ukichwa wa Yehova na kuja duniani? Maandiko yanasema hivi: “Kristo Yesu, ambaye, ingawa alikuwa katika umbo la Mungu, hakufikiria kufanya unyakuzi, yaani, kwamba yeye awe sawa na Mungu. Hapana, bali alijiondolea mwenyewe hali yake na kuchukua umbo la mtumwa na kuwa kama wanadamu. Zaidi ya hayo, alipojikuta katika umbo la mwanadamu, alijinyenyekeza naye akawa mtiifu mpaka kifo, ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso.”—Flp. 2:5-8.

5 Nyakati zote, Yesu alijitiisha kwa unyenyekevu chini ya mapenzi ya Baba yake. Yesu alisema hivi: “Mimi siwezi kufanya lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe; . . . hukumu ninayotoa ni ya uadilifu, kwa sababu ninatafuta, si mapenzi yangu mwenyewe, bali mapenzi yake aliyenituma.” (Yoh. 5:30) Pia, alisema hivi: “Sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza [Baba yangu].” (Yoh. 8:29) Karibu mwisho wa maisha yake duniani, Yesu alisema hivi katika sala kwa Baba yake: “Nimekutukuza duniani, nikiwa nimemaliza kazi ambayo umenipa niifanye.” (Yoh. 17:4) Ni wazi kwamba Yesu alitambua na kukubali ukichwa wa Mungu bila tatizo.

Mwana Alifaidika kwa Kujitiisha Chini ya Baba

6. Ni sifa gani nzuri sana ambazo Yesu alionyesha?

6 Yesu alipokuwa duniani alionyesha sifa nyingi nzuri sana. Kwa mfano, alimpenda sana Baba yake. Alisema hivi: “Ninampenda Baba.” (Yoh. 14:31) Alionyesha pia upendo mkubwa kwa watu. (Soma Mathayo 22:35-40.) Yesu alikuwa mwenye fadhili na mwenye kujali, hakuwa mkali au hakuwakandamiza watu. Alisema hivi: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mt. 11:28-30) Watu wenye umri mbalimbali ambao walikuwa mfano wa kondoo, hasa wale waliokandamizwa na kuonewa, walifarijiwa sana na utu wenye kuvutia wa Yesu na ujumbe wake wenye kutia moyo.

7, 8. Chini ya Sheria, mwanamke mwenye mtiririko wa damu aliwekewa vizuizi gani, lakini Yesu alimtendea jinsi gani?

7 Fikiria jinsi Yesu alivyowatendea wanawake. Katika historia yote, wanaume wengi wamewatendea wanawake vibaya sana. Viongozi wa kidini katika Israeli la kale waliwatendea wanawake vivyo hivyo. Lakini Yesu aliwatendea wanawake kwa heshima. Tunaona hilo wazi kutokana na jinsi alivyomtendea mwanamke ambaye alikuwa na ugonjwa wa kutiririka damu kwa miaka 12. “Alikuwa ameumizwa sana” na matabibu au madaktari wengi na alikuwa ametumia mali zake zote ili aponywe. Hata hivyo, ingawa alijitahidi kabisa kupata matibabu ‘hali yake ilikuwa mbaya zaidi.’ Chini ya Sheria, alionwa kuwa asiye safi. Mtu yeyote aliyemgusa angekuwa pia asiye safi.—Law. 15:19, 25.

8 Mwanamke huyo aliposikia kwamba Yesu anaponya wagonjwa, alijiunga na umati uliokuwa ukimzunguka, huku akisema hivi: “Nikiyagusa tu mavazi yake ya nje nitapona.” Alimgusa Yesu na mara moja akapona. Yesu alijua kwamba mwanamke huyo hakupaswa kugusa vazi lake. Hata hivyo, Yesu hakumkemea. Badala yake, alimtendea kwa fadhili. Alielewa jinsi mwanamke huyo alivyohisi baada ya kuwa mgonjwa kwa miaka mingi sana na alitambua kwamba mwanamke huyo alihitaji sana msaada. Yesu alimwambia hivi kwa huruma: “Binti yangu, imani yako imekuponya. Nenda kwa amani, na uwe na afya njema.”—Marko 5:25-34.

9. Wanafunzi wa Yesu walipojaribu kuwazuia watoto kumkaribia, alitenda jinsi gani?

9 Hata watoto walistarehe walipokuwa na Yesu. Pindi moja, watu walipomletea watoto, wanafunzi wake waliwakemea, inaonekana walifikiri kwamba Yesu hangetaka kusumbuliwa na watoto. Lakini Yesu hakuhisi hivyo. Simulizi hilo la Maandiko linatuambia hivi: “Alipoona hilo, Yesu akaghadhibika na kuwaambia [wanafunzi]: ‘Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwazuia, kwa maana ufalme wa Mungu ni wa wale walio kama hao.’” Kisha, “akachukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki, akiweka mikono yake juu yao.” Yesu hakuvumilia tu kukaa na watoto; aliwakaribisha kwa uchangamfu.—Marko 10:13-16.

