Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wafundishe Watoto Wako

Watu Walioandika Kumhusu Yesu

Watu Walioandika Kumhusu Yesu

JE, UNAFURAHIA kusoma kumhusu Yesu?— * Watu fulani wanashangaa kujua kwamba Yesu hakuandika sehemu yoyote ya Biblia. Hata hivyo, waandikaji wanane wa Biblia waliandika habari nyingi sana kumhusu. Watu hao wote waliishi katika siku za Yesu na waliandika mambo aliyofundisha. Je, unajua majina ya watu hao wanane?— Wanne kati yao ni Mathayo, Marko, Luka, na Yohana. Wale wengine ni Petro, Yakobo, Yuda, na Paulo. Unajua mambo gani kuwahusu waandikaji hao?—

Tuzungumzie kwanza waandikaji watatu ambao ni baadhi ya mitume 12 wa Yesu. Je, unajua majina yao?— Majina yao ni Petro, Yohana, na Mathayo. Petro aliwaandikia Wakristo wenzake barua mbili. Aliwaeleza kuhusu mambo ambayo Yesu alifanya na kusema. Fungua Biblia yako na usome 2 Petro 1:16-18. Hapa Petro anaeleza kuhusu wakati ambapo alimsikia Yehova Mungu akisema na Yesu kutoka mbinguni.—Mathayo 17:5.

Mtume Yohana aliandika vitabu vitano vya Biblia. Alikaa karibu na Yesu wakati wa mlo wa mwisho ambao wanafunzi walikula pamoja na Bwana wao. Pia, Yesu alipokufa, Yohana alikuwa pamoja naye. (Yohana 13:23-26; 19:26) Yohana aliandika kimoja kati ya vitabu vinne vya Biblia vinavyoitwa Injili, ambavyo vinasimulia kuhusu maisha ya Yesu. Pia, aliandika kitabu cha Ufunuo kinachozungumzia maono ambayo Yesu alimpa, na barua tatu za Biblia zinazoitwa kwa jina lake. (Ufunuo 1:1) Mwandikaji wa tatu wa Biblia aliyekuwa mtume wa Yesu ni Mathayo. Alikuwa mkusanya-kodi kabla ya kuwa mwanafunzi wa Yesu.

Waandikaji wengine wawili wa Biblia walimjua Yesu kwa njia ya pekee. Waandikaji hao walikuwa watoto wa Maria na Yosefu, hivyo walikuwa ndugu wa kambo wa Yesu. (Mathayo 13:55) Mwanzoni, hawakuwa wanafunzi wa Yesu. Hata walifikiri kwamba alikuwa amerukwa na akili kwa sababu ya kuhubiri kwa bidii sana. (Marko 3:21) Hao ndugu zake walikuwa nani?— Mmoja wao ni Yakobo. Yeye aliandika kitabu cha Biblia cha Yakobo. Yule mwingine ni Yuda, naye aliandika kitabu cha Biblia cha Yuda.—Yuda 1.

Marko na Luka pia waliandika kuhusu maisha ya Yesu. Mama ya Marko anayeitwa Maria, alikaa katika nyumba kubwa Yerusalemu. Wakristo wa kwanza, kutia ndani Petro, walifanya mikutano nyumbani kwake. (Matendo 12:11, 12) Miaka kadhaa mapema, baada ya Yesu kula mlo wa Pasaka kwa mara ya mwisho pamoja na mitume wake, yaelekea Marko aliwafuata walipokuwa wakienda kwenye bustani ya Gethsemane usiku huo. Yesu alipokamatwa, askari-jeshi walijaribu kumkamata Marko pia, lakini akaponyoka na kuacha vazi lake.—Marko 14:51, 52.

Yaelekea Luka, aliyekuwa tabibu mwenye elimu nzuri, alipata kuwa mwanafunzi baada ya Yesu kufa. Alifanya utafiti kwa uangalifu kuhusu maisha ya Yesu, na akaandika simulizi sahihi na la waziwazi kuyahusu. Baadaye, Luka aliandamana na mtume Paulo katika safari zake, na pia aliandika kitabu cha Biblia cha Matendo.—Luka 1:1-3; Matendo 1:1.

Paulo ni mwandikaji wa Biblia wa nane aliyeandika kumhusu Yesu. Alielimishwa chini ya mwongozo wa wakili maarufu, Gamalieli. Paulo aliyeitwa Sauli wakati huo, alilelewa na kufundishwa na Mafarisayo. Aliwachukia wanafunzi wa Yesu na alishirikiana na watu waliowaua. (Matendo 7:58–8:3; 22:1-5; 26:4, 5) Unajua jinsi Paulo alivyojifunza kweli kumhusu Yesu?—

Paulo alikuwa njiani kwenda Damasko ili kuwakamata wanafunzi wa Yesu wakati ambapo nuru nyangavu kutoka mbinguni ilimpofusha ghafula. Akasikia sauti iliyomuuliza: “Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa?” Yesu ndiye aliyezungumza naye! Alimwambia Paulo aende Damasko. Halafu, Yesu akamwagiza mwanafunzi wake Anania aongee na Paulo, na Paulo akawa mwanafunzi wa Yesu. (Matendo 9:1-18) Paulo aliandika vitabu 14 vya Biblia, kuanzia Waroma mpaka Waebrania.

Je, umeanza kusoma vitabu vya Biblia kumhusu Yesu au umemwomba mtu akusomee vitabu hivyo?— Utanufaika sana ukianza sasa ukiwa mdogo kujifunza mambo ambayo Biblia inasema kumhusu Yesu.

^ fu. 3 Ikiwa unasoma pamoja na mtoto, kistari kirefu kinakukumbusha kwamba unapaswa kutua na kumtia moyo ajieleze.