Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kumsaidia Rafiki Aliye Mgonjwa

Jinsi ya Kumsaidia Rafiki Aliye Mgonjwa

Jinsi ya Kumsaidia Rafiki Aliye Mgonjwa

JE, UMEWAHI kukosa maneno ya kusema ulipokuwa ukizungumza na rafiki mgonjwa sana? Uwe na uhakika kwamba unaweza kushinda tatizo hilo. Jinsi gani? Hakuna sheria hususa za kufuata. Huenda tamaduni zikatofautiana. Huenda watu wakawa na nyutu tofauti. Kwa hiyo, jambo linaloweza kumfariji mgonjwa fulani huenda lisimfariji mwingine. Na pia huenda hali na hisia za mtu zikabadilika siku baada ya siku.

Kwa hiyo, jambo muhimu unalopaswa kufanya ni kujitia katika hali yake na kutambua kile anachohitaji kutoka kwako. Unaweza kufanya hivyo jinsi gani? Madokezo yanayofuata yanategemea kanuni za Biblia.

Msikilize kwa makini

KANUNI ZA BIBLIA:

“Kila mtu lazima awe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema.”YAKOBO 1:19.

“Kuna wakati . . . wa kukaa kimya na wakati wa kusema.”MHUBIRI 3:1, 7.

▪ Unapomtembelea rafiki aliye mgonjwa, msikilize kwa makini na kwa huruma. Usifanye haraka kutoa shauri au suluhisho. Kwa sababu ukifanya hivyo huenda ukamwumiza bila kukusudia. Rafiki yako hatafuti suluhisho, bali anatafuta mtu wa kumsikiliza.

Mruhusu rafiki yako ajieleze kwa uhuru. Usimkatize na kufanya hali yake ionekane kuwa ya kawaida kwa kutumia maneno ambayo watu wamezoea kutumia. “Nilipatwa na homa ya uti wa mgongo iliyofanya niwe kipofu,” anasema Emílio. * “Wakati mwingine mimi hushuka moyo sana, na marafiki hujaribu kunifariji kwa kusema: ‘Si wewe tu uliye na matatizo. Kuna watu walio na matatizo makubwa kuliko yako.’ Hata hivyo, hawajui kwamba kufanya ugonjwa wangu uonekane kuwa jambo ndogo hakunisaidii. Badala yake kunanifanya nikate tamaa.”

Mruhusu rafiki yako aeleze hisia zake kwa uhuru bila kuogopa kuchambuliwa. Akikwambia kuwa ana woga, kubaliana naye badala ya kumwambia tu asiogope. Eliana anayeugua kansa, anasema hivi: “Ninaposhikwa na woga kwa sababu ya hali yangu na kuanza kulia, hilo halimaanishi kwamba nimeacha kumtegemea Mungu.” Jaribu kumwona rafiki yako jinsi alivyo, na si unavyotaka awe. Kumbuka kwamba maneno yako yanaweza kumuudhi kwa urahisi na kwamba hayuko katika hali yake ya kawaida. Uwe mwenye subira. Msikilize—hata kama atasema mambo yaleyale tena na tena. (1 Wafalme 19:9, 10, 13, 14) Huenda akataka kukueleza hisia zake.

Onyesha hisia-mwenzi na uwe mwenye kujali

KANUNI ZA BIBLIA:

“Shangilieni pamoja na watu wanaoshangilia; lieni pamoja na watu wanaolia.”WAROMA 12:15.

“Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.”MATHAYO 7:12.

▪ Jiweke katika hali ya rafiki yako. Ikiwa rafiki yako anajitayarisha kwa ajili ya upasuaji, au anapata matibabu, au anangojea matokeo ya uchunguzi fulani, huenda akawa na wasiwasi mwingi na hisia nyepesi. Jaribu kutambua jambo hilo na ubadilikane kulingana na hisia zake. Huo si wakati wa kumwuliza maswali mengi hasa yale ya kibinafsi.

Mwanasaikolojia Ana Katalifós anasema hivi: “Waruhusu wagonjwa wazungumze kuhusu ugonjwa wao iwapo wanataka kufanya hivyo na bila kuwaharakisha. Ikiwa wanataka kuongea, zungumza nao kuhusu jambo wanalochagua. Lakini ikiwa hawataki kuzungumza, unaweza tu kuketi na unyamaze, kisha ushike mkono wao kwa urafiki. Au hata labda anataka tu mtu wa kumfariji anapolia.”