10. Yesu alijifunza kutoka kwa nani sifa ambazo alionyesha?

10 Yesu alijifunza kutoka kwa nani sifa ambazo alionyesha katika maisha yake duniani? Kabla ya kuwa mwanadamu, alimtazama Baba yake wa mbinguni kwa miaka mingi sana naye akajifunza njia zake. (Soma Methali 8:22, 23, 30.) Akiwa mbinguni, aliona jinsi Yehova alivyotumia ukichwa wake kwa njia ya upendo juu ya viumbe Wake wote naye akaiga sifa hiyo. Je, Yesu angeweza kufanya hivyo ikiwa hakuwa tayari kujitiisha? Alifurahia kujitiisha kwa Baba yake, naye Yehova alifurahi sana kuwa na Mwana anayejitiisha. Alipokuwa duniani, Yesu aliiga kikamili sifa bora za Baba yake wa mbinguni. Ni pendeleo kama nini kwetu kujitiisha kwa Kristo, Mtawala wa Ufalme wa mbinguni aliyewekwa rasmi na Mungu!

Iga Sifa za Kristo

11. (a) Tunapaswa kujitahidi sana kumwiga nani? (b) Kwa nini wanaume hasa walio katika kutaniko wanapaswa kujitahidi kumwiga Yesu?

11 Watu wote katika kutaniko la Kikristo, hasa wanaume, wanapaswa kuendelea kujitahidi kuiga sifa za Kristo. Kama tulivyoona, Biblia inatangaza hivi: “Kichwa cha kila mwanamume ni Kristo.” Wanaume Wakristo wanapaswa kujitahidi kuiga kichwa chao, Kristo, kama vile Kristo alivyomwiga Mungu wa kweli ambaye ni Kichwa chake. Mtume Paulo alifanya hivyo alipogeuka na kuwa Mkristo. Aliwahimiza Wakristo wenzake hivi: “Iweni waigaji wangu, kama vile mimi nilivyo mwigaji wa Kristo.” (1 Kor. 11:1) Naye mtume Petro alisema: “Mliitwa kwenye mwendo huu, kwa sababu hata Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Pet. 2:21) Himizo la kumwiga Kristo linawahusu hasa wanaume kwa sababu nyingine. Kwa sababu hao ndio wanaowekwa kuwa wazee na watumishi wa huduma. Kama Yesu alivyopata shangwe kwa kumwiga Yehova, ndivyo wanaume Wakristo wanavyopaswa kupata shangwe katika kumwiga Kristo na sifa zake.

12, 13. Wazee wanapaswa kuwatendea jinsi gani kondoo walio chini ya utunzaji wao?

12 Wazee katika kutaniko la Kikristo wana wajibu wa kujifunza kuwa kama Kristo. Petro aliwahimiza hivi wanaume wazee, au wazee wa kutaniko: “Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu, si kwa kulazimishwa, bali kwa kupenda; wala si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu; wala si kama kwa kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu, bali kuwa vielelezo kwa kundi.” (1 Pet. 5:1-3) Wazee Wakristo hawapaswi kuwa madikteta, wenye kukandamiza au wasiojali kondoo, au kuwa wakali. Wanaiga mfano wa Kristo kwa kujitahidi kuwa wenye upendo, wenye kujali, wanyenyekevu, na kuwatendea kwa fadhili kondoo walio chini ya utunzaji wao.

13 Wale wanaoongoza katika kutaniko ni wanaume wasio wakamilifu, na hivyo wanapaswa sikuzote kukumbuka udhaifu huo. (Rom. 3:23) Kwa hiyo, wanapaswa kuwa na hamu kubwa ya kujifunza kumhusu Yesu na kuiga upendo wake. Wanahitaji kutafakari kuhusu jinsi Mungu na Kristo wanavyoshughulika na watu na kisha wajitahidi kuwaiga. Petro anatuhimiza hivi: “Ninyi nyote jifungeni unyenyekevu wa akili kuelekeana ninyi wenyewe, kwa sababu Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.”—1 Pet. 5:5.

