Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yale Ambayo Siku ya Yehova Itafunua

Yale Ambayo Siku ya Yehova Itafunua

Yale Ambayo Siku ya Yehova Itafunua

“Siku ya Yehova itakuja kama mwizi, . . . na dunia na kazi zilizo ndani yake zitafunuliwa.”—2 PET. 3:10.

1, 2. (a) Mfumo mwovu wa mambo wa sasa utaisha jinsi gani? (b) Tutachunguza maswali gani?

MFUMO mwovu wa mambo wa sasa umefanyizwa juu ya msingi wa uwongo wa kwamba mwanadamu anaweza kuitawala dunia kwa mafanikio bila kumtegemea Yehova. (Zab. 2:2, 3) Je, jambo lolote ambalo limefanyizwa juu ya msingi wa uwongo linaweza kudumu milele? Bila shaka hapana! Hata hivyo, hatutazamii kwamba ulimwengu wa Shetani utajiangamiza wenyewe. Badala yake, utaharibiwa na Mungu kwa wakati aliochagua na kwa njia yake. Matendo ya Mungu ya kuuharibu ulimwengu huu mwovu yataonyesha kikamili haki yake na pia upendo wake.—Zab. 92:7; Met. 2:21, 22.

2 Mtume Petro aliandika hivi: “Siku ya Yehova itakuja kama mwizi, ambayo katika hiyo mbingu zitapitilia mbali kwa kelele ya kuvuma, lakini vitu vyake vya msingi vikiwa moto sana vitayeyushwa, na dunia na kazi zilizo ndani yake zitafunuliwa.” (2 Pet. 3:10) “Mbingu” na “dunia” zinazotajwa hapa ni nini? ‘Vitu vya msingi’ ambavyo vitayeyushwa ni nini? Na Petro alimaanisha nini aliposema kwamba “dunia na kazi zilizo ndani yake zitafunuliwa”? Kujua majibu ya maswali au maulizo hayo kutatusaidia kujitayarisha kwa ajili ya matukio yenye kuogopesha ambayo yatatokea hivi karibuni.

Mbingu na Dunia Ambazo Zitapitilia Mbali

3. “Mbingu” zinazotajwa kwenye andiko la 2 Petro 3:10 ni nini, na zitapitilia mbali jinsi gani?

3 Katika Biblia, neno “mbingu” linapotumiwa kwa njia ya mfano, mara nyingi linamaanisha mamlaka zinazotawala ambazo zimeinuliwa juu ya raia zake. (Isa. 14:13, 14; Ufu. 21:1, 2) “Mbingu [ambazo] zitapitilia mbali” zinafananisha utawala wa wanadamu juu ya jamii isiyomwogopa Mungu. Kupitilia mbali kwa utawala huo kwa ‘kelele nyingi inayovuma’—au kwa “kishindo kikuu,” kama tafsiri nyingine inavyosema—huenda kunamaanisha kuangamizwa kwa ghafula kwa mbingu hizo.

4. “Dunia” ni nini, nayo itaharibiwa jinsi gani?

4 “Dunia” inafananisha ulimwengu wa wanadamu uliotengwa mbali na Mungu. Ulimwengu kama huo ulikuwepo katika siku za Noa, Mungu akaamuru uangamizwe kupitia Gharika. “Kwa neno hilohilo mbingu na dunia za sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto nazo zinahifadhiwa mpaka ile siku ya hukumu na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.” (2 Pet. 3:7) Ingawa Gharika iliwaangamiza watu wote wasiomwogopa Mungu kwa wakati mmoja, uharibifu unaokuja utatukia hatua kwa hatua wakati wa “ile dhiki kuu.” (Ufu. 7:14) Katika hatua ya kwanza ya dhiki hiyo, Mungu atawachochea viongozi wa kisiasa wa ulimwengu huu waharibu “Babiloni Mkubwa,” na hivyo kuonyesha kwamba amechukizwa na kahaba huyo wa kidini. (Ufu. 17:5, 16; 18:8) Kisha, katika vita vya Har–Magedoni, ambavyo vitakuwa hatua ya mwisho ya ile dhiki kuu, Yehova mwenyewe ataondolea mbali sehemu inayobaki ya ulimwengu wa Shetani.—Ufu. 16:14, 16; 19:19-21.