Usiingilie faragha ya rafiki yako. Mwandishi Rosanne Kalick ambaye ameugua na kupona kansa mara mbili, anaandika hivi: “Unapomsaidia rafiki yako, tambua kwamba jambo lolote analokuambia ni siri. Isipokuwa uwe umeombwa kuzungumza kwa niaba ya familia, usitoe habari zozote. Mwulize mgonjwa mambo ambayo angetaka uwaambie watu wengine.” Edson ambaye aliugua kansa kisha akapona anasema hivi: “Rafiki fulani alieneza uvumi kwamba nina kansa na sitaishi kwa muda mrefu. Nilikuwa nimefanyiwa upasuaji. Nilijua nina kansa, lakini nilikuwa ninasubiri matokeo ya uchunguzi wa tishu zilizokuwa zimetolewa na kupelekwa kwenye maabara. Kansa haikuwa imeenea. Lakini tayari uvumi ulikuwa umeenezwa. Mke wangu aliumizwa sana na maneno na maswali yasiyo ya fadhili.”

Ikiwa rafiki yako anachunguza kwa uangalifu ili aamue aina ya matibabu atakayotumia, usiseme kile ungefanya ikiwa ungekuwa katika hali yake. Mwandishi Lori Hope ambaye aliugua kansa na akapona anasema: “Ni vizuri kumwuliza mgonjwa ambaye anaugua kansa au wakati mmoja aliugua kansa ikiwa angependa kusoma habari fulani kabla hujampa habari hiyo. La sivyo, huenda ukamwumiza rafiki yako bila kujua.” Si kila mtu anayefurahia kupewa habari chungu nzima kuhusu matibabu mbalimbali.

Hata ikiwa wewe ni rafiki wa karibu, usikae kwa muda mrefu unapomtembelea mgonjwa. Ingawa ni muhimu kumtembelea rafiki yako, huenda asitake ukae sana. Labda amechoka sana na hana nguvu za kuzungumza au hata kukusikiliza kwa muda mrefu. Kwa upande mwingine, usionyeshe kuwa una haraka. Rafiki yako anahitaji kuona kuwa unamjali sana.

Ili umwonyeshe kwamba unajali unahitaji kuwa na usawaziko na busara. Kwa mfano, kabla ya kumpikia chakula au hata kumpelekea maua, mwulize ikiwa maua au chakula hicho humdhuru. Ikiwa una mafua au ugonjwa mwingine, lingekuwa jambo la fadhili kungojea hadi upone kabla ya kumtembelea rafiki yako.

Uwe mwenye kujenga

KANUNI ZA BIBLIA:

“Ulimi wa mwenye hekima huponya.” METHALI 12:18.

“Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi.”WAKOLOSAI 4:6.

▪ Ikiwa una mtazamo unaofaa kumwelekea rafiki yako aliye mgonjwa, maneno yako na matendo yako yatathibitisha jambo hilo. Usimwone rafiki yako kana kwamba ni mtu mwingine, kwani bado ana sifa zilezile zilizokuvutia mara ya kwanza. Usiruhusu ugonjwa wake uathiri uhusiano wenu. Ikiwa utazungumza na rafiki yako kana kwamba hajiwezi ataanza kujiona hivyo. Roberta, ambaye amerithi ugonjwa wa mifupa usio wa kawaida, anasema hivi: “Nitendee kama mtu wa kawaida. Hata ingawa nimelemaa bado nina maoni na mapendezi yangu. Usinihurumie kupita kiasi. Usizungumze nami kana kwamba mimi ni mjinga.”

Uwe mwangalifu kuhusu yale unayosema na pia jinsi unavyoyasema. Pia, sauti yako inaweza kumwathiri. Muda mfupi baada ya kugunduliwa kwamba ana kansa, Ernesto alipokea simu kutoka kwa rafiki yake anayeishi ng’ambo aliyesema hivi: “Siamini kwamba wewe una kansa!” Ernesto anaendelea kusema hivi: “Sauti ambayo rafiki yangu alitumia kusema ‘wewe’ na ‘kansa’ ilinitia hofu sana.”

Mwandishi Lori Hope, anatoa mfano mwingine: “Kuuliza ‘Unahisi namna gani?’ kunaweza kumaanisha mambo mengi kwa mgonjwa. Swali hilo linaweza kumtuliza, kumwumiza, au kumfanya mgonjwa awe na hofu ikitegemea sauti ya mwenye kuuliza, ishara za mwili, uhusiano wake na mgonjwa, na hali ya mgonjwa wakati huo.”

Rafiki mgonjwa anataka kuhisi kwamba watu wanamjali, wanamwelewa, na kumheshimu. Kwa hiyo, mhakikishie kuwa yeye ni muhimu kwako na uko tayari kumsaidia wakati wowote. Rosemary aliye na uvimbe kwenye ubongo anasema hivi: “Nilitiwa moyo sana rafiki zangu waliponiambia kuwa wananipenda na kuwa wako tayari kunisaidia wakati wowote ule.”—Methali 15:23; 25:11.