14. Wazee wanapaswa kuwaheshimu wengine kwa kadiri gani?

14 Wanaume waliowekwa rasmi katika kutaniko wanapaswa kuonyesha sifa nzuri wanaposhughulika na kundi la Mungu. Andiko la Waroma 12:10 linasema hivi: “Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake. Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” Wazee na watumishi wa huduma wanawaheshimu wengine. Kama Wakristo wote kwa ujumla, wanaume hao hawapaswi ‘kufanya jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili wakiwaona wengine kuwa ni bora kuliko wao.’ (Flp. 2:3) Bila shaka, wale wanaoongoza wanapaswa kuwaona wengine kuwa ni bora kuliko wao. Wakifanya hivyo, wanaume hao waliowekwa rasmi watakuwa wakifuata shauri hili la Paulo: “Ingawa hivyo, sisi tulio na nguvu tunapaswa kuchukua udhaifu wa wale wasio na nguvu, na tusiwe tukijipendeza wenyewe. Kila mmoja wetu na ampendeze jirani yake katika yaliyo mema kwa ajili ya kujengwa kwake. Kwa maana hata Kristo hakujipendeza mwenyewe.”—Rom. 15:1-3.

‘Kuwapa Wake Heshima’

15. Waume wanapaswa kuwatendea wake zao namna gani?

15 Sasa fikiria shauri la Petro kwa wanaume ambao wameoa. Aliandika hivi: “Enyi waume, endeleeni kukaa [na wake zenu] vivyo hivyo kulingana na ujuzi, mkiwapa heshima kama chombo dhaifu zaidi, yaani, mwanamke.” (1 Pet. 3:7) Kumheshimu mtu kunamaanisha kumwona mtu huyo kuwa wa maana sana. Hivyo, utafikiria maoni, mahitaji, na mambo ambayo mtu huyo anataka na unaweza kukubali maoni yake ikiwa hakuna sababu yoyote nzuri ya kukataa maoni hayo. Hivyo ndivyo mume anavyopaswa kumtendea mke wake.

16. Neno la Mungu linatoa onyo gani kwa waume kuhusu kuwaheshimu wake zao?

16 Petro anapowaambia waume wawaheshimu wake zao, anaongezea onyo hili: “Kusudi sala zenu zisizuiwe.” (1 Pet. 3:7) Hilo linaonyesha wazi kwamba jinsi mwanamume anavyomtendea mke wake ni jambo zito machoni pa Yehova. Mume akikosa kumheshimu mke wake sala zake zinaweza kuzuiwa. Zaidi ya hayo, je, si ni kweli kwamba wake kwa ujumla wanaitikia vizuri wanapotendewa kwa heshima na waume zao?

17. Mume anapaswa kumpenda mke wake kwa kadiri gani?

17 Neno la Mungu linashauri hivi kuhusu mume kumpenda mke wake: “Waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. . . . Kwa maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake kwa vyovyote; bali huulisha na kuutunza kwa upendo, kama vile Kristo pia anavyolitendea kutaniko . . . Kila mtu mmoja-mmoja kati yenu na ampende hivyo mke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe.” (Efe. 5:28, 29, 33) Waume wanapaswa kuwapenda wake zao kwa kadiri gani? Paulo aliandika hivi: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake.” (Efe. 5:25) Ndiyo, mume anapaswa kuwa tayari hata kufa kwa ajili ya mke wake, kama vile Kristo alivyokufa kwa ajili ya wengine. Mume Mkristo anapomtendea mke wake kwa wororo, fadhili, uangalifu, na bila uchoyo, inakuwa rahisi zaidi kwa mke wake kujitiisha chini ya ukichwa wake.

18. Ni msaada gani ambao wanaume wanaweza kupata ili watimize madaraka yao katika ndoa?

18 Je, ni vigumu sana kwa waume kuwaheshimu wake zao kwa njia hiyo? Hapana, Yehova hangeweza kamwe kuwaambia wafanye jambo ambalo hawawezi kufanya. Zaidi ya hayo, waabudu wa Yehova wanaweza kupata nguvu kuu zaidi katika ulimwengu wote—roho takatifu ya Mungu. Yesu alisema hivi: “Ikiwa ninyi, mjapokuwa waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!” (Luka 11:13) Waume wanaweza kumwomba Yehova katika sala awape roho yake ili iwasaidie wanaposhughulika na wengine, kutia ndani wake zao.—Soma Matendo 5:32.

19. Habari yetu inayofuata itazungumzia nini?

19 Kwa kweli, wanaume wana daraka zito la kujifunza jinsi ya kujitiisha chini ya Kristo na kuiga ukichwa wake. Lakini namna gani wanawake, hasa wale walioolewa? Habari inayofuata itazungumzia jinsi wanavyopaswa kuona daraka lao katika mpango wa Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Tunapaswa kuiga sifa gani za Yesu?

• Wazee wanapaswa kuwatendea kondoo namna gani?

• Mume anapaswa kumtendea mke wake jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mwige Yesu kwa kuwaheshimu wengine