‘Vitu vya Msingi Vitayeyushwa’

5. Vitu vya msingi vya mfano vinatia ndani nini?

5 ‘Vitu vya msingi’ ambavyo “vitayeyushwa” ni nini? Kamusi moja ya Biblia inasema kwamba “vitu vya msingi” ni “kanuni za kwanza,” au “misingi.” Kamusi hiyo inasema kwamba maneno hayo “yalitumiwa kuonyesha herufi za alfabeti, ambazo zilikuwa misingi ya maneno.” Kwa hiyo, ‘vitu vya msingi’ ambavyo vinatajwa na Petro vinafananisha mambo ya msingi yanayofanya ulimwengu uwe na tabia, mielekeo, njia za kufanya mambo, na miradi isiyompendeza Mungu. ‘Vitu hivyo vya msingi’ vinatia ndani “roho ya ulimwengu,” ambayo “hutenda katika wana wa kutotii.” (1 Kor. 2:12; soma Waefeso 2:1-3.) Roho hiyo, au “hewa,” imeenea katika ulimwengu wa Shetani. Inawachochea watu wafikiri, wafanye mipango, waseme, na kutenda kwa njia ambayo inapatana na fikira za Shetani, ambaye ni “mtawala wa mamlaka ya hewa” mwenye kiburi na mwasi.

6. Roho ya ulimwengu inaonekana jinsi gani?

6 Kwa hiyo, wawe wanajua au hawajui, watu wanaoongozwa na roho ya ulimwengu wanaruhusu akili na mioyo yao iongozwe na Shetani, na hivyo wanafikiri na kuwa na mtazamo kama wake. Matokeo ni kwamba wanafanya jinsi wanavyotaka, bila kujali mapenzi ya Mungu. Katika hali mbalimbali, wanatenda kwa kuchochewa na kiburi au uchoyo, wanaonyesha roho ya uasi kuelekea mamlaka, na wanaruhusu waongozwe na “tamaa ya mwili na tamaa ya macho.”—Soma 1 Yohana 2:15-17. *

7. Kwa nini ni lazima ‘tuulinde moyo wetu’?

7 Hivyo basi, ni jambo la maana kama nini kwetu ‘kuulinda moyo wetu’ kwa kutumia hekima inayotoka kwa Mungu tunapochagua marafiki, vitabu tunavyosoma, burudani, na Tovuti au vituo ambavyo huenda tunatazama kwenye Intaneti! (Met. 4:23) Mtume Paulo aliandika hivi: “Mjihadhari: labda kuna mtu ambaye atawachukua ninyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyifu mtupu kulingana na pokeo la wanadamu, kulingana na mambo ya msingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.” (Kol. 2:8) Himizo hilo linazidi kuwa la maana sana kadiri siku ya Yehova inavyozidi kukaribia, kwa kuwa ‘joto’ lisilo na kifani la siku hiyo litayeyusha kabisa ‘vitu vyote vya msingi’ vya mfumo wa Shetani, na kufunua kwamba haviwezi kabisa kustahimili joto la hasira ya Yehova. Hilo linatukumbusha maneno ya andiko la Malaki 4:1: “Siku ile inakuja ambayo inawaka kama tanuru, na wote wenye kimbelembele na wote wanaotenda uovu watakuwa kama majani makavu. Na siku hiyo inayokuja itawateketeza.”

