Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kujua Jina la Mungu Kunahusisha Nini?

Kujua Jina la Mungu Kunahusisha Nini?

Kujua Jina la Mungu Kunahusisha Nini?

JE, JINA lako lina maana yoyote? Katika sehemu fulani za ulimwengu, kuna desturi ya kumpa mtoto jina ambalo lina maana. Jina hilo linaweza kuonyesha imani na mapendezi ya wazazi au mambo ambayo wanatarajia mtoto huyo atimize wakati ujao.

Zoea hilo la kuwapa watu majina yenye maana lilianza zamani. Nyakati za Biblia, watu walipewa majina kwa njia hiyo. Majina yangeweza kuonyesha kile ambacho mtu angetimiza maishani. Kwa mfano, Yehova alipokuwa akimwambia Daudi kuhusu mambo ambayo mwana wake Sulemani angetimiza alisema hivi: “Jina lake litakuwa Sulemani, [linalotokana na neno linalomaanisha “Amani”] nami nitaleta juu ya Israeli amani na utulivu katika siku zake.”—1 Mambo ya Nyakati 22:9.

Nyakati nyingine Yehova alimpa mtu jina jipya kwa sababu ya jukumu lake jipya. Mke wa Abrahamu aliyekuwa tasa alipewa jina Sara, linalomaanisha “Binti ya Mfalme.” Kwa nini? Yehova alieleza hivi: “Nami nitambariki yeye na pia nitakupa mwana kupitia yeye; nami nitambariki Sara naye atakuwa mataifa; wafalme wa vikundi vya watu watatoka kwake.” (Mwanzo 17:16) Ni wazi kwamba kuelewa ni kwa nini Sara alipewa jina jipya kungetia ndani kuelewa jukumu lake jipya.

Vipi kuhusu jina muhimu zaidi ya yote, yaani, Yehova? Linamaanisha nini? Musa alipomwuliza Mungu kuhusu jina lake, Yehova alimjibu: “Nitakuwa kile nitakachokuwa.” (Kutoka 3:14) Tafsiri ya Rotherham inasema: “Nitakuwa chochote Nipendacho kuwa.” Jina la Yehova linafunua kwamba yeye ni Mungu anayetimiza majukumu mengi. Fikiria mfano huu: Kila siku mama anaweza kutimiza majukumu mengi kama vile, kutenda kama mwuguzi, mpishi, na hata mwalimu, anapowatunza watoto wake. Ndivyo ilivyo na Yehova, ingawa yeye anatimiza majukumu mengi zaidi. Ili kutimiza kusudi lake kwa wanadamu, anaweza kuwa chochote anachotaka ili atimize jukumu linalohitajika. Kwa hiyo, kujua maana ya jina la Yehova kunahusisha kuelewa na kuheshimu majukumu yake mengi.

Kwa kusikitisha, watu ambao hawajui maana ya jina la Mungu hawawezi kujua utu wake wenye kupendeza. Hata hivyo, kwa kujifunza Biblia, unaweza kuthamini majukumu ya Yehova akiwa Mshauri mwenye hekima, Mkombozi mwenye nguvu, na Mwandalizi mkarimu, na kadhalika. Kwa kweli, jina la Mungu lina maana yenye kutia kicho.

Hata hivyo, si rahisi kujua maana ya jina la Mungu. Habari inayofuata itaeleza sababu.