Msaidie

KANUNI YA BIBLIA:

“Acheni tupendane, si kwa neno wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.”1 YOHANA 3:18.

▪ Mahitaji ya mgonjwa yatabadilika baada ya kupimwa na kuanza matibabu yake. Lakini, wakati huu wote huenda atahitaji msaada. Badala ya kumwambia kijuujuu tu eti “niite ukihitaji chochote,” mwambie kihususa msaada unaoweza kutoa. Unaweza kuonyesha kwamba unamjali kwa kumsaidia kufanya kazi za kila siku kama vile, kupika, kufanya usafi, kufua nguo, kupiga pasi, kununua vitu dukani, na kumpeleka hospitali. Uwe mwenye kutegemeka na utunze wakati. Fanya kila kitu ulichomwahidi.—Mathayo 5:37.

“Chochote tunachofanya, kiwe kidogo au kikubwa, kitamsaidia mgonjwa anapopata nafuu,” anasema mwandishi Rosanne Kalick. Sílvia ambaye amewahi kuugua kansa mara mbili na kupona anaunga mkono wazo hilo. “Marafiki tofauti-tofauti walionipeleka kila siku kwenye mji mwingine kwa ajili ya matibabu walinifanya nihisi nimetulia na kufarijika! Njiani, tuliongea kuhusu mambo mbalimbali, na tulipokuwa tukirudi tulisimama kwenye mkahawa. Hilo lilinifanya nihisi kuwa mtu wa kawaida.”

Usifikiri kwamba unajua kila kitu ambacho rafiki yako anahitaji. “Uliza kila wakati anachohitaji,” anadokeza Kalick. Pia anaongezea: “Unapomsaidia usimfanyie kila kitu. Kwa kuwa hilo linaweza kumfadhaisha. Ukinifanyia kila kitu, hilo litaonyesha kuwa sijiwezi. Ninahitaji kuhisi kuwa nina uwezo wa kufanya mambo fulani. Sitaki kujihisi dhaifu sana. Nisaidie kufanya kile ninachoweza.”

Huenda rafiki yako anahitaji kuhisi kuwa anaweza kutimiza mambo fulani. Adilson, aliye na UKIMWI, anasema hivi: “Unapokuwa mgonjwa hutaki kutengwa na wengine kana kwamba huwezi kufanya lolote. Unataka kusaidia hata kama ni kufanya jambo dogo sana. Ni vizuri kujihisi kuwa bado unaweza kufanya mambo fulani! Hilo hukutia moyo kuendelea kuishi. Mimi hupenda watu waniruhusu nifanye maamuzi yangu na waheshimu maamuzi hayo. Kuwa mgonjwa hakumaanishi kuwa hatuwezi kutimiza majukumu mbalimbali kama vile kuwa baba, mama, na kadhalika.”

Dumisha uhusiano wa karibu

KANUNI YA BIBLIA:

Kwa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.”METHALI 17:17.

▪ Ikiwa huwezi kumtembelea rafiki yako kwa sababu unaishi mbali au kwa sababu ya hali nyingine, unaweza kumpigia simu, kumwandikia barua, au kumtumia barua-pepe. Utaandika kuhusu nini? Alan D. Wolfelt, mshauri wa kuwasaidia watu wenye huzuni anasema hivi: “Mkumbushe kuhusu mambo mliyofurahia pamoja. Mwambie kuwa utamwandikia . . . tena hivi karibuni na uhakikishe kuwa unafanya hivyo.”

Usisite kumtia moyo rafiki anayeugua ukihofia kuwa huenda ukasema jambo lisilofaa au ukakosea. Mara nyingi, kumtembelea kunaonyesha kuwa unamjali. Lori Hope anaandika hivi katika kitabu chake: “Sisi sote husema au kufanya mambo ambayo yanaweza kueleweka vibaya au kumwumiza mtu bila kukusudia. Hilo si tatizo. Tatizo hutokea tunapoogopa sana kukosea hivi kwamba hatumtembelei rafiki anayetuhitaji.”

Rafiki ambaye ni mgonjwa sana huenda akahitaji msaada wako sasa kuliko wakati mwingine wowote. Jithibitishe kuwa “rafiki wa kweli.” Huenda usiondoe maumivu yake, lakini unaweza kumsaidia mtu unayempenda akabiliane na hali yake ngumu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Baadhi ya majina yamebadilishwa.