“Dunia na Kazi Zilizo Ndani Yake Zitafunuliwa”

8. Dunia na kazi zake “zitafunuliwa” jinsi gani?

8 Petro alimaanisha nini alipoandika kwamba “dunia na kazi zilizo ndani yake zitafunuliwa”? Neno “zitafunuliwa” linaweza pia kutafsiriwa “zitafichuliwa” au “zitawekwa wazi.” Petro alimaanisha kwamba wakati wa ile dhiki kuu, Yehova atafunua wazi ulimwengu wa Shetani, na ataonyesha waziwazi kwamba unampinga Yeye na Ufalme Wake na hivyo unastahili kuharibiwa. Likizungumzia kwa njia ya unabii kuhusu wakati huo, andiko la Isaya 26:21 linasema hivi: “Yehova anakuja kutoka mahali pake ili kulitoza hesabu kosa la mkaaji wa nchi juu yake, na nchi hakika itafunua umwagaji wake wa damu wala haitawafunika tena watu wake waliouawa.”

9. (a) Tunapaswa kukataa nini, na kwa nini? (b) Tunapaswa kusitawisha sifa gani, na kwa nini?

9 Wakati wa siku ya Yehova, wale ambao wamefinyangwa na ulimwengu na roho yake mbovu wataonyesha jinsi walivyo kikweli, hata watachinjana wenyewe kwa wenyewe. Kwa kweli, inawezekana kwamba aina mbalimbali za burudani zenye jeuri ambazo zimeenea sana leo zinazoeza akili za wengi kwa ajili ya wakati ambapo mkono wa kila mtu “utainuka juu ya mkono wa mwenzake.” (Zek. 14:13) Hivyo basi, ni jambo la maana kama nini kwetu tuepuke kitu chochote kama vile sinema, vitabu, michezo ya video, na kadhalika, ambacho kinaweza kukuza ndani yetu tabia zinazomchukiza Mungu, kama vile kiburi na kupenda jeuri! (2 Sam. 22:28; Zab. 11:5) Badala yake, acheni tusitawishe sifa za tunda la roho takatifu ya Mungu, kwa kuwa sifa hizo zitastahimili joto kali la siku ya Yehova.—Gal. 5:22, 23.

“Mbingu Mpya na Dunia Mpya”

10, 11. “Mbingu mpya” na “dunia mpya” ni nini?

10 Soma 2 Petro 3:13. “Mbingu mpya” ni Ufalme wa Mungu wa kimbingu, ambao ulisimamishwa mwaka wa 1914 wakati “nyakati zilizowekwa za mataifa” zilipokwisha. (Luka 21:24) Serikali hiyo ya kifalme inatia ndani Kristo Yesu na watawala wenzake 144,000, ambao wengi kati yao tayari wamepokea zawadi au tuzo lao la kimbingu. Katika kitabu cha Ufunuo, watu hao waliochaguliwa wanafananishwa na “lile jiji takatifu, Yerusalemu Jipya, likishuka kutoka mbinguni kwa Mungu na limetayarishwa kama bibi-arusi aliyepambwa kwa ajili ya mume wake.” (Ufu. 21:1, 2, 22-24) Kama vile tu Yerusalemu la kidunia lilivyokuwa kitovu cha serikali ya Israeli la kale, Yerusalemu Jipya na Bwana-arusi wake wanafanyiza serikali ya mfumo mpya wa mambo. Jiji hilo la kimbingu ‘litashuka kutoka mbinguni’ kwa kuilekezea dunia uangalifu.

11 “Dunia mpya” inamaanisha jamii mpya ya kidunia ya wanadamu ambao watakuwa wameonyesha kwamba wanajitiisha kwa kupenda chini ya Ufalme wa Mungu. Paradiso ya kiroho ambayo watu wa Mungu wanafurahia hata sasa, mwishowe itakuwa katika mazingira yanayofaa kabisa katika ‘dunia hiyo maridadi yenye kukaliwa inayokuja.’ (Ebr. 2:5) Tunaweza jinsi gani kuwa sehemu ya mfumo huo mpya wa mambo?

