Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yeye Hutafuta Mema Ndani Yetu

Yeye Hutafuta Mema Ndani Yetu

Mkaribie Mungu

Yeye Hutafuta Mema Ndani Yetu

1 WAFALME 14:13

“YEHOVA anaichunguza mioyo yote, naye anatambua kila mwelekeo wa fikira.” (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Maneno hayo yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu, yanatuchochea tuthamini sana jinsi Yehova anavyotujali. Yehova hutafuta mema katika mioyo yetu hata ingawa sisi si wakamilifu. Hilo linaonekana wazi katika maneno ambayo Mungu alisema kumhusu Abiya kwenye 1 Wafalme 14:13.

Familia ya Abiya walikuwa waovu. Baba yake, Yeroboamu, alikuwa kiongozi wa ukoo wenye kuasi. * Yehova alikusudia kuangamiza kabisa nyumba ya Yeroboamu “kama vile mtu anavyoondoa mavi.” (1 Wafalme 14:10) Lakini Mungu aliamuru kwamba mtu mmoja wa familia ya Yeroboamu, Abiya ambaye alikuwa mgonjwa sana, azikwe kwa heshima. * Kwa nini? Mungu alieleza hivi: “Kwa maana jambo fulani jema kwa Yehova Mungu wa Israeli limeonekana ndani yake katika nyumba ya Yeroboamu.” (1 Wafalme 14:1, 12, 13) Maneno haya yanatufunza nini kumhusu Abiya?

Biblia haisemi kwamba Abiya alikuwa mwabudu mwaminifu wa Mungu. Lakini bado kulikuwa na wema fulani ndani yake. Wema huo ulikuwa “kwa Yehova,” labda ulihusisha ibada Yake. Waandishi wa Kirabi wanadokeza kwamba Abiya alifunga safari kwenda kuabudu kwenye hekalu Yerusalemu au kwamba aliwaondoa askari ambao baba yake alikuwa ameweka kuwazuia Waisraeli wasiende Yerusalemu.

Ingawa hatujui Abiya alioonyesha wema gani, wema wake ulitambuliwa. Kwanza, ulikuwa wa kweli. Wema huo ulikuwa “ndani yake,” yaani, ndani ya moyo wake. Pili, ulikuwa wa pekee. Abiya alionyesha wema huo ingawa alikuwa “katika nyumba ya Yeroboamu.” Msomi mmoja anasema hivi: “Wanaume wanaoendelea kuonyesha wema hata ingawa wanaishi mahali na katika familia mbaya wanapaswa kupongezwa sana.” Msomi mwingine anasema kwamba wema wa Abiya “ulionekana wazi . . . , kama vile tu nyota hung’aa zaidi wakati anga ni nyeusi, na mierezi hupendeza zaidi wakati miti inayoizunguka haina majani.”

Jambo muhimu hata zaidi ni kwamba maneno ya 1 Wafalme 14:13 yanatuambia jambo lenye kupendeza kumhusu Yehova na kile ambacho yeye hutafuta ndani yetu. Kumbuka kwamba jambo fulani jema ‘lilionekana ndani ya’ Abiya. Inaonekana kwamba Yehova aliuchunguza moyo wa Abiya mpaka akapata kiasi fulani cha wema. Kama msomi mmoja alivyosema, akilinganishwa na familia yao, Abiya alikuwa kama lulu pekee “katika rundo la mawe.” Yehova alithamini sana wema wake na kumthawabisha kwa kumwonyesha rehema mtu huyo aliyetoka katika familia ya watu waovu.

Je, haifariji kujua kwamba Yehova hutafuta na kuthamini wema ulio ndani yetu licha ya sisi kuwa watu wasio wakamilifu? (Zaburi 130:3) Kujua hilo kunapaswa kutuchochea tumkaribie zaidi Yehova, Mungu anayechunguza moyo wetu kwa uangalifu akitafuta wema hata uwe wa kiasi kidogo namna gani.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Yeroboamu alikuwa ameanzisha ibada ya ndama katika ufalme wa kaskazini wa yale makabila kumi ya Israeli ili kuwazuia watu wasiende kumwabudu Yehova hekaluni huko Yerusalemu.

^ fu. 2 Katika nyakati za Biblia kukosa kuzikwa kwa heshima kulionyesha kwamba mtu hakuwa na kibali cha Mungu.—Yeremia 25:32, 33.