Jitayarishe kwa Ajili ya Siku Kuu ya Yehova

12. Kwa nini siku ya Yehova itaushtua ulimwengu?

12 Paulo na Petro walitabiri kwamba siku ya Yehova ingekuja “kama mwizi”—kimyakimya, bila kutazamiwa. (Soma 1 Wathesalonike 5:1, 2.) Hata Wakristo wa kweli, ambao wanaingojea siku hiyo, watashangazwa na jinsi itakavyotokea kwa ghafula. (Mt. 24:44) Hata hivyo, ulimwengu utapatwa na mshangao hata zaidi. Paulo aliandika hivi: “Wakati [watu waliotengwa mbali na Yehova] watakapokuwa wakisema: ‘Amani na usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafula utakapokuwa juu yao mara moja kama vile maumivu ya taabu juu ya mwanamke mwenye mimba; nao hawataponyoka hata kidogo.”—1 The. 5:3.

13. Tunaweza jinsi gani kuepuka kudanganywa na mwito wa “Amani na usalama!”?

13 Mwito wa “Amani na usalama!” utakuwa mbinu nyingine tu ya uwongo unaoenezwa na roho waovu, lakini watumishi wa Yehova hawatadanganyika. Paulo aliandika hivi: “Hamko gizani, hivi kwamba siku hiyo iwafikie ninyi kama vile ambavyo ingewafikia wezi, kwa maana ninyi nyote ni wana wa nuru na wana wa mchana.” (1 The. 5:4, 5) Kwa hiyo, acheni tukae katika nuru, mbali kabisa na giza la ulimwengu wa Shetani. Petro aliandika hivi: “Wapendwa, mkiwa na ujuzi huu wa kimbele, jilindeni ili msichukuliwe mbali pamoja nao [walimu wa uwongo ndani ya kutaniko la Kikristo] kwa kosa la watu wanaokaidi sheria, mwanguke kutoka kwenye uimara wenu wenyewe.”—2 Pet. 3:17.

14, 15. (a) Yehova ameonyesha jinsi gani kwamba anatuheshimu? (b) Ni maneno gani yaliyoongozwa na roho ya Mungu ambayo tunapaswa kuchukua kwa uzito?

14 Ona kwamba Yehova hatuambii tu ‘tujilinde’ bila kutuambia jambo lingine lolote. Badala yake, anaonyesha kwamba anatuheshimu kwa kutupatia kwa fadhili ‘ujuzi wa kimbele,’ yaani, anatueleza kwa ujumla mambo yatakayotukia wakati ujao.

15 Hata hivyo, kwa kusikitisha wengine hawajali au hata wanapuuza vikumbusho vya kuendelea kukaa macho. Huenda wakasema, ‘Tumesikia kikumbusho hichohicho kwa makumi ya miaka.’ Hata hivyo, watu hao wanapaswa kukumbuka kwamba kwa kusema maneno kama hayo, kwa kweli wanamtilia shaka Yehova na Mwana wake, si jamii ya mtumwa mwaminifu tu. Yehova alisema hivi: “Endelea kuyatarajia.” (Hab. 2:3) Vivyo hivyo, Yesu alisema: “Endeleeni kukesha kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja.” (Mt. 24:42) Zaidi ya hayo, Petro aliandika hivi: “Mnapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu, mkingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova!” (2 Pet. 3:11, 12) Sikuzote, jamii ya mtumwa mwaminifu na Baraza lake Linaloongoza hawatapuuza kamwe maneno hayo ya kweli!

16. Tunapaswa kuepuka mtazamo gani, na kwa nini?

16 Kwa kweli, ‘mtumwa mwovu’ ndiye anayeamua kwamba Bwana wake anakawia. (Mt. 24:48) Mtumwa huyo mwovu ni sehemu ya kikundi kinachozungumziwa katika andiko la 2 Petro 3:3, 4. Petro aliandika hivi: “Katika siku za mwisho watakuja wadhihaki” ambao “kulingana na tamaa zao wenyewe,” wanawadhihaki wale wanaotii na kuendelea kuingojea siku ya Yehova. Ndiyo, badala ya kukazia fikira mambo ya Ufalme, wadhihaki hao wanajifikiria wao wenyewe na tamaa zao za kichoyo. Na tusikuze kamwe mtazamo huo wa kutotii na ulio hatari! Badala yake, acheni ‘tuone subira ya Bwana wetu kuwa wokovu’ kwa kuendelea kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi na tuepuke kuhangaika kupita kiasi tukitaka kujua wakati wa matukio yanayohusiana na siku ya Yehova, jambo ambalo ni Yehova Mungu tu anayejua.—2 Pet. 3:15; soma Matendo 1:6, 7.

Mtumaini Mungu wa Wokovu

17. Wakristo waaminifu walitenda jinsi gani kupatana na agizo la Yesu la kukimbia kutoka Yerusalemu, na kwa nini?

17 Baada ya majeshi ya Roma kuvamia Yudea katika mwaka wa 66 W.K., Wakristo waaminifu walitii himizo la Yesu la kukimbia kutoka katika jiji la Yerusalemu bila kukawia. (Luka 21:20-23) Kwa nini walifanya uamuzi na kuchukua hatua haraka? Ni wazi kwamba walikumbuka onyo la Yesu. Bila shaka, walitazamia kwamba uamuzi wao ungetokeza hali ngumu, kama vile Kristo alivyokuwa ameonya mapema. Lakini wakati huohuo, walijua kwamba Yehova hawezi kamwe kuwaacha watu wake washikamanifu.—Zab. 55:22.

18. Maneno ya Yesu katika andiko la Luka 21:25-28 yanakufanya uwe na maoni gani kuhusu ile dhiki kuu inayokuja?

18 Ni lazima sisi pia tumtumaini kabisa Yehova, kwa sababu ni yeye tu atakayetuokoa wakati mfumo huu wa mambo utakapopatwa na dhiki iliyo kuu zaidi katika historia yote ya wanadamu. Wakati fulani baada ya dhiki kuu kuanza lakini kabla ya Yehova kutekeleza hukumu juu ya ulimwengu wote, watu ‘watazimia kwa woga na tarajio la mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa.’ Hata hivyo, huku maadui wa Mungu wakitetemeka kwa sababu ya woga, watumishi washikamanifu wa Yehova hawatakuwa na hofu. Badala yake, watashangilia kwa sababu wanajua kwamba ukombozi wao unakaribia.—Soma Luka 21:25-28.

19. Ni nini kitakachozungumziwa katika habari inayofuata?

19 Ndiyo, ni wakati wenye kusisimua kama nini ambao unawangojea wale wanaoendelea kujitenga na ulimwengu na “vitu vyake vya msingi”! Hata hivyo, kama habari inayofuata itakavyoonyesha, ikiwa tunataka kupata uzima, ni lazima tufanye mengi zaidi ya kuepuka tu mambo mabaya. Tunahitaji kukuza sifa zinazompendeza Yehova na kufanya mambo yanayokubalika machoni pake.—2 Pet. 3:11.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Kwa maelezo kamili kuhusu tabia zinazochochewa na roho ya ulimwengu, ona kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, ukurasa wa 246-250.

Je, Unaweza Kueleza?

• Ni nini kinachofananishwa na . . .

“mbingu na dunia” za sasa?

‘vitu vya msingi’?

“mbingu mpya na dunia mpya”?

• Kwa nini tunamtumaini kabisa Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 5]

Unaweza jinsi gani ‘kuulinda moyo wako’ na kuendelea kujitenga na ulimwengu?

[Picha katika ukurasa wa 6]

Tunaonyesha jinsi gani kwamba ‘tunaiona subira ya Bwana wetu kuwa wokovu’?